Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unathamini Urithi Wetu wa Kiroho?

Je, Unathamini Urithi Wetu wa Kiroho?

‘Mungu alielekeza uangalifu wake kwa mataifa ili achukue kutoka kwao watu kwa ajili ya jina lake.’MDO. 15:14.

1, 2. (a) “Kibanda cha Daudi” kilikuwa nini, na kingejengwa upya jinsi gani? (b) Ni nani wanaotumika pamoja wakiwa watumishi wa Yehova leo?

KATIKA mkutano muhimu sana wa baraza linaloongoza uliofanywa Yerusalemu mwaka wa 49 W.K., mwanafunzi Yakobo alisema hivi: “Simioni [Petro] ameeleza kikamili jinsi Mungu kwa mara ya kwanza alivyoelekeza uangalifu wake kwa mataifa ili achukue kutoka kwao watu kwa ajili ya jina lake. Na maneno ya Manabii yanakubaliana na jambo hili, kama vile ambavyo imeandikwa, ‘Baada ya mambo hayo nitarudi na kukijenga upya kibanda cha Daudi ambacho kimeanguka chini; nami nitayajenga upya mabomoko yake na kukisimamisha tena, ili watu wanaobaki wamtafute Yehova kwa bidii, pamoja na watu wa mataifa yote, watu wanaoitwa kwa jina langu, asema Yehova, anayefanya mambo haya, yanayojulikana tangu zamani za kale.’”—Mdo. 15:13-18.

2 “Kibanda cha [au, nyumba ya mfalme] Daudi” kilianguka wakati Mfalme Sedekia alipopinduliwa. (Amo. 9:11) Hata hivyo, “kibanda” hicho kingejengwa upya, na Yesu, mzao wa Daudi, angewekwa kuwa Mfalme wa kudumu. (Eze. 21:27; Mdo. 2:29-36) Kama Yakobo alivyotaja wazi katika mkutano huo wa kihistoria, kukusanywa kwa warithi wa Ufalme kutoka kwa Wayahudi na watu wa Mataifa kulitimiza unabii huo wa Amosi. Leo, mabaki ya Wakristo watiwa-mafuta pamoja na mamilioni ya “kondoo wengine” wa Yesu wameungana katika kutangaza kweli ya Biblia wakiwa watumishi wa Yehova.—Yoh. 10:16.

WATU WA YEHOVA WAKABILI JARIBU

3, 4. Watu wa Yehova walidumishaje hali yao ya kiroho walipokuwa Babiloni?

3 Wayahudi walipopelekwa uhamishoni huko Babiloni, ilikuwa wazi kwamba kile “kibanda cha Daudi” kilikuwa kimeanguka. Kwa kuwa dini ya uwongo ilienea sana huko Babilonia, watu wa Mungu waliwezaje kudumisha hali  yao ya kiroho wakiwa uhamishoni kwa miaka 70, kuanzia mwaka wa 607 K.W.K. hadi 537 K.W.K.? Ni kama tu tunavyodumisha hali yetu ya kiroho tukiwa watu wa Yehova katika ulimwengu huu unaoongozwa na Shetani. (1 Yoh. 5:19) Urithi mwingi wa kiroho umetusaidia kudumisha hali yetu ya kiroho.

4 Neno la Mungu lililoandikwa ni sehemu ya urithi wetu wa kiroho. Wayahudi waliokuwa uhamishoni huko Babiloni hawakuwa na Maandiko yote Matakatifu, lakini waliijua Sheria ya Musa, iliyotia ndani zile Amri Kumi. Walijua “nyimbo za Sayuni,” walikumbuka methali nyingi, na walifahamu mambo mengi ambayo watumishi wa kale wa Yehova walitimiza. Naam, wahamishwa hao walilia walipokumbuka Sayuni, nao hawakumsahau Yehova. (Soma Zaburi 137:1-6.) Hilo liliwasaidia kuendelea kuwa hai kiroho hata walipokuwa Babiloni, ambako kulikuwa na mazoea na mafundisho mengi ya uwongo.

FUNDISHO LA UTATU SI JIPYA

5. Kuna uthibitisho gani kwamba Wababiloni na Wamisri wa kale walitumia sanamu za utatu katika ibada zao?

5 Sanamu za utatu zilikuwa sehemu muhimu ya ibada ya Wababiloni. Sanamu moja ya utatu ya Wababiloni ilikuwa na sura ya Sini (mungu-mwezi), Shamashi (mungu-jua), na ya Ishtari (mungu wa kike wa uzazi na vita). Katika Misri ya kale, mara nyingi mungu alionwa kuwa amemwoa mungu wa kike aliyemzalia mwana, “na hivyo walifanyiza miungu mitatu. Baba hakuonwa sikuzote kuwa mkuu, nyakati nyingine alikuwa mwandamani wa mwana-mfalme, huku mungu wa kike akiwa ndiye mungu mkuu.” (New Larousse Encyclopedia of Mythology) Sanamu moja ya utatu ya Misri ilikuwa na mungu Osirisi, mungu wa kike Isisi, na mwana wao Horusi.

6. Utatu ni nini, na tumelindwaje ili tusiamini uwongo huo?

6 Dini zinazodai kuwa za Kikristo pia zinaamini mungu wa Utatu. Makasisi wanasema kwamba Baba, Mwana, na roho takatifu ni Mungu mmoja. Lakini imani hiyo inaletea suto enzi kuu ya Yehova, wakimfanya aonekane kuwa sehemu ya utatu, yaani, yeye ni sehemu moja tu kati ya sehemu tatu za uungu. Watu wa Yehova wamelindwa kutokana na imani hiyo ya uwongo kwa sababu wanakubaliana na maneno haya yaliyoandikwa kwa mwongozo wa roho: “Sikiliza, Ee Israeli: Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja.” (Kum. 6:4) Yesu aliyanukuu maneno hayo, na kila Mkristo wa kweli anakubaliana naye.—Marko 12:29.

7. Kwa nini mtu anayeamini Utatu hawezi kubatizwa na hivyo hawezi kuonyesha kwamba amejiweka wakfu kihalali kwa Mungu?

7 Fundisho la Utatu halipatani na kazi ambayo Yesu aliwapa wafuasi wake ya ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, na kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu.’ (Mt. 28:19) Ili mtu abatizwe na kuwa Mkristo wa kweli na Shahidi wa Yehova, ni lazima akubali ukuu wa Baba, Yehova, na pia cheo na mamlaka ya Yesu, Mwana wa Mungu. Pia, ni lazima mtu huyo aamini kwamba roho takatifu ni nguvu ya utendaji ya Mungu, wala si sehemu ya Utatu. (Mwa. 1:2) Mtu anayeendelea kuamini Utatu hawezi kubatizwa na hivyo hawezi kuonyesha kwamba amejiweka wakfu kihalali kwa Yehova Mungu. Tunashukuru kama nini kwamba urithi wetu wa kiroho umetulinda tusiamini fundisho hilo linalomkosea Mungu heshima!

MAZOEA YA KUWASILIANA NA PEPO YANAENDELEA KUTIA MIZIZI!

8. Wababiloni walikuwa na maoni gani kuhusu miungu na roho waovu?

8 Dini ya Babilonia iliruhusu mafundisho mengi ya uwongo, miungu mingi, roho waovu, na mazoea ya kuwasiliana na pepo. Kitabu kimoja (The International Standard Bible Encyclopaedia) kinasema hivi: ‘Jambo lililofuata kwa umuhimu baada ya miungu katika dini  ya Babiloni ni roho waovu waliokuwa na nguvu za kuwatesa wanadamu kwa magonjwa mbalimbali ya kimwili au kiakili. Inaonekana kwamba jambo lililokaziwa zaidi katika dini hiyo lilikuwa kupambana na roho hao waovu, na kila mahali watu walisali ili miungu iwasaidie kupambana na roho waovu.’

9. (a) Baada ya kutoka uhamishoni Babiloni, Wayahudi wengi walianzaje kuamini mafundisho ya uwongo ya kidini? (b) Tunalindwaje kutokana na hatari za kujihusisha na roho waovu?

9 Baada ya kutoka utumwani huko Babiloni, Wayahudi wengi walianza kuamini mambo yasiyo ya kimaandiko. Mafundisho ya Kigiriki yalipozidi kuenea, Wayahudi wengi waliathiriwa na roho waovu kwa sababu walianza kuamini wazo la kwamba roho waovu wanaweza kuwa waovu au wazuri. Urithi wetu wa kiroho unatulinda na hatari za kujihusisha kimakusudi na roho waovu, kwa kuwa tunajua kwamba Mungu alishutumu mazoea ya Wababiloni ya kuwasiliana na pepo. (Isa. 47:1, 12-15) Isitoshe, tunaongozwa na maoni ya Mungu kuhusu kuwasiliana na pepo.—Soma Kumbukumbu la Torati 18:10-12; Ufunuo 21:8.

10. Tunaweza kusema nini kuhusu mazoea na mafundisho ya Babiloni Mkubwa?

10 Mbali na Wababiloni, wafuasi wa Babiloni Mkubwa, yaani, milki ya ulimwenguni pote ya dini ya uwongo, wamezoea pia kuwasiliana na pepo. (Ufu. 18:21-24) Kitabu kimoja (The Interpreter’s Dictionary of the Bible) kinasema hivi: “Milki ya Babiloni [Mkubwa] imeenea katika nchi na tamaduni nyingi. Haitambuliwi tu kupitia mipaka ya kijiografia au mipaka mingineyo bali kupitia ibada ya sanamu iliyoenea sana.” (Buku la 1, uku. 338) Milki ya Babiloni Mkubwa bado ipo nayo imejaa mazoea ya kuwasiliana na pepo, ibada ya sanamu, na dhambi nyinginezo, lakini haitadumu kwa muda mrefu.—Soma Ufunuo 18:1-5.

11. Ni maonyo gani ambayo yametolewa katika machapisho yetu kuhusu mazoea ya kuwasiliana na pepo?

11 Yehova alitangaza hivi: “Siwezi kuvumilia matumizi ya nguvu za uchawi.” (Isa. 1:13) Zoea la kuwasiliana na pepo, ambalo mara nyingi huitwa zoea la kuwasiliana na viumbe wa roho, lilipendwa na watu wengi katika karne ya 19. Kwa hiyo, gazeti la Zion’s Watch Tower la Mei 1885 lilisema hivi: “Imani ya kwamba wafu wanaishi mahali pengine au wana hali nyingine si ngeni. Ilikuwa sehemu ya dini ya watu wa kale, na ndiyo chanzo hasa cha hadithi zote za uwongo.” Makala hiyo iliongezea kwamba wazo lisilo la kimaandiko la wafu kuwasiliana na walio hai “limefunika na kukazia uwongo wa ‘roho waovu’ wanaojifanya kuwa roho za wafu. Wametumia kwa bidii mbinu hiyo ya kuficha utambulisho wao, na hivyo wameendelea kutawala akili na maisha ya watu wengi.” Kijitabu chetu cha zamani chenye kichwa Maandiko Yanasema nini Kuhusu Kuwasiliana na Pepo? (cha Kiingereza) kilitoa maonyo kama hayo, ambayo pia yanapatikana katika machapisho yetu ya hivi karibuni.

JE, NAFSI ZINATESEKA KUZIMU?

12. Chini ya mwongozo wa roho takatifu, Sulemani alisema nini kuhusu hali ya wafu?

12 “Wale wote ambao wameijua kweli” wanaweza kujibu swali hilo. (2 Yoh. 1) Bila shaka, tunakubaliana na maneno haya ya Sulemani: “Mbwa aliye hai ni afadhali kuliko simba aliyekufa. Kwa maana walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe . . . Yote ambayo mkono wako unapata kufanya, yafanye kwa nguvu zako zote, kwa maana hakuna kazi, wala utungaji wala ujuzi wala hekima katika Kaburi [la ujumla la wanadamu], mahali unapokwenda.”—Mhu. 9:4, 5, 10.

13. Wayahudi waliathiriwaje na dini na utamaduni wa Wagiriki?

13 Wayahudi walikuwa na fursa nzuri ya kujua ukweli kuhusu wafu. Hata hivyo, milki ya Ugiriki ilipogawanyika kati ya majenerali wa Aleksanda Mkuu, jitihada zilifanywa ili kuunganisha Yuda na Siria kupitia njia kama  vile dini na utamaduni wa Wagiriki. Matokeo ni kwamba Wayahudi walikubali mafundisho ya uwongo ya kwamba nafsi ya mwanadamu haiwezi kufa na kwamba kuna kuzimu, mahali ambapo wafu huteswa. Wagiriki hawakuanzisha fundisho la kwamba kuna mahali ambapo nafsi huteswa, kwa kuwa Wababiloni ndio walioamini kwamba “kuzimu . . . ni mahali panapotisha sana, . . . panaposimamiwa na miungu na roho waovu wakali sana walio na nguvu nyingi.” (The Religion of Babylonia and Assyria) Naam, Wababiloni waliamini kwamba nafsi haifi.

14. Ayubu na Abrahamu walijua nini kuhusu kifo na ufufuo?

14 Ingawa mwanamume mwadilifu Ayubu hakuwa na Biblia, alijua ukweli kuhusu kifo. Alitambua pia kwamba Yehova ni Mungu mwenye upendo ambaye angetamani sana kumfufua. (Ayu. 14:13-15) Abrahamu pia aliamini ufufuo. (Soma Waebrania 11:17-19.) Kwa kuwa haiwezekani kumfufua mtu asiyeweza kufa, wanaume hao waliomwogopa Mungu hawakuamini fundisho la kwamba nafsi ya mwanadamu haifi. Bila shaka, roho takatifu ya Mungu iliwasaidia Ayubu na Abrahamu kuelewa hali ya wafu na kuamini ahadi ya ufufuo. Kweli hizo pia ni sehemu ya urithi wetu wa kiroho.

“KUACHILIWA HURU KWA NJIA YA FIDIA” NI JAMBO MUHIMU

15, 16. Tumeachiliwaje huru kutoka katika dhambi na kifo?

15 Tunathamini kwamba Mungu amefunua pia kweli kuhusu njia anayotumia kutukomboa kutokana na kifo na dhambi tuliyorithi kutoka kwa Adamu. (Rom. 5:12) Tunajua kwamba Yesu “alikuja, si kuhudumiwa, bali kuhudumu na kutoa nafsi yake iwe fidia badala ya wengi.” (Marko 10:45) Ni vizuri kama nini kujua kwamba ‘tuliachiliwa huru kwa njia ya fidia ambayo Kristo Yesu alilipa’!—Rom. 3:22-24.

16 Katika karne ya kwanza, Wayahudi na watu wasio Wayahudi walihitaji kutubu  dhambi zao na kuonyesha imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu. La sivyo, hawangesamehewa. Hali iko hivyo leo. (Yoh. 3:16, 36) Mtu akiendelea kushikilia mafundisho ya uwongo kama vile Utatu na kutokufa kwa nafsi, hawezi kufaidika kutokana na fidia. Lakini sisi tunaweza kufaidika. Tunajua ukweli kuhusu “Mwana wa upendo [wa Mungu], ambaye kwa njia yake tunaachiliwa huru kupitia fidia, kusamehewa dhambi zetu.”—Kol. 1:13, 14.

SONGENI MBELE MKIWA WATU KWA AJILI YA JINA LA YEHOVA!

17, 18. Tunaweza kupata wapi habari muhimu kuhusu historia yetu, na tunaweza kufaidikaje kwa kujifunza historia hiyo?

17 Tunaweza kusema mambo mengi kuhusu mafundisho ya kweli tunayoamini, mambo tuliyojionea tukiwa watumishi wa Mungu, na baraka za kiroho na za kimwili tunazofurahia. Kwa makumi ya miaka, Vitabu vya Mwaka vimekuwa na masimulizi yenye kusisimua ya utendaji wetu katika nchi mbalimbali ulimwenguni pote. Historia yetu imesimuliwa katika video Imani Yenye Matendo, Sehemu ya 1 na ya 2, na katika machapisho kama vile Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu. Pia, magazeti yetu huwa na masimulizi yanayogusa moyo kuhusu waamini wenzetu wapendwa.

18 Tunafaidika tunapochunguza historia ya tengenezo la Yehova tukiwa na nia nzuri, kama vile tu Waisraeli walivyofaidika walipotafakari jinsi Yehova alivyowakomboa kutoka katika utumwa wa Wamisri. (Kut. 12:26, 27) Akiwa mwanamume aliyezeeka na aliyeshuhudia matendo ya Mungu ya ajabu, Musa aliwasihi hivi Waisraeli: “Kumbuka siku za kale, fikirieni miaka iliyopita kutoka kizazi mpaka kizazi; muulize baba yako, naye anaweza kukuambia; wanaume wenu wazee, nao wanaweza kukuambia.” (Kum. 32:7) Tukiwa ‘watu wa Yehova na kundi la watu wa malisho yake,’ sisi sote tunatangaza sifa zake kwa shangwe na kuwajulisha wengine matendo yake makuu. (Zab. 79:13) Isitoshe, ni vizuri tuchunguze historia ya tengenezo letu, tujifunze kutokana nayo, na kuweka miradi inayofaa ya wakati ujao.

19. Kwa kuwa tunafurahia nuru ya kiroho, tunapaswa kufanya nini?

19 Tunathamini sana kwamba hatupapasi gizani, badala yake tunafurahia nuru ya kiroho kutoka kwa Mungu. (Met. 4:18, 19) Basi acheni tujifunze Neno la Mungu na kuwafundisha wengine kweli kwa bidii tukiwa na roho kama ya mtunga-zaburi aliyesali hivi akimtukuza Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova: “Nitautangaza uadilifu wako, naam, wako peke yako. Ee Mungu, umenifundisha tangu ujana wangu, na mpaka sasa ninaendelea kutangaza kazi zako za ajabu. Na mpaka wakati wa uzee na wa kuwa na kichwa chenye mvi, Ee Mungu, usiniache, mpaka nikitangazie kizazi habari za mkono wako, habari za nguvu zako, kwa wale wote watakaokuja.”—Zab. 71:16-18.

20. Kuna masuala gani yanayohusiana, na unahisije kuyahusu?

20 Tukiwa watu wa Yehova waliojiweka wakfu, tunaelewa masuala haya yanayohusiana, yaani, suala la enzi kuu na suala la utimilifu wa wanadamu. Kwa kweli, tunatangaza kweli isiyoweza kukanushwa ya kwamba Yehova ndiye Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, anayestahili ujitoaji wetu wa moyo wote. (Ufu. 4:11) Tukiwa na roho yake, sisi pia tunawatangazia wapole habari njema, tunafunga majeraha ya waliovunjika moyo, na kuwafariji wale wanaoomboleza. (Isa. 61:1, 2) Shetani amejaribu bila mafanikio kuwaongoza watu wa Mungu na wanadamu wote, hata hivyo, sisi tunathamini sana urithi wetu wa kiroho, tumeazimia kudumisha utimilifu wetu kwa Mungu, na tunamsifu Bwana mwenye Enzi Kuu Yehova sasa na tutafanya hivyo milele.—Soma Zaburi 26:11; 86:12.