Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sitawisha Ile Roho ya Aliye Mdogo Zaidi

Sitawisha Ile Roho ya Aliye Mdogo Zaidi

Sitawisha Ile Roho ya Aliye Mdogo Zaidi

“Anayejiendesha kama aliye mdogo zaidi kati yenu nyote ndiye aliye mkuu.”​—LUKA 9:48.

JE, UNAWEZA KUPATA MAJIBU?

Ni nini kinachoweza kutusaidia kusitawisha roho ya aliye mdogo zaidi?

Mtu aliye mdogo zaidi ni “mkuu” katika njia zipi?

Tunawezaje kuonyesha unyenyekevu katika ndoa, kutanikoni, na katika mahusiano yetu na wengine?

1, 2. Yesu aliwapa mitume wake shauri gani, na kwa nini?

ULIKUWA mwaka wa 32 W.K. Yesu alikuwa katika wilaya ya Galilaya wakati matatizo yalipotokea. Baadhi ya mitume wake walikuwa wakibishana kuhusu ni nani aliye mkuu zaidi kati yao. Luka, mwandikaji wa Injili, anaripoti hivi: “Wakaanza kujadiliana kati yao kuhusu ni nani angekuwa mkuu zaidi kati yao. Yesu, akijua mawazo ya mioyo yao, akachukua mtoto mchanga, akamweka kando yake na kuwaambia: ‘Yeyote yule anayempokea mtoto huyu mchanga kwa msingi wa jina langu ananipokea mimi pia, na yeyote anayenipokea, anampokea pia yule aliyenituma. Kwa maana anayejiendesha kama aliye mdogo zaidi kati yenu nyote ndiye aliye mkuu.’” (Luka 9:46-48) Kwa subira, lakini kwa uthabiti, Yesu aliwasaidia mitume hao kutambua umuhimu wa kuwa wanyenyekevu.

2 Je, shauri la Yesu la kujiendesha kama aliye mdogo zaidi lilipatana na mwelekeo wa Wayahudi wa karne ya kwanza? Au je, lilikuwa kinyume kabisa na mtazamo waliokuwa nao kwa ujumla? Kitabu kimoja (Theological Dictionary of the New Testament) kinasema hivi kuhusu mtazamo wa watu wengi wakati huo: “Katika kila jambo, swali kuhusu ni nani aliye mkuu zaidi ya wote lilizuka, na kumpa kila mtu heshima aliyostahili lilikuwa jambo muhimu lililowahangaisha watu kila mara.” Yesu alikuwa akiwashauri mitume wake wawe tofauti na watu kwa ujumla.

3. (a) Kujiendesha kama aliye mdogo zaidi kunamaanisha nini, na kwa nini inaweza kuwa vigumu kwetu kujiendesha kwa njia hiyo? (b) Ni maswali gani yanayozuka kuhusu kusitawisha roho ya aliye mdogo zaidi?

3 Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “aliye mdogo zaidi” linamaanisha mtu mwenye kiasi, mnyenyekevu, mpole, wa hali ya chini, na ambaye si mashuhuri. Yesu alitumia mtoto mchanga kuwaonyesha wazi mitume wake kwamba wanapaswa kuwa wanyenyekevu na wenye kiasi. Shauri hilo linawahusu Wakristo leo kama tu lilivyowahusu Wakristo wa karne ya kwanza. Katika hali fulani, huenda ikawa vigumu kwetu kujiendesha kama walio wadogo zaidi. Mwelekeo wa wanadamu wa kuwa na kiburi unaweza kutusukuma tujitafutie umaarufu. Roho ya mashindano na roho ya ulimwengu unaotuzunguka inaweza kutufanya tuwe watu wenye ubinafsi, ugomvi, au wenye hila. Ni nini kinachoweza kutusaidia kusitawisha roho ya aliye mdogo zaidi? ‘Aliye mdogo zaidi kati yetu ni mkuu’ kwa njia gani? Tunapaswa kujitahidi kuonyesha roho ya unyenyekevu katika mambo gani maishani?

“LO! JINSI KILIVYO KINA CHA UTAJIRI WA MUNGU NA HEKIMA NA UJUZI!”

4, 5. Ni nini kinachoweza kutuchochea kusitawisha unyenyekevu? Toa mfano.

4 Njia moja ya kusitawisha unyenyekevu ni kukumbuka kwamba Yehova ni mkuu zaidi kuliko sisi. Ukweli ni kwamba “haiwezekani kuchunguza kikamilifu uelewaji wake.” (Isa. 40:28) Alipokuwa akizungumzia mambo fulani kuhusu ukuu wa Yehova, mtume Paulo aliandika hivi: “Lo! jinsi kilivyo kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi! Jinsi hukumu zake zisivyochunguzika na njia zake zisivyotafutika!” (Rom. 11:33) Ingawa wanadamu wamejifunza mambo mengi sana tangu Paulo alipoandika maneno hayo miaka 2,000 hivi iliyopita, maneno hayo bado ni ya kweli. Haidhuru tunajua mambo mengi kadiri gani, tunapaswa kunyenyekea tunapotambua kwamba hakuna mwisho wa mambo tunayoweza kujifunza kumhusu Yehova, kazi zake, na njia zake.

5 Kutambua kwamba hatuwezi kuzijua njia zote za Yehova kulimsaidia Leo * kujiendesha kama aliye mdogo zaidi. Alipokuwa kijana, Leo alivutiwa sana na sayansi. Akiwa na hamu ya kuelewa mambo mengi kadiri alivyoweza kuhusu ulimwengu, alisomea sayansi ya nyota naye akafikia mkataa huu muhimu: “Kutokana na elimu yangu, nilitambua kwamba nadharia za kisayansi pekee haziwezi kuwasaidia wanadamu kuuelewa ulimwengu kikamili. Kwa hiyo, nilibadili masomo yangu, nikasomea sheria.” Baada ya muda, Leo akawa wakili wa wilaya na kisha hakimu. Hatimaye, yeye na mke wake walijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, wakakubali kweli na wakawa watumishi wa Mungu waliojiweka wakfu. Licha ya elimu yake, ni nini ambacho kimemsaidia Leo kujiendesha kama aliye mdogo zaidi? Anajibu hivi bila kusitasita: “Ni kutambua kwamba hata tujifunze mambo mengi kadiri gani kumhusu Yehova na ulimwengu, bado kuna mengi zaidi ya kuvumbua.”

6, 7. (a) Yehova ni mfano bora sana wa unyenyekevu jinsi gani? (b) Unyenyekevu wa Mungu unawezaje kumfanya mtu awe “mkuu”?

6 Jambo lingine linalotusaidia kuwa wanyenyekevu ni kwamba Yehova mwenyewe anaonyesha unyenyekevu. Fikiria jambo hili: “Sisi ni wafanyakazi wenzi wa Mungu.” (1 Kor. 3:9) Hebu wazia jambo hilo! Yehova, Mungu mwenye ukuu usio na kifani, anatuheshimu kwa njia hiyo kwa kutupatia fursa ya kutimiza huduma yetu kwa kutumia Neno lake, Biblia. Ingawa Yehova ndiye anayekuza mbegu tunazopanda na kutia maji, anatupatia pendeleo lenye heshima la kufanya kazi pamoja naye. (1 Kor. 3:6, 7) Je, huo si mfano bora sana wa unyenyekevu ambao Mungu anaonyesha? Kwa kweli, mfano wa Yehova wa unyenyekevu unapaswa kumchochea sana kila mmoja wetu kujiendesha kama aliye mdogo zaidi.

7 Mfano wa Mungu wa unyenyekevu ulimchochea sana mtunga-zaburi Daudi. Alimwimbia Yehova hivi: “Utanipa ngao yako ya wokovu, na unyenyekevu wako ndio hunifanya niwe mkuu.” (2 Sam. 22:36) Daudi alisema kwamba alitimiza mambo makuu katika Israeli kwa sababu ya unyenyekevu wa Yehova, yaani, Mungu alijishusha chini, au kujinyenyekeza, ili amkazie fikira. (Zab. 113:5-7) Je, anatutendea kwa njia hiyohiyo? Je, tuna sifa, uwezo, au mapendeleo yoyote ambayo ‘hatukupokea’ kutoka kwa Yehova? (1 Kor. 4:7) Mtu anayejiendesha kama aliye mdogo zaidi ni “mkuu” katika maana ya kwamba anakuwa mtumishi mwenye thamani zaidi wa Yehova. (Luka 9:48) Acheni tuone inakuwaje hivyo.

‘ALIYE MDOGO ZAIDI KATI YENU NI MKUU’

8. Unyenyekevu unatusaidia kuwa na mtazamo gani kuelekea tengenezo la Yehova?

8 Ni muhimu sana tuwe wanyenyekevu ili turidhike katika tengenezo la kitheokrasi la Mungu na kuunga mkono mpango wa kutaniko. Kwa mfano, mfikirie Petra, mwanamke kijana aliyelelewa katika familia ya Mashahidi wa Yehova. Petra alijitenga na kutaniko kwa sababu alitaka kufanya mambo kwa njia yake mwenyewe. Baada ya miaka mingi kupita, alianza tena kushirikiana na kutaniko. Sasa, anafurahi kuwa katika tengenezo la Yehova na anaunga mkono kwa bidii mpango wa kutaniko. Ni nini kilichofanya abadili mtazamo wake? Anaandika hivi: “Ili nijihisi nikiwa sehemu ya tengenezo la Mungu, nilihitaji kuelewa na kusitawisha sifa mbili muhimu zaidi, unyenyekevu na kiasi.”

9. Mtu mnyenyekevu ana mtazamo gani kuelekea chakula cha kiroho tunachopokea, na kwa nini jambo hilo linamfanya awe mwenye thamani zaidi?

9 Mtu mnyenyekevu anathamini kutoka moyoni maandalizi ya Yehova, kutia ndani chakula cha kiroho. Kwa hiyo, mtu kama huyo hujifunza Biblia kwa bidii na anasoma kwa hamu magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Kama tu watumishi wengine wengi waaminifu wa Yehova, anaweza kuwa na zoea la kusoma kila chapisho jipya kabla ya kuliweka kwenye maktaba yake. Tunapoonyesha unyenyekevu na uthamini kwa kusoma na kujifunza machapisho yetu yanayotegemea Biblia, tutafanya maendeleo ya kiroho, na Yehova ataweza kututumia kwa ukamili zaidi katika utumishi wake.​—Ebr. 5:13, 14.

10. Tunaweza kuonyeshaje mtazamo wa aliye mdogo zaidi kutanikoni?

10 Mtu anayejiendesha kama aliye mdogo zaidi ni “mkuu” katika njia nyingine. Kila kutaniko lina wanaume wenye sifa za kustahili waliowekwa rasmi chini ya mwongozo wa roho takatifu ya Yehova ili watumike wakiwa wazee. Wanapanga mambo ya kiroho kama vile mikutano ya kutaniko, utumishi wa shambani, na uchungaji. Tunapoonyesha mtazamo wa aliye mdogo zaidi kwa kuunga mkono kwa hiari mipango hiyo, tunachangia furaha, amani, na umoja kutanikoni. (Soma Waebrania 13:7, 17.) Ikiwa unatumika ukiwa mzee au mtumishi wa huduma, je, humshukuru Yehova kwa unyenyekevu kwa kukukabidhi pendeleo hilo la utumishi?

11, 12. Ni mtazamo gani utakaotufanya tuwe wenye thamani zaidi katika tengenezo la Yehova, na kwa nini inakuwa hivyo?

11 Mtu anayejiendesha kama aliye mdogo zaidi ni “mkuu,” au ana thamani zaidi katika tengenezo la Yehova kwa sababu unyenyekevu wake unamfanya awe mtumishi muhimu wa Mungu. Yesu alilazimika kuwashauri wanafunzi wake wajiendeshe kama walio wadogo zaidi kwa sababu baadhi yao waliathiriwa na roho iliyokuwa imeenea wakati huo. Andiko la Luka 9:46 linasema hivi: “Wakaanza kujadiliana kati yao kuhusu ni nani angekuwa mkuu zaidi kati yao.” Je, tunaweza pia kuanza kufikiri kwamba kwa njia fulani sisi ni bora kuliko waamini wenzetu au sisi ni bora kuliko watu wengine kwa ujumla? Watu wengi katika ulimwengu unaotuzunguka wanachochewa na kiburi na uchoyo. Acheni tuepuke kabisa kiburi kwa kutenda kwa unyenyekevu. Tukifanya hivyo na kutanguliza mapenzi ya Yehova, tutawaburudisha zaidi ndugu na dada zetu.

12 Shauri la Yesu kwamba tujiendeshe kama walio wadogo zaidi linatuchochea kwelikweli. Je, hatupaswi kujitahidi kuonyesha roho ya aliye mdogo zaidi katika sehemu zote za maisha yetu? Acheni tukazie uangalifu sehemu tatu za maisha yetu.

JITAHIDI KUWA ALIYE MDOGO ZAIDI

13, 14. Mke au mume anapaswa kujiendesha kama aliye mdogo jinsi gani, na hilo linaweza kuimarishaje ndoa?

13 Katika ndoa. Watu wengi leo wanahangaikia sana haki zao hivi kwamba wanadai haki hizo hata kama wataingilia haki za wengine. Hata hivyo, mtu aliye mdogo zaidi anaongozwa na mtazamo ambao Paulo anatutia moyo kuwa nao. Katika barua yake kwa Waroma, anaandika hivi: “Na tufuatilie mambo yanayofanya kuwe na amani na mambo ambayo ni ya kujengana.” (Rom. 14:19) Mtu anayejiendesha kama aliye mdogo zaidi hufuatilia amani na kila mtu, hasa mwenzi wake wa ndoa anayemthamini sana.

14 Fikiria burudani. Wenzi wa ndoa wanaweza kuwa na mapendezi tofauti inapohusu burudani. Huenda mume anapenda kusoma kitabu anapopumzika nyumbani. Kwa upande mwingine, huenda mke anafurahia kula chakula kwenye mkahawa au kuwatembelea marafiki. Je, si rahisi zaidi kwa mke kumheshimu mumewe akiona kwamba anaonyesha unyenyekevu na kufikiria kwa unyoofu mambo yanayompendeza na yasiyompendeza mke wake badala ya kukazia fikira mapendezi yake mwenyewe? Naye mume atampenda na kumthamini sana mke wake akiona kwamba mke hajaribu kumlazimisha kufanya atakacho bali anafikiria mapendezi ya mume wake. Kifungo cha ndoa huimarika wakati kila mmoja katika ndoa anapojiendesha kama aliye mdogo zaidi.​—Soma Wafilipi 2:1-4.

15, 16. Katika Zaburi ya 131, Daudi alitutia moyo tuwe na mtazamo gani, na hilo linapaswa kutuchochea kujiendesha namna gani kutanikoni?

15 Kutanikoni. Katika ulimwengu, watu wengi huhangaikia tu kutosheleza tamaa zao papo hapo. Watu hao hawana subira na wanachukia kungoja. Kusitawisha roho ya aliye mdogo zaidi hutusaidia kumngojea Yehova. (Soma Zaburi 131:1-3.) Tutapata usalama na baraka, faraja na uradhi tukiwa wanyenyekevu na kumngojea Yehova. Ndiyo maana Daudi aliwatia moyo Waisraeli wenzake wamngojee Mungu wao kwa subira!

16 Unaweza kupata faraja kama hiyo ukimngojea Yehova kwa unyenyekevu. (Zab. 42:5) Huenda ‘unatamani kazi njema,’ na hivyo, ‘unajitahidi kufikia cheo cha mwangalizi.’ (1 Tim. 3:1-7) Bila shaka, unapaswa kujitahidi kadiri uwezavyo kuiruhusu roho takatifu ikuze ndani yako sifa unazohitaji ili kuwa mwangalizi. Lakini namna gani ikiwa muda mrefu zaidi umepita na hujapendekezwa huku wenzako wakipendekezwa? Mtu aliye mdogo zaidi, anayengojea kwa subira pendeleo la utumishi, ataendelea kumtumikia Yehova kwa shangwe na atafurahia mgawo wowote anaopewa.

17, 18. (a) Tunafaidikaje tunapoomba msamaha na kuwa tayari kuwasamehe wengine? (b) Andiko la Methali 6:1-5 linatutia moyo tufanye nini?

17 Katika mahusiano yetu na wengine. Ni vigumu kwa watu wengi leo kuomba msamaha. Hata hivyo, watumishi wa Mungu husitawisha roho ya aliye mdogo zaidi kwa kukubali makosa yao na kuomba msamaha. Wako tayari pia kuwasamehe wengine wanaowakosea. Kiburi huleta migawanyiko na mashindano, lakini kusameheana hudumisha amani kutanikoni.

18 Huenda tukahitaji ‘kujinyenyekeza’ na kumwomba msamaha kutoka moyoni mtu mwingine wakati tunapokosa kutimiza ahadi yetu kwa sababu ya hali zisizoepukika. Ingawa anaweza kuwa na sababu ya kumlaumu mtu mwingine, Mkristo aliye mnyenyekevu hukazia fikira udhaifu wake mwenyewe na yuko tayari kukubali makosa yake.​—Soma Methali 6:1-5.

19. Ni kwa nini kila mmoja wetu anapaswa kuthamini shauri la Biblia la kujiendesha kama aliye mdogo zaidi?

19 Tunashukuru kama nini kwamba Maandiko yanatutia moyo tusitawishe roho ya aliye mdogo zaidi! Ingawa nyakati nyingine huenda ikawa vigumu kwetu kuonyesha roho hiyo, kuwa na maoni yanayofaa kuhusu hali yetu tunapoilinganisha na ukuu wa Muumba wetu, na kuuthamini unyenyekevu wake kunaweza kutuchochea kusitawisha sifa hiyo nzuri. Tukifanya hivyo, bila shaka, tutathibitika kuwa watumishi wa Yehova wenye thamani zaidi. Basi, acheni kila mmoja wetu ajiendeshe kama aliye mdogo zaidi.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Majina yamebadilishwa.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16]

Yehova anatuheshimu kwa kutupatia pendeleo la kuhubiri habari njema

[Picha katika ukurasa wa 19]

Una fursa zipi za kujiendesha kama aliye mdogo zaidi?