Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yesu Aliweka Kielelezo Cha Unyenyekevu

Yesu Aliweka Kielelezo Cha Unyenyekevu

Yesu Aliweka Kielelezo Cha Unyenyekevu

“Niliweka kielelezo kwa ajili yenu, ili, kama vile nilivyowafanyia ninyi, ninyi pia mfanye hivyo.”​—YOH. 13:15.

UNGEJIBUJE?

Mwana wa Mungu alionyeshaje unyenyekevu kabla hajawa mwanadamu?

Akiwa mwanadamu, Yesu alionyeshaje unyenyekevu?

Maisha ya Yesu ya unyenyekevu yameleta manufaa gani?

1, 2. Ni somo gani muhimu ambalo Yesu aliwafundisha mitume wake usiku wa mwisho wa maisha yake duniani?

NI USIKU wa mwisho wa maisha ya Yesu duniani, naye yuko pamoja na mitume wake katika chumba cha juu katika nyumba fulani huko Yerusalemu. Wakati wa mlo wa jioni, Yesu anasimama na kuyaweka kando mavazi yake ya nje. Anachukua kitambaa na kujifunga kiunoni. Kisha anatia maji ndani ya beseni na kuanza kuiosha miguu ya wanafunzi wake na kuikausha kwa kitambaa. Halafu, anavaa mavazi yake ya nje. Kwa nini Yesu alifanya tendo hilo la unyenyekevu?​—Yoh. 13:3-5.

2 Yesu mwenyewe alisema hivi: “Je, mnajua jambo ambalo nimewafanyia ninyi? . . . Ikiwa mimi, nijapokuwa Bwana na Mwalimu, niliiosha miguu yenu, ninyi pia mnapaswa kuoshana miguu. Kwa maana niliweka kielelezo kwa ajili yenu, ili, kama vile nilivyowafanyia ninyi, ninyi pia mfanye hivyo.” (Yoh. 13:12-15) Kwa kuwa tayari kufanya kazi hiyo ya hali ya chini, Yesu aliwafundisha mitume wake somo muhimu ambalo wangekumbuka kwa muda mrefu na lingewachochea kuwa wanyenyekevu baadaye.

3. (a) Katika pindi mbili, Yesu alikaziaje umuhimu wa unyenyekevu? (b) Tutazungumzia nini katika makala hii?

3 Yesu alipowaosha miguu mitume wake, hiyo haikuwa mara yake ya kwanza kukazia umuhimu wa unyenyekevu. Pindi fulani, baadhi ya mitume walipoonyesha roho ya kushindana, Yesu alimweka mtoto mchanga kando yake, na kuwaambia hivi: “Yeyote yule anayempokea mtoto huyu mchanga kwa msingi wa jina langu ananipokea mimi pia, na yeyote anayenipokea, anampokea pia yule aliyenituma. Kwa maana anayejiendesha kama aliye mdogo zaidi kati yenu nyote ndiye aliye mkuu.” (Luka 9:46-48) Akijua kwamba Mafarisayo walitafuta umashuhuri, Yesu alisema hivi baadaye katika huduma yake: “Kila mtu anayejiinua atanyenyekezwa na yule anayejinyenyekeza atainuliwa.” (Luka 14:11) Ni wazi kwamba Yesu anataka wafuasi wake wawe wanyenyekevu katika akili, yaani, wasiwe na kiburi wala majivuno. Ili tumwige, acheni tuchunguze kwa makini kielelezo chake cha unyenyekevu. Tutaona pia jinsi sifa hiyo inavyoweza kumfaidi si yule tu anayeionyesha bali pia wengine.

“SIKUGEUKA UPANDE ULIO KINYUME”

4. Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu alionyeshaje unyenyekevu kabla hajawa mwanadamu?

4 Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu alionyesha unyenyekevu hata kabla ya kuja duniani. Kabla ya kuwa mwanadamu, Yesu aliishi miaka mingi sana pamoja na Baba yake wa mbinguni. Kitabu cha Biblia cha Isaya kinasema hivi kuhusu uhusiano wa karibu ambao Mwana huyo alikuwa nao pamoja na Baba yake: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova amenipa ulimi wa waliofundishwa, ili nijue jinsi ya kumjibu neno yeye aliyechoka. Yeye huamka asubuhi baada ya asubuhi; huliamsha sikio langu ili lisikie kama wale waliofundishwa. Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova mwenyewe amelifungua sikio langu, nami kwa upande wangu sikuwa mwasi. Sikugeuka upande ulio kinyume.” (Isa. 50:4, 5) Mwana wa Mungu alionyesha mtazamo wa unyenyekevu na alisikiliza kwa makini mambo ambayo Yehova alimfundisha. Alitamani na alikuwa tayari kujifunza kutoka kwa Mungu wa kweli. Ni wazi kwamba Yesu alitazama kwa makini mfano wa unyenyekevu ambao Yehova aliweka alipowaonyesha rehema wanadamu wenye dhambi!

5. Akiwa Mikaeli yule malaika mkuu, Yesu aliwekaje kielelezo cha unyenyekevu na kiasi aliposhughulika na Ibilisi?

5 Si viumbe wote mbinguni waliokuwa na mtazamo kama wa Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu. Badala ya kutamani kujifunza kutoka kwa Yehova, malaika aliyekuja kuwa Shetani Ibilisi alijiruhusu aongozwe na ubinafsi na kiburi, tabia ambazo ni kinyume cha sifa ya unyenyekevu, na hivyo akamwasi Yehova. Kwa upande mwingine, Yesu aliridhika na cheo chake mbinguni naye hakuwa na mwelekeo wa kutumia vibaya mamlaka yake. Akiwa Mikaeli yule malaika mkuu, Yesu hakuvuka mipaka ya mamlaka aliyopewa alipokuwa na ‘tofauti na Ibilisi juu ya mwili wa Musa.’ Badala yake, Mwana wa Mungu alionyesha unyenyekevu na kiasi. Alifurahi kumwachia Yehova, Hakimu Mkuu wa ulimwengu mzima, ashughulikie mambo kwa njia Yake na kwa wakati Wake mwenyewe.​—Soma Yuda 9.

6. Yesu alionyeshaje unyenyekevu kwa kukubali mgawo wa kuwa Masihi?

6 Bila shaka, mambo ambayo Yesu alijifunza kabla ya kuwa mwanadamu yalitia ndani unabii uliotabiri mambo mbalimbali ambayo angetimiza duniani akiwa Masihi. Kwa hiyo, inaelekea alijua mapema kwamba angepatwa na mambo mabaya. Ingawa hivyo, Yesu aliukubali mgawo wa kuishi duniani na kufa akiwa Masihi aliyeahidiwa. Kwa nini? Akikazia unyenyekevu wa Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu, mtume Paulo aliandika hivi: “Ingawa alikuwa katika umbo la Mungu, [yeye] hakufikiria kufanya unyakuzi, yaani, kwamba yeye awe sawa na Mungu. Hapana, bali alijiondolea mwenyewe hali yake na kuchukua umbo la mtumwa na kuwa kama wanadamu.”​—Flp. 2:6, 7.

AKIWA MWANADAMU, “ALIJINYENYEKEZA”

7, 8. Yesu alionyeshaje unyenyekevu akiwa mtoto na katika huduma yake duniani?

7 Paulo aliandika hivi: “[Yesu] alipojikuta katika umbo la mwanadamu, alijinyenyekeza naye akawa mtiifu mpaka kifo, ndiyo, kifo juu ya mti wa mateso.” (Flp. 2:8) Tangu akiwa mtoto, Yesu alituwekea kielelezo cha unyenyekevu. Ingawa alilelewa na wazazi wasio wakamilifu, yaani, Yosefu na Maria, kwa unyenyekevu Yesu ‘aliendelea kujitiisha kwao.’ (Luka 2:51) Huo ni mfano mzuri kama nini kwa vijana watakaobarikiwa na Mungu kwa sababu wanajitiisha kwa hiari chini ya wazazi wao!

8 Akiwa mtu mzima, Yesu alionyesha unyenyekevu kwa kutanguliza mapenzi ya Yehova, wala si yake mwenyewe. (Yoh. 4:34) Wakati wa huduma yake, Yesu Kristo alilitumia jina binafsi la Mungu na kuwasaidia watu wanyoofu kupata ujuzi sahihi kuhusu sifa za Yehova na kusudi Lake kwa ajili ya wanadamu. Yesu aliishi pia kupatana na mambo aliyofundisha kumhusu Yehova. Kwa mfano, katika ile sala ya kielelezo, jambo la kwanza ambalo Yesu alitaja ni hili: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.” (Mt. 6:9) Hivyo, Yesu aliwafundisha wafuasi wake kwamba wanapaswa kuhangaikia hasa kutakaswa kwa jina la Yehova. Yeye mwenyewe alifanya hivyo maishani. Ndiyo sababu, mwishoni mwa huduma yake duniani, Yesu alisali hivi kwa Yehova: “Nimewajulisha [mitume] jina lako nami nitalijulisha.” (Yoh. 17:26) Zaidi ya hayo, katika huduma yake yote, Yesu alimsifu Yehova kwa mambo yote ambayo yeye alitimiza duniani.​—Yoh. 5:19.

9. Zekaria alitoa unabii gani kumhusu Masihi, na unabii huo ulitimizwaje na Yesu?

9 Zekaria aliandika unabii huu kumhusu Masihi: “Shangilia sana, Ee binti Sayuni. Piga kelele za ushindi, Ee binti Yerusalemu. Tazama! Mfalme wako anakuja kwako. Yeye ni mwadilifu, ndiyo, ameokolewa; ni mnyenyekevu, naye amepanda juu ya punda, juu ya mnyama mkomavu, mwana wa punda-jike.” (Zek. 9:9) Unabii huo ulitimizwa wakati Yesu alipoingia Yerusalemu kabla ya Pasaka ya mwaka wa 33 W.K. Umati ulitandaza mavazi yao ya nje na matawi ya miti barabarani. Kwa Kweli, jiji lote likawa na msukosuko alipoingia. Hata watu walipomsifu hadharani kuwa yeye ni Mfalme, Yesu alibaki mnyenyekevu.​—Mt. 21:4-11.

10. Yesu alithibitisha nini alipotii kwa hiari hadi kifo?

10 Katika maisha yake yote duniani, Yesu Kristo alionyesha unyenyekevu na utii mpaka alipouawa juu ya mti wa mateso. Kwa njia hiyo, alithibitisha bila shaka yoyote kwamba wanadamu wanaweza kubaki washikamanifu kwa Yehova hata wanapojaribiwa vikali sana. Pia, Yesu alionyesha kwamba Shetani alikosea kwa kudai kuwa wanadamu humtumikia Yehova kwa sababu za kichoyo. (Ayu. 1:9-11; 2:4) Utimilifu kamili ambao Kristo alionyesha ulitetea haki na uadilifu wa enzi kuu ya Yehova ya ulimwenguni pote. Bila shaka, Yehova alishangilia alipoona ushikamanifu usioyumba-yumba wa Mwana wake mnyenyekevu.​—Soma Methali 27:11.

11. Dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo iliwapa wanadamu wenye imani matumaini gani?

11 Pia, Yesu alilipa bei ya fidia ya wanadamu alipokufa juu ya mti wa mateso. (Mt. 20:28) Fidia hiyo iliwapa wanadamu wenye dhambi fursa ya kuishi milele, nayo ikatimiza matakwa ya uadilifu. Paulo aliandika hivi: “Kupitia tendo moja la kutetewa kuwa haki matokeo kwa watu wa namna zote ni wao kutangazwa kuwa waadilifu kwa ajili ya uzima.” (Rom. 5:18) Kifo cha Yesu kiliwapa Wakristo watiwa-mafuta tumaini la kupata uhai usioweza kufa mbinguni na kuwapa “kondoo wengine” tumaini la kupata uzima wa milele duniani.​—Yoh. 10:16; Rom. 8:16, 17.

MIMI NI “MNYENYEKEVU MOYONI”

12. Aliposhughulika na wanadamu wasio wakamilifu, Yesu alionyeshaje upole na unyenyekevu?

12 Yesu aliwaalika wote ‘wanaotaabika na kulemewa na mizigo’ waje kwake. Alisema hivi: “Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu.” (Mt. 11:28, 29) Sifa ya unyenyekevu na ya upole zilimfanya Yesu awe mwenye fadhili na asiye na ubaguzi aliposhughulika na wanadamu wasio wakamilifu. Alikuwa na usawaziko kuhusu mambo aliyotarajia wanafunzi wake watimize. Yesu aliwapongeza na kuwatia moyo. Hakuwafanya wahisi kwamba wamepungukiwa au hawafai. Bila shaka, Yesu hakuwa mkali wala hakuwakandamiza watu. Badala yake, aliwahakikishia wafuasi wake kwamba kwa kumkaribia yeye na kwa kufanya mambo aliyowafundisha, wangeburudishwa, kwa maana nira yake ilikuwa laini na mzigo wake mwepesi. Watu wa jinsia zote na kila umri walifurahi kuwa pamoja naye.​—Mt. 11:30.

13. Yesu aliwaonyeshaje huruma watu waliokuwa na matatizo?

13 Aliposhughulika na watu wa kawaida katika Israeli, Yesu aliwahurumia kwa sababu ya hali yao ya kusikitikiwa, na aliwasaidia kwa upendo. Alipokuwa karibu na mji wa Yeriko, alikutana na kipofu mwombaji aliyeitwa Bartimayo pamoja na kipofu mwingine ambaye hatajwi jina. Waliendelea kumsihi sana Yesu awasaidie, lakini umati ulijaribu kuwashurutisha wanaume hao wakae kimya. Ingekuwa rahisi sana kupuuza sihi za wanaume hao vipofu! Badala yake, Yesu aliagiza waletwe kwake, naye akawasikitikia na kuwaponya. Naam, Yesu alimwiga Baba yake, Yehova, kwa kuonyesha sifa ya unyenyekevu na kuwarehemu watenda-dhambi wapole.​—Mt. 20:29-34; Marko 10:46-52.

“YEYOTE YULE ANAYEJINYENYEKEZA ATAINULIWA”

14. Maisha ya Yesu ya unyenyekevu yameleta manufaa gani?

14 Maisha ya Yesu Kristo ya unyenyekevu yameleta shangwe na faida kubwa. Yehova alishangilia alipomwona Mwana wake mpendwa akijinyenyekeza ili kufanya mapenzi Yake. Mitume na wanafunzi waliburudishwa na tabia pole na unyenyekevu wa moyoni wa Yesu. Kielelezo chake, mafundisho yake, na pongezi yake changamfu iliwachochea kufanya maendeleo ya kiroho. Watu wa kawaida walinufaika kutokana na unyenyekevu wa Yesu kwa sababu aliwasaidia, aliwafundisha, na kuwatia moyo. Ukweli ni kwamba wanadamu wote wanaoweza kukombolewa watapata manufaa ya muda mrefu kwa sababu ya dhabihu ya fidia ya Yesu.

15. Yesu alinufaikaje kwa kuwa mnyenyekevu?

15 Namna gani Yesu? Je, unyenyekevu wake ulimnufaisha? Ndiyo, kwa kuwa Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Yeyote yule anayejinyenyekeza atainuliwa.” (Mt. 23:12) Maneno hayo yalithibitika kuwa ya kweli maishani mwake. Paulo anaeleza hivi: “Mungu alimpandisha [Yesu] kwenye cheo cha juu zaidi na kumpa kwa fadhili jina lililo juu ya kila jina lingine, ili katika jina la Yesu kila goti lipigwe la wale walio mbinguni na wale walio duniani na wale walio chini ya nchi, na kila ulimi ukiri waziwazi kwamba Yesu Kristo ni Bwana kwa utukufu wa Mungu Baba.” Kwa sababu ya maisha ya Yesu ya unyenyekevu na uaminifu duniani, Yehova Mungu alimkweza Mwana wake, akampa mamlaka juu ya viumbe walio mbinguni na duniani.​—Flp. 2:9-11.

YESU ‘ATAPANDA KWA KUTETEA KWELI NA UNYENYEKEVU’

16. Ni nini kinachoonyesha kwamba Mwana wa Mungu ataendelea kutenda kwa unyenyekevu?

16 Mwana wa Mungu ataendelea kutenda kwa unyenyekevu. Akitabiri kuhusu jinsi Yesu atakavyochukua hatua dhidi ya adui Zake akiwa katika cheo chake kilichotukuka mbinguni, mtunga-zaburi aliimba hivi: “Katika fahari yako endelea mpaka ufanikiwe; panda kwa kutetea kweli na unyenyekevu na uadilifu.” (Zab. 45:4) Yesu Kristo atapanda ili kutetea kweli na unyenyekevu na uadilifu katika vita vya Har–Magedoni. Ni nini kitakachotokea mwishoni mwa Utawala wake wa Miaka Elfu Moja wakati Mfalme huyo wa Kimasihi “atakapokuwa ameangamiza serikali yote na mamlaka yote na nguvu zote”? Je, ataonyesha unyenyekevu? Ndiyo, kwa kuwa ‘atamkabidhi ufalme Mungu wake ambaye pia ni Baba yake.’​—Soma 1 Wakorintho 15:24-28.

17, 18. (a) Kwa nini ni muhimu watumishi wa Yehova wafuate mfano wa Yesu wa unyenyekevu? (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

17 Namna gani sisi? Je, tutafuata mfano tuliowekewa na Kielelezo chetu kwa kuwa wanyenyekevu? Itakuwaje kwetu wakati Mfalme Yesu Kristo atakapokuja kutekeleza hukumu katika vita vya Har–Magedoni? Kwa kuwa Yesu atapanda ili kutetea unyenyekevu na uadilifu, atawakomboa wale tu ambao ni wanyenyekevu na waadilifu. Basi, ni muhimu sana tusitawishe unyenyekevu ili tuokolewe. Isitoshe, kama vile tu maisha ya Yesu ya unyenyekevu yalivyomnufaisha yeye na wengine, unyenyekevu wetu utaleta manufaa mbalimbali.

18 Ni nini kinachoweza kutusaidia kufuata mfano wa Yesu wa unyenyekevu? Tunaweza kujitahidi jinsi gani kuwa wanyenyekevu licha ya matatizo ambayo huenda tukakabili? Maswali hayo yatazungumziwa katika makala inayofuata.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 12]

Tunaweza kunufaikaje kutokana na mfano wa Yesu wa unyenyekevu?

[Picha katika ukurasa wa 13]

Yesu aliweka mfano mzuri katika kuonyesha huruma