Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Sababu Gani Mungu Alimutuma Yesu Duniani?

Sababu Gani Mungu Alimutuma Yesu Duniani?

Neno La Mungu Linafundisha Nini?

Sababu Gani Mungu Alimutuma Yesu Duniani?

Habari hii inazungumuzia maulizo fulani ambayo labda umekwisha kujiuliza na inaonyesha mahali ambapo unaweza kupata majibu katika Biblia yako. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia upate majibu ya maulizo hayo.

1. Yesu alikuwa wapi mbele Mungu amutume duniani?

Yesu aliishi mbinguni akiwa mutu wa roho mbele ya kuzaliwa huko Bethlehemu. Yeye ndiye aliumbwa kwanza na Mungu na ni yeye tu ndiye Mungu aliumba moja kwa moja. Kwa hiyo, Yesu anaitwa kwa kufaa Mwana muzaliwa-pekee wa Mungu. Huko mbinguni, alizungumuza mara nyingi akiwa muwakilishi wa Mungu. Ndiyo sababu anaitwa Neno. Pia, alitenda akiwa musaidizi wa Mungu na alisaidia katika kuumba vitu vingine vyote. (Yohana 1:2, 3, 14) Yesu aliishi pamoja na Mungu huko mbinguni kwa miaka mingi sana mbele ya kuumbwa kwa wanadamu.​—Soma Mika 5:2; Yohana 17:5.

2. Namna gani Mungu alimutuma Mwana wake duniani?

Yehova alihamisha uzima wa Yesu toka mbinguni na kuutia katika tumbo la Maria kwa njia ya roho takatifu. Kwa hiyo, Yesu alizaliwa bila musaada wa baba wa kibinadamu. Malaika walijulisha wachungaji fulani juu ya kuzaliwa kwa Yesu, wachungaji hao walikuwa inje usiku wakichunga makundi yao. (Luka 2:8-12) Hivyo, Yesu hakuzaliwa katika majira ya baridi kali, lakini inawezekana alizaliwa mwanzoni mwa Mwezi wa 10, wakati hali ya hewa haikuwa yenye baridi. Kisha wakati fulani, Maria na bwana yake, Yosefu, walimupeleka Yesu nyumbani kwao huko Nazareti na wakamulea huko. Yosefu alimulea Yesu kama baba yake mulezi.​—Soma Mathayo 1:18-23.

Yesu alipokuwa na miaka karibu 30, alibatizwa, na Mungu akatangaza waziwazi kwamba Yesu ni Mwana wake. Kisha, Yesu alianza kazi ambayo Mungu alimutuma afanye.​—Soma Mathayo 3:16, 17.

3. Sababu gani Mungu alimutuma Yesu duniani?

Mungu alimutuma Yesu ili kufundisha watu kweli. Yesu alifundisha juu ya Ufalme wa Mungu, serikali ya mbinguni ambayo italeta amani duniani pote. Alitolea watu tumaini la uzima wa milele. (Yohana 4:14; 18:36, 37) Pia, Yesu alifundisha watu mambo mengi juu ya namna ya kupata furaha ya kweli. (Mathayo 5:3; 6:19-21) Alifundisha kupitia mufano wake. Kwa mufano, alionyesha namna ya kufanya mapenzi ya Mungu hata katika hali ngumu. Alipotendewa vibaya, hakulipiza kisasi.​—Soma 1 Petro 2:21-24.

Yesu aliwafundisha wafuasi wake upendo wa kujizabihu ao kujitoa. Aliishi pamoja na Baba yake huko mbinguni na alikuwa na mapendeleo mengi ya pekee, hata hivyo alimutii Baba yake kwa unyenyekevu na akaja duniani kuishi pamoja na wanadamu. Hakuna mutu mwengine ambaye angetuonyesha mufano muzuri zaidi wa upendo kuliko Yesu.​—Soma Yohana 15:12, 13; Wafilipi 2:5-8.

4. Yesu alitimiza nini kupitia kifo chake?

Pia, Mungu alimutuma Yesu ili afe kwa ajili ya zambi zetu. (Yohana 3:16) Sisi wote ni watenda-zambi, ni kusema kwamba sisi ni watu wasio wakamilifu na wenye zambi. Ndiyo sababu tunagonjwa na tunakufa. Sisi ni tofauti na mutu wa kwanza, Adamu, ambaye alikuwa mukamilifu. Yeye hakuwa na zambi na hangekufa wala kugonjwa hata siku moja. Lakini alipoteza ukamilifu wake alipokosa kumutii Mungu. Tuliriti zambi kutoka kwa Adamu na pia mushahara wa zambi, ni kusema, kifo.​—Soma Waroma 5:12; 6:23.

Yesu, ambaye alikuwa mutu mukamilifu, alikufa si kwa sababu ya zambi zake mwenyewe, lakini alikufa kwa ajili ya zambi zetu. Kifo cha Yesu kinatuwezesha kupata uzima wa milele na kubarikiwa na Mungu.​—Soma 1 Petro 3:18.

Ili kupata habari zingine, usome sura ya 4 na ya 5 ya kitabu hiki, Biblia Inafundisha Kabisa Nini?, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.