Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Roho Ya Aina Gani Unayoonyesha?

Ni Roho Ya Aina Gani Unayoonyesha?

“Fadhili zisizostahiliwa za Bwana Yesu Kristo na ziwe pamoja na roho mnayoonyesha.”​—FLM. 25.

1. Paulo alitumaini nini alipowaandikia waamini wenzake?

ALIPOKUWA akiwaandikia waamini wenzake, mtume Paulo alisema tena na tena kwamba alitumaini kuwa Mungu na Kristo wangependezwa na roho ambayo makutaniko yalionyesha. Kwa mfano, aliwaandikia Wagalatia hivi: “Akina ndugu, fadhili zisizostahiliwa za Bwana wetu Yesu Kristo ziwe pamoja na roho ambayo mnaonyesha. Amina.” (Gal. 6:18) Alimaanisha nini aliposema “roho ambayo mnaonyesha”?

2, 3. (a) Nyakati nyingine Paulo alikuwa akirejelea nini alipotumia neno “roho”? (b) Ni maswali gani tunayoweza kujiuliza kuhusu roho tunayoonyesha?

2 Neno “roho” ambalo Paulo alitumia katika muktadha huo linarejelea nguvu inayotuchochea kusema au kufanya mambo kwa njia fulani. Huenda mtu akawa mwenye kujali, asiye mkali, mwenye tabia-pole, mkarimu, au mwenye kusamehe. Biblia inasema vizuri kuhusu “roho ya utulivu na ya upole” na pia inamsifu mtu mwenye “roho ya utulivu.” (1 Pet. 3:4; Met. 17:27) Kwa upande mwingine, huenda mtu mwingine akawa mwenye dhihaka, anayependa vitu vya kimwili, mwenye kukasirika upesi, au huenda akawa na roho ya kujitegemea. Na jambo baya hata zaidi ni kwamba kuna wale wanaoonyesha roho isiyo safi, roho ya kutotii, au hata roho ya uasi.

3 Kwa hiyo, Paulo alipotumia maneno kama vile “Bwana na awe pamoja na roho unayoonyesha,” alikuwa akiwatia ndugu zake moyo waonyeshe roho inayopatana na mapenzi ya Mungu na utu kama wa Kristo. (2 Tim. 4:22; soma Wakolosai 3:9-12.) Ni vizuri tujiulize hivi: ‘Ni roho ya aina gani ninayoonyesha? Ninawezaje kuonyesha kwa ukamili zaidi roho inayompendeza Mungu? Je, ninaweza kuboresha mtazamo wangu na hivyo kuchangia roho nzuri ya kutaniko?’ Kwa mfano, katika shamba la maua ya alizeti, uzuri wa kila ua unachangia umaridadi wa shamba lote la maua. Je, sisi ni mojawapo ya “maua” hayo yanayoongeza uzuri wa kutaniko? Bila shaka, tunapaswa kujitahidi kuwa mojawapo ya maua hayo. Acheni sasa tuone yale tunayoweza kufanya ili kuonyesha roho inayompendeza Mungu.

EPUKA ROHO YA ULIMWENGU

4. “Roho ya ulimwengu” ni nini?

4 Maandiko yanatuambia hivi: “Sisi tulipokea, si roho ya ulimwengu, bali roho inayotoka kwa Mungu.” (1 Kor. 2:12) “Roho ya ulimwengu” ni nini? Ni roho ileile inayotajwa katika andiko la Waefeso 2:2, linalosema hivi: “Wakati fulani mlitembea ndani yake kulingana na mfumo wa mambo wa ulimwengu huu, kulingana na mtawala wa mamlaka ya hewa, roho ambayo sasa hutenda katika wana wa kutotii.” “Hewa” hiyo ni roho ya ulimwengu, au mtazamo wa akili, na inatuzunguka pande zote kama hewa halisi. Roho hiyo iko kila mahali. Mara nyingi inaonyeshwa kupitia mtazamo ambao watu wengi wanao leo, mtazamo wa ‘Hakuna mtu yeyote anayepaswa kuniambia jambo la kufanya!’ au, ‘Unapaswa kupigania haki zako!’ Watu hao ni “wana wa kutotii” wa ulimwengu wa Shetani.

5. Ni roho gani mbaya ambayo baadhi ya watu walionyesha katika taifa la Israeli?

5 Mitazamo kama hiyo imekuwapo kwa muda mrefu. Wakati wa Musa, Kora aliinuka dhidi ya wale waliokuwa na mamlaka katika kutaniko la Israeli. Alimlenga hasa Haruni na wanawe, ambao walikuwa na pendeleo la kutumikia wakiwa makuhani. Huenda Kora aliona makosa yao ya kutokamilika. Au huenda alidai kwamba Musa aliwapendelea watu wake wa ukoo kwa kuwapa mapendeleo. Kwa vyovyote vile, ni wazi kwamba Kora alianza kuona mambo kwa maoni ya kibinadamu na kuwashutumu wale waliowekwa rasmi na Yehova, kwa kuwaambia hivi bila heshima: “Imetosha . . . Kwa nini, basi, mjiinue wenyewe juu ya kutaniko?” (Hes. 16:3) Vivyo hivyo, Dathani na Abiramu walilalamika dhidi ya Musa, kwa kumwambia kwamba alikuwa ‘akijaribu kujifanya mkuu juu yao kabisa.’ Walipoitwa waje mbele ya Musa, walijibu hivi kwa kiburi: “Sisi hatutakuja!” (Hes. 16:12-14) Ni wazi kwamba Yehova hakupendezwa na roho yao. Aliwaua waasi hao wote.​—Hes. 16:28-35.

6. Baadhi ya watu katika karne ya kwanza walionyeshaje kwamba walikuwa na mtazamo mbaya, na kwa nini huenda walionyesha mtazamo huo?

6 Baadhi ya watu katika karne ya kwanza walianza pia kuwachambua-chambua wale waliopewa mamlaka kutanikoni, na hivyo “kupuuza mamlaka.” (Yuda 8) Inaelekea wanaume hao hawakuridhika na mapendeleo yao na walijaribu kuwashawishi wengine dhidi ya wanaume waliowekwa rasmi ambao walikuwa wakitimiza kwa moyo wote majukumu waliyopewa na Mungu​.—Soma 3 Yohana 9, 10.

7. Kwa nini huenda tukahitaji kujihadhari kutanikoni leo?

7 Ni wazi kwamba roho kama hiyo haina nafasi katika kutaniko la Kikristo. Ndiyo sababu tunahitaji kujihadhari kuhusiana na jambo hilo. Wanaume wazee kutanikoni si wakamilifu, kama vile tu ambavyo wanaume wazee hawakuwa wakamilifu katika siku za Musa na katika siku za mtume Yohana. Huenda wazee wakafanya makosa ambayo yanatuathiri kibinafsi. Ikiwa hilo linatukia, halitakuwa jambo linalofaa kwa mshiriki yeyote wa kutaniko kutenda kupatana na roho ya ulimwengu, kwa kudai kwa hasira “haki” itendeke, au kusema “ndugu huyu anapaswa kuchukuliwa hatua”! Huenda Yehova akaamua kupuuza makosa fulani madogo-madogo. Je, tunaweza kufanya vivyo hivyo? Kwa sababu ya ule wanaouona kuwa udhaifu wa wazee, watu fulani ambao wanatenda dhambi nzito kutanikoni wamekataa kukutana na halmashauri ya wazee waliopewa mgawo wa kuwasaidia. Jambo hilo linaweza kulinganishwa na mgonjwa anayekataa matibabu kwa sababu hapendezwi na jambo fulani kumhusu daktari.

8. Ni maandiko gani yanayoweza kutusaidia kudumisha maoni yanayofaa kuhusu wale wanaoongoza kutanikoni?

8 Tunaweza kuepuka roho ya aina hiyo tukikumbuka kwamba katika Biblia, Yesu anaonyeshwa akiwa na ‘nyota saba katika mkono wake wa kuume.’ “Nyota” hizo zinafananisha waangalizi watiwa-mafuta, na kwa maana kubwa zaidi, waangalizi wote katika makutaniko. Yesu anaweza kuziongoza “nyota” hizo zilizo mkononi mwake katika njia yoyote ile anayoona kuwa inafaa. (Ufu. 1:16, 20) Kwa hiyo, akiwa Kichwa cha kutaniko la Kikristo, Yesu anayaongoza kikamili mabaraza ya wazee. Ikiwa kwa kweli mtu fulani katika baraza la wazee anahitaji kurekebishwa, Yule aliye na ‘macho kama mwali wa moto,’ atahakikisha kwamba hatua fulani imechukuliwa kwa wakati Wake na kwa njia Yake mwenyewe. (Ufu. 1:14) Kwa sasa, tunawaheshimu inavyofaa wale waliowekwa rasmi na roho takatifu, kwa kuwa Paulo aliandika hivi: “Watiini wale wanaoongoza katikati yenu na mnyenyekee, kwa maana wanaendelea kuzilinda nafsi zenu kama wale watakaotoa hesabu; ili wafanye hivyo kwa shangwe na si kwa kuugua, kwa maana kufanya hivyo kungewadhuru ninyi.”​—Ebr. 13:17.

9. (a) Ni jaribu gani ambalo Mkristo anaweza kupata akirekebishwa au kutiwa nidhamu? (b) Ni njia gani nzuri zaidi ya kuitikia karipio?

9 Roho ya Mkristo inaweza pia kujaribiwa akirekebishwa au kuachishwa mapendeleo kutanikoni. Ndugu mmoja kijana alishauriwa kwa busara na wazee kuhusu kucheza michezo ya video yenye jeuri. Inasikitisha kwamba hakukubali mashauri na hivyo ikawa lazima aachishwe kuwa mtumishi wa huduma kwa sababu alikuwa hatimizi tena sifa za kustahili za Kimaandiko. (Zab. 11:5; 1 Tim. 3:8-10) Baadaye, ndugu huyo alisambaza habari kwamba hakubaliani na uamuzi wa wazee, akaandikia ofisi ya tawi tena na tena barua za kuwachambua wazee na hata kuwashawishi wengine kutanikoni wafanye vivyo hivyo. Hata hivyo, hakuna faida ya kuhatarisha amani ya kutaniko zima tukijaribu kutetea matendo yetu. Ni jambo zuri zaidi kuliona karipio kuwa njia inayotufungua macho ili tuone udhaifu wetu ambao hatukujua na kisha kukubali kurekebishwa bila kulalamika.​Soma  Maombolezo 3:28, 29.

10. (a) Eleza jambo tunalojifunza kutokana na andiko la Yakobo 3:16-18 kuhusu roho nzuri na roho mbaya. (b) Kuonyesha “hekima inayotoka juu” kuna matokeo gani?

10 Andiko la Yakobo 3:16-18 ni mwongozo mzuri kuhusu roho inayopaswa kuonyeshwa na roho isiyopaswa kuonyeshwa kutanikoni. Linasema hivi: “Mahali ambapo pana wivu na ugomvi, hapo pana machafuko na kila jambo baya. Lakini hekima inayotoka juu kwanza kabisa ni safi kiadili, kisha yenye kufanya amani, yenye usawaziko, tayari kutii, yenye kujaa rehema na matunda mema, haifanyi tofauti zenye ubaguzi, si ya kinafiki. Zaidi ya hayo, mbegu ya tunda la uadilifu hupandwa chini ya hali zenye amani kwa wale wanaofanya amani.” Tunapojiendesha kupatana na “hekima inayotoka juu,” sifa zetu za Kikristo zitatuwezesha kuchangia roho nzuri miongoni mwa akina ndugu.

ONYESHA ROHO YA HESHIMA KUTANIKONI

11. (a) Kudumisha roho inayofaa kutatusaidia kuepuka nini? (b) Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Daudi?

11 Tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova amewapa wazee mgawo wa “kulichunga kutaniko la Mungu.” (Mdo. 20:28; 1 Pet. 5:2) Kwa hiyo, tunatambua kwamba ni jambo la hekima kuheshimu mpango wa Mungu, iwe tuna pendeleo la kutumikia tukiwa wazee au la. Kudumisha roho inayofaa kunaweza kutusaidia kuepuka kuhangaikia sana mapendeleo. Mfalme Sauli wa Israeli alipohisi kwamba Daudi alikuwa tishio kwa ufalme wake, Sauli “akawa akimtilia Daudi shaka tangu siku hiyo na kuendelea.” (1 Sam. 18:9) Mfalme huyo alisitawisha roho mbaya na hata alitaka kumuua Daudi. Badala ya kuhangaikia sana mapendeleo au mamlaka kama Sauli, ni vizuri zaidi kuwa kama Daudi. Licha ya matendo yote yasiyo ya haki aliyotendewa, kijana huyo aliendelea kumheshimu yule aliyepewa mamlaka na Mungu.​—Soma 1 Samweli 26:23.

12. Ni nini kitakachochangia umoja kutanikoni?

12 Kuwa na maoni yanayotofautiana kunaweza kuwa chanzo cha hasira kutanikoni, hata kati ya waangalizi. Mashauri haya ya Biblia yanaweza kutusaidia katika jambo hilo: “Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza” na, “Msiwe wenye busara machoni penu wenyewe.” (Rom. 12:10, 16) Badala ya kusisitiza kwamba maoni yetu ndiyo sahihi, tunapaswa kukubali kwamba mara nyingi kuna njia mbalimbali zinazofaa za kushughulikia mambo. Tukijitahidi kuelewa maoni ya wengine, tunaweza kuchangia umoja kutanikoni.​—Flp. 4:5.

13. Tunapaswa kuyaonaje maoni yetu, na ni mfano gani katika Biblia unaoonyesha hilo?

13 Je, hilo linamaanisha kwamba ni jambo lisilofaa kutoa maoni yetu ikiwa tunaona jambo fulani ambalo linahitaji kurekebishwa kutanikoni? La hasha. Katika karne ya kwanza, kulikuwa na jambo fulani lililosababisha ubishi mkubwa sana. Akina ndugu “wakapanga Paulo na Barnaba na wengine kati yao wapande kwenda kwa mitume na wanaume wazee katika Yerusalemu kuhusu bishano hilo.” (Mdo. 15:2) Bila shaka, kila mmoja wa akina ndugu hao alikuwa na maoni yake mwenyewe kuhusu jambo hilo na pia mawazo kuhusu jinsi ambavyo jambo hilo lingeweza kushughulikiwa. Hata hivyo, baada ya kila mmoja kueleza mawazo yake na uamuzi kufanywa kwa mwongozo wa roho takatifu, ndugu hao hawakuendelea kutoa maoni yao. Baada ya barua iliyokuwa na uamuzi huo kuyafikia makutaniko, akina ndugu “walishangilia juu ya kitia-moyo hicho” na “kufanywa imara katika imani.” (Mdo. 15:31; 16:4, 5) Vivyo hivyo leo, baada ya kuwajulisha ndugu wenye madaraka jambo fulani, tunapaswa kuridhika na kuwaachia walishughulikie kupitia sala.

ONYESHA ROHO NZURI KATIKA UHUSIANO WAKO PAMOJA NA WENGINE

14. Tunawezaje kuonyesha roho nzuri tunaposhughulika na wengine?

14 Katika uhusiano wetu pamoja na wengine, tuna fursa nyingi za kuonyesha roho nzuri. Kila mmoja wetu anaweza kuboresha sana hali ya kutaniko ikiwa ataonyesha roho ya kuwasamehe wengine wanapomkosea. Neno la Mungu linatuambia hivi: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia.” (Kol. 3:13) Maneno “ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika” yanaonyesha kwamba huenda kukawa na sababu halali za kuwakasirikia wengine. Hata hivyo, badala ya kuhangaishwa sana na udhaifu mdogo wa wengine na hivyo kuvuruga amani ya kutaniko, tunajitahidi kumwiga Yehova kwa kuwa tayari kusamehe kwa hiari, na kusonga mbele pamoja katika utumishi wetu.

15. (a) Tunaweza kujifunza nini kutokana na Ayubu kuhusu kusamehe? (b) Sala inaweza kutusaidiaje kuonyesha roho nzuri?

15 Tunaweza kujifunza kuhusu kusamehe kutokana na mwanamume Ayubu. Wanaume watatu waliopaswa kumfariji walimkasirisha kwa kusema maneno mengi yenye kuumiza. Hata hivyo, Ayubu aliwasamehe. Jinsi gani? “Aliposali kwa ajili ya wale rafiki zake.” (Ayu. 16:2; 42:10) Kusali kwa ajili ya wengine kunaweza kubadili mtazamo wetu kuwaelekea. Kusali kwa ajili ya Wakristo wenzetu wote kunatusaidia kusitawisha roho kama ya Kristo. (Yoh. 13:34, 35) Zaidi ya kusali kwa ajili ya ndugu zetu, tunapaswa kusali ili tupewe roho takatifu. (Luka 11:13) Roho ya Mungu itatusaidia kuonyesha sifa za kweli za Kikristo tunaposhughulika na wengine.​—Soma Wagalatia 5:22, 23.

CHANGIA ROHO NZURI KATIKA TENGENEZO LA MUNGU

16, 17. Kuhusu ‘roho tunayoonyesha,’ wewe binafsi umeazimia kufanya nini?

16 Matokeo yanaweza kuwa mazuri sana kila mshiriki wa kutaniko akiazimia kuchangia roho nzuri ya kutaniko. Baada ya kuchunguza mambo haya, huenda tukaamua kwamba sisi binafsi tunaweza kufanya maendeleo katika kuonyesha roho yenye kujenga. Ikiwa ndivyo, hatupaswi kusitasita kuruhusu Neno la Mungu lituchunguze. (Ebr. 4:12) Paulo, ambaye alikuwa mwangalifu sana kuhusu jinsi alivyojiendesha katika makutaniko, alisema hivi: “Sifahamu kitu chochote dhidi yangu mwenyewe. Lakini kwa hilo sionyeshwi kuwa mwadilifu, bali yeye anayenichunguza ni Yehova.”​—1 Kor. 4:4.

17 Tunapojitahidi kutenda kulingana na hekima inayotoka juu, badala ya kujiona au kuona pendeleo letu kuwa la maana sana, tutachangia roho nzuri kutanikoni. Tukiwa na roho ya kusamehe na kuwa na maoni mazuri kuwahusu wengine, tutafurahia uhusiano wenye amani pamoja na waamini wenzetu. (Flp. 4:8) Tukifanya mambo hayo, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova na Yesu watapendezwa na ‘roho tunayoonyesha.’​—Flm. 25.