Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka Kwa Wasomaji

Maswali Kutoka Kwa Wasomaji

Maswali Kutoka Kwa Wasomaji

Je, maneno ya Yesu katika Mathayo 19:10-12 yanamaanisha kwamba wale wanaoamua kubaki waseja wamepewa zawadi ya useja kimuujiza?

▪ Fikiria hali zilizomfanya Yesu azungumzie useja. Mafarisayo walipomjia na kumuuliza kuhusu talaka, Yesu alitaja wazi kiwango cha Yehova kuhusu ndoa. Ingawa Sheria ilimruhusu mwanamume kumwandikia mke wake cheti cha talaka kwa sababu amepata “kitu fulani kisichofaa” katika mke huyo, hali haikuwa hivyo kutoka mwanzo. (Kum. 24:1, 2) Kisha Yesu akasema hivi: “Mtu yeyote anayemtaliki mke wake na kumwoa mwingine, ila kwa sababu ya uasherati, anafanya uzinzi.”​—Mt. 19:3-9.

Waliposikia maneno hayo, wanafunzi wa Yesu walisema hivi: “Ikiwa hivyo ndivyo ilivyo kati ya mwanamume na mke wake, ni afadhali kutooa.” Yesu akawajibu hivi: “Si watu wote wanaolipa nafasi neno hilo, ila tu wale walio na hiyo zawadi. Kwa maana kuna matowashi waliozaliwa namna hiyo kutoka katika tumbo la uzazi la mama yao, na kuna matowashi waliofanywa matowashi na watu, na kuna matowashi ambao wamejifanya wenyewe matowashi kwa sababu ya ufalme wa mbinguni. Yule anayeweza kulipa nafasi na alipe nafasi.”​—Mt. 19:10-12.

Matowashi halisi ni wale waliozaliwa wakiwa na kasoro hiyo au wale waliopata kasoro hiyo kiaksidenti au kwa kuhasiwa. Hata hivyo, kulikuwa pia na wale walioamua kwa hiari yao wenyewe kuwa matowashi. Ingawa walikuwa huru kufunga ndoa, walijizuia na kubaki waseja “kwa sababu ya ufalme wa mbinguni.” Kama Yesu, walichagua kubaki waseja ili waweze kujitoa kabisa kufanya kazi ya Ufalme. Hawakuzaliwa wakiwa na zawadi ya useja wala hawakupewa zawadi hiyo. Waliupa nafasi useja. Yaani, walipata zawadi hiyo kwa kutaka.

Kwa msingi wa maneno ambayo Yesu alisema, mtume Paulo alieleza kwamba ingawa Wakristo wote, waseja na waliofunga ndoa wanaweza kumtumikia Mungu kwa njia inayokubalika, waseja ambao ‘wametulia katika moyo wao’ kuhusu hali yao ‘wanafanya vema.’ Jinsi gani? Watu waliofunga ndoa lazima pia watenge wakati na kutumia nguvu zao kuwafurahisha na kuwatunza wenzi wao wa ndoa. Kwa upande mwingine, Wakristo waseja wanaweza kujitoa kabisa katika utumishi wa Bwana bila kuwa na daraka hilo. Wanaiona hali yao kuwa “zawadi” kutoka kwa Mungu​.—1 Kor. 7:7, 32-38.

Kwa hiyo, Maandiko hayatuambii kwamba Mkristo hupata zawadi ya useja kimuujiza. Badala yake, anaisitawisha kwa kubaki bila kufunga ndoa ili aendeleze masilahi ya Ufalme bila kukengeushwa. Wengi leo wameazimia moyoni mwao kubaki waseja kwa sababu hiyo, na wengine wanafanya vyema kwa kuwatia moyo.