Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Ujiendeshe Kama Aliye Mudogo Zaidi

Ujiendeshe Kama Aliye Mudogo Zaidi

Ujiendeshe Kama Aliye Mudogo Zaidi

‘Anayejiendesha kama aliye mudogo zaidi kati yenu nyote ndiye aliye mukubwa.’​—LU. 9:48.

UNAWEZA KUJIBU?

Ni nini itatusaidia kujiendesha kama aliye mudogo zaidi?

Ni katika njia gani yule aliye mudogo zaidi ndiye aliye ‘mukubwa’?

Namna gani tunaweza kuonyesha unyenyekevu katika maisha ya ndoa, katika kutaniko, na katika uhusiano wetu na wengine?

1, 2. Yesu aliwapa mitume wake shauri gani, na kwa nini alifanya hivyo?

 TUKO katika mwaka wa 32. Yesu anapatikana katika wilaya ya Galilaya. Kunatokea matatizo fulani. Mitume wake fulani wanaanza kubishana ili kujua ni nani kati yao aliye mukubwa. Luka anaripoti hivi: “Ndipo wakaanza kujadiliana kati yao kuhusu ni nani angekuwa mukubwa zaidi kati yao. Yesu, akijua mawazo ya mioyo yao, akachukua mutoto muchanga, akamuweka kando yake na kuwaambia: ‘Yeyote yule anayemupokea mutoto huyu muchanga kwa musingi wa jina langu ananipokea mimi pia, na yeyote anayenipokea, anamupokea pia yule aliyenituma. Kwa maana anayejiendesha kama aliye mudogo zaidi kati yenu nyote ndiye aliye mukubwa.’” (Lu. 9:46-48) Yesu aliwavumilia mitume wake, lakini aliwaambia waziwazi kama walipaswa kuwa wanyenyekevu.

2 Je, shauri la Yesu la kujiendesha kama aliye mudogo zaidi lilipatana na maoni ya watu wa wakati huo? Ao je, watu wa wakati huo walikuwa na maoni tofauti? Kinapozungumuzia hali za watu wa wakati huo, kitabu kimoja kinasema hivi: “Katika kila jambo, kila mutu alitaka kujua ni nani aliyekuwa mukubwa na kila mutu alihangaikia heshima yake.” Yesu aliwashauri mitume wake wasiwe kama watu wa wakati huo.

3. (a) Kujiendesha kama aliye mudogo zaidi kunamaanisha nini, na sababu gani ni vigumu kufanya hivyo? (b) Kujiendesha kama aliye mudogo zaidi kunatokeza maulizo gani?

3 Neno la Kigiriki linalotafsiriwa ‘mudogo zaidi’ linamaanisha mutu munyenyekevu, mwenye kiasi, mwenye kujishusha, asiyejiona kuwa maana sana, ao asiye na roho ya kuwatawala wengine. Yesu aliwaonyesha mitume wake mutoto mudogo ili kuwafundisha waziwazi kwamba wanapaswa kuwa wanyenyekevu na wenye kiasi. Shauri hilo la Yesu kwa Wakristo wa kwanza linatuhusu sisi pia leo. Wakati fulani inaweza kuwa vigumu kwetu kujiendesha kama walio wadogo zaidi. Muelekeo wa wanadamu wa kuwa na kiburi unaweza kutuchochea tutafute kujionyesha. Roho ya mashindano iliyo katika ulimwengu tunamoishi inaweza kutufanya tuanze kujipenda wenyewe, kupenda mabishano, ao kuwatawala wengine. Ni nini itatusaidia kujiendesha kama aliye mudogo zaidi? Namna gani yule ‘aliye mudogo zaidi kati yetu ndiye aliye mukubwa’? Tunapaswa kujikaza kuwa wanyenyekevu katika mambo gani?

“LO! JINSI KILIVYO KINA CHA UTAJIRI WA MUNGU NA HEKIMA NA UJUZI!”

4, 5. Ni nini inayoweza kutusaidia kuwa wanyenyekevu? Toa mufano.

4 Njia moja ya kutusaidia kuwa wanyenyekevu ni kufikiria sana ukubwa wa Yehova. Kwa kweli, “haiwezekani kuchunguza kikamilifu uelewaji wake.” (Isa. 40:28) Alipozungumuzia mambo fulani kuhusu utukufu wa Yehova, mutume Paulo aliandika hivi: “Lo! Jinsi kilivyo kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi! Jinsi hukumu zake zisivyochunguzika na njia zake zisivyotafutika!” (Rom. 11:33) Paulo aliandika maneno hayo miaka 2 000 hivi iliyopita, kuanzia wakati huo ujuzi wa wanadamu wamejifunza mambo mengi sana, hata hivyo maneno hayo yangali ya kweli mupaka leo. Hata ikiwa tumejua mambo mengi kadiri gani, tunapaswa kuwa wanyenyekevu kwa sababu kujifunza kuhusu Yehova, kazi zake, na njia zake hakutakuwa na mwisho.

5 Kujua kama kungali mambo mengi ya kujifunza kulimusaidia Leon * awe munyenyekevu. Akiwa kijana, Leon alifurahia sana sayansi. Kwa sababu alitaka kujua mambo mengi kadiri angeweza kuhusu ulimwengu unaotuzunguka, Leon aliamua kujifunza astronomia (masomo ya vitu vya anga) na alifikia kutambua jambo moja la maana. Yeye alisema hivi: “Nilipofikiria mambo niliyojifunza, nilianza kutambua kama sayansi pekee haiweze kuwasaidia wanadamu kuelewa ulimwengu vizuri. Kwa hiyo, niliamua kujifunza sheria.” Kisha, Leon alikuwa mwanasheria na baadaye muamuzi. Wakati huo, yeye na bibi yake walijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, waliikubali kweli, na wakabatizwa. Hata ikiwa alisoma masomo mengi, ni nini iliyomusaidia Leon ajiendeshe kama aliye mudogo zaidi? Bila kusita, anajibu hivi: “Ni kujua kama hata tujifunze mambo mengi kadiri gani kumuhusu Yehova na ulimwengu, hatuwezi kujua mambo yote.”

6, 7. (a) Yehova anatutolea mufano gani muzuri wa unyenyekevu? (b) Namna gani unyenyekevu wa Mungu unaweza kumufanya mutu kuwa ‘mukubwa’?

6 Kukumbuka kwamba Yehova pia ni munyenyekevu ni jambo lingine linalotusaidia kuwa wanyenyekevu. Fikiria jambo hili: “Sisi ni wafanyakazi wenzi wa Mungu.” (1 Kor. 3:9) Fikiri kidogo! Yehova, Mungu aliye mukubwa zaidi, anatuheshimu kwa kutupa pendeleo la kuhubiri habari njema kwa kutumia Neno lake, Biblia. Yehova ndiye anayefanya mbegu zikomae, hata hivyo anatupa pendeleo la kutumika pamoja naye. (1 Kor. 3:6, 7) Kwa kufanya hivyo, Mungu anatuwekea mufano muzuri wa unyenyekevu, sivyo? Kwa kweli mufano wa Mungu wa unyenyekevu unatutia moyo ili tujiendeshe kama aliye mudogo zaidi.

7 Unyenyekevu wa Mungu ulimutia moyo mutunga​-zaburi Daudi. Yeye alimuimbia Yehova hivi: ‘Utanipa ngao yako ya wokovu, na unyenyekevu wako ndio hunifanya niwe mukubwa.’ (2 Sam. 22:36) Daudi alijua kama ikiwa aliweza kufanya mambo mengi makubwa katika Israeli ni kwa sababu Yehova alimutendea kwa unyenyekevu kwa kumuchagua na kumusaidia. (Zab. 113:5-7) Namna gani sisi? Tukifikiria sifa, uwezo, ao mapendeleo mbalimbali tuliyonayo, je, kuna jambo ambalo ‘hatukupokea’ kutoka kwa Yehova? (1 Kor. 4:7) Mutu anayejiendesha kama aliye mudogo zaidi ni ‘mukubwa’ kwa sababu unyenyekevu unamufanya awe na samani machoni pa Yehova. (Lu. 9:48) Namna gani? Acheni tuone.

‘ALIYE MUDOGO ZAIDI KATI YENU NDIYE ALIYE MUKUBWA’

8. Unyenyekevu unatusaidia tuone tengenezo la Yehova namna gani?

8 Unyenyekevu unatusaidia kufurahia tengenezo la Mungu na kutegemeza mipango ya kutaniko. Kwa mufano, fikiria Petra, mwanamuke kijana aliyekomalia katika jamaa ya Kikristo. Petra alitaka kujiongoza maishani, kwa hiyo aliacha kutaniko. Miaka fulani baadaye, alianza tena kushirikiana na kutaniko. Sasa anafurahia kuwa katika tengenezo la Yehova na iko tayari kutegemeza mipango ya kutaniko. Ni nini ilimusaidia kubadili maoni yake? Petra anaandika hivi: “Ili nifurahie tengenezo la Mungu nilipaswa kuonyesha sifa mbili za maana sana ambazo ni unyenyekevu na kiasi.”

9. Mutu munyenyekevu anaona namna gani chakula cha kiroho, na sababu gani hilo linamufanya kuwa mutu wa maana sana?

9 Mutu munyenyekevu anafurahia mambo yote ambayo Yehova anatutolea, kutia ndani chakula cha kiroho. Mutu huyo anajifunza Biblia kwa bidii na anasoma magazeti yote ya Munara wa Mulinzi na Amkeni! Kama vile watumishi wengine waaminifu wa Yehova, anajiwekea muradi wa kusoma kwa ukawaida kila kichapo kipya mbele ya kukiweka katika kabati lake la vitabu. Tunapoonyesha unyenyekevu kwa kufurahia kusoma na kujifunza vichapo vyetu vinavyotegemea Biblia, tutafanya maendeleo ya kiroho, na Yehova atatupatia mapendeleo zaidi katika kazi yake.​—Ebr. 5:13, 14.

10. Namna gani tunaweza kujiendesha kama aliye mudogo zaidi katika kutaniko?

10 Mutu anayejiendesha kama aliye mudogo zaidi ni ‘mukubwa’ katika njia nyingine. Katika kila kutaniko kuna wanaume wanaochaguliwa kuwa wazee kupitia uongozi wa roho takatifu ya Yehova. Wazee wanapanga mambo ya kiroho kama vile mikutano ya kutaniko, mahubiri, na ziara za uchungaji. Tunapojiendesha kama aliye mudogo zaidi kwa kutegemeza mipango hiyo, hilo linaleta furaha, amani, na umoja katika kutaniko. (Soma Waebrania 13:7, 17.) Ikiwa wewe ni muzee ao mutumishi wa huduma, je, unamushukuru Yehova kwa pendeleo hilo?

11, 12. Ni sifa gani itakayotufanya tuwe watu wa maana sana katika tengenezo la Yehova, na sababu gani sifa hiyo ni ya maana sana?

11 Mutu anayejiendesha kama aliye mudogo zaidi ni ‘mukubwa’ kwa sababu unyenyekevu wake unamufanya awe mutumishi muzuri wa Yehova na Yehova anamutumia. Yesu aliwashauri wanafunzi wake wajiendeshe kama walio wadogo zaidi kwa sababu wengine kati yao walikuwa na maoni yaliyoenea sana ya wakati huo. Andiko la Luka 9:46 linasema kwamba wanafunzi ‘walianza kujadiliana kuhusu ni nani angekuwa mukubwa zaidi kati yao.’ Je, sisi pia tumeanza kufikiri kwamba katika njia fulani tunawashinda ndugu na dada zetu ao kwamba tunawashinda watu wengine? Watu wengi tunaoishi nao wanatenda kwa kiburi na wanatafuta tu faida yao. Acheni tusiwe kama wao kwa kutenda kwa unyenyekevu. Ikiwa tunafanya hivyo na kutia kazi ya Yehova pa nafasi ya kwanza, ndugu na dada zetu watatiwa moyo na watafurahia kuwa marafiki wetu.

12 Kwa kweli shauri la Yesu la kujiendesha kama aliye mudogo zaidi ni lenye kutia moyo. Tunapaswa kujikaza kujiendesha kama aliye mudogo zaidi katika sehemu zote za maisha yetu. Acheni tuzungumuzie sehemu tatu.

UJIKAZE KUJIENDESHA KAMA ALIYE MUDOGO ZAIDI

13, 14. Namna gani bibi ao bwana anaweza kujiendesha kama aliye mudogo zaidi, na kufanya hivyo kunaweza kuisaidia ndoa namna gani?

13 Katika maisha ya ndoa. Wengi leo wanahangaikia tu haki zao, bila kujali haki za wengine. Lakini mutu anayejiendesha kama aliye mudogo zaidi, anaongozwa na mashauri ambayo mutume Paulo alitutia moyo tufuate. Katika barua yake kwa Waroma, Paulo aliandika hivi: “Na tufuatilie mambo yanayofanya kuwe na amani na mambo ambayo ni ya kujengana.” (Rom. 14:19) Mutu anayejiendesha kama aliye mudogo zaidi anaendelea kufanya amani pamoja na kila mutu na zaidi sana pamoja na bibi ao bwana yake anayemupenda.

14 Fikiria viburudisho. Bibi na bwana wanaweza kuwa na maoni yanayotofautiana juu ya viburudisho. Labda bwana anafurahia kubaki nyumbani na kusoma kitabu wakati wa mapumuziko, lakini bibi yake anafurahia kuenda kula kwenye restora ao kuwatembelea marafiki. Ikiwa bwana ni munyenyekevu na anamufikiria bibi yake kuliko kujifikiria tu, bibi yake atamuheshimu kabisa kwa urahisi. Pia, ikiwa bibi anamufikiria bwana yake na hatafute tu kupata mambo anayotaka, bwana yake atamupenda na kumufurahia. Ndoa yao itakuwa nzuri sana wakati kila mumoja anajiendesha kama aliye mudogo zaidi.—Soma Wafilipi 2:1-4.

15, 16. Daudi anatutia moyo kufanya nini katika Zaburi 131, na namna gani tunaweza kufanya hivyo katika kutaniko?

15 Katika kutaniko. Katika ulimwengu watu wengi wanataka wapate mambo wanayohitaji bila kungojangoja. Wanakosa uvumilivu na wanaona kuwa vigumu kungojea. Kujiendesha kama aliye mudogo zaidi kunatusaidia kumungojea Yehova. (Soma Zaburi 131:1-3.) Ikiwa tuko wanyenyekevu, tutapata baraka, tutajisikia salama, tutakuwa wenye kutulia na wenye kutosheka. Daudi alijua hilo, kwa hiyo aliwatia moyo Waisraeli waendelee kumungojea Yehova!

16 Wewe pia unaweza kujisikia mwenye kutulia unapomungojea Yehova. (Zab. 42:5) Labda ‘unajitahidi kufikia cheo cha mwangalizi’ kwa sababu ‘unatamani kazi njema.’ (1 Tim. 3:1-7) Kwa kweli, unapaswa kufanya kulingana na uwezo wako ili roho takatifu ikusaidie kutimiza sifa zinazoombwa ili kuwa muzee. Lakini namna gani ikiwa miaka mingi inapita na bado haujakuwa muzee? Mutu anayejiendesha kama aliye mudogo zaidi, atangojea kwa uvumilivu pendeleo la utumishi na ataendelea kumutumikia Yehova kwa furaha katika mugawo wowote ambao amepewa.

17, 18. (a) Tunaweza kupata faida gani ikiwa tunaomba musamaha na ikiwa tuko tayari kuwasamehe wengine? (b) Andiko la Methali 6:1-5 linatutia moyo kufanya nini?

17 Katika uhusiano wetu na wengine. Watu wengi wanaona kuwa jambo ngumu kuomba musamaha. Hata hivyo, watumishi wa Yehova wanajiendesha kama walio wadogo zaidi kwa kukubali makosa yao na kuomba musamaha. Pia wako tayari kusamehe wengine. Kiburi kinaleta mugawanyiko na kutoelewana, lakini kusamehe wengine kunaleta amani katika kutaniko.

18 Ikiwa tulifanya mapatano na mutu fulani, na kisha tukashindwa kutimiza mapatano yetu kwa sababu fulani, ni lazima ‘tujinyenyekeze’ kwa kumuomba kabisa musamaha. Labda si kosa letu kabisa, lakini Mukristo munyenyekevu anatambua na kukubali kwamba yeye pia ana uzaifu fulani.—Soma Methali 6:1-5.

19. Sababu gani kila mumoja wetu anapaswa kufurahia shauri la Biblia la kujiendesha kama aliye mudogo zaidi?

19 Tunafurahi sana kwa sababu Biblia inatutia moyo tujiendeshe kama walio wadogo zaidi! Wakati fulani inaweza kuwa vigumu kwetu kufanya hivyo, lakini ikiwa tunafikiri namna Yehova alivyo mukubwa zaidi kuliko sisi, tutafurahia unyenyekevu wake na hilo litatuchochea kuonyesha sifa hiyo nzuri. Tukifanya hivyo, tutakuwa watu wa maana sana machoni pa Yehova. Kwa hiyo, acheni kila mumoja wetu ajiendeshe kama aliye mudogo zaidi.

[Maelezo ya chini]

^ Majina yamebadilishwa.

[Maulizo ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16]

Yehova anatuheshimu sana kwa kutupa pendeleo la kuhubiri habari njema

[Picha katika ukurasa wa 19]

Unaweza kujiendesha kama aliye mudogo zaidi katika hali gani?