Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Endelea Kumkaribia Yehova

Endelea Kumkaribia Yehova

“Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”—YAK. 4:8.

YEHOVA MUNGU aliwaumba wanadamu wakiwa na uhitaji wa kumkaribia yeye. Hata hivyo, Shetani anataka tufikiri kama yeye, kwamba hatumhitaji Yehova. Huo ni uwongo ambao Shetani ameeneza tangu alipoutumia kumdanganya Hawa katika bustani ya Edeni. (Mwa. 3:4-6) Katika historia yote, wanadamu wengi wamefanya kosa hilohilo.

1, 2. (a) Shetani anatumia “mbinu” zipi? (b) Ni nini kitakachotusaidia tumkaribie Mungu?

2 Tunafurahi kwamba si lazima tunaswe na mtego huo wa Shetani. “Sisi hatukosi kuzijua mbinu zake.” (2 Kor. 2:11) Shetani anajaribu kututenganisha na Yehova kwa kutuchochea tufanye maamuzi yasiyofaa. Lakini kama makala iliyotangulia ilivyoonyesha, tunaweza kufanya maamuzi yanayofaa tunapochagua kazi ya kimwili, tafrija na burudani, na tunaposhughulikia masuala ya kifamilia. Makala hii itatuonyesha jinsi ya kuwa na usawaziko kuhusiana na teknolojia, afya, pesa, na jinsi kujivunia mambo yanayofaa kunavyoweza kutusaidia ‘kumkaribia Mungu.’—Yak. 4:8.

TEKNOLOJIA

3. Toa mifano inayoonyesha jinsi teknolojia inavyoweza kutumiwa kwa njia nzuri au mbaya.

3 Vifaa vya hali ya juu vya kielektroniki vimeenea ulimwenguni pote. Vifaa hivyo vinaweza kuwa na manufaa mengi sana vikitumiwa vizuri. Lakini tukivitumia isivyofaa, vinaweza kututenganisha na Baba yetu wa mbinguni. Fikiria kuhusu kompyuta. Gazeti unalosoma sasa liliandikwa na kuchapishwa kwa kutumia kompyuta. Kompyuta inaweza kutusaidia sana kufanya utafiti, kuwasiliana, na nyakati nyingine tunaweza kuitumia kufurahia burudani. Hata hivyo, tunaweza pia kuwa waraibu wa teknolojia ya kompyuta. Wafanyabiashara huwasadikisha watu kwa ujanja waamini kwamba ni lazima wawe na vifaa vya kisasa zaidi. Mwanamume mmoja kijana alitamani sana kuwa na kompyuta ya kisasa ya mkononi hivi kwamba aliuza figo yake moja kisiri ili ainunue. Hiyo ni dhabihu ya kipumbavu kama nini!

4. Mkristo mmoja alikabilianaje na tatizo lake la kutumia kompyuta kupita kiasi?

 4 Ni jambo la kuhuzunisha hata zaidi kudhabihu urafiki wako pamoja na Yehova kwa sababu ya kuitumia teknolojia vibaya au kupita kiasi. Jon, Mkristo anayekaribia umri wa miaka 30 anasema hivi: “Ninajua Biblia inasema kwamba tunapaswa ‘kununua wakati unaofaa’ kwa ajili ya mambo ya kiroho. Lakini inapohusu kompyuta, ninashindwa kujizuia.” * Mara nyingi, Jon alijikuta akitumia Intaneti hadi usiku wa manane. Anasema hivi: “Kadiri nilivyochoka, ndivyo ilivyokuwa vigumu zaidi kuacha kuwasiliana na wengine kwenye mtandao au kutazama sinema fupifupi, na baadhi ya sinema hizo zilikuwa chafu.” Ili ashinde tabia hiyo mbaya, ilimbidi Jon atumie programu inayozima kompyuta wakati wa kulala unapofika.—Soma Waefeso 5:15, 16.

Wazazi, wasaidieni watoto wenu kutumia teknolojia kwa hekima

5, 6. (a) Wazazi wana madaraka gani kuelekea watoto wao? (b) Wazazi wanawezaje kuhakikisha kwamba watoto wao wana mashirika mazuri?

5 Wazazi, hamhitaji kudhibiti kila jambo ambalo watoto wenu wanafanya, lakini mnahitaji kuchunguza jinsi wanavyotumia kompyuta. Msiwaache waingie katika vituo vya Intaneti vilivyo na maadili mapotovu, michezo yenye jeuri, mashirika mabaya, na mazoea ya kuwasiliana na pepo eti kwa sababu hamtaki kusumbuliwa. Mkifanya hivyo, huenda wakafikiria hivi: ‘Kwa kuwa Baba na Mama hawajali, ni sawa kutazama mambo hayo.’ Mkiwa wazazi, ni kazi yenu kuwalinda watoto wenu, kutia ndani matineja, ili jambo lolote lisiwatenganishe na Yehova. Hata wanyama huwalinda watoto wao kutokana na hatari. Fikiria jinsi ambavyo dubu mwenye watoto angefanya ikiwa watoto wake wangekuwa hatarini!—Linganisha na Hosea 13:8.

6 Wasaidie watoto wako washirikiane na Wakristo wengine, wadogo kwa wakubwa, ambao ni mifano mizuri. Kumbuka kwamba watoto wako wanataka utumie wakati pamoja nao! Kwa hiyo, tenga wakati wa kucheka nao, kucheza nao, na ‘kumkaribia Mungu’ pamoja nao. *

AFYA

7. Kwa nini sote tunajitahidi kudumisha afya nzuri?

7 “U hali gani?” Salamu hiyo ya kawaida inathibitisha ukweli wenye kuhuzunisha. Kwa kuwa wazazi wetu wa kwanza walimruhusu Shetani awatenganishe na Yehova, sisi sote hupatwa na magonjwa. Shetani hutumia ugonjwa kutimiza kusudi lake, kwa kuwa ni vigumu zaidi kumtumikia Yehova tukiwa wagonjwa. Na tukifa, hatuwezi kamwe kumtumikia Yehova. (Zab. 115:17) Hivyo basi, tunajitahidi kadiri tuwezavyo kudumisha afya nzuri. * Na tunapaswa pia kuhangaikia afya na hali njema ya ndugu zetu.

8, 9. (a) Tunawezaje kuepuka kupita mipaka katika masuala ya kiafya? (b) Kuna faida gani za kusitawisha shangwe?

8 Hata hivyo, ni muhimu kuepuka kupita  mipaka kuhusiana na jambo hilo. Baadhi ya watu wamewapendekezea wengine kwa bidii vyakula, madawa, au bidhaa fulani, na wamefanya hivyo kwa bidii kuliko wanavyotangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu. Huenda wanaamini kwa unyoofu kwamba wanawasaidia wengine. Hata hivyo, haifai kuwapendekezea wengine bidhaa za afya au za urembo na mbinu za matibabu kabla au baada ya mikutano katika Jumba la Ufalme au kwenye makusanyiko. Kwa nini?

9 Sisi hukusanyika ili tuzungumzie mambo ya kiroho na kuongeza shangwe yetu, ambayo ni sehemu ya tunda la roho takatifu ya Mungu. (Gal. 5:22) Kutoa mawaidha ya kiafya au kupendekeza madawa katika pindi hizo, iwe umeombwa mawaidha au la, kunaweza kuwakengeusha wengine wasizingatie kusudi la kiroho lililofanya tukusanyike na kuwanyang’anya wengine shangwe yao. (Rom. 14:17) Ni lazima kila mtu ajiamulie mwenyewe jinsi anavyoshughulikia masuala ya kiafya. Isitoshe, hakuna mtu anayeweza kutibu magonjwa yote. Hata madaktari bora zaidi wanazeeka na kuwa wagonjwa, na hatimaye hufa. Na kuhangaikia kupita kiasi afya yetu hakuwezi kurefusha maisha yetu. (Luka 12:25) Badala yake, “moyo wenye shangwe ni dawa nzuri.”—Met. 17:22.

10. (a) Ni sifa gani ambazo zinampendeza Yehova? (b) Tunawezaje kufurahia afya kamilifu?

10 Vivyo hivyo, si vibaya kuhangaikia kuwa na sura nzuri. Lakini hatupaswi kung’ang’ana sana kuondoa dalili zote za uzee. Dalili hizo zinaweza kuonyesha ukomavu, heshima, na uzuri wa moyoni. Kwa mfano, Biblia inasema hivi: “Kichwa chenye mvi ni taji la uzuri kinapopatikana katika njia ya uadilifu.” (Met. 16:31) Hivyo ndivyo Yehova anavyotuona, na tunapaswa kujitahidi kuwa na maoni kama yake. (Soma 1 Petro 3:3, 4.) Basi, je, ni jambo la hekima kuhatarisha isivyo lazima afya yetu kwa kufanyiwa upasuaji hatari au kutafuta madawa ya kubadili sura yetu ili tuvutie zaidi? “Shangwe ya Yehova” ndiyo chanzo cha uzuri wa kweli unaong’aa kutoka moyoni, na uzuri huo hautegemei umri au afya ya mtu. (Neh. 8:10) Tutapata afya kamilifu na uzuri wa ujanani katika ulimwengu mpya tu. (Ayu. 33:25; Isa. 33:24) Kabla ya wakati huo, kutumia hekima na kuwa na imani kutatusaidia kubaki karibu na Yehova huku tukiridhika na hali zetu za sasa.—1 Tim. 4:8.

PESA

11. Pesa zinawezaje kuwa mtego?

11 Pesa si mbaya, wala si vibaya kufanya biashara kwa njia ya unyoofu. (Mhu. 7:12; Luka 19:12, 13) Hata hivyo, kusitawisha ‘upendo wa pesa’ kwa hakika kutatutenganisha na Yehova. (1 Tim. 6:9, 10) “Mahangaiko ya mfumo huu wa mambo,” yaani, kuhangaikia kupita kiasi mahitaji ya lazima maishani, kunaweza kusonga hali yetu ya kiroho. Ndivyo ilivyo pia na “nguvu za udanganyifu wa utajiri,” yaani, kuamini uwongo wa kwamba utajiri huleta usalama na furaha ya kudumu. (Mt. 13:22) Yesu alisema wazi kwamba “hakuna” anayeweza kumtumikia Mungu na utajiri wakati uleule.—Mt. 6:24.

12. Ni mitego gani ya kifedha iliyoenea leo, na tunawezaje kuiepuka?

12 Maoni yasiyofaa kuhusu pesa yanaweza kumfanya mtu atende kwa njia isiyofaa. (Met. 28:20) Ahadi za kupata pesa haraka na kwa njia rahisi zimewafanya watu fulani wanunue tiketi za bahati nasibu au kujiingiza katika miradi ya kibiashara ambayo faida hutegemea idadi ya watu unaowashawishi wajiunge nayo. Wakristo fulani wamewashawishi washiriki wenzao wa kutaniko wajiunge na miradi hiyo. Wengine wamedanganywa kwamba watapata faida kubwa isivyo kawaida wakiwekeza pesa katika biashara fulani. Usiruhusu pupa ikufanye ulaghaiwe. Tumia hekima. Ikiwa unaahidiwa jambo linaloonekana kuwa haliwezekani, basi inaelekea ni la uwongo.

13. Maoni ya Yehova kuhusu pesa yanatofautianaje na ya watu ulimwenguni?

13 Tukitanguliza kwanza “ufalme na uadilifu wake,” Yehova hubariki jitihada zetu zenye  usawaziko za kutafuta mahitaji ya lazima. (Mt. 6:33; Efe. 4:28) Yehova hataki tusinzie mikutanoni kwa sababu ya kufanya kazi kupita kiasi wala hapendi tuketi kwenye Jumba la Ufalme huku akili zetu zikitangatanga tukihangaikia pesa. Lakini watu wengi katika ulimwengu wanaamini kwamba ili wawe salama kifedha na kuishi maisha ya starehe wakati ujao, ni lazima watafute pesa kwa kila njia. Mara nyingi, wanawachochea watoto wao kuwa na mradi huohuo wa kimwili. Yesu alionyesha kwamba kufikiria kwa njia hiyo ni kukosa akili. (Soma Luka 12:15-21.) Huenda hilo likatukumbusha kuhusu Gehazi, aliyefikiri kwamba angeweza kutosheleza ulafi wake na bado aendelee kuwa na msimamo mzuri mbele za Yehova.—2 Fal. 5:20-27.

14, 15. Kwa nini hatupaswi kutegemea pesa ili kupata usalama? Toa mfano.

14 Inaripotiwa kwamba tai fulani wamekufa maji kwa sababu hawakumwachilia kutoka kwenye makucha yao samaki aliyekuwa mzito kuliko walivyoweza kubeba. Je, Mkristo anaweza kuwa kama tai hao? Alex, mzee Mkristo anaeleza hivi: “Mimi hutumia vitu kwa uangalifu sana. Ninapokosea na kumimina mafuta mengi ya kujipaka kwenye kiganja, ninarudisha kiasi fulani katika chupa yake.” Hata hivyo, Alex alijiingiza katika biashara ya kununua na kuuza hisa akidhani kwamba baada ya muda mfupi angeacha kazi yake na kuanza utumishi wa upainia. Alitumia wakati mwingi sana kufanya utafiti kuhusu thamani ya hisa na ripoti za soko la hisa. Akitumia pesa alizoweka akibani na mikopo kutoka kwa wauzaji wa hisa, alinunua hisa ambazo wakadiriaji walikuwa wametabiri kwamba zingepanda thamani haraka sana. Kinyume chake, thamani ya hisa hizo ilishuka haraka sana. Alex anasema hivi: “Nilikuwa nimeazimia kupata tena pesa zangu. Nilifikiri kwamba nikiendelea kungoja, thamani ya hisa zangu itapanda tena.”

15 Kwa miezi kadhaa, Alex hangeweza kufikiria jambo lingine lolote. Ilikuwa vigumu kwake kukazia fikira mambo ya kiroho, na alikosa usingizi. Lakini thamani ya hisa zake haikupanda kamwe. Alex alipoteza pesa zake zote na ilimbidi auze nyumba yake. Anakiri hivi: “Niliiumiza sana familia yangu.” Lakini alijifunza jambo muhimu. Anasema hivi: “Sasa ninajua kwamba mtu yeyote anayetegemea mfumo wa Shetani atavunjika moyo kabisa.” (Met. 11:28) Bila shaka, kutumaini pesa, biashara, au uwezo wetu wa kutafuta pesa katika mfumo huu ni sawa na kumtumaini Shetani, “mungu wa mfumo huu wa mambo.” (2 Kor. 4:4; 1 Tim. 6:17) Tangu wakati huo, Alex amerahisisha maisha yake “kwa ajili ya habari njema.” Anasema kwamba kufanya hivyo kumemwezesha yeye na familia yake kupata furaha zaidi na kumkaribia Yehova zaidi.Soma Marko 10:29, 30.

KIBURI

16. Kujivunia mambo yanayofaa kunatofautianaje na kiburi?

16 Si vibaya kujivunia mambo yanayofaa. Kwa mfano, sikuzote tunapaswa kujivunia kuwa Mashahidi wa Yehova. (Yer. 9:24) Kujiheshimu kwa njia inayofaa kunatusaidia kufanya maamuzi mazuri na kuepuka kushusha viwango vyetu vya maadili. Lakini kufikiri kwamba mapendeleo au maoni yetu ni yenye thamani sana kunaweza kututenganisha na Yehova.—Zab. 138:6; Rom. 12:3.

Badala ya kutamani pendeleo fulani kutanikoni, furahia kazi yako katika huduma!

17, 18. (a) Taja mifano ya watu fulani katika Biblia waliokuwa wanyenyekevu na wale waliokuwa na kiburi. (b) Ni kwa njia gani ndugu mmoja hakuruhusu kiburi kimtenganishe na Yehova?

17 Biblia ina mifano ya watu waliokuwa na kiburi na wale waliokuwa wanyenyekevu. Mfalme Daudi alitegemea kwa unyenyekevu mwongozo wa Yehova, na Yehova akambariki. (Zab. 131:1-3) Lakini Yehova alimnyenyekeza Mfalme Nebukadneza na Mfalme Belshaza waliokuwa na kiburi. (Dan. 4:30-37; 5:22-30) Hata katika nyakati zetu, tunakabili hali zinazojaribu unyenyekevu wetu. Ryan, mtumishi wa huduma mwenye umri wa miaka 32,  alihamia kutaniko lingine. Ryan anasema hivi: “Nilitazamia kwamba ningependekezwa haraka kuwa mzee, lakini mwaka mzima ulipita bila kupendekezwa.” Je, Ryan angekasirika au kuwa na uchungu, akihisi kwamba wazee hawakumheshimu? Je, angeacha kuhudhuria mikutano, na kuruhusu kiburi kimtenganishe na Yehova na watu Wake? Wewe ungefanya nini?

18 Ryan anakumbuka hivi: “Nilisoma kila makala katika machapisho yetu kuhusu matarajio ambayo hayajatimia.” (Met. 13:12) “Nikaanza kutambua kwamba nilihitaji kujifunza subira na unyenyekevu. Nilihitaji kukubali kuzoezwa na Yehova.” Badala ya kujifikiria, Ryan alianza kufikiria jinsi anavyoweza kuwatumikia wengine kutanikoni na shambani. Baada ya muda, alikuwa akiongoza mafunzo kadhaa ya Biblia yenye maendeleo. Anasema hivi: “Bila kutarajia, niliwekwa kuwa mzee mwaka mmoja na nusu baadaye. Sikuhangaikia tena jambo hilo kwa sababu nilikuwa nikifurahia sana huduma yangu.”—Soma Zaburi 37:3, 4.

KAA KARIBU NA YEHOVA!

19, 20. (a) Tunawezaje kuhakikisha kwamba mambo tunayofuatilia kila siku hayatutenganishi na Yehova? (b) Tunaweza kuwaiga watu gani waliokaa karibu na Yehova?

19 Mambo yote yaliyozungumziwa katika makala hii na ile iliyotangulia yana mahali panapofaa katika maisha yetu. Tunajivunia kuwa watumishi wa Yehova. Familia yenye afya nzuri na yenye furaha ni miongoni mwa zawadi bora kutoka kwa Yehova. Tunaelewa kwamba kazi ya kimwili na pesa zinaweza kutusaidia kutosheleza mahitaji yetu. Tunajua kwamba tafrija inaweza kutuburudisha na teknolojia inaweza kutunufaisha. Lakini kufuatilia vitu hivyo wakati usiofaa, kupita kiasi, au kwa njia inayoathiri ibada yetu kunaweza kututenganisha na Yehova.

Usiruhusu kitu chochote kikutenganishe na Yehova!

20 Bila shaka Shetani anataka mambo hayo yatutenganishe na Yehova. Hata hivyo, unaweza kuuzuia msiba huo usikupate na usiipate familia yako! (Met. 22:3) Mkaribie Yehova na ukae karibu naye. Tuna mifano mingi katika Biblia inayoweza kutuelimisha kuhusiana na jambo hili. Enoko na Noa ‘walitembea pamoja na Mungu wa kweli.’ (Mwa. 5:22; 6:9) Musa “aliendelea kuwa imara kama mtu anayemwona Yeye asiyeonekana.” (Ebr. 11:27) Yesu alitegemezwa daima na Mungu kwa sababu sikuzote alifanya yale yaliyompendeza Baba yake wa mbinguni. (Yoh. 8:29) Iga mfano wao. ‘Shangilia sikuzote. Sali bila kuacha. Kuhusiana na kila jambo toa shukrani.’ (1 The. 5:16-18) Na usiruhusu kitu chochote kikutenganishe na Yehova!

^ fu. 4 Majina yamebadilishwa.

^ fu. 6 Tazama habari yenye kichwa “Kuwalea Watoto Wenye Kutegemeka” katika gazeti la Amkeni! la Oktoba 2011.

^ fu. 7 Tazama habari yenye kichwa “Njia Tano za Kuwa na Afya Bora” katika gazeti la Amkeni! la Machi 2011.