Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 SIMULIZI LA MAISHA

“Niliona, Lakini Sikuelewa”

“Niliona, Lakini Sikuelewa”

Nilikuwa na umri wa miaka miwili mwaka wa 1975 mama yangu aliposhuku kwamba nilikuwa na tatizo. Mama alipokuwa amenibeba mikononi, rafiki yake aliangusha kitu kizito sakafuni, na kukatokea kishindo kikubwa. Mama alitambua kwamba hata sikusogea. Nilipokuwa na umri wa miaka mitatu, bado sikuweza kuongea. Kisha familia yetu ikapokea habari za kushtua, wataalamu walithibitisha kwamba nilikuwa kiziwi kabisa!

Nilipokuwa bado mchanga, wazazi wangu walitalikiana, na mama akalazimika kutulea—mimi, kaka zangu wawili, na dada yangu mkubwa—akiwa peke yake. Wakati huo, nchini Ufaransa watoto viziwi walifundishwa kwa njia tofauti na za sasa, na wakati mwingine njia zilizotumiwa ziliwasababishia mateso mengi. Hata hivyo, tangu utotoni, nimekuwa na hali bora ambayo viziwi wengi hawana. Acheni niwasimulie.

Nilipokuwa na umri wa miaka mitano hivi

Kwa muda fulani, walimu wengi waliamini kwamba watoto viziwi wanapaswa kufundishwa kwa kutazama midomo ya mwalimu. Kwa kweli, nchini Ufaransa nilikolelewa, ilikuwa marufuku kuzungumza kwa lugha ya ishara. Hata mikono ya watoto fulani viziwi ilifungwa mgongoni walipokuwa darasani.

Kwa miaka kadhaa utotoni, nilitumia muda fulani kila juma pamoja na mtaalamu wa matamshi. Nilishikwa taya au kichwa na nikaamuriwa kutoa tena na tena sauti ambazo sikuzisikia. Sikuweza kuwasiliana na watoto wengine. Niliteseka sana kipindi hicho.

Kisha, nilipokuwa na umri wa miaka sita, nilipelekwa kwenye shule maalumu ya bweni. Kwa mara ya kwanza, nikakutana na watoto wengine viziwi. Huko pia, lugha ya ishara ilikuwa imepigwa marufuku. Tulipozungumza kwa ishara darasani, tuliadhibiwa kwa kugongwa kwenye vidole au kuvutwa nywele. Hata hivyo, tuliwasiliana kisiri, tukitumia ishara tulizobuni. Mwishowe nilifaulu kuwasiliana na watoto wengine. Ilikuwa miaka minne yenye furaha.

Hata hivyo, nilipokuwa na umri wa miaka kumi, nilipelekwa kwenye shule ya watoto wanaosikia. Nilivunjika moyo sana! Nilifikiri wale watoto wote viziwi walikuwa wamekufa na kwamba ni mimi tu niliyebaki duniani. Kufuatia ushauri wa madaktari, ambao waliogopa ningepoteza ustadi wa kutambua matamshi, familia yangu haikuwa imejifunza lugha ya ishara na sikuruhusiwa kushirikiana na watoto viziwi. Bado ninakumbuka nilipomtembelea daktari fulani. Alikuwa na kitabu cha lugha ya ishara kwenye dawati lake. Nilipoona picha zilizokuwa kwenye jalada, nilimwonyesha  kitabu hicho na kusema, “Ninakitaka!” Mara moja yule daktari akakificha. *

JINSI NILIVYOANZA KUJIFUNZA BIBLIA

Mama alijitahidi kutulea sisi watoto kulingana na kanuni za Kikristo. Alitupeleka kwenye mikutano ya Kutaniko la Mashahidi wa Yehova la Mérignac, karibu na Bordeaux. Nikiwa mtoto, sikuelewa mengi mikutanoni. Hata hivyo, watu mbalimbali waliketi karibu nami kwa zamu na kuandika mambo makuu yaliyosemwa. Niliguswa moyo na upendo na hangaiko lao. Tukiwa nyumbani, mama alinifundisha Biblia, lakini sikuelewa kikamili mambo niliyofundishwa. Nilihisi kama nabii Danieli, ambaye baada ya kupokea unabii kutoka kwa malaika alisema: “Nikasikia, lakini sikuweza kuelewa.” (Danieli 12:8) Katika kisa changu “Niliona, lakini sikuelewa.”

Hata hivyo, pole kwa pole kweli za msingi za Biblia zilitia mizizi moyoni mwangu. Nilithamini mambo niliyoelewa na nikajaribu kuyatumia maishani. Pia, nilijifunza kwa kutazama tabia za wengine. Kwa mfano, Biblia inatuhimiza tuonyeshe subira. (Yakobo 5:7, 8) Lakini sikuelewa subira ni nini. Hata hivyo, kwa kuwatazama waabudu wenzangu wakionyesha sifa hiyo, nilielewa maana ya subira. Kwa kweli, kutaniko la Kikristo limekuwa msaada mkubwa kwangu.

KUVUNJIKA SANA MOYO, KISHA MSISIMKO MKUBWA

Stéphane alinisaidia kuielewa Biblia

Siku moja nilipokuwa tineja, niliwaona vijana fulani viziwi wakizungumza kwa ishara. Nilianza kushirikiana nao kisiri na nikaanza kujifunza Lugha ya Ishara ya Ufaransa. Niliendelea kuhudhuria mikutano ya Kikristo, ambako kijana fulani Shahidi anayeitwa Stéphane alifanya urafiki nami. Alijitahidi sana kuwasiliana nami, na tukawa marafiki wa karibu. Hata hivyo, muda mfupi baadaye jambo baya lilitokea. Stéphane alifungwa gerezani kwa kukataa kujiunga na jeshi. Nilivunjika sana moyo! Stéphane alipokuwa gerezani, nilitamauka sana na nikaacha kuhudhuria mikutano.

Miezi kumi na moja baadaye, Stéphane aliachiliwa huru na akarudi nyumbani. Wazia nilivyoshangaa Stéphane alipoanza kuwasiliana nami akitumia lugha ya ishara. Sikuamini macho yangu! Ni nini kilichotukia? Alipokuwa gerezani Stéphane alijifunza Lugha ya Ishara ya Ufaransa. Nilitazama ishara za mikono na uso wa Stéphane, na nikasisimuka nilipofikiria jinsi ambavyo ningefaidika.

MWISHOWE NIKAZIELEWA KWELI ZA BIBLIA

Stéphane alianza kunifundisha Biblia. Tangu wakati huo, nilianza kuunganisha kweli mbalimbali za Biblia nilizokuwa nimejifunza. Nilipokuwa mtoto nilipenda kutazama picha maridadi kwenye machapisho yetu ya Biblia, na kuwalinganisha wahusika huku nikichunguza kwa makini kila kitu ili nikumbuke hadithi hizo. Nilijua kumhusu Abrahamu, “uzao” wake, na ule “umati mkubwa,” lakini ni wakati tu mambo hayo yalipofafanuliwa katika lugha ya ishara ndipo nilipoyaelewa kikamili. (Mwanzo 22:15-18; Ufunuo 7:9) Ni wazi kwamba nilikuwa nimeipata lugha yangu, lugha iliyogusa moyo wangu.

Sasa, kwa vile nililelewa mambo yaliyosemwa mikutanoni, moyo wangu ulichochewa na nikatamani kujifunza mengi. Kwa msaada wa Stéphane, niliendelea kuielewa Biblia, na kufikia mwaka wa 1992, nikajiweka wakfu kwa Yehova Mungu na kubatizwa. Hata hivyo, licha ya maendeleo niliyofanya, nilikuwa mwenye haya kwa sababu sikuweza kuwasiliana nilipokuwa mtoto.

 KUPAMBANA NA WOGA

Mwishowe, kikundi chetu kidogo cha viziwi kiliunganishwa na kutaniko la Pessac, lililo kwenye kitongoji cha jiji la Bordeaux. Hilo lilinisaidia sana na nikaendelea kufanya maendeleo ya kiroho. Ingawa bado nilikuwa nikipambana na tatizo la kuwasiliana, rafiki zangu wenye uwezo wa kusikia walihakikisha kwamba nilielewa kila kitu. Wenzi wa ndoa Gilles na Elodie, walijitahidi sana kuwasiliana nami. Mara kwa mara, baada ya mikutano walinialika kula chakula au kunywa kahawa pamoja, na hivyo tukawa marafiki wakubwa. Inafurahisha sana kuwa miongoni mwa watu wanaofuata njia za Mungu zenye upendo!

Mke wangu, Vanessa, amenisaidia sana

Huko ndiko nilikokutana na msichana mrembo Vanessa. Nilivutiwa na tabia yake ya kuwajali watu na mtazamo wa kupenda haki. Hakuona kamwe hali yangu ya kuwa kiziwi kama kizuizi, badala yake, aliiona kuwa nafasi ya kujifunza mengi. Tulipendana, na tukaoana mwaka wa 2005. Ingawa ni vigumu kwangu kuwasiliana vizuri, Vanessa amenisaidia kupambana na woga na kujieleza waziwazi. Ninathamini sana msaada wake ninaposhughulikia majukumu yangu.

ZAWADI NYINGINE KUTOKA KWA YEHOVA

Mwaka tulioona, nilialikwa kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Ufaransa huko Louviers kwa mwezi mmoja kwa ajili ya mazoezi ya kutafsiri. Hivi karibuni, ofisi hiyo imekuwa na kazi nyingi ya kutayarisha DVD za machapisho mbalimbali katika Lugha ya Ishara ya Ufaransa. Lakini kwa sababu kazi ni nyingi, watafsiri zaidi walihitajika.

Nikitoa hotuba inayotegemea Biblia kwa kutumia Lugha ya Ishara ya Ufaransa

Mimi na Vanessa tuliliona kuwa pendeleo na zawadi kubwa kutoka kwa Yehova Mungu kutumika kwenye ofisi ya tawi. Hata hivyo, tulikuwa na wasiwasi. Ingekuwaje kwa kikundi chetu cha lugha ya ishara? Tungefanya nini na nyumba yetu? Je, Vanessa angepata kazi katika eneo hilo? Kwa njia ya ajabu, Yehova alisuluhisha kila tatizo. Kwa kweli nilihisi upendo wa Yehova kutuelekea na pia kuwaelekea viziwi.

KUTEGEMEZWA NA WATU WENYE UMOJA

Baada ya kufanya kazi ya kutafsiri, sasa ninaelewa vizuri kazi inayohusika katika kuwasaidia viziwi wamjue Mungu. Na inafurahisha kama nini kuona wafanyakazi wenzangu wakijitahidi kuwasiliana nami! Ninaguswa moyo sana ninapoona wakijitahidi kuzungumza kwa ishara. Sijihisi mpweke, hata kidogo. Matendo hayo yote ya upendo ni wonyesho wa umoja usio na kifani miongoni mwa watu wa Yehova.—Zaburi 133:1.

Nikifanya kazi katika Idara ya Tafsiri kwenye ofisi ya tawi

Ninathamini kwamba kupitia kutaniko la Kikristo, sikuzote Yehova amehakikisha nimepata mtu wa kunisaidia. Pia, ninathamini sehemu ndogo ambayo nimetimiza katika kuwasaidia viziwi wenzangu kumjua Muumba wetu mpendwa na kumkaribia. Ninatazamia siku ambayo vizuizi vyote vya mawasiliano vitaondolewa na wanadamu wote kwa umoja watazungumza ile “lugha safi,” inayohusiana na kujua ukweli kumhusu Yehova Mungu na makusudi yake.—Sefania 3:9.

^ fu. 9 Mwaka wa 1991, Serikali ya Ufaransa iliidhinisha rasmi matumizi ya lugha ya ishara katika kuwaelimisha watoto viziwi.