Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Yesu Alituachia Mufano Wa Unyenyekevu

Yesu Alituachia Mufano Wa Unyenyekevu

Yesu Alituachia Mufano Wa Unyenyekevu

‘Niliweka kielelezo kwa ajili yenu, ili, kama vile nilivyowafanyia ninyi, ninyi pia mufanye hivyo.’​—YOH. 13:15.

UNGEJIBU NAMNA GANI?

Namna gani Mwana wa Mungu alionyesha unyenyekevu mbele ya kuja duniani?

Namna gani Yesu alionyesha unyenyekevu alipokuwa duniani?

Unyenyekevu wa Yesu umeleta baraka gani?

1, 2. Usiku wa mwisho wa maisha yake duniani, Yesu aliwafundisha mitume wake somo gani?

 NI USIKU wa mwisho wa maisha ya Yesu duniani; usiku huo iko pamoja na wanafunzi wake katika chumba cha juu cha nyumba moja huko Yerusalemu. Wanapokula chakula cha mangaribi, Yesu anasimama na kutia pembeni mavazi yake ya inje. Anachukua kitambaa cha kupanguza maji. Kisha anatia maji katika beseni na kuanza kunawisha na kupanguza wanafunzi wake miguu. Kisha anavaa tena mavazi yake ya inje. Sababu gani Yesu alifanya tendo hilo la unyenyekevu?​—Yoh. 13:3-5.

2 Yeye mwenyewe alieleza hivi: ‘Je, munajua jambo ambalo nimewafanyia ninyi? Ikiwa mimi, nijapokuwa Bwana na Mwalimu, niliiosha miguu yenu, ninyi pia munapaswa kuoshana miguu. Kwa maana niliweka kielelezo kwa ajili yenu, ili, kama vile nilivyowafanyia ninyi, ninyi pia mufanye hivyo.’ (Yoh. 13:12-15) Kwa kufanya tendo hilo la unyenyekevu, Yesu aliwafundisha mitume wake somo ambalo hawangesahau hata kidogo na ambalo lingewasaidia kuwa wanyenyekevu katika siku zilizokuwa mbele yao.

3. (a) Katika hali mbili tofauti-tofauti, namna gani Yesu alikazia umaana wa unyenyekevu? (b) Tutajifunza nini katika habari hii?

3 Yesu aliponawisha mitume wake miguu, hiyo haikuwa mara yake ya kwanza kukazia umaana wa unyenyekevu. Hapo mbele wakati mitume fulani walibishana na kupenda kujua ni nani aliye mukubwa kati yao, Yesu aliweka mutoto mudogo pembeni yake, kisha aliwaambia hivi: ‘Yeyote yule anayemupokea mutoto huyu muchanga kwa musingi wa jina langu ananipokea mimi pia, na yeyote anayenipokea, anamupokea pia yule aliyenituma. Kwa maana anayejiendesha kama aliye mudogo zaidi kati yenu nyote ndiye aliye mukubwa.’ (Lu. 9:46-48) Kwa kuwa alijua kama Mafarisayo walitafuta kujionyesha, baadaye Yesu alisema hivi: ‘Kwa maana kila mutu anayejiinua atanyenyekezwa na yule anayejinyenyekeza atainuliwa.’ (Lu. 14:11) Kwa kweli, Yesu alitaka wafuasi wake wawe wanyenyekevu, ni kusema, wajishushe na wasiwe na kiburi na majivuno. Ili kumuiga, acheni tujifunze namna alivyoonyesha unyenyekevu. Tutajifunza pia namna tunaweza kufaidika na sifa hiyo na namna inavyoweza kuwafaidi wengine.

“SIKUGEUKA UPANDE ULIO KINYUME”

4. Namna gani Mwana muzaliwa-pekee wa Mungu alionyesha unyenyekevu mbele aje duniani?

4 Mwana muzaliwa-pekee wa Mungu alionyesha unyenyekevu mbele hata ya kuja duniani. Yesu alipitisha miaka mingi pamoja na Baba yake wa mbinguni mbele ya kuja duniani. Kitabu cha Isaya kinazungumuzia uhusiano wa karibu uliokuwa kati ya Yehova na Mwana wake, kitabu hicho kinasema hivi: ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova amenipa ulimi wa waliofundishwa, ili nijue jinsi ya kumujibu neno yeye aliyechoka. Yeye huamuka asubuhi baada ya asubuhi; huliamusha sikio langu ili lisikie kama wale waliofundishwa. Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova mwenyewe amelifungua sikio langu, nami kwa upande wangu sikuwa mwasi. Sikugeuka upande ulio kinyume.’ (Isa. 50:4, 5) Mwana wa Mungu alionyesha unyenyekevu na alisikiliza kwa uangalifu sana mambo ambayo Yehova alimufundisha. Alikuwa tayari kufundishwa na Mungu wa kweli na alifurahia jambo hilo sana. Yesu alitazama kwa uangalifu kabisa namna Yehova alivyoonyesha unyenyekevu kwa kuwahurumia wanadamu wenye zambi.

5. Akiwa Mikaeli, malaika mukubwa, namna gani Yesu alionyesha unyenyekevu na kiasi alipobishana na Shetani?

5 Si kila kiumbe mbinguni kilionyesha unyenyekevu kama ule wa Mwana muzaliwa​-pekee wa Mungu. Kuliko kufurahia kufundishwa na Yehova, malaika mumoja aliyeitwa baadaye Shetani Ibilisi hakuonyesha unyenyekevu lakini alimuasi Yehova kwa kujiacha atawaliwe na majivuno na kiburi. Lakini Yesu kwa upande wake, alitosheka na cheo alichopewa huko mbinguni na hakutaka kutumia vibaya mamlaka yake. Akiwa Mikaeli, malaika mukubwa, Yesu hakutumia vibaya mamlaka yake ‘alipobishana na Shetani juu ya mwili wa Musa.’ Lakini Mwana wa Mungu alionyesha unyenyekevu na kiasi. Alingojea kwa furaha wakati ambao Yehova, Muamuzi Mukubwa wa ulimwengu wote, angeshugulikia mambo kwa njia na kwa wakati unaofaa.​—Soma Yuda 9.

6. Namna gani Yesu alionyesha unyenyekevu kwa kukubali kuwa Masiya?

6 Bila shaka mambo ambayo Yesu alijifunza mbele ya kuja duniani yalitia ndani unabii mbalimbali uliotabiri namna atakuwa Masiya. Kwa hiyo, inaonekana alijua mbele ya wakati kwamba majaribu yalimungojea. Hata hivyo, Yesu alikubali kuja duniani na kufa akiwa Masiya aliyeahidiwa. Sababu gani? Mutume Paulo alizungumuzia unyenyekevu wa Mwana muzaliwa-pekee wa Mungu, aliandika hivi: ‘Ingawa alikuwa katika umbo la Mungu, hakufikiria kufanya unyakuzi, yaani, kwamba yeye awe sawa na Mungu. Hapana, bali alijiondolea mwenyewe hali yake na kuchukua umbo la mutumwa na kuwa kama wanadamu.’​—Flp. 2:6, 7.

“ALIJINYENYEKEZA”

7, 8. Namna gani Yesu alionyesha unyenyekevu alipokuwa mutoto na katika huduma yake duniani?

7 Mutume Paulo aliandika pia hivi: ‘[Yesu] alipojikuta katika umbo la mwanadamu, alijinyenyekeza naye akawa mutiifu mupaka kifo, ndiyo, kifo juu ya muti wa mateso.’ (Flp. 2:8) Tangu utoto wake na kuendelea, Yesu alituachia mufano wa unyenyekevu. Ijapokuwa alikomalishwa na wazazi wasio wakamilifu, Yosefu na Maria, Yesu ‘aliendelea kujitiisha kwao’ kwa unyenyekevu. (Lu. 2:51) Yesu aliachia watoto mufano muzuri. Ikiwa wanajitiisha kwa wazazi wao bila kunungunika, watabarikiwa!

8 Alipokuwa mutu muzima, Yesu alionyesha unyenyekevu kwa kutia mapenzi ya Yehova pa nafasi ya kwanza, wala si mapenzi yake. (Yoh. 4:34) Wakati wa huduma yake, Yesu Kristo alitumia jina la Mungu na aliwasaidia watu waliokuwa tayari kumusikiliza kupata ujuzi wa kweli kuhusu sifa za Yehova na kusudi Lake kuelekea wanadamu. Yesu aliishi pia kulingana na mambo aliyofundisha kumuhusu Yehova. Katika sala ya mufano, jambo la kwanza ambalo Yesu alitaja lilikuwa: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.” (Mt. 6:9) Kupitia maneno hayo, Yesu aliwafundisha wanafunzi kwamba jambo la kwanza la kuhangaikia ni kutakaswa kwa jina la Yehova. Yeye pia alifanya hivyo katika maisha yake yote. Mwishoni mwa huduma yake duniani, Yesu alisali kwa Yehova hivi: “Nami nimewajulisha [mitume] jina lako nami nitalijulisha.” (Yoh. 17:26) Zaidi ya hayo, katika huduma yake yote, Yesu aliacha sifa zimuendee Yehova katika mambo yote aliyotimiza duniani.​—Yoh. 5:19.

9. Nabii Zekaria alitabiri nini kumuhusu Masiya, na Yesu alitimiza namna gani unabii huo?

9 Nabii Zekaria alitabiri hivi kumuhusu Masiya: ‘Shangilia sana, Ee binti Sayuni. Piga kelele za ushindi, Ee binti Yerusalemu. Tazama! mufalme wako anakuja kwako. Yeye ni mwadilifu, ndiyo, ameokolewa; ni munyenyekevu, naye amepanda juu ya punda, juu ya munyama mukomavu, mwana wa punda​-jike.’ (Zek. 9:9) Maneno hayo yalitimia wakati Yesu aliingia Yerusalemu mbele ya Pasaka ya mwaka wa 33. Watu wengi walianza kutandaza nguo zao na matawi ya miti katika barabara. Muji wote ulijaa makelele wakati Yesu aliingia ndani yake. Hata ikiwa Yesu alishangiliwa kama Mufalme wakati huo, yeye alibaki munyenyekevu.​—Mt. 21:4-11.

10. Kwa kubaki mutiifu mupaka kifo, Yesu alionyesha nini?

10 Yesu alibaki munyenyekevu na mutiifu mupaka kifo kwenye muti wa mateso. Kwa njia hiyo, Yesu alionyesha waziwazi kama mwanadamu anaweza kubaki mwaminifu kwa Mungu hata katika majaribu makali. Yesu alionyesha pia kama Shetani alisema uongo kwa kudai kama wanadamu wanamutumikia Yehova kwa sababu tu ya vitu anavyowapatia. (Ayu. 1:9-11; 2:4) Uaminifu-mushikamanifu wa Yesu ulionyesha pia kama Yehova ndiye aliye na haki ya kutawala ulimwengu wote muzima kwa njia inayofaa zaidi. Bila shaka, Yehova alifurahi alipotazama uaminifu usioyumba​-yumba wa Mwana wake munyenyekevu.​—Soma Methali 27:11.

11. Zabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo iliwatolea wanadamu watiifu matumaini gani?

11 Kupitia kifo chake juu ya muti wa mateso, Yesu aliwakomboa pia wanadamu. (Mt. 20:28) Kupitia ukombozi huo, Yehova anawatolea wanadamu wasio wakamilifu tumaini ya kuishi milele, na ukombozi huo ulilingana na kanuni zake za haki. Mutume Paulo aliandika hivi: “Kupitia tendo moja la kutetewa kuwa haki matokeo kwa watu wa namna zote ni wao kutangazwa kuwa waadilifu kwa ajili ya uzima.” (Rom. 5:18) Kifo cha Yesu kinawatolea Wakristo watiwa​-mafuta tumaini la kupata uzima usioweza kufa huko mbinguni na uzima wa milele duniani kwa “kondoo wengine.”​—Yoh. 10:16; Rom. 8:16, 17.

MIMI NI ‘MUNYENYEKEVU MOYONI’

12. Namna gani Yesu alionyesha upole na unyenyekevu katika uhusiano wake na wanadamu wasio wakamilifu?

12 Yesu aliwaalika wote wenye ‘kutaabika na kulemewa na mizigo’ waje kwake. Yeye alisema hivi: ‘Chukueni nira yangu na mujifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia​-pole na munyenyekevu moyoni, nanyi mutapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu.’ (Mt. 11:28, 29) Sifa za Unyenyekevu na upole zilimuchochea Yesu kuwatendea wanadamu wasio wakamilifu kwa upole na bila ubaguzi. Hakuwaomba wanafunzi wake wafanye mambo yanayozidi uwezo wao. Yesu aliwapongeza na kuwatia moyo. Hakuwafanya wajisikie kuwa watu wa bure. Bila shaka, Yesu hakuwa mukali. Badala yake, aliwahakikishia kwamba wakimukaribia na kutenda kulingana na mafundisho yake, wataburudishwa, kwa sababu nira yake ni laini na muzigo wake ni mwepesi. Wanaume, wanawake, na watu wa umri wote walifurahia kuwa karibu naye.​—Mt. 11:30.

13. Namna gani Yesu aliwatendea kwa huruma watu wa hali ya chini?

13 Aliposhugulika na watu wa hali ya chini, Yesu aliwahurumia sababu walikuwa watu wenye kuzarauliwa, na aliwahangaikia na kutosheleza mahitaji yao. Yesu alikutana na kipofu mumoja mwenye kuomba-omba aliyeitwa Bartimayo pamoja na kipofu mwenzake. Wote wawili walimusihi Yesu awasaidie, lakini watu waliwaambia kwa ukali wanyamaze. Ilikuwa rahisi kwa Yesu kupuuza ombi la wanaume hao vipofu! Kuliko kufanya hivyo, yeye aliomba wamuletee vipofu hao, na kwa sababu ya kuwasikitikia, alifungua macho yao. Bila shaka, Yesu alimuiga Baba yake, Yehova, kwa kuwatendea wafanya​-zambi wa hali ya chini kwa unyenyekevu na huruma.​—Mt. 20:29-34; Mk. 10:46-52.

“YEYOTE YULE ANAYEJINYENYEKEZA ATAINULIWA”

14. Unyenyekevu wa Yesu umeleta baraka gani?

14 Unyenyekevu wa Yesu unafurahisha na kuletea watu wengi baraka. Yehova alifurahi alipoona Mwana wake akijitiisha ili kufanya mapenzi yake kwa unyenyekevu. Mitume na wanafunzi wa Yesu walifurahia tabia pole na unyenyekevu wake wa moyoni. Mufano wake, mafundisho yake, na pongezi zake changamufu ziliwachochea kufanya maendeleo ya kiroho. Watu wa kawaida walifaidika na unyenyekevu wa Yesu kwa sababu aliwasaidia, aliwafundisha, na aliwatia moyo. Kwa kweli, wanadamu wote walio na imani katika zabihu ya ukombozi ya Yesu watavuna baraka nyingi milele na milele.

15. Yesu alibarikiwa namna gani kwa sababu ya kubaki munyenyekevu?

15 Namna gani Yesu? Je, unyenyekevu wake ulimuletea baraka? Ndiyo, kwa sababu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Yeyote yule anayejinyenyekeza atainuliwa.” (Mt. 23:12) Yesu mwenyewe alijionea ukweli wa maneno hayo. Paulo anaeleza hivi: ‘Mungu alimupandisha [Yesu] kwenye cheo cha juu zaidi na kumupa kwa fazili jina lililo juu ya kila jina lingine, ili katika jina la Yesu kila goti lipigwe la wale walio mbinguni na wale walio duniani na wale walio chini ya inchi, na kila ulimi ukiri waziwazi kwamba Yesu Kristo ni Bwana kwa utukufu wa Mungu Baba.’ Kwa sababu Yesu alikuwa munyenyekevu na mwaminifu alipokuwa duniani, Yehova Mungu alimuinua Mwana wake, alimupatia mamlaka juu ya viumbe walio mbinguni na duniani.​—Flp. 2:9-11.

YESU ‘ATATETEA KWELI NA UNYENYEKEVU’

16. Ni nini inayoonyesha kama Yesu ataendelea kutenda kwa unyenyekevu?

16 Yesu ataendelea kutenda kwa unyenyekevu. Alipotabiri namna Yesu atakavyoshinda maadui wake akiwa mbinguni, mutunga-zaburi aliimba hivi: ‘Katika fahari yako endelea mupaka ufanikiwe; panda kwa kutetea kweli na unyenyekevu na uadilifu.’ (Zab. 45:4) Kwenye vita ya Har-magedoni, Yesu Kristo atawatetea wenye haki na wanyenyekevu. Ni jambo gani litakalotokea mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu, wakati Mufalme wa Kimasiya atakuwa ‘ameangamiza serikali zote, mamlaka yote na nguvu zote?’ Je, ataonyesha unyenyekevu? Ndiyo, kwa sababu ‘atamukabizi ufalme Mungu wake ambaye pia ni Baba yake.’​—Soma 1 Wakorintho 15:24-28.

17, 18. (a) Sababu gani ni jambo la maana kwa watumishi wa Yehova kufuata mufano wa Yesu wa unyenyekevu? (b) Habari inayofuata itajibu maulizo gani?

17 Namna gani sisi? Je, tutafuata mufano wa unyenyekevu ambao Yesu alituachia? Je, tutaendelea kuonyesha unyenyekevu wakati Mufalme Yesu Kristo atakuja kupigana vita ya Har-magedoni? Yesu atakuja tu kuwaokoa wale walio wanyenyekevu na wenye haki. Kwa hiyo, kuonyesha unyenyekevu ni jambo la maana ili kupata wokovu. Zaidi ya hayo, kama vile unyenyekevu wa Yesu ulivyoletea yeye na wengine baraka, kuonyesha unyenyekevu kutatuletea baraka katika njia nyingi.

18 Ni nini itatusaidia kufuata mufano wa Yesu wa unyenyekevu? Namna gani tunaweza kujikaza kuwa wanyenyekevu ijapokuwa matatizo tunayoweza kupata? Maulizo hayo yatazungumuziwa katika habari inayofuata.

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 12]

Namna gani mufano wa Yesu wa unyenyekevu unaweza kutuletea baraka?

[Picha katika ukurasa wa 13]

Yesu alituachia mufano muzuri wa kuonyesha huruma