Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kukabiliana Na Matatizo Ya Leo Kwa Ujasiri

Kukabiliana Na Matatizo Ya Leo Kwa Ujasiri

“Kwetu Mungu ni kimbilio na nguvu, msaada unaopatikana kwa utayari wakati wa taabu.”​—ZAB. 46:1.

1, 2. Watu wengi wamepatwa na matatizo gani, lakini watumishi wa Mungu wanatamani nini?

TUNAISHI wakati wa matatizo. Dunia imejaa misiba. Matatizo kama vile matetemeko ya ardhi, tsunami, mioto, mafuriko, volkano, tufani, na vimbunga yamewaumiza sana wanadamu. Isitoshe, matatizo ya kifamilia na ya kibinafsi yamesababisha woga na huzuni. Ni kweli kabisa kwamba “wakati na tukio lisilotazamiwa” hutupata sote.​—Mhu. 9:11.

2 Watumishi wa Mungu kwa ujumla wamekabiliana vyema na hali ngumu kama hizo. Hata hivyo, tungependa kuwa tayari kupambana na hali zozote ngumu ambazo huenda tukakabiliana nazo wakati ujao mfumo huu unapokaribia mwisho wake. Tunawezaje kukabiliana na matatizo hayo badala ya kulemewa nayo? Ni nini kitakachotusaidia kukabiliana kwa ujasiri na matatizo ya leo?

JIFUNZE KUTOKANA NA WALE WALIOKABILIANA NA MATATIZO KWA UJASIRI

3. Kama andiko la Waroma 15:4 linavyoonyesha, tunawezaje kupata faraja tunapokabiliana na hali zenye kufadhaisha?

3 Ingawa watu wengi leo wanakumbwa na hali ngumu kuliko wakati mwingine wowote ule, matatizo yenye kufadhaisha si mageni kwa wanadamu. Acheni tuone yale tunayoweza kujifunza kutokana na watumishi fulani wa kale wa Mungu ambao walifanikiwa kukabiliana na matatizo ya maisha kwa ujasiri.​—Rom. 15:4.

4. Daudi alivumilia matatizo gani, na ni nini kilichomsaidia?

4 Fikiria mfano wa Daudi. Miongoni mwa mambo mengine, Daudi alilazimika kuvumilia hasira ya Mfalme Sauli, mashambulizi ya maadui, kutekwa nyara kwa wake zake, kusalitiwa na marafiki wake mwenyewe, na kuteseka kihisia. (1 Sam. 18:8, 9; 30:1-5; 2 Sam. 17:1-3; 24:15, 17; Zab. 38:4-8) Masimulizi ya Biblia kuhusu maisha ya Daudi yanaonyesha wazi jinsi alivyoumia moyoni kwa sababu ya matatizo hayo. Hata hivyo, matatizo hayo hayakuharibu hali yake ya kiroho. Akiwa amejaa imani, alisema hivi: “Yehova ni ngome ya uhai wangu. Nitamhofu nani?”​—Zab. 27:1; soma Zaburi 27:5, 10.

5. Ni nini kilichowasaidia Abrahamu na Sara kukabiliana na maisha magumu?

5 Abrahamu na Sara waliishi muda mrefu katika mahema wakiwa wageni katika nchi za kigeni. Maisha yao hayakuwa rahisi sikuzote. Hata hivyo, walikabiliana kwa ujasiri na mambo kama vile njaa na hatari kutoka kwa mataifa yaliyowazunguka. (Mwa. 12:10; 14:14-16) Ni nini kilichowawezesha kukabiliana na hali hizo? Neno la Mungu linatuambia kwamba Abrahamu “alikuwa akingojea jiji lililo na misingi ya kweli, ambalo mjenzi na mtengenezaji wa jiji hilo ni Mungu.” (Ebr. 11:8-10) Abrahamu na Sara walikazia fikira mambo yaliyokuwa mbele yao, nao hawakujiruhusu wakengeushwe na watu waliowazunguka.

6. Tunawezaje kumwiga Ayubu?

6 Ayubu aliteseka sana. Wazia jinsi alivyohisi wakati kila kitu katika maisha yake kilipoonekana kuwa kinaenda kombo. (Ayu. 3:3, 11) Kilichofanya hali iwe mbaya hata zaidi ni kwamba hakuelewa kikamili kwa nini alipatwa na mambo hayo yote. Hata hivyo, hakukata tamaa kamwe. Alidumisha utimilifu wake na imani yake katika Mungu. (Soma Ayubu 27:5.) Alituwekea mfano mzuri kama nini wa kuiga!

7. Paulo alikabili nini alipokuwa akimtumikia Mungu, lakini ni nini kilichompa ujasiri wa kuendelea?

7 Fikiria pia mfano wa mtume Paulo. Alikabili ‘hatari ndani ya jiji, nyikani, na baharini.’ Anataja kuhusu ‘njaa na kiu, baridi na uchi.’ Pia, Paulo anataja kuhusu kukaa ‘usiku mmoja na mchana mmoja katika kilindi,’ inaelekea kwa sababu alivunjikiwa na meli wakati fulani. (2 Kor. 11:23-27) Licha ya hayo yote, ona mtazamo aliokuwa nao baada ya kukabili hatari ya kifo kwa sababu ya kumtumikia Mungu: “Ilikuwa hivyo ili uhakika wetu uwe, si katika sisi wenyewe, bali katika Mungu ambaye huwafufua wafu. Kutoka katika kitu kikubwa sana kama kifo alituokoa naye atatuokoa.” (2 Kor. 1:8-10) Si watu wengi ambao wamewahi kukabili mambo mengi mabaya kama Paulo. Hata hivyo, wengi wetu tumewahi kuhisi kama Paulo na tunaweza kufarijiwa na mfano wake wa ujasiri.

USILEMEWE NA MATATIZO

8. Matatizo ya leo yanawezaje kutuathiri? Toa mfano.

8 Katika ulimwengu wa leo uliojaa misiba, taabu, na mikazo, watu wengi wanahisi kwamba wanalemewa na matatizo. Hata baadhi ya Wakristo wamehisi vivyo hivyo. Lani, * aliyekuwa akifurahia utumishi wa wakati wote pamoja na mume wake huko Australia anasema ilipogunduliwa kwamba ana kansa ya matiti, habari hizo zilimfadhaisha sana na zilikuja kwa ghafla kama mpigo wa radi. Anasema hivi: “Matibabu yalinifanya niwe mgonjwa sana, na nilijihisi sifai kamwe.” Na zaidi ya hayo, alipaswa kumtunza mume wake, ambaye alikuwa amefanyiwa upasuaji wa uti wa mgongo. Tunaweza kufanya nini tukijikuta katika hali kama hiyo?

9, 10. (a) Hatupaswi kumruhusu Shetani afanye nini? (b) Tunaweza kukabilianaje na ukweli unaotajwa katika andiko la Matendo 14:22?

9 Ni vizuri tukumbuke kwamba Shetani anataka kutumia dhiki mbalimbali tunazokabili ili kudhoofisha imani yetu. Hata hivyo, hatupaswi kumruhusu atunyang’anye shangwe yetu kwa njia hiyo. Andiko la Methali 24:10 linasema hivi: “Je, umejionyesha kuwa umevunjika moyo siku ya taabu? Nguvu zako zitakuwa chache.” Kutafakari juu ya mifano inayotajwa katika Biblia, kama ile ambayo tumezungumzia mapema, kutatusaidia kupata ujasiri wa kukabiliana na matatizo.

10 Ni vizuri pia kukumbuka kwamba hatuwezi kuondoa matatizo yote. Kwa kweli, tunaweza kutarajia yatupate. (2 Tim. 3:12) Andiko la Matendo 14:22 linatuambia hivi: “Lazima tuingie katika ufalme wa Mungu kupitia dhiki nyingi.” Badala ya kushuka moyo, kwa nini usione matatizo kuwa fursa ya kuonyesha ujasiri unaotegemea imani yako katika uwezo wa Mungu wa kukusaidia?

11. Tunaweza kufanya nini ili tusilemewe na matatizo ya maisha?

11 Tunahitaji kukazia fikira mambo mazuri. Neno la Mungu linatuambia hivi: “Moyo wenye shangwe huchangamsha sura, lakini kwa sababu ya maumivu ya moyo roho hupata pigo.” (Met. 15:13) Watafiti wa kitiba wametambua kwa miaka mingi ukweli wa kwamba mgonjwa hupona haraka ikiwa anafikiria mambo mazuri. Wagonjwa wengi ambao wamepewa vidonge vya sukari wakiamini kuwa ni dawa, wamepata nafuu kwa sababu tu walifikiri kwamba walikuwa wakisaidiwa. Kinyume na hilo, wagonjwa wakiwa na mtazamo usiofaa matokeo yanakuwa mabaya. Afya ya wagonjwa wengi imezorota kwa sababu tu waliambiwa kwamba kutumia dawa fulani kutakuwa na matokeo mabaya. Kuendelea kufikiria hali fulani ambazo hatuwezi kubadili huenda kukatuvunja tu moyo. Kinyume na hilo, Yehova hatupatii “vidonge vya sukari.” Badala yake, hata nyakati za misiba, anatoa msaada wa kweli kwa kututia moyo kupitia Neno lake, ndugu na dada zetu wanaotutegemeza, na pia anatupa nguvu kupitia roho takatifu. Kukazia fikira mambo hayo kutatuimarisha. Badala ya kuendelea kufikiria mambo mabaya, fanya unayoweza ili ukabiliane na kila tatizo na ukazie fikira mambo mazuri katika maisha yako.​—Met. 17:22.

12, 13. (a) Ni nini ambacho kimewasaidia watumishi wa Mungu kuvumilia matokeo mabaya ya misiba? Toa mfano. (b) Misiba inapotokea, tunawezaje kujua jambo lililo muhimu zaidi katika maisha ya mtu?

12 Katika nyakati za hivi karibuni, baadhi ya nchi zimepatwa na misiba mibaya sana. Ndugu zetu wengi katika nchi hizo wameonyesha uvumilivu wa ajabu. Hilo halimaanishi kwamba ilikuwa rahisi kwao kuvumilia. Mwanzoni mwa mwaka wa 2010, tetemeko kubwa la ardhi na tsunami huko Chile iliharibu nyumba na mali nyingi za ndugu zetu, na ndugu fulani walipoteza njia yao ya kupata riziki. Licha ya hali hiyo, akina ndugu waliendelea vizuri kiroho. Samuel, ambaye nyumba yake iliharibiwa kabisa, alisema hivi: “Hata wakati wa hali hizo ngumu sana, mimi na mke wangu hatukuacha kamwe kuhudhuria mikutano na kuhubiri. Ninaamini kwamba mazoea hayo yalitusaidia tusikate tamaa.” Wao pamoja na ndugu na dada wengine wengi hawakuruhusu msiba huo uwavunje moyo, waliendelea kumtumikia Yehova kwa bidii.

13 Mnamo Septemba 2009, zaidi ya asilimia 80 ya mji wa Manila, Ufilipino, ilikumbwa na mafuriko kwa sababu ya mvua kubwa iliyonyesha. Mwanamume mmoja tajiri aliyepoteza vitu vingi alisema, “Mafuriko hayo yaliathiri kila mtu na kusababisha matatizo na mateso kwa matajiri na maskini pia.” Jambo hilo linatukumbusha shauri hili la Yesu lenye busara: “Jiwekeeni hazina mbinguni, ambako nondo na kutu havili, na ambako wezi hawavunji na kuiba.” (Mt. 6:20) Kutanguliza vitu vya kimwili maishani, ambavyo vinaweza kutoweka haraka sana, mara nyingi kunakatisha tamaa. Ni jambo la hekima zaidi kutanguliza maishani uhusiano wetu pamoja na Yehova, ambao unaweza kudumu hata hali gani itokee.​—Soma Waebrania 13:5, 6.

SABABU ZA KUONYESHA UJASIRI

14. Tuna sababu zipi za kuonyesha ujasiri?

14 Yesu alikiri kwamba kungekuwa na matatizo wakati wa kuwapo kwake, lakini alisema hivi: “Msiogope.” (Luka 21:9) Yesu akiwa Mfalme wetu na kwa msaada wa Muumba wa ulimwengu wote, tuna kila sababu ya kuwa na uhakika. Paulo alimtia moyo hivi Timotheo: “Mungu hakutupa sisi roho ya woga, bali ile ya nguvu na ya upendo na ya utimamu wa akili.”​—2 Tim. 1:7.

15. Toa mifano inayoonyesha usadikisho wa watumishi wa Mungu, na ueleze jinsi tunavyoweza kuwa na ujasiri kama huo.

15 Ona baadhi ya maneno yaliyosemwa na watumishi wa Mungu yanayoonyesha usadikisho wenye nguvu. Daudi alisema hivi: “Yehova ni nguvu zangu na ngao yangu. Moyo wangu umemtegemea yeye, nami nimesaidiwa, hivi kwamba moyo wangu unashangilia.” (Zab. 28:7) Paulo alisema hivi kuhusu usadikisho wake usioyumba-yumba: “Katika mambo haya yote tunatokea tukiwa tumeshinda kabisa kupitia yeye aliyetupenda.” (Rom. 8:37) Vivyo hivyo, hatari ilipokuwa ikikaribia, Yesu aliwasadikishia kabisa wasikilizaji wake kwamba alikuwa na uhusiano wenye nguvu pamoja na Mungu kwa kusema hivi: “Siko peke yangu, kwa sababu Baba yuko pamoja nami.” (Yoh. 16:32) Ni jambo gani linaloonekana wazi katika maneno hayo ya watumishi wa Mungu? Kila mmoja wao anaonyesha kwamba alimtegemea Yehova bila kuyumba-yumba. Tukisitawisha usadikisho kama huo katika Mungu tunaweza kupata ujasiri wa kukabiliana na tatizo lolote leo.​—Soma Zaburi 46:1-3.

FAIDIKA KUTOKANA NA MAANDALIZI YANAYOTUSAIDIA KUDUMISHA UJASIRI

16. Kwa nini kujifunza Neno la Mungu ni muhimu kwetu?

16 Kuwa na ujasiri wa Kikristo hakumaanishi kujitegemea mwenyewe. Badala yake, tunakuwa na ujasiri tunapomjua Mungu na kumtegemea. Tunaweza kufanya hivyo kwa kujifunza Neno lake lililoandikwa, Biblia. Dada mmoja aliye na ugonjwa wa kushuka moyo anaeleza kinachomsaidia, “Ninasoma tena na tena hasa maandiko yenye kufariji.” Je, tumetii mwongozo wa kuwa na ibada ya kawaida ya familia? Kufanya mambo hayo kutatusaidia kuwa na mtazamo wa mtunga-zaburi ambaye alisema hivi: “Jinsi ninavyoipenda sheria yako! Ndiyo ninayoihangaikia mchana kutwa.”​—Zab. 119:97.

17. (a) Ni uandalizi gani unaoweza kutusaidia kudumisha mtazamo wa ujasiri? (b) Eleza kuhusu simulizi moja la maisha ambalo limekusaidia.

17 Pia, tuna machapisho yanayotegemea Biblia yenye habari zinazoimarisha usadikisho wetu katika Yehova. Ndugu wengi wameona kwamba masimulizi ya maisha yaliyo katika magazeti yetu yanawasaidia sana. Dada mmoja huko Asia aliye na ugonjwa wa kubadilika-badilika kwa hisia alitiwa moyo aliposoma simulizi la maisha kuhusu ndugu mmoja aliyekuwa mmishonari zamani na aliyefanikiwa kukabiliana na ugonjwa huohuo. Dada huyo aliandika hivi: “Simulizi hilo lilinisaidia kuelewa tatizo langu na lilinipa tumaini.”

18. Kwa nini tunapaswa kutumia uandalizi wa sala?

18 Sala inaweza kutusaidia katika kila hali. Mtume Paulo alikazia thamani ya msaada huo, kwa kusema: “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Flp. 4:6, 7) Je, tunafaidika kikamili na uandalizi huo unaotusaidia kupata nguvu wakati wa matatizo? Alex, ndugu mmoja nchini Uingereza ambaye amesumbuliwa kwa muda mrefu na ugonjwa wa kushuka moyo, alisema hivi: “Kuzungumza na Yehova katika sala na kumsikiliza kwa kusoma Neno lake kumenitegemeza maishani.”

19. Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu kuhudhuria mikutano ya Kikristo?

19 Kushirikiana na wengine kwenye mikutano ni uandalizi mwingine muhimu unaotusaidia. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Nafsi yangu imetamani sana na pia imedhoofika kwa kutamani nyua za Yehova.” (Zab. 84:2) Je, tunahisi vivyo hivyo? Lani, aliyetajwa mapema, anaeleza maoni yake kuhusu ushirika wa Kikristo: “Ilikuwa lazima kwangu kuhudhuria mikutano. Nilijua kwamba nilipaswa kuwa kwenye mikutano ikiwa nilimtazamia Yehova anisaidie kukabiliana na hali yangu.”

20. Kushiriki katika kazi ya kuhubiri kutatusaidiaje?

20 Tunapata pia ujasiri kwa kuendelea kushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme. (1 Tim. 4:16) Dada mmoja nchini Australia ambaye amepatwa na matatizo mengi anasema hivi: “Sikupenda sana kuhubiri, lakini mzee mmoja alinialika nihubiri pamoja naye. Nikaenda. Ni wazi kwamba Yehova alikuwa akinisaidia; kila mara niliposhiriki katika huduma, nilifurahi sana.” (Met. 16:20) Wengi wameona kwamba wanaimarisha imani yao wenyewe wanapowasaidia wengine wajenge imani katika Yehova. Wanapofanya hivyo, hawafikirii sana matatizo yao wenyewe na wanaendelea kukazia fikira mambo yaliyo muhimu zaidi.​—Flp. 1:10, 11.

21. Tuna uhakikisho gani kuhusu matatizo tunayokabiliana nayo?

21 Yehova ametupatia maandalizi mengi ya kutusaidia kukabiliana kwa ujasiri na matatizo ya leo. Tunapoyatumia vizuri maandalizi yote hayo, tunapotafakari na kuiga mifano mizuri ya watumishi wa Mungu wenye ujasiri, tunakuwa na uhakika kwamba tunaweza kukabiliana na matatizo kwa mafanikio. Ingawa mambo mengi mabaya huenda yakatokea mfumo huu unapokaribia mwisho wake, tunaweza kuhisi kama Paulo aliyesema hivi: “Tunaangushwa chini, lakini hatuangamizwi. . . . Hatufi moyo.” (2 Kor. 4:9, 16) Kwa msaada wa Yehova, tunaweza kukabiliana na matatizo ya leo kwa ujasiri.​—Soma 2 Wakorintho 4:17, 18.

^ fu. 8 Baadhi ya majina yamebadilishwa.