Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wazee Wakristo Ni ‘Wafanyakazi Wenzi kwa Shangwe Yetu’

Wazee Wakristo Ni ‘Wafanyakazi Wenzi kwa Shangwe Yetu’

“Sisi ni wafanyakazi wenzi kwa shangwe yenu.”—2 KOR. 1:24.

ULIKUWA mwaka wa 55 W.K. Mtume Paulo alikuwa katika jiji la bandarini la Troa, lakini aliendelea kulifikiria jiji la Korintho. Mwanzoni mwa mwaka huo, alihuzunika sana alipopata habari kwamba kulikuwa na ugomvi kati ya ndugu Wakorintho. Kwa hiyo, kwa kuwa aliwahangaikia kama baba, aliwatumia barua ili iwarekebishe. (1 Kor. 1:11; 4:15) Alikuwa pia amemtuma Tito, mfanyakazi mwenzake awatembelee na kumletea ripoti huko Troa. Sasa Paulo alikuwa akimngojea Tito huko Troa, akitamani kujua jinsi Wakorintho walivyokuwa wakiendelea. Lakini Paulo alikata tamaa sana kwa sababu Tito hakuja. Paulo angefanya nini? Alisafiri kwa meli hadi Makedonia, na alishangilia alipokutana na Tito huko. Tito alimwambia Paulo kwamba ndugu Wakorintho waliitikia vizuri barua yake na walitamani kumwona. Paulo aliposikia ripoti hiyo nzuri, ‘alishangilia zaidi tena.’—2 Kor. 2:12, 13; 7:5-9.

2. (a) Paulo aliwaandikia nini Wakorintho kuhusu imani na shangwe? (b) Ni maswali gani tutakayozungumzia?

2 Muda mfupi baadaye, Paulo aliwaandikia Wakorintho barua ya pili. Aliwaambia hivi: “Si kwamba sisi ndio mabwana juu ya imani yenu, bali sisi ni wafanyakazi wenzi kwa shangwe yenu, kwa maana ni kwa imani yenu kwamba ninyi mnasimama.” (2 Kor. 1:24) Paulo alimaanisha nini aliposema maneno hayo? Na wazee Wakristo leo wanajifunza nini kutokana nayo?

IMANI YETU NA SHANGWE YETU

3. (a) Paulo alimaanisha nini alipoandika hivi: “Kwa imani yenu . . . ninyi mnasimama”? (b) Wazee leo wanaigaje mfano wa Paulo?

3 Paulo alitaja mambo mawili muhimu katika ibada yetu, yaani, imani na shangwe. Kumbuka kwamba aliandika hivi kuhusu imani: “Si kwamba sisi ndio mabwana  juu ya imani yenu, . . . kwa maana ni kwa imani yenu kwamba ninyi mnasimama.” Paulo aliposema maneno hayo, alikiri kwamba ndugu Wakorintho walisimama imara, si kwa sababu yake au mwanadamu mwingine yeyote, bali kwa sababu ya imani yao wenyewe katika Mungu. Kwa hiyo, Paulo hakuona uhitaji wa kutawala imani ya ndugu zake, naye hakutaka kufanya hivyo. Alikuwa na uhakika kwamba walikuwa Wakristo waaminifu ambao walitaka kufanya yaliyo sawa. (2 Kor. 2:3) Leo, wazee wanaiga mfano wa Paulo kwa kuonyesha kwamba wana uhakika kuhusu imani ya ndugu zao na nia yao ya kumtumikia Mungu. (2 The. 3:4) Badala ya kutunga sheria kali kwa ajili ya kutaniko, wazee hutegemea kanuni za Kimaandiko na mwongozo kutoka kwa tengenezo la Yehova. Bila shaka, sawa tu na Paulo, wazee wa leo si mabwana juu ya imani ya ndugu zao.—1 Pet. 5:2, 3.

4. (a) Paulo alimaanisha nini alipoandika hivi: “Sisi ni wafanyakazi wenzi kwa shangwe yenu”? (b) Wazee leo wanaigaje mtazamo wa Paulo?

4 Paulo alisema hivi pia: “Sisi ni wafanyakazi wenzi kwa shangwe yenu.” Paulo aliposema hivyo, alimaanisha yeye na watu alioshirikiana nao kwa ukaribu. Kwa nini tunafikia mkataa huo? Katika barua hiyohiyo, Paulo aliwakumbusha Wakorintho kuhusu wawili kati ya wafanyakazi hao wenzake alipoandika hivi: “Yesu, aliyehubiriwa katikati yenu kupitia sisi, yaani, kupitia mimi na Silvano na Timotheo.” (2 Kor. 1:19) Isitoshe, kila mara Paulo alipotaja maneno “wafanyakazi wenzi” katika barua zake, alikuwa akirejelea watu alioshirikiana nao kwa ukaribu, kama vile Apolo, Akila, Priska, Timotheo, Tito, na wengine. (Rom. 16:3, 21; 1 Kor. 3:6-9; 2 Kor. 8:23) Kwa hiyo, aliposema: “Sisi ni wafanyakazi wenzi kwa shangwe yenu,” Paulo aliwahakikishia Wakorintho kwamba yeye na wenzake walitaka kufanya yote waliyoweza ili kudumisha shangwe ya washiriki wote wa kutaniko. Leo, wazee Wakristo wanataka kufanya vivyo hivyo. Wanataka kufanya yote wawezayo ili kuwasaidia ndugu zao ‘wamtumikie Yehova kwa kushangilia.’—Zab. 100:2; Flp. 1:25.

5. Tutazungumzia majibu ya swali gani, na tunapaswa kufikiria nini?

5 Hivi karibuni, kikundi cha ndugu na dada wenye bidii kutoka sehemu mbalimbali ulimwenguni kiliombwa kitoe maoni kuhusu swali hili: “Ni maneno na matendo gani ya mzee ambayo yameongeza shangwe yako?” Tunapozungumzia maoni yaliyotolewa na kikundi hicho cha waamini wenzetu, linganisha maelezo yao na maoni yako. Zaidi ya hayo, acheni sisi sote tufikirie jinsi tunavyoweza kuchangia roho ya shangwe katika kutaniko letu. *

“SALIMUNI PERSISI MPENDWA WETU”

6, 7. (a) Ni kwa njia gani moja wazee wanaweza kumwiga Yesu, Paulo, na watumishi wengine wa Mungu? (b) Kwa nini kukumbuka majina ya ndugu zetu kunaongeza shangwe yao?

6 Ndugu na dada zetu wengi wanasema kwamba shangwe yao inaongezeka wazee wanapopendezwa nao kibinafsi. Njia moja ya msingi ambayo wazee wanafanya hivyo ni kwa kuiga mfano wa Daudi, Elihu, na Yesu mwenyewe. (Soma 2 Samweli 9:6; Ayubu. 33:1; Luka 19:5.) Kila mmoja wa watumishi hao wa Yehova alipendezwa kikweli na mtu fulani kwa kumwita kwa jina lake. Paulo pia alithamini umuhimu wa kukumbuka na kutumia majina ya waamini wenzake. Alimalizia moja ya barua zake kwa kuwasalimu ndugu na dada zaidi ya 25 kwa majina, kutia ndani Persisi, dada Mkristo ambaye Paulo alisema hivi kumhusu: “Salimuni Persisi mpendwa wetu.”—Rom. 16:3-15.

 7 Si rahisi kwa baadhi ya wazee kukumbuka majina. Hata hivyo, wanapojitahidi kabisa kukumbuka majina, ni kana kwamba wanawaambia waamini wenzao, ‘Wewe ni mtu muhimu kwangu.’ (Kut. 33:17) Wazee hasa wataongeza shangwe ya ndugu zao wakikumbuka majina yao wanapowaomba watoe maelezo katika Funzo la Mnara wa Mlinzi au katika mikutano mingine.—Linganisha na Yohana 10:3.

“ALIFANYA KAZI NYINGI KATIKA BWANA”

8. Paulo aliwaiga Yehova na Yesu kwa njia gani moja muhimu?

8 Paulo pia alipendezwa na wengine kwa kuwapongeza kwa unyoofu, na hiyo ni njia nyingine ya msingi ya kuongeza shangwe ya waamini wenzetu. Hivyo, baada ya Paulo kusema kwamba alitamani kufanya kazi kwa shangwe ya ndugu zake, aliandika hivi katika barua hiyohiyo: “Ninajisifu kwa njia kubwa kuhusiana nanyi.” (2 Kor. 7:4) Bila shaka, maneno hayo ya pongezi yaliichangamsha mioyo ya ndugu huko Korintho. Paulo aliyasifu makutaniko mengine kwa njia hiyohiyo. (Rom. 1:8; Flp. 1:3-5; 1 The. 1:8) Baada ya kumtaja Persisi katika barua yake kwa kutaniko la Roma, Paulo aliongezea hivi: “Alifanya kazi nyingi katika Bwana.” (Rom. 16:12) Dada huyo mwaminifu alitiwa moyo kama nini na pongezi hiyo! Paulo aliwaiga Yehova na Yesu katika kuwapongeza wengine.—Soma Marko 1:9-11; Yohana 1:47; Ufu. 2:2, 13, 19.

9. Kwa nini kupongezwa na kuwapongeza wengine kunaongeza roho ya shangwe kutanikoni?

9 Wazee leo wanajua pia umuhimu wa kuwaambia ndugu zao kwamba wanawathamini sana. (Met. 3:27; 15:23) Kila mara mzee anapofanya hivyo, ni kana kwamba anawaambia hivi ndugu zake: ‘Niliona ulichofanya. Ninakujali.’ Na bila shaka waamini wenzetu wanahitaji kumsikia mzee akiwahakikishia kwamba anawathamini. Dada mmoja mwenye umri wa miaka zaidi ya 50 alieleza jinsi wengine wanavyohisi pia aliposema hivi: “Ni vigumu kupongezwa kazini. Watu hawajali na wana roho ya mashindano. Basi mzee anaponipongeza kwa sababu ya jambo fulani ambalo nimefanya kutanikoni, ninaburudishwa sana na kuimarishwa! Jambo hilo linanifanya nihisi kwamba ninapendwa na Baba yangu wa mbinguni.” Ndugu anayewalea watoto wawili akiwa mzazi mmoja alihisi vivyo hivyo. Hivi karibuni mzee mmoja alimpongeza kutoka moyoni. Ndugu yetu alihisije? Anasema: “Maneno ya mzee huyo yalinitia moyo sana!” Kwa kweli, mzee anapowapongeza kwa unyoofu waamini wenzake anawatia moyo na kuongeza shangwe yao. Na hilo linawapa nguvu za kuendelea kutembea kwenye barabara ya uzima ‘bila kuchoka.’—Isa. 40:31.

‘LICHUNGENI KUTANIKO LA MUNGU’

10, 11. (a) Wazee wanawezaje kuiga mfano wa Nehemia? (b) Ni nini kitakachomsaidia mzee kuwapa wengine zawadi ya kiroho anapofanya ziara za uchungaji?

10 Wazee wanaweza kuonyesha kwa njia gani muhimu kwamba wanapendezwa kibinafsi na ndugu zao na hivyo kuongeza shangwe ya kutaniko? Kwa kuchukua hatua ya kuwatafuta na kuwasaidia wale wanaohitaji kutiwa moyo. (Soma Matendo 20:28.) Wazee wanapofanya hivyo, wanawaiga wachungaji wa kiroho wa kale. Kwa mfano, fikiria jambo ambalo mwangalizi mwaminifu Nehemia alifanya alipoona kuwa baadhi ya ndugu zake Wayahudi wamedhoofika kiroho. Simulizi hilo linasema kwamba alisimama mara moja na kuwatia moyo. (Neh. 4:14) Wazee wanahitaji kufanya vivyo hivyo leo. ‘Wanasimama,’ yaani, wanachukua hatua ya kuwasaidia waamini wenzao wawe imara katika imani. Ili kuwatia moyo kibinafsi, wanawatembelea ndugu na dada zao nyumbani hali zikiruhusu. Katika ziara hizo  za uchungaji, lengo lao ni ‘kuwapa zawadi fulani ya kiroho.’ (Rom. 1:11) Ni nini kitakachowasaidia wazee kufanya hivyo?

11 Kabla ya kufanya ziara ya uchungaji, mzee anahitaji kuchukua wakati kumfikiria mtu ambaye atamtembelea. Ndugu au dada huyo anakabili matatizo gani? Ni mambo gani yanayoweza kumjenga? Ni andiko au simulizi la mtu gani katika Biblia linalofaa hali zake? Kufikiria mapema mambo hayo kutamsaidia mzee kuwa na mazungumzo yenye kujenga, badala ya kuzungumzia mambo madogo-madogo tu. Katika ziara za uchungaji, mzee huwapa ndugu na dada zake fursa ya kujieleza huku akisikiliza kwa makini. (Yak. 1:19) Dada mmoja alisema hivi: “Inafariji sana wakati mzee anaposikiliza na kutia moyoni mambo unayomwambia.”—Luka 8:18.

Kujitayarisha humsaidia mzee ‘kutoa zawadi ya kiroho’ katika ziara ya uchungaji

12. Ni nani wanaohitaji kutiwa moyo kutanikoni, na kwa nini?

12 Ni nani watakaonufaishwa na ziara za uchungaji? Paulo aliwahimiza wazee wenzake Wakristo ‘waliangalie kundi lote.’ Kwa kweli, washiriki wote wa kutaniko wanahitaji kutiwa moyo, kutia ndani wahubiri na mapainia wote ambao wamekuwa wakihubiri kwa uaminifu mwaka baada ya mwaka. Kwa nini wanahitaji kutegemezwa na wachungaji wa kiroho? Kwa sababu nyakati nyingine wahubiri hao wenye nguvu kiroho wanakabili pia hatari ya kulemewa na mikazo ya ulimwengu huu mwovu. Ili kuonyesha kwa nini nyakati nyingine hata mtumishi mwenye nguvu wa Mungu anahitaji msaada wa wengine, acheni tuzungumzie jambo fulani lililotukia katika maisha ya Mfalme Daudi.

‘ABISHAI AKAJA KUMSAIDIA’

13. (a) Ishbi-benobu alitumia hali gani ya Daudi? (b) Ni nini kilichomwezesha Abishai amwokoe Daudi?

13 Muda mfupi baada ya kijana Daudi kutiwa mafuta ili awe mfalme, alikabiliana uso kwa uso na Goliathi, wa jamii ya Warefaimu, waliokuwa majitu. Daudi aliyekuwa jasiri aliliua jitu hilo. (1 Sam. 17:4, 48-51; 1 Nya. 20:5, 8) Miaka mingi baadaye, katika vita na Wafilisti, Daudi alikabiliana tena  uso kwa uso na jitu lingine. Jitu hilo lililoitwa Ishbi-benobu, lilikuwa pia la jamii ya Warefaimu. (2 Sam. 21:16) Hata hivyo, wakati huo karibu jitu hilo limuue Daudi. Kwa nini? Si kwa sababu Daudi alipoteza ujasiri wake bali kwa sababu alikuwa amepoteza nguvu zake. Biblia inasema hivi: “Daudi akachoka.” Mara tu Ishbi-benobu alipogundua kwamba Daudi amedhoofika kimwili, “akafikiria kumpiga na kumuua Daudi.” Lakini kabla tu ya jitu hilo kumpiga Daudi kwa silaha, “Abishai mwana wa Seruya akaja mara moja kumsaidia [Daudi], akampiga yule Mfilisti na kumuua.” (2 Sam. 21:15-17) Daudi aliponea chupuchupu! Bila shaka Daudi alishukuru sana kwamba Abishai alikuwa akimtazama naye akaja haraka kumsaidia wakati uhai wake ulipokuwa hatarini! Ni mambo gani tunayoweza kujifunza kutokana na simulizi hilo?

14. (a) Ni nini kinachotuwezesha kushinda matatizo makubwa ambayo ni kama Goliathi? (b) Wazee wanawezaje kuwasaidia wengine wapate tena nguvu na shangwe yao? Toa mfano.

14 Tukiwa watu wa Yehova tunatimiza huduma yetu, ulimwenguni pote licha ya kwamba tunakabili vipingamizi kutoka kwa Shetani na watumishi wake. Baadhi yetu tumekabiliana uso kwa uso na matatizo makubwa ambayo ni kama majitu, lakini tumepambana na “Magoliathi” hao na kuwashinda kwa kumtegemea Yehova kikamili. Hata hivyo, nyakati nyingine tunachoka na kuvunjika moyo kwa sababu ya kuendelea kupambana na mikazo ya ulimwengu huu. Tukiwa dhaifu hivyo, tunakuwa hoi na hivyo kukabili hatari ya ‘kupigwa’ kwa njia ya mfano na mikazo ambayo kwa kawaida tungefanikiwa kuishinda. Katika pindi kama hizo, utegemezo tunaopewa na mzee kwa wakati unaofaa unaweza kutusaidia kupata tena shangwe na nguvu zetu, na wengi wamejionea jambo hilo. Painia mmoja mwenye umri wa miaka zaidi ya 60 alisema hivi: “Wakati fulani nilikuwa mgonjwa na utumishi wa shambani ulinichosha sana. Mzee mmoja aligundua kwamba nimeshuka moyo naye akanifikia. Tulikuwa na mazungumzo yenye kutia moyo yaliyotegemea andiko fulani la Biblia. Nilitumia mapendekezo aliyonipa, nayo yalinisaidia.” Dada huyo aliongezea hivi: “Mzee huyo alionyesha upendo kama nini kwa kugundua hali yangu dhaifu na kunisaidia!” Naam, inatia moyo kujua kwamba tuna wazee wanaotuangalia na kututunza kwa upendo na ambao wako tayari ‘kuja kutusaidia’ kama Abishai alivyofanya zamani.

“MUUJUE UPENDO NILIO NAO . . . KWA AJILI YENU”

15, 16. (a) Kwa nini Paulo alipendwa sana na waamini wenzake? (b) Kwa nini tunawapenda wazee wetu wa kutaniko wanaotujali?

15 Kuwa mchungaji si kazi rahisi. Nyakati nyingine wazee hukosa usingizi usiku wakisali na kulihangaikia kundi la Mungu au wakiwasaidia kiroho waamini wenzao. (2 Kor. 11:27, 28) Hata hivyo, wazee hutimiza jukumu lao kikamili na kwa furaha, kama Paulo alivyofanya. Aliwaandikia hivi Wakorintho: “Mimi nitatumia kwa furaha zaidi na kutumiwa kabisa kwa ajili ya nafsi zenu.” (2 Kor. 12:15) Kwa kweli, kwa sababu aliwapenda ndugu zake, Paulo alijitumikisha kabisa ili awatie nguvu. (Soma 2 Wakorintho 2:4; Flp. 2:17; 1 The. 2:8) Si ajabu kwamba akina ndugu walimpenda sana Paulo!—Mdo. 20:31-38.

16 Leo, tukiwa watumishi wa Mungu tunawapenda pia wazee wetu Wakristo wanaojali na tunamshukuru Yehova katika sala zetu kwa kutupatia wazee hao. Wanaongeza shangwe yetu kwa kutuonyesha upendezi wa kibinafsi. Tunaimarishwa sana na ziara zao za uchungaji. Isitoshe, tunathamini kwamba wako tayari kutusaidia tunapolemewa na mikazo ya ulimwengu huu. Naam, wazee hawa Wakristo wenye kujali kwa kweli ni ‘wafanyakazi wenzi kwa shangwe yetu.’

^ fu. 5 Ndugu na dada haohao waliulizwa swali hili pia: “Ni sifa gani unayothamini sana mzee akiwa nayo?” Wengi wao walijibu hivi: “Mwenye urafiki.” Sifa hiyo muhimu itazungumziwa katika toleo la wakati ujao la gazeti hili.