Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Ulikuwa Ujumbe Bora Zaidi Uliowahi Kusikiwa’

‘Ulikuwa Ujumbe Bora Zaidi Uliowahi Kusikiwa’

Kutoka Katika Hifadhi Ya Vitu Vyetu Vya Kale

‘Ulikuwa Ujumbe Bora Zaidi Uliowahi Kusikiwa’

“YOTE hayo ni ya nini?” akauliza George Naish, huku akinyooshea kidole rundo la magogo yenye urefu wa mita 18 yaliyowekwa katika ghala lililotumiwa kuhifadhi vifaa vya kivita huko Saskatoon, Saskatchewan, Kanada. Aliambiwa kwamba magogo hayo yalitumiwa kujengea minara ya kutolea ishara wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Baadaye Ndugu Naish alisema hivi: “Niliona kwamba tungeweza kutumia magogo hayo kujengea minara ya redio, na hivyo ndivyo wazo la kuwa na stesheni ya redio ya kitheokrasi lilivyoanza.” Mwaka mmoja tu baadaye, mnamo 1924, stesheni ya CHUC ilianza kurusha matangazo hewani. Ilikuwa mojawapo ya stesheni za kwanza za redio kutangaza mambo ya kidini nchini Kanada.

Nchi ya Kanada ambayo ni kubwa kama Bara la Ulaya, ilikuwa eneo zuri sana la kutoa ushahidi kupitia redio. “Kupitia vipindi vyetu vya redio, kweli iliwafikia watu wengi ambao tusingeweza kuzungumza nao kibinafsi,” akasema Florence Johnson, aliyefanya kazi kwenye stesheni hiyo huko Saskatoon. “Kuwa na redio wakati huo lilikuwa jambo jipya, hivyo, watu walikuwa na hamu ya kusikiliza chochote kilichotangazwa katika redio.” Kufikia mwaka 1926, Wanafunzi wa Biblia (kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo) walikuwa wakiendesha stesheni zao wenyewe za redio katika miji minne ya Kanada. *

Ungesikia nini ikiwa ungesikiliza stesheni hizo za redio? Mara nyingi waimbaji kutoka katika makutaniko yaliyo katika maeneo ya karibu waliimba nyimbo wakiambatana na wapiga ala za muziki au hata vikundi vidogo vya okestra. Bila shaka, akina ndugu walitoa pia hotuba na kuongoza mazungumzo ya Biblia. Amy Jones, aliyeshiriki katika mazungumzo hayo, alikumbuka hivi: “Tukiwa katika huduma ya shambani, nilijitambulisha na pindi fulani mwenye nyumba alisema, ‘Ah, ni sawa, nimekusikia kwenye redio.’”

Wanafunzi wa Biblia katika Halifax, Nova Scotia, walitumia njia mpya kwenye redio, walifanya kipindi cha mazungumzo kilichowaruhusu wasikilizaji kupiga simu ili kuuliza maswali ya Biblia. “Itikio la watu lilikuwa zuri sana katika vipindi hivyo,” akaandika ndugu mmoja. “Simu zilizopigwa zilikuwa nyingi kupindukia.”

Kama ilivyokuwa katika siku za mtume Paulo, watu waliitikia ujumbe wa Wanafunzi wa Biblia kwa njia tofauti-tofauti. (Mdo. 17:1-5) Baadhi ya wasikilizaji waliupenda ujumbe wao. Kwa mfano, Hector Marshall alipowasikia Wanafunzi wa Biblia wakitaja katika redio mabuku ya Studies in the Scriptures, aliagiza mabuku sita. Aliandika hivi baadaye: “Nilifikiri kwamba vitabu hivyo vingenisaidia kufundisha shule ya Jumapili.” Hata hivyo, Hector alipomaliza kusoma Buku la Kwanza, aliamua kuacha kanisa lake. Akawa mweneza-injili mwenye bidii na alimtumikia Yehova kwa uaminifu mpaka alipokufa katika mwaka wa 1998. Mashariki mwa Nova Scotia, siku moja baada ya hotuba yenye kichwa, “Ufalme, Tumaini la Ulimwengu” kutolewa kupitia redio, Kanali J. A. MacDonald alimwambia hivi ndugu mmoja mwenyeji: “Watu wa Kisiwa cha Cape Breton walisikia jana ujumbe bora zaidi kuwahi kusikiwa katika sehemu hii ya ulimwengu.”

Hata hivyo, makasisi walikasirika. Wakatoliki fulani huko Halifax walitishia kulipua stesheni iliyokuwa ikitangaza vipindi vya Wanafunzi wa Biblia. Mnamo mwaka 1928, serikali ikishinikizwa na viongozi wa kidini ilitangaza kwa ghafla kwamba haingetoa tena vibali kwa stesheni zilizomilikiwa na Wanafunzi wa Biblia. Kwa sababu hiyo, ndugu na dada waligawanya trakti yenye kichwa Ni nani Anayemiliki Hewa? Trakti hiyo ilikuwa na ujumbe uliopinga hatua hiyo isiyo na haki. Hata hivyo, maofisa wa serikali walikataa kuwapa Wanafunzi wa Biblia vibali vya kuendelea kutoa ushahidi kupitia redio.

Je, jambo hilo lilipunguza bidii ya kikundi hicho kidogo cha watumishi wa Yehova nchini Kanada? Isabel Wainwright alikiri hivi: “Mwanzoni, bila shaka ilionekana kwamba adui amepata ushindi mkubwa. Lakini nilijua kwamba Yehova angemzuia adui ikiwa jambo hilo lingepatana na kusudi lake. Kwa hiyo, ilimaanisha kwamba tulipaswa kuanza kutumia njia nyingine inayofaa zaidi ya kutangaza habari njema ya Ufalme.” Badala ya kutegemea kabisa redio ili kutoa ushahidi, Wanafunzi wa Biblia nchini Kanada walianza kukazia fikira kuwatembelea watu katika nyumba zao. Hata hivyo, wakati redio ilipokuwa ikitumiwa, bila shaka ilisaidia sana katika kutangaza ‘ujumbe bora zaidi uliowahi kusikiwa.’​—Kutoka katika hifadhi ya vitu vyetu vya kale nchini Kanada.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Ili kutoa ushahidi kupitia redio, ndugu huko Kanada walilipa stesheni nyingine za redio ili watangaze ujumbe wa Biblia.

[Blabu katika ukurasa wa 32]

“Simu zilizopigwa zilikuwa nyingi kupindukia”

[Picha katika ukurasa wa 32]

(1) Stesheni ya redio huko Edmonton, Alberta (2) Ndugu akishughulikia mitambo ya redio huko Toronto, Ontario (3) Studio ya CHUC huko Saskatoon, Saskatchewan