Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Endelea Kumukaribia Yehova

Endelea Kumukaribia Yehova

‘Mumukaribie Mungu, naye atawakaribia ninyi.’—YAK. 4:8.

1, 2. (a) Namna gani Shetani anawadanganya watu? (b) Ni nini itatusaidia tumukaribie Mungu?

 YEHOVA MUNGU aliwaumba wanadamu na tamaa ya kumukaribia. Hata hivyo, Shetani anataka tuwe kama yeye, tufikiri kama hatuna lazima ya Yehova. Tangu wakati alimudanganya Eva katika shamba la Edeni, Shetani anaendelea kuwafanya watu waamini uongo huo. (Mwa. 3:4-6) Katika historia yote, wanadamu wengi wameamini kwamba hawana lazima ya Yehova.

2 Jambo lenye kufurahisha ni kwamba sisi ‘tunajua mbinu zake [ao njia zake za kudanganya].’ Kwa hiyo, si lazima tuanguke katika mitego ya Shetani (2 Kor. 2:11) Shetani anajaribu kututenganisha na Yehova kwa kutufanya tuchukue maamuzi mabaya. Lakini kama tulivyojifunza katika habari iliyotangulia, tunaweza kufanya maamuzi mazuri kuhusu kazi, kujifurahisha, na kuhusu mambo mengine yanayoweza kutokea katika familia. Habari hii itatuonyesha namna gani kufanya maamuzi ya hekima kuhusu mambo ya kiteknolojia, matunzo, feza na kujivuna kunakofaa, yanavyoweza kutusaidia ‘tumukaribie Mungu.’​—Yak. 4:8.

MAMBO YA KITEKNOLOJIA

3. Fasiria namna gani vyombo ambavyo teknolojia inatutolea vinaweza kutumiwa vizuri ao vibaya.

3 Mashini ao vyombo vya kielektroniki vya kila namna vinapatikana sasa mahali pote. Vyombo hivyo vinaweza kutusaidia ikiwa tunavitumia vizuri. Ikiwa tunavitumia vibaya vinaweza kututenganisha na Baba yetu wa mbinguni. Tuchukue mufano wa ordinatere. Gazeti hili unalosoma sasa liliandikwa na kuchapishwa kwa kutumia ordinatere. Tunaweza kutumia ordinatere ili kutafuta habari fulani, kupashana habari na wengine, na wakati fulani tunaweza kuitumia ili kujifurahisha. Lakini, ordinatere inaweza pia kututawala. Wafanya-biashara wanawachochea watu wanunue ordinatere za kisasa. Kijana mumoja alitamani sana kupata ordinatere ndogo ya hali ya juu, na ili apate feza za kuinunua aliuzisha kwa siri figo yake moja. Huo ni upumbavu kabisa!

4. Namna gani Joni alifikia kuachana na tabia ya kutumia ordinatere kupita kiasi?

4 Ni jambo la kusikitisha hata zaidi ikiwa mutu anaharibu uhusiano wake na Yehova sababu ya kutumia vibaya vyombo ambavyo teknolojia inatutolea. Ndugu Joni *, mwenye miaka karibu 30 anasema hivi: “Ninajua kwamba Biblia inashauri ‘tujinunulie wakati unaofaa’ kwa ajili ya mambo ya kiroho. Lakini, ninapokuwa mbele ya ordinatere, ninashindwa kufuata shauri hilo.” Mara nyingi Joni alitumia Internete mupaka usiku sana. Yeye anaeleza hivi: “Kadiri nilivyokuwa mwenye kuchoka, ndivyo ilivyokuwa vigumu kwangu kutoka mbele ya ordinatere, kwa hiyo niliendelea kutumia wengine habari mbalimbali ao kutazama video, hata video fulani zisizofaa.” Ili kuachana na tabia hiyo, Joni alifanya ordinatere yake iwe ikijizimisha wakati saa yake ya kulala inafika.​—Soma Waefeso 5:15, 16.

Wazazi, muwafundishe watoto wenu kutumia vyombo vya kiteknolojia kwa hekima

5, 6. (a) Kazi ya wazazi ni nini? (b) Wazazi wanaweza kufanya nini ili kuwasaidia watoto wao wawe na marafiki wazuri?

5 Wazazi, si lazima mujue kila jambo ambalo watoto wenu wanafanya, lakini munapaswa kuangalia sana matumizi yao ya ordinatere. Musiwaache watazame mambo ya uasherati, michezo ya kuuana, mambo ya uchawi ao maji, na kurafikiana na marafiki wabaya kwenye Internete ili tu kuwafanya wawe na jambo fulani la kufanya ao ili wasiwasumbue. Mukiwaacha wafanye hivyo, wanaweza kuwaza hivi: ‘Mambo haya si mabaya sababu Papa na Mama hawaseme kitu.’ Wazazi, kazi yenu ni kuwalinda watoto wenu na jambo lolote linaloweza kuwatenganisha na Yehova. Hata wanyama wanawalinda watoto wao wasipatwe na hatari. Wazia jambo ambalo dubu anaweza kufanya wakati mutu fulani anawachokoza watoto wake.​—Linganisha na Hosea 13:8.

6 Wafundishe watoto wako namna wanaweza kufanya urafiki na Wakristo vijana na wazee walio mifano mizuri. Na usisahau kama watoto wako wanataka wewe upitishe wakati pamoja nao! Kwa hiyo, tafuta wakati wa kucheka, kucheza, kufanya jambo fulani pamoja na watoto wako, na ‘mumukaribie Mungu’ pamoja. *

MAMBO YA MATUNZO

7. Sababu gani sisi sote tunataka kuendelea kuwa na afya nzuri?

7 “Habari gani?” Kila mara tunauliza wengine ulizo hilo ili kujua ikiwa wana afya nzuri ao hapana. Sisi sote tunagonjwa sababu wazazi wetu wa kwanza waliruhusu Shetani awatenganishe na Yehova. Shetani anafurahi wakati tunagonjwa, sababu katika hali hiyo inakuwa vigumu kwetu kumutumikia Yehova. Na ikiwa tunakufa, hatuweze kumutumikia Yehova hata kidogo. (Zab. 115:17) Kwa hiyo, ni jambo la kawaida, kufanya yote tunayoweza ili kuendelea kuwa na afya nzuri. * Na tunapaswa kuhangaikia afya ya ndugu na dada zetu.

8, 9. (a) Namna gani tunapaswa kuepuka kuhangaikia afya yetu kupita kiasi? (b) Kuwa na furaha kunaleta faida gani?

8 Hata hivyo, tunapaswa kuepuka kuhangaikia afya yetu kupita kiasi. Wahubiri fulani wanatia watu moyo sana kuhusu aina fulani ya vyakula, matunzo na dawa mbalimbali, na wanafanya hivyo kwa bidii sana kuliko hata bidii walio nayo katika kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu. Wanaweza kufikiri kwa moyo wote kwamba wanapofanya hivyo wanawasaidia wengine. Hata hivyo, hatupaswe kuja na madawa fulani ao vitu vya kujipondoa kwenye Jumba la Ufalme ao kwenye mikusanyiko na kuanza kutapatapa vitu hivyo mbele na kisha mikutano. Sababu gani hatupaswe kufanya hivyo?

9 Kusudi letu la kuja kwenye mikutano ao mikusanyiko ni kuzungumuzia habari za kiroho na kuongeza furaha yetu, ambayo ni sehemu moja ya tunda la roho ya Mungu. (Gal. 5:22) Kuzungumuzia ufundi fulani wa matunzo ao madawa kwenye mikutano, hata ikiwa wengine wanatuuliza ao hapana, kunaweza kufanya tusahau kusudi la mikutano yetu na kufanya wengine wapoteze furaha yao. (Rom. 14:17) Mambo ya matunzo ni uamuzi wa pekee. Zaidi ya hayo, hakuna mutu aliye na dawa ya magonjwa yote. Hata waganga wakubwa wanagonjwa na kuzeeka, na mwishowe wanakufa. Na hata ikiwa tunahangaikia afya yetu kupita kiasi, hatuweze kurefusha maisha yetu. (Lu. 12:25) Lakini, “moyo wenye shangwe [ao furaha] ni dawa nzuri.”​—Met. 17:22.

10. (a) Ni sifa gani zinazotufanya tuwe wenye kupendeza machoni pa Yehova? (b) Ni wakati gani tutakuwa na afya nzuri kabisa?

10 Vilevile, ni jambo la kawaida mutu kuhangaikia namna anavyoonekana mbele ya watu wengine. Lakini hatupaswe kujitesa ili kuondoa alama zote za uzee. Alama hizo zinaonyesha kwamba tumekomaa, zinawafanya watu watuheshimu na zinaonyesha uzuri wa ndani. Kwa mufano, Biblia inasema hivi: “Kichwa chenye mvi ni taji la uzuri kinapopatikana katika njia ya uadilifu.” (Met. 16:31) Yehova anatuona namna tulivyo, na sisi tunapaswa kuwa na maoni hayo. (Soma 1 Petro 3:3, 4.) Kwa hiyo, je, ni jambo la hekima kufanyiwa upasuaji hatari ao kutumia njia fulani za utunzaji zilizo hatari ili tu sura yetu iwe yenye kuvutia? “Shangwe ya Yehova” ndio uzuri wetu unaotoka ndani, iwe tuna afya nzuri ao hapana. (Neh. 8:10) Ni katika dunia mupya tu ndio tutakuwa na afya kamilifu na kurudilia tena uzuri wa ujana. (Ayu. 33:25; Isa. 33:24) Lakini sasa, kuwa na hekima inayofaa na kuwa na imani kutatusaidia tubaki karibu ya Yehova na kuendelea kutumia maisha yetu kadiri iwezekanavyo ili kufanya mapenzi yake, iwe tuna afya nzuri ao hapana.​—1 Tim. 4:8.

MAMBO YA FEZA

11. Namna gani feza zinaweza kuwa mutego?

11 Si vibaya kuwa na feza ao kufanya biashara isiyo ya udanganyifu. (Mhu. 7:12; Lu. 19:12, 13) Hata hivyo, ‘kupenda pesa’ kunaweza kabisa kututenganisha na Yehova. (1 Tim. 6:9, 10) ‘Mahangaiko ya mufumo huu wa mambo’ ni kusema, kuhangaikia kupita kiasi mahitaji ya kimwili, kunaweza kusonga hali yetu ya kiroho. “Nguvu za udanganyifu wa utajiri,” ni kusema, kufikiri kama utajiri unaweza kutuletea furaha ya kudumu na kutuepusha na matatizo, kunaweza pia kusonga hali yetu ya kiroho. (Mt. 13:22) Yesu alionyesha waziwazi kama “hakuna anayeweza” kutumikia Mungu na utajiri.​—Mt. 6:24.

12. Watu wameangukia katika mitego gani leo kwa sababu ya tamaa ya feza, na namna gani tunaweza kuiepuka?

12 Ikiwa tuna maoni yasiyofaa kuhusu feza, jambo hilo linaweza kutuingiza katika matendo mabaya. (Met. 28:20) Kwa sababu wameahidiwa kupata feza haraka, ndugu fulani wamejiingiza katika mambo ya tombola; ao katika ahadi nyingi za kupata feza na kisha wanatafuta watu wengine wa kujiunga nao, ili waweze kulipwa zaidi. Wamewachochea hata ndugu na dada katika kutaniko wajiunge nao. Wengine wamedanganywa kwa kuahidiwa kama watapata feza nyingi ikiwa wanatia kiasi fulani cha feza katika mipango fulani. Usidanganywe kwa sababu ya tamaa ya feza. Tumia akili. Ikiwa unaambiwa kama utapata feza nyingi sana kuliko ilivyo kawaida, ni uongo.

13. Maoni ya Yehova kuhusu feza yanatofautiana namna gani na maoni ya watu wa ulimwengu?

13 Tunapotia “Ufalme na uadilifu wake,” pa nafasi ya kwanza Yehova atabariki mipango tunayofanya ili kupata mahitaji ya lazima ya maisha. (Mt. 6:33; Efe. 4:28) Yehova hapende tuanze kusinzia kwenye mikutano kwa sababu tulitumika kupita kiasi ao hapende tuanze kuwaza-waza juu ya feza tunapokuwa katika Jumba la Ufalme. Watu wengi wanafikiri kama ikiwa wanatumia nguvu zao zote ili kutafuta feza, hawatakosewa kitu wakati wa uzee na maisha yao haitakuwa na mahangaiko wakati huo. Kila mara wanawachochea watoto wao kwenye miradi hiyohiyo ya kupata vitu vya kimwili. Yesu alionyesha kama mawazo hayo ni upumbavu. (Soma Luka 12:15-21.) Hilo linatukumbusha mufano wa Gehazi aliyefikiri kama anaweza kuwa na pupa na wakati huohuo kuendelea kuwa na uhusiano muzuri pamoja na Yehova.​—2 Fal. 5:20-27.

14, 15. Sababu gani si jambo la hekima kufikiri kama feza zinaweza kumuondolea mutu mahangaiko katika ulimwengu huu? Toa mufano.

14 Imeripotiwa kwamba tai fulani zimezama katika maji kwa sababu ya kugangania tu samaki iliyokuwa na uzito mwingi zaidi. Mukristo anaweza kujikuta katika hali kama hiyo kuhusiana na mambo ya feza. Muzee mumoja anayeitwa Alex, anasema hivi: “Kwa kawaida mimi situpetupe feza zangu, ninapenda kuweka feza, sina tabia ya kutumia feza.” Lakini wakati fulani, Alex alifikiri kama ikiwa anapata feza nyingi zaidi ataacha kazi yake ili kuwa painia. Kwa hiyo alijifunza biashara ya kununua vitu ili kuviuzisha wakati ambapo bei ingepanda. Na alitumia feza zote alizokuwa ameweka na alijikopesha zingine ili kununua vitu ambavyo aliambiwa kama vitapanda bei. Kuliko kupanda, bei ilishuka sana. Alex anaeleza hivi: “Sikutaka feza zangu zipotee. Nilifikiri kama ikiwa ninangojea kidogo, bei itapanda na feza zangu zitarudia.”

15 Kwa miezi mingi, Alex alikuwa tu akiwaza kuhusu biashara yake. Hakuwa tena anawaza mambo ya kiroho, na alikosa usingizi. Lakini bei ya vitu haikupanda na feza zake zilihomba kabisa. Alex alipoteza feza zake zote na alilazimika kuuzisha nyumba yake. Yeye anasema hivi: “Nilihuzunisha sana familia yangu.” Lakini alipata somo. Anaongeza hivi: “Sasa nimetambua kama kila mutu anayetumainia ulimwengu huu wa Shetani anajichokesha bure na atavunjika moyo.” (Met. 11:28) Kwa kweli, katika ulimwengu huu kutumainia feza ulizo nazo, uwezo ulio nao wa kutafuta feza ni kutumainia “mungu wa mufumo huu wa mambo,” ni kusema, Shetani. (2 Kor. 4:4; 1 Tim. 6:17) Kwa sasa Alex amerahisisha maisha yake “kwa ajili ya habari njema.” Ukimuuliza, atakuambia kwamba kufanya hivyo kumemuletea furaha zaidi yeye na familia yake na kumewasaidia wamukaribie Yehova zaidi.​—Soma Marko 10:29, 30.

KUJIVUNA KUNAKOFAA

16. Kuna tofauti gani kati ya kujivuna kunakofaa na kiburi?

16 Si vibaya kujivuna kwa sababu ya mambo mazuri. Kwa mufano, kila siku tunapaswa kujivuna kwa sababu sisi ni Mashahidi wa Yehova. (Yer. 9:24) Kujivuna kwa njia inayofaa kunatusaidia tuchukue maamuzi mazuri na kufuata sheria za Mungu. Lakini kuwa na kiburi na kufikiri kama tunajua mambo mengi sana kupita wengine kunaweza kututenganisha na Yehova.​—Zab. 138:6; Rom. 12:3.

Kuliko kutafuta madaraka juu chini katika kutaniko, furahia kazi ya kuhubiri!

17, 18. (a) Biblia inazungumuzia watu gani waliokuwa wanyenyekevu, na watu waliokuwa wenye kiburi? (b) Ndugu mumoja alifanya nini ili kiburi kisimutenganishe na Yehova?

17 Biblia inazungumuzia watu waliokuwa na kiburi na wengine waliokuwa wanyenyekevu. Mufalme Daudi alimuomba Yehova kwa unyenyekevu amuongoze, na Yehova alimubariki. (Zab. 131:1-3) Lakini Yehova aliwanyenyekeza Nebukadneza na Belshaza sababu walikuwa na kiburi. (Dan. 4:30-37; 5:22-30) Leo, hali fulani zinaweza kufunua ikiwa sisi ni wanyenyekevu ao hapana. Fikiria mufano wa ndugu Ryan, mutumishi wa huduma mwenye miaka 32, aliyehamia katika kutaniko fulani. Yeye anasema hivi: “Nilitazamia kwamba nitapendekezwa mara moja kuwa muzee. Lakini mwaka mumoja ukapita bila mimi kupendekezwa.” Je, Ryan aliwakasirikia wazee na kufikiri kama hawamupende? Je, aliacha kukusanyika, na kuruhusu kiburi kimutenganishe na Yehova na watu Wake? Wewe ungefanya nini?

18 Ndugu Ryan anasema hivi: “Nilisoma habari mbalimbali kuhusu namna ya kungojea jambo nzuri linalochelewa.” (Met. 13:12) “Nilianza kutambua kama ninapaswa kujifunza kuwa na uvumilivu na unyenyekevu. Nilipaswa kumuacha Yehova anizoeze.” Ryan aliacha kujifikiria sana na akaanza kufikiria namna gani anaweza kuwasaidia ndugu na dada katika kutaniko na wale anaokutana nao katika mahubiri. Kwa wakati kidogo tu alianza kuongoza mafunzo mengi ya Biblia yenye kufanya maendeleo. Yeye anasema hivi: “Kisha mwaka mumoja na nusu baadaye, nilitiwa kuwa muzee. Hilo lilikuwa jambo ambalo sikutazamia. Nilikuwa nimeacha kufikiria jambo hilo sababu kazi ya mahubiri ilikuwa yenye kufurahisha sana.”​—Soma Zaburi 37:3, 4.

BAKI KARIBU NA YEHOVA!

19, 20. (a) Tunaweza kufanya nini ili mambo ambayo tumezungumuzia yasitutenganishe na Yehova? (b) Tunaweza kuiga mifano gani ya watu waliobaki karibu na Yehova?

19 Mambo yote ambayo tumezungumuzia katika habari hii na ile iliyotangulia si mabaya kabisakabisa. Tunajivunia kuwa watumishi wa Yehova. Familia yenye furaha na afya nzuri ni kati ya zawadi nzuri sana ambazo Yehova ametutolea. Tunajua kwamba kazi ya kimwili na feza vinaweza kutusaidia ili kutimiza mahitaji yetu. Kujifurahisha kunaweza kutupumuzisha na vyombo vya kiteknolojia vinaweza kutusaidia sana. Lakini vitu hivyo vinaweza kututenganisha na Yehova ikiwa tunavifuatilia pa wakati usiofaa, ikiwa tunavihangaikia kupita kiasi ao vinatufanya tukose wakati kwa ajili ya mambo ya kiroho.

Usiruhusu kitu chochote kikutenganishe na Yehova!

20 Kwa kweli, Shetani anataka vitu hivyo visivyokuwa vibaya kabisakabisa vitutenganishe na Yehova. Lakini, unaweza kuepuka jambo hilo lisikufikie ao kufikia familia yako! (Met. 22:3) Umukaribie Yehova na ubaki karibu naye. Biblia ina mifano mingi inayoweza kutusaidia kufanya hivyo. Enoko na Noa ‘walitembea pamoja na Mungu wa kweli.’ (Mwa. 5:22; 6:9) Musa ‘aliendelea kuwa imara kama mutu anayemuona Yeye asiyeonekana.’ (Ebr. 11:27) Yesu aliendelea kutegemezwa na Mungu kwa sababu siku zote alifanya mambo yanayomupendeza Baba yake wa mbinguni. (Yoh. 8:29) Iga mifano hiyo. ‘Shangilia sikuzote. Sali bila kuacha. Kuhusiana na kila jambo toa shukrani.’ (1 Thes. 5:16-18) Na usiache kitu chochote kikutenganishe na Yehova!

^ Majina yamebadilishwa.

^ Soma habari “Kuwalea Watoto Wenye Kutegemeka” katika Amkeni! ya Mwezi wa 10, 2011.

^ Soma “Njia Tano Ili Kuwa na Afya Bora” katika Amkeni! ya Mwezi wa 3, 2011.