Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Matumizi ya Vitu vya Kujipodoa Wakati wa Zamani

Matumizi ya Vitu vya Kujipodoa Wakati wa Zamani

Matumizi ya Vitu vya Kujipodoa Wakati wa Zamani

Kisha kuoga, mwanamuke anajipaka mafuta yenye harufu nzuri kwenye mwili wake ulio laini. Halafu, anafungua kibweta chenye kuchorwa na rangi mbalimbali kilicho na chupa ndogo​-ndogo, vyombo, na chupa zenye kutengenezwa kwa vioo, pembe ya tembo, kombe, ao jiwe. Ndani ya vyombo hivyo, mwanamuke huyo ana aina mbalimbali ya mafuta na manukato ao marashi ambayo yanachanganywa vizuri sana kwa zeri, iliki, mudalasini, ubani ao uvumba, asali, manemane, na vitu vingine.

Katika kibweta hicho, mwanamuke huyo anachukua aina mbalimbali ya vijiko vidogo​-vidogo vilivyochongwa vizuri, sahani na bakuli ndogo​-ndogo. Anatumia vyombo hivyo ili kuchanganya vitu vyake vya kujipodoa ambavyo alichagua kwa ajili ya siku hiyo. Anaanza kujipodoa kwa uangalifu kwa kujiangalia ndani ya kioo cha shaba.

INAONEKANA kwamba tangu nyakati za zamani, wanawake walihangaikia sana kuwa na sura nzuri. Makaburi ya zamani yaliyochorwa, picha za ukutani, na majiwe yaliyochorwa vizuri, vitu vyote hivyo vinaonyesha kwamba watu walitumia vitu vya kujipodoa katika Mezopotamia na Misri ya zamani. Macho yenye kupakwa vitu vingi yaliyoonekana kwenye picha za wanawake wa Misri yalivutia sana.

Basi, tuseme nini juu ya Waisraeli? Je, wanawake wa taifa la zamani la Israeli walitumia vitu vya kujipodoa? Ikiwa ndiyo, ni vitu vya aina gani walivyotumia? Bila shaka, hakuna makaburi yaliyochorwa ao picha za ukutani za taifa la zamani la Israeli ambazo zinaweza kutusaidia kujua hilo. Lakini masimulizi fulani katika Biblia pamoja na vitu vya zamani vilivyochimbuliwa ndani ya udongo katika maeneo yanayotajwa katika Biblia, vyote hivyo vinaweza kutusaidia kuwa na wazo fulani juu ya vitu vya kujipodoa vilivyotumiwa wakati wa zamani.

Vyombo Vilivyotumiwa

Vyombo vingi sana vilivyotumiwa ili kuwekea vitu vya kujipodoa na marashi vilichimbuliwa ndani ya udongo katika maeneo yote ya inchi ya Israeli. Kati ya vitu vilivyopatikana, kulikuwa mabakuli ya majiwe ao sahani zilizotumiwa kuponda na kuchanganya vitu vya kujipodoa, chupa za marashi zenye kuwa na umbo la karote, chupa za mafuta ya alabasta, na vioo vidogo vya mukononi vilivyotengenezwa kwa shaba. Kijiko kimoja kilichotengenezwa kwa pembe ya tembo kilikuwa na muchoro wa majani ya muti wa mungazi kwenye upande mumoja wa mukono wa kijiko hicho na kichwa cha mwanamuke anayezungukwa na njiwa kwenye upande mwengine.

Inaonekana kwamba matajiri wengi walitumia makombe yenye kuchorwa kuwa vyombo vya kuwekea vitu vya kujipodoa. Katika maeneo ya Misri na Kanaani ambako kunachimbuliwa vitu vya zamani, kulipatikana pia vijiko vidogo​-vidogo vilivyotengenezwa kwa pembe ya tembo ao muti, ambavyo vilitumiwa katika kujipodoa, vingine kati ya vijiko hivyo vilikuwa vyenye kuchongwa kwa umbo la watoto wanawake wanaoogelea na maumbo mengine mbalimbali ya ajabu-ajabu. Vitu vyote hivyo vinaonyesha kwamba wanawake wengi wa wakati huo walitumia vitu vya kujipodoa.

Vitu Vilivyotumiwa Kupodoa Macho

Katika Biblia, mumoja wa mabinti wa Ayubu aliitwa “Kereni​-hapuku.” Katika Kiebrania jina hilo linaweza kumaanisha “Pembe ya Rangi Nyeusi (ya Macho),” ni kusema, chombo ao kibweta kilichotumiwa kuwekea vitu vya kujipodoa, labda maskara, ao wanja. (Ayubu 42:14) Labda alipewa jina hilo kwa sababu ya sura yake nzuri, lakini jina hilo linaonyesha pia kama vitu vya kujipodoa vilijulikana wakati huo.

Ni vizuri kujua kwamba Biblia inataja kila mara macho yenye kupakwa rangi inapozungumuzia wanawake wenye sifa mbaya ambao nabii Yeremia na Ezekieli waliita kahaba, kama vile Malkia mujanja Yezebeli na muji wa Yerusalemu uliokosa uaminifu. (2 Wafalme 9:30; Yeremia 4:30; Ezekieli 23:40) Kulingana na hesabu kubwa ya vyombo vya kioo ao vya majiwe pamoja na vyombo vingine vidogo​-vidogo vya kupaka wanja kwenye macho ambavyo vilichimbuliwa ndani ya udongo, ni wazi kwamba wanawake wengi katika taifa la Israeli lenye kuasi​-imani, zaidi sana wanawake wa makao ya kifalme na matajiri, walikuwa na zoea la kujipaka wanja nyingi kwenye macho yao na pia walitumia aina nyingine ya vitu vya kujipodoa.

Mafuta ya Marashi Yalitumiwa kwa Ajili ya Utumishi Mutakatifu ao Utumishi Mwengine

Marashi yaliyotokana na mafuta ya muzeituni yalitengenezwa na kutumiwa katika taifa la Israeli tangu zamani. Kitabu cha Biblia cha Kutoka kina maagizo juu ya namna ya kutengeneza marashi matakatifu yaliyotumiwa na makuhani katika utumishi wao mbalimbali wa hekalu. Marashi hayo matakatifu yalikuwa ni muchanganyiko wa mudalasini, manemane, na mimea mingine yenye harufu nzuri. (Kutoka 30:22-25) Huko Yerusalemu, wachimbuaji wa vitu vya zamani wamevumbua kile wanachoamini kuwa ni kiwanda ambapo kulitengenezwa marashi na uvumba uliotumiwa katika hekalu wakati wa mitume wa Yesu. Kuna Maandiko mengi ya Biblia yanayotaja marashi, yaliyotumiwa kwa ajili ya utumishi mbalimbali mutakatifu na kwa ajili ya matumizi ya kawaida ya kila siku.​—2 Mambo ya Nyakati 16:14; Luka 7:37-46; 23:56.

Kwa kuwa kulikuwa shida ya kupata maji katika sehemu hiyo ya dunia, watu walitumia mafuta yenye harufu nzuri ili kubaki safi. Mafuta hayakutumiwa tu ili kulinda ngozi katika wakati wa joto lakini pia yalitumiwa ili kujipodoa. (Ruthu 3:3; 2 Samweli 12:20) Kabla ya kupelekwa mbele ya Mufalme Ahasuero, mwanamuke kijana Muyahudi aliyeitwa Esta, alikandwa mwili kwa muda wa miezi 12, ni kusema, kwa miezi 6 alikandwa mwili kwa kutumia mafuta ya manemane na kwa miezi mingine 6 akakandwa mwili kwa kutumia mafuta ya zeri.​—Esta 2:12.

Marashi ao mafuta yenye harufu ya marashi yalionwa kuwa kitu cha maana sana kama vile tu feza na zahabu zilivyoonwa. Malkia wa Sheba alipofunga safari yake ndefu yenye kujulikana sana ili kumutembelea Mufalme Sulemani, kati ya zawadi za maana sana alizoleta kulikuwa zahabu, majiwe ya bei, na mafuta ya zeri. (1 Wafalme 10:2, 10) Mufalme Hezekia alipowaonyesha wajumbe kutoka Babiloni hazina za nyumba yake, “mafuta ya zeri na mafuta mazuri” yalikuwa kati ya vitu alivyoonyesha kwa kiburi pamoja na feza, zahabu, na gala lake lote la silaha.​—Isaya 39:1, 2.

Maua mbalimbali, matunda, majani, utomvu (umajimaji wa mumea) ao ngozi ya miti, vitu vyote hivyo vilitengeneza tu kiasi kidogo sana cha marashi ao mafuta. Biblia inataja mimea mingi yenye harufu nzuri kama vile udi, zeri, ulimbo wa bedola, kane, kida, mudalasini, ubani ao uvumba, manemane, zafrani, na nardo. Mimea mingine kati ya hiyo ilipatikana katika eneo la Israeli na ililimwa katika Bonde la Yordani. Mimea mingine ilitoka inje ya Israeli kupitia barabara zilizojulikana sana ambamo watu waliofanya biashara ya uvumba walipitia wakitoka India, Arabia ya Kusini, na mahali pengine.

Mafuta ya Zeri Hayajulikane Ni Nini na Yalitoka Wapi

Mafuta ya zeri yanatajwa katika masimulizi ya Biblia juu ya Malkia Esta, malkia wa Sheba, na Mufalme Hezekia, kama tulivyoona hapo juu. Katika mwaka wa 1988, chombo kidogo cha mafuta kilivumbuliwa ndani ya shimo karibu na Qumran, kando ya Bahari ya Chumvi upande wa mangaribi. Watu walisema mambo mengi juu ya chombo hicho. Je, hayo ndiyo yalikuwa mabaki ya mwisho ya mafuta ya zeri yenye kujulikana sana? Wachunguzi wa mambo hawana jibu la kweli. Leo, walimaji wanajaribu kujua mahali ambapo kulikuwa mashamba ya zeri.

Mambo ya hakika yanaonyesha kama inawezekana mimea iliyotumiwa kutengeneza mafuta ya zeri yanayotajwa katika Biblia ililimwa katika eneo karibu na En-gedi. Wachimbuaji wa vitu vya zamani wamevumbua matanuru, vyombo, na vitu mbalimbali vya chuma na mifupa, vilivyotengenezwa tangu miaka ya 500 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, ambavyo vinafanana na vile vilivyotumiwa katika maeneo mengine ambako watu walitengeneza marashi. Watu wengi wenye elimu wanaamini kama miti ya zeri ilitoka Arabia ao Afrika. Marashi hayo yalitengenezwa kutokana na utomvu ao umajimaji wa muti huo wa zeri. Mafuta ya zeri yalionwa kuwa ya maana sana na ndiyo sababu ufundi wa kulima mumea wa zeri na kutengeneza mafuta yake ulilindwa kuwa jambo la siri.

Mumea wa zeri ulitumiwa hata ili kufanya makubaliano ya kisiasa. Kwa mufano, kulingana na mwanahistoria Yosefu, Mark Antony alipata shamba nzima la mimea hiyo ya maana sana na akamutolea mupenzi wake Cleopatra, Malkia Mumisri, shamba hilo kuwa zawadi. Pliny mwanahistoria Muroma alisema kwamba wakati wa Vita ya Wayahudi iliyotokea katika miaka ya 70 kisha kuzaliwa kwa Yesu, wapiganaji Wayahudi walijaribu kuharibu mimea yote ya zeri ili kuwazuia Waroma wasiikamate.

Kulingana na Maandiko ya Biblia na vitu vya zamani vilivyovumbuliwa, tunaweza kupata wazo fulani juu ya namna watu wa zamani walivyotumia vitu vya kujipodoa. Biblia haikataze kutumia vitu vya kujipodoa na vya kujipamba, lakini inaonyesha kwamba vinapaswa kutumiwa kwa kiasi na utimamu wa akili. (1 Timotheo 2:9) Mutume Petro alionyesha kuwa jambo ‘la samani kubwa machoni pa Mungu’ ni “roho ya utulivu na ya upole.” Kwa sababu ya mitindo inayoendelea kubadilika, kwa kweli shauri hilo ni nzuri kwa wanawake Wakristo, vijana na wazee.​—1 Petro 3:3, 4.

[Picha katika ukurasa wa 24, 25]

Kati ya vitu vya kujipodoa vya wanawake fulani wakati wa zamani, kulikuwa vitu vya kupodoa macho, sura, na ngozi

[Picha katika ukurasa wa 25]

Sahani za majiwe za kuwekea vitu vya kujipodoa, huko Israeli

[Picha katika ukurasa wa 25]

Chombo cha udongo cha marashi, huko Israeli

[Picha katika ukurasa wa 25]

Chombo kilichotengenezwa kwa pembe ya tembo cha kuwekea vitu vya kujipodoa, huko Israeli

[Maneno ili kueleza mahali picha ilitokea, ukurasa wa 25]

Vyombo vyote vya zamani: Erich Lessing/Art Resource, NY