Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Umutii Mungu ili Ufaidike na Viapo Vyake

Umutii Mungu ili Ufaidike na Viapo Vyake

Umutii Mungu ili Ufaidike na Viapo Vyake

‘Kwa kuwa [Mungu] hangeweza kuapa kwa yeyote aliye mukubwa zaidi, aliapa kwa nafsi yake mwenyewe.’​—EBR. 6:13.

UNAWEZA KUJIBU?

Sababu gani tunaweza kuwa hakika kama makusudi ya Mungu yatatimia?

Mungu alitoa ahadi gani kisha Adamu na Eva kufanya zambi?

Namna gani tunafaidika na ahadi ambayo Mungu alimuapia Abrahamu?

1. Kuna tofauti gani kati ya Yehova na wanadamu wasio wakamilifu?

 YEHOVA ni “Mungu wa ukweli.” (Zab. 31:5) Kwa sababu wanadamu si wakamilifu kuna wakati hatuweze kutumainia yale wanayosema, lakini ‘Mungu haweze kamwe kusema uongo.’ (Ebr. 6:18; soma Hesabu 23:19.) Mambo yote anayokusudia kufanyia wanadamu yanatimia. Kwa mufano, mwanzoni mwa kila siku ya uumbaji Mungu alikuwa anasema kama atafanya kitu fulani na “ilikuwa hivyo.” Kwa hiyo, mwishoni mwa siku ya sita ya uumbaji, ‘Mungu aliona kila kitu alichokuwa amefanya na, tazama! kilikuwa [kizuri] sana.’​—Mwa. 1:6, 7, 30, 31.

2. Siku ya pumuziko la Mungu ni nini, na sababu gani Mungu ‘aliifanya takatifu’?

2 Kisha kuangalia kazi yake ya uumbaji na kuona kama kila kitu alichoumba kilikuwa kizuri sana, Yehova Mungu alitangaza mwanzo wa siku ya saba. Hiyo si siku yenye saa 24, lakini ni kipindi kirefu cha wakati. Katika kipindi hicho Mungu amepumuzika, ni kusema, ameacha kuumba kitu kingine duniani. (Mwa. 2:2) Mupaka sasa ile siku ya Mungu ya kupumuzika haijamalizika. (Ebr. 4:9, 10) Biblia haionyeshe waziwazi ni wakati gani siku hiyo ilianza. Lakini tunajua kama siku hiyo ilianza wakati fulani kisha kuumbwa kwa bibi ya Adamu, ni kusema, Eva, kumepita sasa miaka 6 000 hivi. Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Yesu Kristo uko mbele yetu, utawala huo utatimiza kusudi ambalo Mungu alikuwa nalo alipoiumba dunia; aliiumba ili iwe paradiso yenye kuikaliwa milele na wanadamu wakamilifu. (Mwa. 1:27, 28; Ufu. 20:6) Je, unawaza kama inawezekana kuwa na maisha kama hayo katika paradiso? Bila shaka, inawezekana! Kwa sababu ‘Mungu aliibariki siku ya saba na kuifanya takatifu.’ Maneno hayo yalitoa uhakikisho kwamba hata kutokee jambo gani lisilotazamiwa, kusudi la Mungu lilipaswa kutimia mwishoni mwa siku ya saba ya kupumuzika kwake.​—Mwa. 2:3.

3. (a) Ni mambo gani yaliyotokea kisha siku ya kupumuzika ya Mungu kuanza? (b) Ni maneno gani ambayo Yehova alisema ili kuonyesha kama angemaliza uasi huo?

3 Hata hivyo, kisha tu siku ya Mungu ya kupumuzika kuanza, matatizo yalitokea. Shetani, ambaye alikuwa malaika na mwana wa Mungu alitaka aabudiwe kama Mungu. Alisema uongo wa kwanza na kumudanganya Eva ili amuasi Yehova. (1 Tim. 2:14) Eva naye alimuingiza bwana yake katika uasi huo. (Mwa. 3:1-6) Hata ikiwa wakati huo Shetani alitaka kuonyesha kama Mungu ni muongo, Yehova hakuona ulazima wa kuapa ili kuhakikisha kama kusudi lake kuelekea dunia litatimia. Lakini, Mungu alitoa ahadi kupitia maneno ambayo yangeeleweka pa wakati ambao yeye mwenyewe aliweka. Kupitia maneno hayo alionyesha namna uasi huo ungemalizika, alisema hivi: ‘Nitaweka uadui kati yako [Shetani] na yule mwanamuke na kati ya uzao wako na uzao wake. Yeye [uzao ulioahidiwa] atakuponda kichwa nawe utamutia jeraha kwenye kisigino.’​—Mwa. 3:15; Ufu. 12:9.

KIAPO NI MUPANGO WA KISHERIA UNAOHAKIKISHA UKWELI WA JAMBO FULANI

4, 5. Ni mupango gani wa kisheria ambao Abrahamu alitumia mara tatu?

4 Inaonekana kama, wakati huo haikuwa lazima kuapa ili kuonyesha kama jambo fulani ni la kweli, na Mungu hakuwapatia Adamu na Eva maneno ya kutumia ili kuapa. Viumbe wakamilifu wanaomupenda Mungu na kuiga sifa zake hawana lazima ya kufanya kiapo; wanasema kweli kila siku na wanaaminiana. Lakini kwa sababu wanadamu walifanya zambi na kupoteza ukamilifu, mambo yalibadilika. Basi, kwa sababu ilianza kuwa jambo la kawaida kwa watu kusema uongo na kudanganya, iliomba sasa wanadamu waanze kuapa ili kuonyesha kama mambo fulani ya maana sana ambayo wanasema ni ya kweli kabisa.

5 Mara tatu Abrahamu alitumia mupango huo wa kisheria vizuri ili kuonyesha kama mambo aliyosema yalikuwa ya kweli. (Mwa. 21:22-24; 24:2-4, 9) Kwa mufano, Abrahamu alipotoka kushinda mufalme wa Elamu na wafalme waliokuja kumusaidia, alifanya kiapo. Wafalme wa Salemu na Sodoma walikuja kukutana na Abrahamu. Melkizedeki, mufalme wa Salemu, alikuwa pia “kuhani wa Mungu Aliye Juu Zaidi.” Kwa hiyo alimubariki na kumusifu Mungu kwa sababu alimusaidia Abrahamu kushinda maadui wake. (Mwa. 14:17-20) Kisha, mufalme wa Sodoma alipotaka kumupatia Abrahamu zawadi kwa sababu aliokoa watu wake kutokana na majeshi yaliyowashambulia, Abrahamu aliapa hivi: “Nainua mukono wangu katika kiapo kwa Yehova Mungu Aliye Juu Zaidi, Mutokezaji wa mbingu na dunia, kwamba, wala uzi wala kamba ya kiatu, sitachukua kitu kutoka kwa chochote kilicho chako, usije ukasema, ‘Ni mimi niliyemutajirisha Abramu.’”​—Mwa. 14:21-23.

YEHOVA ANAFANYA KIAPO

6. (a) Abrahamu alituachia mufano gani? (b) Namna gani tutafaidika kupitia utii wa Abrahamu?

6 Ili wanadamu wasio wakamilifu waamini maneno yake, Yehova pia anaapa kwa kutumia maneno kama vile “‘Kama ninavyoishi,’ asema Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.” (Eze. 17:16) Biblia inamuonyesha Yehova Mungu akifanya kiapo mara zaidi ya 40. Labda mufano unaojulikana zaidi ni namna Mungu alivyomuapia Abrahamu. Kwa miaka mingi, Yehova alimutolea Abrahamu ahadi kupitia agano nyingi, zinazoonyesha kama uzao ulioahidiwa utatokea katika jamaa ya Abrahamu, kupitia mwana wake Isaka. (Mwa. 12:1-3, 7; 13:14-17; 15:5, 18; 21:12) Kisha Yehova alimuomba Abrahamu amutoe mwana wake mupendwa, hilo lilikuwa jaribu kali kabisa. Lakini, bila kusita, Abrahamu alitii na alipokuwa karibu kumutoa mwana wake Isaka, malaika wa Mungu alimuzuia. Kwa hiyo Mungu alimuapia hivi: ‘Naapa kwa nafsi yangu kwamba kwa sababu ya uhakika wa kwamba wewe umefanya jambo hili nawe hukuzuia mwana wako, mwana wako wa pekee, hakika nitakubariki nami nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni na kama chembe za muchanga zilizo kando ya bahari; na uzao wako utamiliki lango la adui zake. Na kupitia kwa uzao wako mataifa yote ya dunia hakika yatajibariki kwa sababu wewe umeisikiliza sauti yangu.’​—Mwa. 22:1-3, 9-12, 15-18.

7, 8. (a) Sababu gani Mungu alimuapia Abrahamu? (b) “Kondoo wengine” wa Yesu Kristo watafaidika namna gani na ahadi ambayo Mungu alimuapia Abrahamu?

7 Sababu gani Mungu alimuapia Abrahamu ili kumuonyesha kama ahadi Zake zitatimia? Alifanya hivyo ili kuwahakikishia wale watakaotawala na Kristo, ni kusema, wale wanaounda sehemu ya pili ya ule “uzao” ulioahidiwa kama ahadi ya Mungu itatimia. Alipenda pia kutia imani yao nguvu. (Soma Waebrania 6:13-18; Gal. 3:29) Mutume Paulo anafasiria jambo hilo hivi, Yehova ‘aliingilia kati kwa kiapo, ili, kupitia mambo mawili yasiyobadilika [ahadi yake na kiapo chake] ambayo katika hayo Mungu haweze kamwe kusema uwongo . . . tupate kuwa na kitia​-moyo chenye nguvu kushikilia tumaini lililowekwa mbele yetu.’

8 Si Wakristo watiwa​-mafuta tu ndio watakaofaidika na kiapo ambacho Mungu alimuapia Abrahamu. Yehova aliapa kama watu wa ‘mataifa yote ya dunia yangejibariki’ kupitia “uzao” wa Abrahamu. (Mwa. 22:18) “Kondoo wengine” wanaomutii Kristo, wamo kati ya watu hao wa mataifa yote, naye amewatolea tumaini la kuishi milele katika dunia paradiso. (Yoh. 10:16) Iwe tumaini lako ni la kuishi mbinguni ao duniani, “shikilia” tumaini hilo kwa kuendelea kumutii Mungu katika maisha yako.​—Soma Waebrania 6:11, 12.

VIAPO VINGINE VINAVYOHUSIANA NA AHADI HIYO

9. Mungu alifanya kiapo gani wakati wazao wa Abrahamu walikuwa katika utumwa huko Misri?

9 Miaka mingi baadaye, Yehova aliapa tena kuhusiana na ahadi aliyomupatia Abrahamu. Alifanya hivyo alipomutuma Musa kwa wazao wa Abrahamu waliokuwa katika utumwa huko Misri. (Kut. 6:6-8) Akizungumuzia wakati huo, Mungu alisema hivi: ‘Katika siku ile nilipochagua Israeli, niliuinua mukono wangu katika kiapo kwao ili kuwatoa katika inchi ya Misri mupaka katika inchi niliyokuwa nimeipeleleza kwa ajili yao, yenye kutiririka maziwa na asali.’​—Eze. 20:5, 6.

10. Yehova aliwatolea Waisraeli ahadi gani kisha kuwakomboa kutoka Misri?

10 Kisha Waisraeli kukombolewa katika utumwa wa Misri, Yehova aliwaapia tena hivi: ‘Ikiwa mutaitii sauti yangu kabisa na kulishika kwa kweli agano langu, ndipo hakika mutakapokuwa mali yangu ya pekee kutoka kati ya vikundi vingine vyote vya watu, kwa sababu dunia nzima ni yangu. Na ninyi wenyewe mutakuwa kwangu ufalme wa makuhani na taifa takatifu.’ (Kut. 19:5, 6) Waisraeli walipewa pendeleo nzuri kabisa! Ikiwa wangekuwa watiifu, watu wa taifa hilo wangekuwa na tumaini la kutumiwa na Mungu ili kufanyiza ufalme wa makuhani ambao ungeletea wanadamu wote baraka. Baadaye, ili kueleza kama amekwisha kuwatimizia kiapo hicho, Yehova alisema hivi: ‘Nilikutolea ahadi yenye kiapo na kuingia katika agano pamoja nawe.’​—Eze. 16:8.

11. Waisraeli walijibu namna gani Mungu alipofanya agano pamoja nao ili wawe watu wake aliochagua?

11 Wakati huo, Yehova hakuwalazimisha Waisraeli kuapa kama watamutii; wala hakuwalazimisha wakubali pendeleo hilo la kuwa na uhusiano wa pekee pamoja naye. Lakini, Waisraeli wao wenyewe walisema hivi: “Yote ambayo Yehova amesema tuko tayari kuyafanya.” (Kut. 19:8) Siku tatu baadaye, Yehova Mungu alijulisha taifa lake chaguliwa mambo ambayo walipaswa kufanya. Kwanza, walipokea Amri Kumi, na kisha Musa aliwatolea amri zingine zinazopatikana katika kitabu cha Kutoka 20:22 mupaka Kutoka 23:33. Waisraeli waliitikia namna gani? “Watu wote wakajibu kwa sauti moja na kusema: ‘Maneno yote ambayo Yehova amesema tuko tayari kuyafanya.’” (Kut. 24:3) Kisha Musa akaandika sheria hizo katika “kitabu cha agano” na akazisomea watu kwa sauti kubwa ili taifa lote lisikie tena. Kwa mara ya tatu, watu walifanya naziri hii: “Yote ambayo Yehova amesema tuko tayari kuyafanya na kuyatii.”​—Kut. 24:4, 7, 8.

12. Kupatana na agano ambalo Yehova alifanya kati yake na Waisraeli, Yehova alifanya nini kwa upande wake, na Waisraeli walifanya nini?

12 Yehova alianza mara moja kutimiza sehemu yake kuhusu yale aliyosema katika agano la Sheria; alichukua mipango ili hema ya ibada ijengwe na kusimamisha makuhani ili wanadamu wasio wakamilifu wamukaribie Mungu. Lakini, Waisraeli walisahau mbio naziri yao ya kujitoa kwa Mungu na ‘wakamutia uchungu Mutakatifu wa Israeli.’ (Zab. 78:41) Kwa mufano, Musa alipokuwa kwenye Mulima Sinai ili kupokea maagizo mengine kutoka kwa Mungu, Waisraeli walishindwa kuvumilia na walipoteza imani, na kuanza kufikiri kama Musa amewakimbia. Kwa hiyo walifanya sanamu ya ndama na wakaanza kusema hivi: ‘Huyu ndiye Mungu wako, Ee Israeli, aliyekuongoza kutoka inchi ya Misri.’ (Kut. 32:1, 4) Kisha wakafanya karamu ambayo waliita “sherehe kwa ajili ya Yehova” na kuinamia sanamu hiyo iliyofanywa na mikono ya mwanadamu na kuitolea zabihu. Yehova alipoona hayo, alimuambia Musa hivi: “Wamegeuka kando haraka kutoka katika njia niliyowaamuru waende.” (Kut. 32:5, 6, 8) Jambo la kuhuzunisha ni kwamba kuanzia wakati huo Waisraeli walikuwa wakifanya naziri kwa Mungu na kuzivunja baadaye.​—Hes. 30:2.

VIAPO VINGINE VIWILI

13. Yehova alimuapia Mufalme Daudi kiapo gani, na kiapo hicho kinahusiana namna gani na Uzao ulioahidiwa?

13 Daudi alipokuwa akitawala, Yehova alifanya viapo vingine viwili ili kutimiza ahadi zake kwa faida ya wale wanaomutii. Kwanza, Mungu alimuapia Daudi kama kiti chake cha ufalme kitadumu milele. (Zab. 89:35, 36; 132:11, 12) Hilo lilimaanisha kama uzao ulioahidiwa utaitwa “mwana wa Daudi.” (Mt. 1:1; 21:9) Kwa unyenyekevu, Daudi alimuita muzao huyo “Bwana” wake, kwa sababu Kristo angekuwa mukubwa kuliko yeye.​—Mt. 22:42-44.

14. Yehova alifanya kiapo gani kuhusu Uzao ulioahidiwa, na tunafaidika namna gani kutokana na kiapo hicho?

14 Jambo la pili, Yehova alimuongoza Daudi kuandika kama Mufalme huyo wa pekee atakuwa Kuhani Mukubwa kwa ajili ya wanadamu. Katika taifa la Israeli haingewezekana mutu kuwa mufalme na kuhani. Makuhani walichaguliwa katika kabila la Lawi, na wafalme katika kabila la Yuda. Lakini kuhusu muriti wake wa pekee, Daudi alitabiri hivi: “Neno la Yehova kwa Bwana wangu ni: ‘Keti kwenye mukono wangu wa kuume mupaka niwaweke adui zako kuwa kiti cha miguu yako.’ Yehova ameapa (naye hatajuta): ‘Wewe ni kuhani mupaka wakati usio na kipimo kwa mufano wa Melkizedeki!’” (Zab. 110:1, 4) Unabii huo umetimia kwa sababu Yesu Kristo, Uzao ulioahidiwa, anatawala sasa huko mbinguni akiwa kwenye mukono wa kuume wa Mungu. Yeye pia ni Kuhani Mukubwa kwa sababu anawasaidia wanadamu wanaotubu wakubaliwe na Mungu na wawe na uhusiano muzuri pamoja naye.​—Soma Waebrania 7:21, 25, 26.

TAIFA JIPYA LA ISRAELI WA MUNGU

15, 16. (a) Biblia inazungumuzia Waisraeli gani wa namna mbili, na ni Waisraeli gani ambao Mungu anabariki leo? (b) Yesu aliwapa wanafunzi wake amri gani kuhusu viapo?

15 Taifa la Israeli lilimukataa Yesu Kristo, kwa hiyo lilipoteza pendeleo la kuwa taifa chaguliwa la Mungu na pendeleo la kuwa “ufalme wa makuhani.” Yesu aliwaambia hivi viongozi Wayahudi hivi: “Ufalme wa Mungu utachukuliwa kutoka kwenu na kupewa taifa lenye kuzaa matunda yake.” (Mt. 21:43) Taifa hilo jipya lilizaliwa kwenye Pentekoste ya mwaka wa 33, wakati wanafunzi 120 wa Yesu Kristo, waliokusanyika katika Yerusalemu, walipokea roho ya Mungu. Wanafunzi hao walianza kuitwa “Israeli wa Mungu” na bila kukawia hesabu yao ikawa kubwa. Hesabu hiyo ilifanyizwa na watu kutoka kila taifa lililojulikana wakati huo.​—Gal. 6:16.

16 Taifa hilo jipya la Mungu si kama taifa la kale la Israeli, kwa sababu linaendelea kuzaa matunda mazuri kwa kuendelea kumutii Mungu. Wakristo hao wanatii sheria za Mungu, moja kati ya sheria hizo inahusu viapo. Yesu alipokuwa duniani, watu hawakuheshimu viapo vyao, na walifanya viapo juu ya mambo yasiyo ya lazima. (Mt. 23:16-22) Lakini Yesu aliwafundisha wanafunzi wake hivi: ‘Musiape hata kidogo. Acheni tu neno lenu Ndiyo limaanishe Ndiyo, Siyo yenu, Siyo; kwa maana linalozidi hayo linatoka kwa yule muovu.’​—Mt. 5:34, 37.

17. Habari inayofuata itajibu maulizo gani?

17 Je, hilo linamaanisha kama ni vibaya kabisa kuapa? Zaidi ya hilo, inamaanisha nini kuacha Ndiyo yetu iwe Ndiyo? Habari inayofuata itajibu maulizo hayo. Tunapoendelea kutafakari Neno la Mungu, acheni litusaidie tuendelee kumutii Yehova. Tukifanya hivyo, yeye atatubariki milele kulingana na ahadi zake alizofanya kupitia viapo.

[Maulizo ya Funzo]

[Wazo la fungu kwenye ukurasa 26]

Sikuzote Mungu anatimiza ahadi zake

[Picha katika ukurasa wa 24]

Abrahamu atajionea utimizo wa ahadi za Yehova hivi karibuni