Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Ni Roho ya Aina Gani Unayoonyesha?

Ni Roho ya Aina Gani Unayoonyesha?

Ni Roho ya Aina Gani Unayoonyesha?

‘Fazili zisizostahiliwa za Bwana Yesu Kristo na ziwe pamoja na roho munayoonyesha.’​—FLM. 25.

UNAWEZA KUJIBU?

Kwa nini tunapaswa kuchunguza ile roho tunayoonyesha?

Ni mawazo gani ambayo tunapaswa kuepuka, na tutayaepuka namna gani?

Tunaweza kufanya nini ili kuonyesha roho nzuri katika kutaniko?

1. Paulo alisema nini mara nyingi alipowaandikia waamini wenzake?

 ALIPOANDIKIA waamini wenzake, mutume Paulo alisema mara nyingi kama anatumaini kwamba Mungu na Yesu Kristo wangefurahia roho ambayo makutaniko yalionyesha. Kwa mufano, aliwaandikia Wagalatia hivi: ‘Fazili zisizostahiliwa za Bwana wetu Yesu Kristo ziwe pamoja na roho ambayo munaonyesha. Amina.’ (Gal. 6:18) Paulo alimaanisha nini aliposema ‘roho ambayo munaonyesha’?

2, 3. (a) Paulo alimaanisha nini alipotumia nyakati fulani neno “roho”? (b) Ni maulizo gani tunayopaswa kujiuliza kuhusu roho tunayoonyesha?

2 Paulo alitumia neno “roho” katika andiko hilo ili kuzungumuzia nguvu inayotusukuma kufanya ao kusema mambo kwa njia fulani. Mutu fulani anaweza kuwa mupole, mwenye adabu, mutulivu, mukarimu, ao mwenye kusamehe. Biblia inasema kama ni vizuri kuwa na “roho ya utulivu na ya upole.” (1 Pet. 3:4; Met. 17:27) Mutu mwengine anaweza kuwa na tabia ya kuwacheka wengine, mwenye kupenda sana vitu vya kimwili, mwenye kukasirika haraka, ao asiyetaka wengine wamuambie jambo la kufanya. Wengine hata wana mawazo machafu, ni wasiotii, na waasi.

3 Kwa hiyo, Paulo alitumia maneno kama vile “Bwana na awe pamoja na roho unayoonyesha,” ili kuwatia moyo ndugu zake waonyeshe roho inayopatana na mapenzi ya Mungu na ile iliyo kama ya Kristo. (2 Tim. 4:22; soma Wakolosai 3:9-12.) Leo, kila mumoja wetu anapaswa kujiuliza hivi: ‘Ni roho ya aina gani ninayoonyesha? Namna gani ninaweza kuonyesha vizuri zaidi roho inayomupendeza Mungu? Je, ninapaswa kufanya mabadiliko ili kuendeleza roho nzuri katika kutaniko?’ Fikiria mufano huu. Kila liua katika shamba la maua linafanya shamba lote liwe na uzuri. Je, sisi ni moja ya “maua” yanayofanya kutaniko lote liwe na uzuri? Bila shaka, tunapaswa kujikaza ili kuwa moja ya maua hayo. Acheni tuzungumuzie mambo tunayoweza kufanya ili kuonyesha roho inayomupendeza Mungu.

EPUKA ROHO YA ULIMWENGU

4. “Roho ya ulimwengu” ni nini?

4 Biblia inatuambia hivi: “sisi tulipokea, si roho ya ulimwengu, bali roho inayotoka kwa Mungu.” (1 Kor. 2:12) “Roho ya ulimwengu” ni nini? Ni ile roho inayozungumuziwa tena katika andiko la Waefeso 2:2, linalosema hivi: ‘Wakati fulani mulitembea ndani yake kulingana na mufumo wa mambo wa ulimwengu huu, kulingana na mutawala wa mamlaka ya hewa, roho ambayo sasa hutenda katika wana wa kutotii.’ Ile “hewa” ndiyo roho ya ulimwengu, ao namna ya kufikiri ya watu wa ulimwengu, na inatuzunguka kama vile hewa tunayopumua. Inapatikana mahali pote. Watu wengi wanaonyesha roho hiyo wanaposema maneno kama vile: “Niko huru kufanya mambo ninayotaka” ao “Unapaswa kupigania haki yako.” Watu wanaofikiri hivyo ni “wana wa kutotii” wa ulimwengu wa Shetani.

5. Watu fulani katika Israeli walionyesha roho gani?

5 Namna hiyo ya kufikiri haikuanza leo. Wakati wa Musa, Kora alianza kupinga wale waliokuwa na mamlaka katika taifa la Israeli. Kora alipinga zaidi sana mamlaka ya Haruni na wana wake waliokuwa makuhani. Labda kwa sababu alijua uzaifu wao mbalimbali. Ao alifikiri kama Musa alikuwa anawapendelea tu watu wa jamaa yake kwa kuwatolea wao tu mapendeleo mbalimbali. Kwa vyovyote, Kora alianza kuwa na maoni yasiyofaa na aliwachambua wale waliopewa mamlaka na Yehova; aliwaambia hivi bila heshima: ‘Imetosha. Kwa nini, basi, mujiinue wenyewe juu ya kutaniko la Yehova?’ (Hes. 16:3) Vilevile, Dathani na Abiramu walimunungunikia Musa, na kumuambia kwamba ‘alijaribu kujifanya mukubwa juu yao kabisa.’ Musa alipotuma watu wawaite, walijibu hivi kwa majivuno: “Sisi hatutakuja!” (Hes. 16:12-14) Bila shaka Yehova hakufurahia roho walioonyesha. Kwa hiyo aliangamiza waasi wote hao.​—Hes. 16:28-35.

6. Namna gani watu fulani walionyesha maoni mabaya wakati wa mitume, na labda walifanya hivyo sababu gani?

6 Watu fulani wakati wa mitume walianza, “kupuuza mamlaka” kwa kuwachambua wale waliokuwa na mamlaka katika kutaniko. (Yuda 8) Labda watu hao hawakutosheka na mapendeleo yao katika kutaniko na walitaka kuwashawishi wengine ili wasiwaheshimu wanaume waliochaguliwa na Mungu waliokuwa wakitimiza migawo yao vizuri.​—Soma 3 Yohana 9, 10.

7. Sababu gani tunapaswa kufanya angalisho katika kutaniko leo?

7 Hatupaswe kuonyesha roho ya namna hiyo katika kutaniko la Kikristo. Kwa hiyo tufanye angalisho. Wazee katika makutaniko ni watu wasio wakamilifu, kama vile wale waliokuwa na mamlaka wakati wa Musa na wakati wa mutume Yohana. Makosa ya wazee yanaweza kutuvunja moyo. Ikiwa jambo hilo linatokea, haingefaa mushiriki wa kutaniko aonyeshe roho ya ulimwengu, kwa kusisitiza wazee wengine watende kwa “haki” ao kuwaomba “wamukaripie muzee huyo!” Yehova anaweza kuvumilia makosa fulani madogo madogo. Je, hatuweze kumuiga? Kisha kufanya zambi nzito, watu fulani wanapoalikwa na halmashauri ya hukumu ili wasaidiwe, wanakataa kwa sababu wanajua uzaifu mbalimbali wa wazee walio katika halmashauri hiyo. Wale wanaofanya hivyo wanafanana na mugonjwa anayekataa kutunzwa na muganga fulani kwa sababu hafurahie tabia fulani ya muganga huyo.

8. Ni maandiko gani yanayoweza kutusaidia tuwe na maoni yanayofaa kuhusu wale wanaotuongoza katika kutaniko?

8 Ili kuepuka roho hiyo, tunapaswa kukumbuka kama Biblia inazungumuzia Yesu akiwa na ‘nyota saba’ katika mukono wake wa kuume. “Nyota” hizo zinafananisha wazee watiwa​-mafuta kutia ndani wazee wengine wote katika makutaniko. Yesu anaweza kuongoza “nyota” zilizo katika mukono wake kadiri anavyopenda. (Ufu. 1:16, 20) Kwa hiyo, Yesu Kristo, aliye Kichwa cha kutaniko, anaongoza mabaraza yote ya wazee. Ikiwa muzee fulani anahitaji kukaripiwa, Yule aliye na “macho kama mwali wa moto” atashugulikia jambo hilo kwa wakati na kwa namna inayofaa. (Ufu. 1:14) Tunapongojea jambo hilo lishugulikiwe, tuendelee kuwaheshimu kabisa wale waliowekwa na roho takatifu kwa sababu Paulo aliandika hivi: ‘Watiini wale wanaoongoza katikati yenu na munyenyekee, kwa maana wanaendelea kuzilinda nafsi zenu kama wale watakaotoa hesabu; ili wafanye hivyo kwa shangwe na si kwa kuugua, kwa maana kufanya hivyo kungewazuru ninyi.’​—Ebr. 13:17.

9. (a) Mutu anaweza kuitikia namna gani anaposhauriwa ao kukaripiwa? (b) Ni jambo la hekima kufanya nini tunapokaripiwa?

9 Wazee wanapomushauria ndugu fulani ao kumuondoa madaraka, anaweza kuitikia inavyofaa ao kupinga uamuzi huo. Katika kutaniko moja, wazee walimushauri kwa busara ndugu mumoja kijana kuhusu michezo ya video yenye jeuri. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba, kijana huyo, aliyekuwa mutumishi wa huduma, hakutii shauri hilo; kwa hiyo alipoteza madaraka yake kwa sababu hakutimiza tena matakwa ya Maandiko. (Zab. 11:5; 1 Tim. 3:8-10) Baadaye, ndugu huyo alianza kuwajulisha ndugu na dada waziwazi kama hakubali uamuzi huo, mara nyingi aliandikia biro ya tawi barua za kuchambua wazee hao na aliwashawishi wengine katika kutaniko wafanye hivyo pia. Lakini, kuvuruga amani ya kutaniko lote ili tu kutafuta kutetea matendo yetu hakuwezi kubadili jambo lolote. Ni jambo la hekima kutambua kama karipio linatusaidia kuona uzaifu ambao hatukujua; kwa hiyo basi tukubali karipio kwa utulivu.​—Soma Maombolezo 3:28, 29.

10. (a) Andiko la Yakobo 3:16-18 linatufundisha nini kuhusu roho nzuri na roho isiyofaa? (b) Tutapata faida gani ikiwa tunaonyesha “hekima inayotoka juu”?

10 Andiko la Yakobo 3:16-18 linaonyesha roho isiyofaa tunayopaswa kuepuka na roho nzuri tunayopaswa kuonyesha katika kutaniko. Andiko hilo linasema hivi: “Kwa maana mahali ambapo pana wivu na ugomvi, hapo pana machafuko na kila jambo baya. Lakini hekima inayotoka juu kwanza kabisa ni safi kiadili, kisha yenye kufanya amani, yenye usawaziko, tayari kutii, yenye kujaa rehema na matunda mema, haifanyi tofauti zenye ubaguzi, si ya kinafiki. Zaidi ya hayo, mbegu ya tunda la uadilifu hupandwa chini ya hali zenye amani kwa wale wanaofanya amani.” Ikiwa tunaonyesha “hekima inayotoka juu,” sifa za Kikristo zitatusaidia kuendeleza roho nzuri katika kutaniko na kuishi kwa amani pamoja na ndugu zetu.

ONYESHA HESHIMA KATIKA KUTANIKO

11. (a) Kuwa na maoni yanayofaa kuhusu mamlaka kutatusaidia tusifanye nini? (b)  Mufano wa Daudi unatufundisha nini?

11 Tunapaswa kukumbuka kama Yehova amewapatia wazee kazi ya “kulichunga kutaniko la Mungu.” (Mdo. 20:28; 1 Pet. 5:2) Kwa hiyo, iwe sisi ni wazee ao hapana, ni jambo la hekima kuheshimu mupango wa Mungu. Kuwa na maoni yanayofaa kuhusu mamlaka kutatusaidia tusitamani kupita kiasi madaraka ao mapendeleo katika kutaniko. Mufalme Sauli wa Israeli alipojua kama Daudi anaweza kuwa mufalme pa nafasi yake, yeye alianza ‘kumutilia Daudi shaka tangu siku hiyo na kuendelea.’ (1 Sam. 18:9) Mufalme alionyesha roho mbaya na alitaka hata kumuua Daudi. Kuliko kutamani mamlaka kupita kiasi kama Sauli, ni vizuri tuige mufano muzuri wa Daudi. Ijapokuwa alitendewa isivyo haki, kijana Daudi aliendelea kuheshimu wale waliopewa mamlaka na Mungu.​—Soma 1 Samweli 26:23.

12. Tunapaswa kufanya nini ili kuendeleza umoja katika kutaniko?

12 Ndugu na dada wanaweza kuwa na maoni tofauti kuhusu jambo fulani na hilo linaweza kutokeza hasira, hata kati ya wazee wa kutaniko. Kuhusiana na hali hiyo, Biblia inatushauri hivi: “Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza” na ‘musiwe wenye busara machoni penu wenyewe.’ (Rom. 12:10, 16) Kuliko kusisitiza kama maoni yetu ndiyo ya kweli, tunapaswa kujua kwamba jambo moja linaweza kushugulikiwa vizuri kwa njia nyingi. Ikiwa tunaheshimu maoni ya wengine, tutaendeleza umoja katika kutaniko.​—Flp. 4:5.

13. Je, ni vibaya kutoa maoni yetu kuhusu mambo fulani yasiyoendeka katika kutaniko, na ni mufano gani wa Biblia unaotusaidia?

13 Si vibaya kutoa maoni yetu ikiwa tunatambua kama mambo fulani hayaendeki katika kutaniko. Katika siku za mitume, kulitokea jambo moja lililotokeza ubishi sana kati ya ndugu. Ndugu ‘walipanga Paulo na Barnaba na wengine kati yao wapande kwenda kwa mitume na wanaume wazee katika Yerusalemu kuhusu bishano hilo.’ (Mdo. 15:2) Bila shaka kila mumoja wa ndugu hao alikuwa na maoni yake kuhusu jambo hilo na alijua namna ya kutatua tatizo hilo. Lakini, kisha kila mutu kueleza maoni yake na uamuzi ulioongozwa na roho takatifu ulipochukuliwa, ndugu hawakundelea tena kubishana, wote waliheshimu uamuzi huo. Kisha kupokea barua katika makutaniko kuhusu uamuzi uliochukuliwa, ndugu “walishangilia juu ya kitia-moyo hicho” na makutaniko ‘yalifanywa imara katika imani.’ (Mdo. 15:31; 16:4, 5) Leo pia, tukisha kuwajulisha wazee mambo fulani yasiyoendeka katika kutaniko, tunapaswa kuamini kwamba watayafikiria kwa uzito.

ONYESHA ROHO NZURI KATIKA UHUSIANO WAKO NA WENGINE

14. Namna gani kila mumoja wetu anaweza kuonyesha roho nzuri katika kutaniko?

14 Kila mumoja wetu ana nafasi nyingi za kuonyesha roho nzuri katika kutaniko. Tunaweza kuendeleza roho nzuri katika kutaniko kwa kuwasamehe wengine wanapotukosea. Neno la Mungu linatuambia hivi: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia.” (Kol. 3:13) Maneno “ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika” yanaonyesha kama tunaweza kuwa na sababu nzuri za kukasikirikia wengine. Hata hivyo, kuliko kuona tu uzaifu wao na kuvuruga amani ya kutaniko, tunapaswa kumuiga Yehova na kuwa tayari kuwasamehe wengine, na kuendelea kufanya kazi ya Mungu pamoja nao.

15. (a) Ayubu anatuwekea mufano gani kuhusu kuwasamehe wengine? (b) Namna gani sala inaweza kutusaidia kuonyesha roho nzuri?

15 Ayubu alituachia mufano muzuri wa kuwasamehe wengine. Wanaume watatu waliodai kwamba walikuja kumufariji walitumia maneno makali ya kumuvunja moyo. Hata hivyo, Ayubu aliwasamehe. Namna gani? ‘Alisali kwa ajili ya rafiki zake.’ (Ayu. 16:2; 42:10) Kusali kwa ajili ya wengine kunaweza kutusaidia kuwa na maoni mazuri kuwahusu. Kusali kwa ajili ya Wakristo wenzetu kunaweza kutusaidia kuwa na roho kama ya Kristo. (Yoh. 13:34, 35) Zaidi ya kusali kwa ajili ya ndugu zetu, tunapaswa kuomba Mungu atupatie roho takatifu. (Lu. 11:13) Roho ya Mungu itatusaidia kuonyesha sifa za Kikristo katika uhusiano wetu na wengine.​—Soma Wagalatia 5:22, 23.

ENDELEA KUONYESHA ROHO NZURI KATIKA KUTANIKO

16, 17. Unaazimia kufanya nini kuhusiana na ‘roho’ ambayo tumezungumuzia?

16 Bila shaka kila mumoja wetu akijiwekea muradi wa kuonyesha roho nzuri katika kutaniko, hilo litakuwa na matokeo mazuri sana! Kisha funzo hili, labda umetambua kama unapaswa kufanya mabadiliko fulani ili kuonyesha roho nzuri katika kutaniko. Ikiwa ni hivyo, basi usisite kujichunguza kupitia Neno la Mungu. (Ebr. 4:12) Mutume Paulo, aliyekuwa anachunguza sana matendo yake katika kutaniko, alisema hivi: ‘Sifahamu kitu chochote zidi yangu mwenyewe. Lakini kwa hilo sionyeshwi kuwa mwadilifu, bali yeye anayenichunguza ni Yehova.’​—1 Kor. 4:4.

17 Tujikaze basi kutenda kulingana na hekima ya Mungu, tuepuke kujiona kuwa watu wa maana kupita kiasi ao kuona madaraka yetu kuwa ya maana kupita kiasi, hilo litafanya kuwe na roho nzuri katika kutaniko. Tukiwasamehe wengine na kuwa na maoni yanayofaa kuwahusu, tutafurahia uhusiano wenye amani pamoja na waabudu wenzetu. (Flp. 4:8) Tukifanya yote hayo, tunaweza kuwa hakika kama Yehova na Yesu Kristo watafurahia ‘roho tunayoonyesha.’​—Flm. 25.

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 14]

Namna gani kufikiri sana juu ya daraka la Yesu kunaweza kukusaidia kukubali mashauri?