Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kupambana na Matatizo ya Leo kwa Ujasiri

Kupambana na Matatizo ya Leo kwa Ujasiri

Kupambana na Matatizo ya Leo kwa Ujasiri

‘Kwetu Mungu ni kimbilio na nguvu, musaada unaopatikana kwa utayari wakati wa taabu.’​—ZAB. 46:1.

UNAWEZA KUJIBU?

Tunapaswa kufanya nini ili matatizo yasituvunje moyo?

Sababu gani tunapaswa kutenda kwa ujasiri?

Ni njia gani ambazo Yehova anatumia ili kutusaidia tupambane na matatizo?

1, 2. Ni matatizo gani ambayo wengi wamepambana nayo, lakini watumishi wa Mungu wanapaswa kufanya nini?

 TUNAISHI wakati wa taabu nyingi. Watu wanaendelea kuteseka sana kwa sababu ya matetemeko ya inchi, tsunami, moto, mvua kubwa-kubwa, volkeno, na upepo mukali. Zaidi ya hayo, matatizo ya familia na matatizo ya kibinafsi yamewafanya watu wengi wawe na huzuni na woga. Kama Biblia inavyosema, sisi wote tunapatwa na “wakati na tukio lisilotazamiwa.”​—Mhu. 9:11.

2 Watumishi wote wa Yehova wamevumilia mambo yenye kuvunja moyo. Hata hivyo, kwa kuwa ulimwengu huu unakaribia mwisho wake, tunapaswa kujitayarisha kwa ajili ya matatizo yanayoweza kutokea wakati ujao. Namna gani tunaweza kuvumilia matatizo hayo bila kupoteza furaha yetu? Ni nini itatusaidia kupambana na matatizo ya leo kwa ujasiri?

WALE WALIOPAMBANA NA MATATIZO KWA UJASIRI

3. Kama inavyoonyeshwa katika Waroma 15:4, ni nini inayoweza kutufariji tunapopambana na hali zenye kuhuzunisha?

3 Ijapokuwa watu wengi wanapatwa na hali zenye kuhuzunisha sana kuliko zamani, matatizo hayakuanza leo. Acheni tuone mambo tunayoweza kujifunza kutokana na watumishi fulani wa Mungu wa zamani waliopambana na matatizo ya maisha kwa ujasiri.​—Rom. 15:4.

4. Daudi alivumilia matatizo gani, na alipata musaada wapi?

4 Fikiria matatizo ambayo Daudi alivumilia. Mufalme Sauli alitaka kumuua, wakati fulani maadui walipigana naye na kuchukua bibi zake, watu fulani katika jeshi lake na familia yake na marafiki wake walimusaliti, na mara nyingi alivunjika moyo sana. (1 Sam. 18:8, 9; 30:1-5; 2 Sam. 17:1-3; 24:15, 17; Zab. 38:4-8) Biblia inaonyesha waziwazi namna Daudi alivyosumbuliwa na matatizo hayo. Hata hivyo, matatizo hayo hayakuvunja urafiki wake pamoja na Mungu. Kwa imani, alisema hivi: ‘Yehova ni ngome ya uhai wangu. Nitamuhofu nani?’​—Zab. 27:1; soma Zaburi 27:5, 10.

5. Ni nini iliyosaidia Abrahamu na Sara kupambana na matatizo ya maisha?

5 Kwa miaka mingi, Abrahamu na Sara waliishi katika mahema kama wakaaji wageni katika inchi ambayo hawakufahamia vizuri. Maisha yao hayakuwa rahisi. Hata hivyo, waliazimia kupambana na mambo kama vile njaa na hatari mbalimbali kutoka mataifa yaliyowazunguka. (Mwa. 12:10; 14:14-16) Ni nini iliyowasaidia? Neno la Mungu linatuambia kama Abrahamu ‘alikuwa akingojea jiji lililo na misingi ya kweli, ambalo mujenzi na mutengenezaji wa jiji hilo ni Mungu.’ (Ebr. 11:8-10) Abrahamu na Sara walikaza macho kwenye mambo yaliyokuwa mbele yao, hawakudanganywa na mataifa yaliyowazunguka.

6. Namna gani tunaweza kumuiga Ayubu?

6 Ayubu aliteseka sana. Wazia namna alivyojisikia wakati kila jambo halikuendeka katika maisha yake. (Ayu. 3:3, 11) Zaidi ya hayo, Ayubu hakuelewa kwa nini mambo yote hayo yalimufikia. Hata hivyo, aliendelea kuvumilia. Aliendelea kubaki mwaminifu na kushikamana na Mungu. (Soma Ayubu 27:5.) Bila shaka yeye ni mufano muzuri kwetu!

7. Ni matatizo gani ambayo Paulo alipambana nayo, lakini ni nini iliyomusaidia aendelee kuwa na ujasiri?

7 Fikiria pia mutume Paulo. Alivumilia ‘hatari ndani ya jiji, nyikani, na baharini.’ Alivumilia ‘njaa na kiu, baridi na uchi.’ Paulo anaonyesha pia kama alipitisha ‘usiku na muchana katika kilindi,’ labda ni kwa sababu mashua aliyokuwa ndani ilivunjika. (2 Kor. 11:23-27) Ijapokuwa matatizo yote hayo, Paulo aliyekuwa karibu kupoteza maisha yake kwa sababu ya kumutumikia Mungu, alisema hivi: “Ilikuwa hivyo ili uhakika wetu uwe, si katika sisi wenyewe, bali katika Mungu ambaye huwafufua wafu. Kutoka katika kitu kikubwa sana kama kifo alituokoa naye atatuokoa.” (2 Kor. 1:8-10) Ni wachache tu ndio wamepambana na matatizo kama yale yaliyomupata Paulo. Hata hivyo, tunapopambana na matatizo kama hayo, mufano wake wa ujasiri unaweza kutufariji.

MATATIZO YASIKUVUNJE MOYO

8. Matatizo yaliyo katika ulimwengu huu yanaweza kutufanya tujisikie namna gani? Toa mufano.

8 Leo tunaweza kupoteza furaha yetu sababu ulimwengu umejaa misiba, matatizo na mikazo mbalimbali. Hata Wakristo fulani wamepoteza furaha yao kwa sababu ya matatizo hayo. Dada Lani, * aliyekuwa katika utumishi wa wakati wote pamoja na bwana yake huko Australie, anasema kama muganga alipomuambia kama ana ugonjwa wa kansere ya liziba (cancer du sein), habari hiyo ilimushtua kama mutu anayepigwa na radi. Lani anasema hivi: “Dawa niliyopata iliniongezea maumivu, na nilijisikia wa bure.” Ijapokuwa Dada Lani alikuwa na tatizo hilo, alipaswa kumutunza bwana yake, aliyekuwa amefanyiwa upasuaji wa uti wa mugongo (colonne vertébrale). Dada Lani aliteseka sana. Ikiwa tunajikuta katika hali kama hiyo, tunaweza kufanya nini?

9, 10. (a) Hatupaswe kumuruhusu Shetani afanye nini? (b) Tunapaswa kufanya nini tunapokutana na ziki inayozungumuziwa katika andiko la Matendo 14:22?

9 Ni vizuri tukumbuke kama Shetani anatumia mateso ili kuregeza imani yetu. Hata hivyo, hatupaswi kumuruhusu atunyanganye furaha yetu. Methali 24:10 inasema hivi: “Je, umejionyesha kuwa umevunjika moyo siku ya taabu? Nguvu zako zitakuwa chache.” Kufikiri sana juu ya mifano ya watumishi wa Mungu wa zamani, kama vile wale tuliozungumuzia, kunaweza kutusaidia tupambane na matatizo kwa ujasiri.

10 Ni vizuri pia tukumbuke kama hatuwezi kutatua matatizo yote. Lakini, tukumbuke pia kwamba hatuwezi kuyaepuka. (2 Tim. 3:12) Andiko la Matendo 14:22 linasema hivi: ‘Lazima tuingie katika ufalme wa Mungu kupitia ziki nyingi.’ Kuliko kuvunjika moyo, acheni tupambane na matatizo hayo kwa ujasiri, hilo litaonyesha kama tuko hakika kabisa kama Mungu anaweza kutusaidia tushinde.

11. Tunapaswa kufanya nini ili matatizo ya maisha yasituvunje moyo?

11 Ni lazima tuendelee kufikiria mambo mazuri tuliyo nayo maishani. Neno la Mungu linatuambia hivi: ‘Moyo wenye shangwe huchangamusha sura, lakini kwa sababu ya maumivu ya moyo roho hupata pigo.’ (Met. 15:13) Waganga wanajua kama mugonjwa akiwa na tumaini la kupona, hilo linaweza kumusaidia sana hata kama anatumia dawa isiyokuwa ya ugonjwa wake. Kwa upande mwengine, afya ya wagonjwa ilikuwa mbaya zaidi walipoambiwa kama dawa wanayotumia haiwezi kuwaponesha. Kuendelea kufikiria mambo ambayo hatuwezi kubadili kunaweza tu kutuvunja moyo. Tunapopatwa na musiba, Yehova anatutolea musaada wa kweli kupitia vitia​-moyo kutoka katika Neno lake, anatusaidia kupitia ndugu na dada zetu wanaotutegemeza wakati wa taabu, na anatutia nguvu kupitia roho yake takatifu. Huo ni musaada mukubwa sana kutoka kwa Yehova ili tusivunjike moyo. Kuliko kufikiria tu matatizo yako, fanya yale unayoweza ili kupambana na kila tatizo na ufikirie mambo mazuri uliyo nayo maishani.​—Met. 17:22.

12, 13. (a) Ni mambo gani ambayo yamewasaidia watumishi wa Mungu wavumilie misiba? Toa mufano. (b) Namna gani misiba inatusaidia kujua mambo yaliyo ya maana maishani?

12 Katika miaka ya hivi karibuni, inchi nyingi zimepigwa na misiba. Lakini, ndugu wengi katika inchi hizo wameonyesha utulivu mukubwa. Hilo halimaanishe kama mambo yalikuwa rahisi kwao. Katika Mwezi wa 2, 2010, inchi ya Chili ilipigwa na tetemeko kubwa la inchi na tsunami. Ndugu na dada zetu walipoteza nyumba na vitu vyao, na wengine walipoteza vitu vyao vyote. Hata hivyo, ndugu na dada waliendelea kuhubiri na kukusanyika. Ndugu Samuel, ambaye nyumba yake iliharibiwa kabisa, alisema hivi: “Hata ikiwa hali ilikuwa ngumu sana, mimi na muke wangu hatukuacha kuhuzuria mikutano na kuhubiri. Niko hakika kama kufanya hivyo kulitusaidia tusivunjike moyo.” Kuliko kuendelea kufikiria matatizo waliyopata kwa sababu ya musiba huo, ndugu zetu wa huko Chili waliendelea kufanya kazi ya Yehova.

13 Katika Mwezi wa 9, 2009, mvua kubwa ilinyesha katika Manila, muji mukubwa wa Philippines, na sehemu nyingi za muji huo zilijaa maji. Mwanaume mumoja tajiri aliyepoteza vitu vingi alisema hivi: “Mvua hiyo kubwa, iliwatesa watu wote, matajiri kama vile maskini.” Hilo linatukumbusha shauri hili lenye hekima la Yesu: “Jiwekeeni hazina mbinguni, ambako nondo na kutu havili, na ambako wezi hawavunji na kuiba.” (Mt. 6:20) Mara nyingi, watu wanaotumia maisha yao ili kufuatia tu vitu vya kimwili, visivyoweza kudumu, wanavunjika moyo. Kwa hiyo ni jambo la hekima kutumia maisha yetu ili kuwa na uhusiano muzuri pamoja na Yehova. Hakuna jambo linaloweza kuvunja uhusiano huo!​—Soma Waebrania 13:5, 6.

KWA NINI TUTENDE KWA UJASIRI?

14. Sababu gani hatupaswe kuogopa?

14 Yesu alijua kama kutakuwa matatizo mengi katika siku za mwisho, kwa hiyo alisema hivi: ‘Musiogope.’ (Lu. 21:9) Kwa kuwa Mufalme wetu Yesu na Muumbaji wa ulimwengu wote muzima wanatutegemeza, hatupaswe kuogopa. Ili kumutia Timotheo moyo, Paulo alimuambia hivi: “Mungu hakutupa sisi roho ya woga, bali ile ya nguvu na ya upendo na ya utimamu wa akili.”​—2 Tim. 1:7.

15. Toa mifano ya watu waliomutumainia Mungu, na ni nini inaweza kutusaidia kupambana na matatizo kwa ujasiri kama wao?

15 Fikiria maneno fulani yanayoonyesha namna watumishi wa Mungu walivyomutumainia. Daudi alisema hivi: ‘Yehova ni nguvu zangu na ngao yangu. Moyo wangu umemutegemea yeye, nami nimesaidiwa, hivi kwamba moyo wangu unashangilia.’ (Zab. 28:7) Paulo alionyesha tumaini lake lisilo yumba-yumba aliposema hivi: “Katika mambo haya yote tunatokea tukiwa tumeshinda kabisa kupitia yeye aliyetupenda.” (Rom. 8:37) Vilevile, Yesu alipokuwa karibu kukamatwa na kuuawa, aliwaonyesha waziwazi wasikilizaji wake kwamba alimutumainia sana Mungu, kwa hivyo alisema hivi: “Siko peke yangu, kwa sababu Baba yuko pamoja nami.” (Yoh. 16:32) Maneno yote hayo yanaonyesha nini? Yote yanaonyesha kama watumishi hao walimutumainia Yehova bila kuyumba-yumba. Nasi tukimutumainia Yehova kama wao, tunaweza kupambana na matatizo ya leo kwa ujasiri.​—Soma Zaburi 46:1-3.

JINSI YEHOVA ANAVYOTUSAIDIA

16. Sababu gani tunapaswa kujifunza Neno la Mungu?

16 Hatuwezi kupata ujasiri kwa nguvu yetu wenyewe. Lakini, ili tupate ujasiri, tunapaswa kumujua Mungu na kumutegemea. Kujifunza Neno lake, Biblia, kutatusaidia tumujue Mungu. Akieleza jambo linalomusaidia, dada mumoja mwenye ugonjwa wa kushuka moyo anasema hivi: “Ninasoma tena na tena maandiko yenye kufariji.” Je, tunafanya ibada ya familia kwa ukawaida? Kufanya hivyo kutatusaidia kuwa na maoni kama ya mutunga-zaburi aliyesema hivi: ‘Jinsi ninavyoipenda sheria yako! Ndiyo ninayoihangaikia muchana kutwa.’​—Zab. 119:97.

17. (a) Ni jambo gani linaloweza kutusaidia kuwa na ujasiri? (b) Eleza namna masimulizi kuhusu maisha ya mutu fulani yalivyokusaidia.

17 Tuna pia vichapo vinavyotegemea Biblia. Vichapo hivyo vinajaa habari zinazoweza kutia nguvu imani yetu. Ndugu wengi wamefaidika na masimulizi kuhusu maisha ya watu yanayopatikana katika magazeti yetu. Dada mumoja katika Asia aliye na ugonjwa unaofanya hisia zibadilike-badilike alifurahi aliposoma masimulizi kuhusu maisha ya ndugu mumoja aliyekuwa misionere hapo zamani aliyekuwa na ugonjwa huo. Dada huyo aliandika hivi: “Habari hiyo ilinisaidia kuelewa ugonjwa wangu na ilinipa tumaini.”

18. Sababu gani tusali tunapopambana na matatizo?

18 Sala inaweza kutusaidia tunapopambana na matatizo ya kila namna. Akieleza faida ya sala, mutume Paulo alisema hivi: ‘Musihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.’ (Flp. 4:6, 7) Tunapopambana na matatizo, je, sisi tunasali ili kupata ujasiri? Ndugu Alex, anayeishi Grande-Bretagne, ambaye alisumbuliwa na ugonjwa wa kushuka moyo kwa muda murefu, alisema hivi: “Kusali kwa Yehova na kusikiliza sauti yake kwa kusoma Biblia ndiyo mambo ambayo yamenisaidia kuvumilia.”

19. Namna gani tunapaswa kuona mikutano ya Kikristo?

19 Mikutano ni njia ingine ya maana ambayo Mungu anatumia ili kutupa ujasiri. Mutunga​-zaburi aliandika hivi: ‘Nafsi yangu imetamani sana na pia imezoofika kwa kutamani nyua za Yehova.’ (Zab. 84:2) Je, wewe pia unajisikia hivyo? Akieleza namna anavyoona mikutano, dada Lani tuliyezungumuzia, alisema hivi: “Kuhuzuria mikutano haikuwa jambo la kufanya tu wakati sikuwa na jambo lingine la kufanya. Nilijua kama nilipaswa kuwa kwenye mikutano ili Yehova anisaidie kupambana na matatizo yangu.”

20. Namna gani kazi ya kuhubiri inatusaidia?

20 Tunapata pia ujasiri tunapohubiri kwa bidii. (1 Tim. 4:16) Dada mumoja katika Australie ambaye amepambana na matatizo mengi anasema hivi: “Sikufurahia mahubiri, lakini muzee mumoja alinialika kuhubiri naye. Nilikubali. Yehova amenisaidia; kila mara ninapohubiri, ninajisikia mwenye furaha.” (Met. 16:20) Watu wengi wametambua kama wanapowasaidia wengine wawe na imani yenye nguvu, imani yao pia inatiwa nguvu. Kufanya hivyo kunawasaidia waache kufikiria sana matatizo yao na kukazia akilini mambo ya maana zaidi.​—Flp. 1:10, 11.

21. Tuna uhakika gani kuhusu matatizo tunayopambana nayo?

21 Yehova ametutolea njia nyingi ili kutusaidia tupambane na matatizo ya leo kwa ujasiri. Tukitumia vizuri njia hizo na kufikiria sana mifano mizuri ya watumishi wa Mungu walioonyesha ujasiri, tunaweza kupambana na matatizo bila kupoteza furaha yetu. Ijapokuwa matatizo mengine yanaweza kutokea kwa sababu tunakaribia mwisho, tunaweza kujisikia kama Paulo aliyesema hivi: “Tunaangushwa chini, lakini hatuangamizwi . . . hatufi moyo.” (2 Kor. 4:9, 16) Kwa musaada wa Yehova, tunaweza kupambana na matatizo ya leo kwa ujasiri.​—Soma 2 Wakorintho 4:17, 18.

[Maelezo ya chini]

^ Majina fulani yamebadilishwa.

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10, 11]

Unapopambana na matatizo, tumia musaada ambao Yehova ametutolea