Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Simulizi la Maisha

Wamekuwa Marafiki kwa Miaka 60 na Ni Kama Urafiki wao Umeanza Tu

Wamekuwa Marafiki kwa Miaka 60 na Ni Kama Urafiki wao Umeanza Tu

Jioni moja katika majira ya kiangazi mnamo mwaka wa 1951, wanaume wanne vijana, wote wakiwa na umri wa miaka 20 hivi, walisimama katika vibanda vya simu vilivyokaribiana huko Ithaca, New York, Marekani, na kupiga simu kwa msisimko Michigan, Iowa, na California. Walikuwa na habari nzuri za kuwajulisha wengine!

MWEZI wa Februari, mapainia 122 walifika South Lansing, New York, ili kuhudhuria darasa la 17 la Shule ya Gileadi. Lowell Turner, William (Bill) Kasten, Richard Kelsey, na Ramon Templeton walikuwa kati ya mapainia hao ambao wangekuwa wamishonari. Lowell na Bill walitoka Michigan, Richard alitoka Iowa na Ramon alitoka California. Punde si punde, vijana hao wakawa marafiki.

Miezi mitano hivi baadaye, kulikuwa na msisimko mkubwa ilipotangazwa kwamba Ndugu Nathan Knorr kutoka katika makao makuu ya ulimwenguni pote angekuja kuzungumza na wanafunzi. Ndugu hao wanne walimweleza tamaa yao ya kutumika pamoja katika nchi moja, ikiwezekana. Je, sasa wangepata habari zaidi kuhusu migawo yao ya umishonari? Bila shaka!

Msisimko wao uliongezeka wakati Ndugu Knorr alipoanza kutangaza darasani migawo ya wanafunzi wote. Wale vijana wanne wenye wasiwasi ndio walioitwa kwanza jukwaani, lakini walifurahi sana walipojua kwamba wangetumika pamoja! Wangetumikia wapi? Wanafunzi wenzao walishangaa na kupiga makofi mfululizo kwa msisimko Ndugu Knorr alipotangaza kwamba wangetumwa Ujerumani.

Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote waliguswa moyo sana na uaminifu ambao Mashahidi wenzao walionyesha nchini Ujerumani chini ya utawala wa Hitler, kuanzia mwaka wa 1933 na kuendelea. Wanafunzi wengi walikumbuka jinsi walivyotayarisha nguo na mafurushi ya misaada kwa ajili ya ndugu zao wa Ulaya baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu. Watu wa Mungu nchini Ujerumani walikuwa mifano mizuri sana katika kuonyesha imani, ujasiri, kuwa thabiti, na kumtegemea Yehova. Lowell anakumbuka akiwaza hivi: ‘Sasa kwa kweli tutawajua kibinafsi ndugu na dada hao wapendwa.’ Ndiyo sababu wanafunzi wote walisisimka sana na kupiga simu jioni hiyo!

WAELEKEA UJERUMANI

Mnamo Julai 27, 1951, meli ya SS Homeland iling’oa nanga kutoka katika bandari ya East River, huko New York, na marafiki hao wanne wakaanza safari yao ya siku 11 baharini kwenda Ujerumani. Ndugu Albert Schroeder, mmoja wa walimu wao wa Gileadi ambaye baadaye alikuja kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alikuwa amewafundisha maneno machache ya Kijerumani. Sasa, huenda wangejifunza maneno zaidi kutoka kwa wasafiri wenzao Wajerumani waliokuwa melini. Lakini wasafiri hao walikuwa wakizungumza lahaja mbalimbali za Kijerumani. Ilikuwa hali yenye kutatanisha kama nini!

Baada ya kutatizwa sana na kichefuchefu katika safari hiyo ya baharini, hatimaye ndugu hao walifika Hamburg, Ujerumani, siku ya Jumanne asubuhi, Agosti 7. Kila mahali, waliona madhara ya vita ambavyo vilikwisha miaka sita tu iliyotangulia. Wakiwa wamehuzunishwa na mambo waliyoona, walisafiri usiku kwa gari-moshi hadi Wiesbaden, ambako ofisi ya tawi ilikuwa wakati huo.

Mapema Jumatano asubuhi, walikutana na Shahidi kwa mara ya kwanza kabisa nchini Ujerumani, naye alikuwa na jina la Kijerumani! Shahidi huyo aliyeitwa Hans aliwachukua katika kituo cha magari-moshi na kuwapeleka Betheli, na akawaacha mikononi mwa dada mkali aliyezeeka asiyejua Kiingereza. Hata hivyo, inaonekana kwamba dada huyo alifikiri kwamba angeweza kutatua tatizo la kutoelewana lugha kwa kuzungumza kwa sauti ya juu zaidi. Lakini kadiri alivyozungumza kwa sauti ya juu zaidi, ndivyo yeye pamoja na ndugu hao wanne walivyozidi kuchanganyikiwa. Hatimaye Ndugu Erich Frost, mtumishi wa tawi, akaja na kuwasalimu kwa uchangamfu kwa lugha ya Kiingereza. Mambo yalianza kuboreka.

Kuelekea mwishoni mwa Agosti, ndugu hao wanne walihudhuria kusanyiko lao la kwanza la Kijerumani, lenye kichwa “Ibada Safi” huko Frankfurt am Main. Ndugu hao walipoona kilele cha wahudhuriaji 47,432 na watu 2,373 wakibatizwa kwenye kusanyiko hilo, walichochewa tena kuwa na bidii katika kazi ya umishonari na wakawa na tamaa zaidi ya kuhubiri. Lakini baada ya siku chache, Ndugu Knorr aliwaambia kwamba wangekaa na kufanya kazi Betheli.

Shangwe nyingi waliyopata katika mgawo wao iliwasadikisha kwamba sikuzote Yehova anajua jambo linalotufaa zaidi

Wakati fulani Ramon alikataa mgawo wa kufanya kazi katika Betheli ya Marekani kwa sababu alipenda sana kazi ya umishonari. Richard na Bill hawakufikiria kamwe utumishi wa Betheli. Lakini shangwe waliyopata katika mgawo wao wa Betheli iliwasadikisha kwamba sikuzote Yehova anajua jambo linalotufaa zaidi. Basi ni jambo la hekima kama nini kutegemea mwongozo wake badala ya kutegemea tamaa zetu za kibinafsi! Yule ambaye amejifunza somo hilo atafurahia kumtumikia Yehova mahali popote na katika mgawo wowote anaopewa.

VERBOTEN!

Washiriki wengi wa familia ya Betheli ya Ujerumani walifurahia kuishi na Wamarekani ambao wangewafundisha kuongea Kiingereza. Lakini siku moja katika chumba cha kulia chakula, matumaini hayo yalikatizwa kwa ghafla. Ndugu Frost, akiwa mwenye shauku kama kawaida, alianza kusema jambo fulani katika Kijerumani lililoonekana kuwa zito sana. Wengi katika familia walikaa kimya kabisa, huku wakitazama tu sahani zao. Ingawa Wanabetheli hao wapya hawangeweza kuelewa jambo lililokuwa likisemwa, pole kwa pole walianza kutambua kwamba liliwahusu. Kwa hiyo, Ndugu Frost aliposema kwa mshindo, “VERBOTEN!” (“Marufuku!”) na kukazia neno hilo tena na tena kwa sauti kubwa zaidi, ndugu hao waliogopa. Ni nini walichofanya kilichomkasirisha sana?

Baada ya chakula, watu wote walienda haraka katika vyumba vyao. Baadaye, ndugu mmoja alitueleza hivi: “Ili mweze kutusaidia, ni lazima mjue kuongea Kijerumani. Ndiyo sababu Ndugu Frost alisema kwamba kuzungumza nanyi Kiingereza ni VERBOTEN (marufuku) hadi mtakapojua Kijerumani.”

Familia ya Betheli ilitii agizo hilo mara moja. Shauri hilo halikuwasaidia tu Wanabetheli hao wapya kujifunza Kijerumani bali pia liliwafundisha kwamba shauri linalotolewa na ndugu mwenye upendo, mara nyingi linatufaidi hata ingawa mwanzoni ni vigumu kulifuata. Shauri la Ndugu Frost lilionyesha kwamba anapendezwa na hali nzuri ya tengenezo la Yehova naye anawapenda ndugu zake. * Si ajabu kwamba ndugu hao wanne walimpenda sana!

KUJIFUNZA KUTOKANA NA MARAFIKI WETU

Tunaweza kujifunza mambo muhimu kutokana na marafiki wanaomwogopa Mungu. Na mambo hayo yanaweza kutusaidia kuwa marafiki wazuri zaidi wa Yehova. Marafiki hao wanne walijifunza mengi kutokana na ndugu na dada wengi waaminifu Wajerumani tusioweza kuwataja wote kwa majina, na walijifunza pia mengi kutokana na urafiki wao. Richard anaeleza hivi: “Lowell alijua Kijerumani kidogo naye alikitumia vizuri, lakini haikuwa rahisi kwetu sisi watatu kuzungumza lugha hiyo. Kwa kuwa Lowell ndiye aliyekuwa na umri mkubwa kati yetu, tulimtegemea ili atufundishe lugha na kutuongoza.” Ramon anakumbuka hivi: “Nilisisimka kama nini ndugu mmoja Mswisi alipoturuhusu tukae katika nyumba yake ndogo huko Uswisi tulipochukua likizo yetu ya kwanza baada ya kukaa Ujerumani kwa mwaka mmoja! Nilifikiri kwamba tungekaa majuma mawili peke yetu bila kupambana na Kijerumani! Lakini sikujua maoni ya Lowell. Alisisitiza kwamba tusome na kuzungumzia andiko la siku kila asubuhi​—kwa lugha ya Kijerumani! Sikufurahi hata kidogo, lakini hakuyumba-yumba. Hata hivyo, tulijifunza somo muhimu. Fuata mwongozo wa wale ambao wanajali kwa unyoofu hali yako njema, hata ikiwa nyakati nyingine hukubaliani nao. Mtazamo huo umetufaidi sana kwa miaka mingi na umefanya iwe rahisi zaidi kwetu kufuata mwongozo wa kitheokrasi.”

Marafiki hao wanne wamejifunza pia kuthamini sifa nzuri za wengine, kama andiko la Wafilipi 2:3 linavyosema: “Kwa unyenyekevu wa akili [waoneni] wengine kuwa ni bora kuliko ninyi.” Kwa hiyo, mara nyingi Bill aliheshimiwa na wenzake kwa kupewa kazi ambazo watatu hao walikubaliana kwamba angeweza kushughulikia vizuri kuliko wao. Lowell anakumbuka hivi: “Tulipohitaji kufanya uamuzi mzito au usiopendeza ili kutatua matatizo mazito, tulimwomba Bill atusaidie. Alikuwa na kipawa cha kushughulikia hali ngumu kwa njia ambayo tulikubaliana, jambo ambalo sisi hatukuwa na ujasiri au uwezo wa kufanya.”

NDOA ZENYE FURAHA

Mmoja baada ya mwingine, kila mmoja wa marafiki hao wanne aliamua kuoa. Urafiki wao ulitegemea kumpenda Yehova na huduma ya wakati wote, kwa hiyo, waliazimia kutafuta wenzi wa ndoa walio tayari kumtanguliza Yehova maishani. Utumishi wa wakati wote uliwafundisha kwamba kuna thawabu zaidi katika kutoa kuliko katika kupokea na kwamba mapendezi ya kibinafsi hayapaswi kamwe kutangulizwa badala ya mambo ya Ufalme. Kwa hiyo, waliwachagua akina dada ambao tayari walikuwa katika utumishi wa wakati wote kwa sababu ya uamuzi wao wa kibinafsi. Matokeo ni kwamba marafiki hao wanne walikuwa na ndoa imara zenye furaha.

Ili urafiki au ndoa idumu kikweli, ni lazima Yehova awe katika uhusiano huo. (Mhu. 4:12) Hata ingawa baadaye Bill na Ramon walipoteza wenzi wao katika kifo, wote wawili walikuwa wamepata shangwe na utegemezo ambao mke mwaminifu anaweza kutoa. Lowell na Richard wanaendelea kufurahia utegemezo huo, naye Bill, aliyeoa tena, alimchagua mwenzi wa ndoa kwa hekima ili aendelee na utumishi wa wakati wote.

Katika miaka ya baadaye, walipewa migawo katika nchi mbalimbali, hasa Ujerumani, Austria, Luxembourg, Kanada, na Marekani. Kwa hiyo, marafiki hao wanne hawakuweza kuendelea kukaa pamoja kama ambavyo wangependa. Lakini ingawa waliishi katika maeneo yaliyo mbalimbali, waliendelea kuwasiliana na kushangilia pamoja baraka walizopata na hata kulia pamoja wakati wa huzuni. (Rom. 12:15) Marafiki wa aina hiyo wanapaswa kuthaminiwa sana na hawapaswi kamwe kupuuzwa. Wao ni zawadi zenye thamani kutoka kwa Yehova. (Met. 17:17) Ni vigumu kama nini kupata marafiki wa kweli katika ulimwengu wa leo! Lakini kila Mkristo wa kweli anaweza kupata marafiki wengi sana wazuri. Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tunafurahia urafiki wetu pamoja na waamini wenzetu ulimwenguni pote, na zaidi ya yote, tunafurahia urafiki pamoja na Yehova Mungu na Yesu Kristo.

Kama ilivyo kwetu sote, nyakati nyingine marafiki hao wanne walikabili matatizo, iwe ni uchungu wa kumpoteza mwenzi wa ndoa katika kifo, mkazo unaosababishwa na ugonjwa mbaya, mahangaiko ya kuwatunza wazazi waliozeeka, matatizo ya kumlea mtoto ukiwa katika utumishi wa wakati wote, wasiwasi tunaohisi tunapokubali migawo mipya ya kitheokrasi, na kwa sasa matatizo yanayoongezeka ya uzeeni. Lakini wanajua pia kutokana na mambo waliyojionea kwamba marafiki, walio karibu na wale walio mbali, wanawasaidia watu wanaompenda Yehova kuvumilia kila tatizo kwa mafanikio.

URAFIKI UTAKAODUMU MILELE

Ni vizuri kama nini kwamba Lowell, Ramon, Bill, na Richard walijiweka wenyewe wakfu kwa Yehova wakiwa na umri wa miaka 18, 12, 11, na 10, na wote wakaingia katika utumishi wa wakati wote wakiwa na umri wa kati ya miaka 17 na 21. Walifanya kama andiko la Mhubiri 12:1 lilivyowahimiza wafanye: “Mkumbuke, sasa, Muumba wako Mkuu katika siku za ujana wako.”

Ikiwa wewe ni kijana Mkristo mwanamume, kubali mwaliko wa Yehova wa kuingia katika utumishi wa wakati wote ikiwezekana. Kisha kwa sababu ya fadhili zisizostahiliwa za Yehova, huenda utapata shangwe nyingi kama marafiki hao wanne, ya kutumikia ukiwa mwangalizi wa mzunguko, wa wilaya, au wa eneo la dunia; utapata shangwe ya kutumika Betheli, na hata katika Halmashauri za Tawi; shangwe ya kufundisha shule za Huduma ya Ufalme na shule za Utumishi wa Painia; na shangwe ya kutoa hotuba katika makusanyiko madogo na makubwa. Marafiki hao wanne walifurahi kama nini kujua kwamba utendaji wao ulifaidi maelfu ya watu! Waliweza kutimiza yote hayo kwa sababu wakiwa vijana, walikubali mwaliko wenye upendo wa Yehova wa kumtumikia kwa nafsi yote.​—Kol. 3:23.

Sasa, Lowell, Richard, na Ramon wanatumikia pamoja tena katika ofisi ya tawi ya Selters, Ujerumani. Inahuzunisha kwamba Bill alikufa mwaka wa 2010 akiwa painia wa pekee nchini Marekani. Urafiki wa pekee sana uliodumu kwa miaka karibu 60 kati ya ndugu hao wanne ulikatishwa na kifo! Lakini Mungu wetu, Yehova, hawasahau kamwe marafiki wake. Tunaweza kuwa na hakika kwamba chini ya utawala wa Ufalme, kila urafiki wa Kikristo uliokatishwa kwa muda na kifo utarudishwa.

“Katika miaka yote 60 ya urafiki wetu, sikumbuki kamwe tukiwa na pindi yoyote isiyofurahisha”

Muda mfupi kabla ya kufa, Bill aliandika hivi: “Sikumbuki kamwe pindi yoyote isiyofurahisha katika miaka yote 60 ya urafiki wetu. Sikuzote urafiki wetu umekuwa wa pekee sana kwangu.” Wakiwa wameazimia kuendelea na urafiki wao katika ulimwengu mpya, marafiki wenzake watatu wanaongezea hivi: “Na ni kama urafiki wetu umeanza tu.”

^ fu. 17 Simulizi lenye kusisimua la maisha ya Ndugu Frost lilichapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Kiingereza la Aprili 15, 1961, ukurasa wa 244-249.