Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Una ‘Moyo wa Kumujua’ Yehova?

Je, Una ‘Moyo wa Kumujua’ Yehova?

“Nami nitawapa moyo wa kunijua, kwamba mimi ni Yehova; nao watakuwa watu wangu.”​—YER. 24:7.

1, 2. Kwa nini watu wengi wanavutiwa na matunda ya tini?

 JE, UNAPENDA kula matunda ya tini, yenye kukauka ao mabichi? Watu wengi wanapenda kula matunda hayo, na kwa hiyo, tini inapandwa sana. Wayahudi walipenda sana matunda hayo. (Nah. 3:12; Lu. 13:6-9) Matunda ya tini yana nyuzinyuzi, na vitu vinavyozuia chembe zisiharibike upesi; kwa hiyo watu fulani wanasema kama matunda hayo ni mazuri kwa ajili ya moyo.

2 Wakati fulani Yehova alilinganisha mioyo na matunda ya tini. Mungu hakupenda kuzungumuzia faida ya kula matunda ya tini ya kawaida. Alikuwa akizungumuzia matunda ya mufano. Yale aliyosema kupitia nabii Yeremia yanahusu moyo wako na mioyo ya wale unaowapenda. Tunapozungumuzia yale aliyosema, tufikirie maana yake kwa Wakristo.

3. Tini zinazozungumuziwa katika Yeremia sura ya 24 zinamaanisha nini?

3 Acheni tuzungumuzie kwanza jambo fulani ambalo Mungu alisema katika siku za Yeremia kuhusu matunda ya tini. Katika mwaka wa 617 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, taifa la Yuda lilikuwa katika hali mbaya ya kiroho. Mungu alimuonyesha Yeremia katika maono jambo ambalo lingepata taifa hilo wakati ujao, akitumia aina mbili ya tini: “Nzuri sana” na “mbaya sana.” (Soma Yeremia 24:1-3.) Tini mbaya zilifananisha Mufalme Sedekia na wengine kama yeye, waliotendewa kwa ukali na Mufalme Nebukadneza na jeshi lake. Tuseme nini basi kuhusu Ezekieli, Danieli na wenzake watatu ambao tayari walikuwa Babiloni, na Wayahudi fulani ambao karibuni wangepelekwa huko? Wote hao walifananisha tini nzuri. Mabaki yao wangerudi kujenga upya Yerusalemu na hekalu lake. Jambo hilo lilitokea kwa wakati wake.​—Yer. 24:8-10; 25:11, 12; 29:10.

4. Ni kitia-moyo gani tunachoweza kupata kutokana na yale ambayo Mungu alisema kuhusu tini nzuri?

4 Yehova aliwaambia hivi wale waliofananisha tini nzuri: “Nitawapa moyo wa kunijua, kwamba mimi ni Yehova; nao watakuwa watu wangu.” (Yer. 24:7) Hilo ndilo andiko la musingi la habari hii, na ni lenye kutia moyo kabisa. Mungu iko tayari kupatia watu ‘moyo wa kumujua.’ Katika andiko hilo, “moyo” unafananisha mwelekeo wa mutu. Bila shaka, unapenda kuwa na moyo kama huo na kuwa kati ya watu wa Mungu. Hatua zinazotusaidia tuwe na moyo kama huo na kuwa kati ya watu wa Mungu ni kujifunza Neno lake, kutubu na kugeuka, kumutolea maisha yetu katika sala, na kubatizwa katika jina la Baba, na la Mwana, na roho takatifu. (Mt. 28:19, 20; Mdo. 3:19) Labda umekwisha kufanya hatua hizo, ao labda unakusanyika na Mashahidi wa Yehova na unaendelea kutimiza hatua hizo.

5. Yeremia aliandika kuhusu moyo wa nani hasa?

5 Iwe tumekwisha kufanya hatua fulani ao hatua zote, tunapaswa kuendelea kuwa waangalifu sana kuhusu maoni yetu na mwenendo wetu. Sababu gani? Tutajua sababu tutakapozungumuzia mambo mengi ambayo Yeremia aliandika kuhusu moyo. Sura fulani za kitabu cha Yeremia zilihusu mataifa yaliyozunguka taifa la Yuda, zaidi sana wakati wa utawala wa wafalme watano wa taifa hilo. (Yer. 1:15, 16) Yeremia aliandikia zaidi sana wanaume, wanawake, na watoto waliokuwa katika taifa ambalo lilijitoa tayari kwa Yehova. Mababu zao walikubali kwa kujipendea kuwa taifa la Yehova. (Kut. 19:3-8) Na katika siku za Yeremia, watu walisema waziwazi kwamba wamejitoa kwa Mungu. Walisema hivi: “Tumekuja kwako, kwa maana wewe, Ee Yehova, ni Mungu wetu.” (Yer. 3:22) Lakini, unafikiri moyo wao ulikuwa katika hali gani?

JE, MOYO WETU WA MUFANO UNAHITAJI UPASUAJI?

6. Sababu gani tunapaswa kupendezwa na yale ambayo Mungu alisema kuhusu moyo?

6 Waganga wa siku zetu wanaweza kutumia ufundi wa kisasa ili kuona hali ya moyo na namna unavyotumika. Hata hivyo, Yehova anaweza kufanya zaidi ya kile waganga wanafanya, kama alivyofanya katika siku za Yeremia. Mungu anajua vizuri zaidi hali ya moyo, hilo linaonekana katika maneno aliyosema: ‘Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari. Ni nani anayeweza kuujua? Mimi, Yehova, ninauchunguza moyo, ili kumupa kila mumoja kulingana na njia zake, kulingana na matunda ya matendo yake.’ (Yer. 17:9, 10) ‘Uchunguzi huo wa moyo’ si uchunguzi ambao waganga wanafanya kuhusu moyo wa kawaida ambao kwa muda wa miaka 70 ao 80 unaweza kupiga-piga mara miliare tatu hivi. Lakini, katika andiko hilo Yehova alikuwa akizungumuzia moyo wa mufano. “Moyo” huo unamaanisha mutu wote wa ndani, ni kusema, tamaa, mawazo, mwelekeo, nia, na miradi ya mutu. Huo ndio moyo wako. Mungu anaweza kuuchunguza, na kwa kiasi fulani, wewe pia unaweza kuuchunguza.

7. Katika siku za Yeremia moyo wa Wayahudi wengi ulikuwa katika hali gani?

7 Ili kuwa tayari kuchunguza moyo wetu, tunapaswa kujiuliza hivi: “Moyo wa mufano wa Wayahudi wengi wa wakati wa Yeremia ulikuwa katika hali gani?” Ili kujibu fikiria musemwa huu usio wa kawaida ambao Yeremia alitumia: “Nyumba yote ya Israeli hawakutahiriwa moyoni.” Hakuwa akizungumuzia kutahiriwa kwa wanaume Wayahudi, kwa kuwa aliongeza hivi: “‘Tazama! Siku zinakuja,’ asema Yehova, ‘nami nitamutoza hesabu kila mutu aliyetahiriwa lakini ambaye bado yumo katika hali ya kutotahiriwa.’” Kwa hiyo, hata ikiwa wanaume Wayahudi walikuwa wenye kutahiriwa kimwili, kwa njia ya mufano “hawakutahiriwa moyoni.” (Yer. 9:25, 26) Hilo lilimaanisha nini?

8, 9. Wayahudi wengi walihitaji kufanya nini kuhusiana na mioyo yao?

8 Jambo linalotusaidia kuelewa maana ya usemi “hawakutahiriwa moyoni” ni yale ambayo Mungu aliwaomba Wayahudi kufanya: ‘Muondoe magovi ya mioyo yenu, ninyi watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalemu; ili gazabu yangu isitoke kwa sababu ya ubaya wa matendo yenu.’ Lakini ubaya wa matendo yao ulitoka wapi? Katika moyo wao, ni kusema, mutu wao wa ndani. (Soma Marko 7:20-23.) Ndiyo, kupitia Yeremia, Mungu aliona vizuri mahali ambapo ubaya wa matendo yao ulitoka. Moyo wao uliazimia kuasi. Nia yao na mawazo yao yalimuchukiza Mungu. (Soma Yeremia 5:23, 24; 7:24-26.) Mungu aliwaambia hivi: “Tahiriweni kwa ajili ya Yehova, na kuondoa magovi ya mioyo yenu.”​—Yer. 4:4; 18:11, 12.

9 Kwa hiyo, Wayahudi wa siku za Yeremia walihitaji upasuaji wa moyo wao wa mufano, ni kusema, ‘kutahiriwa moyo’ kama vile wale walioishi katika siku za Musa walivyofanya. (Kum. 10:16; 30:6) ‘Kuondoa magovi ya mioyo yao’ kulimaanisha kuachana na mambo yaliyofanya mioyo yao iwe migumu, kama vile mawazo yao, mambo waliyohangaikia ao kupenda sana, ao nia yao iliyopingana na mapenzi ya Mungu.​—Mdo. 7:51.

KUWA NA ‘MOYO WA KUMUJUA’ YEHOVA LEO

10. Kama Daudi alivyoonyesha, tunapaswa kuwa na tamaa ya kufanya nini?

10 Sisi ni wenye shukrani kabisa leo kwa kuwa Mungu ametusaidia tuelewe moyo wa mufano. Lakini, watu fulani wanaweza kujiuliza hivi: “Sababu gani Mashahidi wa Yehova leo wanahangaikia sana hali ya moyo wa mufano?” Hawafanye hivyo kwa sababu wengi katika makutaniko yao wanafanya mabaya ao wamekuwa “tini mbaya,” kama Wayahudi wengi walivyokuwa. Tofauti na hilo, watumishi wa Mungu leo ni watu safi wanaojitoa kwa Mungu. Hata hivyo wanafikiria sana jambo hili ambalo Mufalme Daudi alimuomba Yehova: ‘Unichunguze kabisa, Ee Mungu, uujue moyo wangu. Unichunguze, na uzijue fikira zangu zinazofazaisha, na uone kama ndani yangu muna njia yoyote yenye kuumiza.’​—Zab. 17:3; 139:23, 24.

11, 12. (a) Sababu gani kila mutu anapaswa kuchunguza moyo wake? (b) Kuhusiana na moyo, Mungu hatafanya nini?

11 Yehova anataka kila mumoja wetu aendelee kuwa katika hali inayomupendeza [Yehova]. Kuhusu mutu mwenye haki, Yeremia anasema hivi: ‘Wewe, Ee Yehova wa majeshi, unamuchunguza mwadilifu; unaziona figo na moyo.’ (Yer. 20:12) Ikiwa Mweza-yote anachunguza moyo hata wa mutu mwadilifu (ao mwenye haki), hatuone kwamba sisi pia tunapaswa kujichunguza vizuri? (Soma Zaburi 11:5.) Tunapofanya hivyo, tunapaswa kuchunguza kwa uangalifu mielekeo, miradi, ao mawazo yetu ya ndani kabisa. Tukifanya hivyo tunaweza kujua jambo linalofanya moyo wetu uwe mugumu, jambo fulani lililo kama ‘govi la moyo,’ ambalo tunapaswa kuondoa. Kufanya hivyo ni kufanya upasuaji wa moyo wa mufano. Ikiwa unakubali kwamba ni vizuri kuchunguza moyo wako wa mufano, unapaswa kutafuta nini unapofanya hivyo? Na namna gani unaweza kufanya marekebisho yoyote yanayohitajiwa?​—Yer. 4:4.

12 Tunapaswa kuchunga jambo hili katika akili: Yehova hatukaze tubadilike. Kuhusu wale wanaofananishwa na “tini nzuri,” alisema kwamba ‘atawapa moyo wa kumujua.’ Hakusema kwamba atabadili moyo wao wapende ao wasipende. Wao wenyewe wanapaswa kuchagua kuwa na moyo usio mugumu unaotokana na kumujua Mungu. Je, hatungependa kuwa na moyo kama huo?

Kuchunguza moyo wetu na kuondoa nia mbaya zilizo ndani yake kutatuletea baraka nyingi

13, 14. Moyo wa Mukristo unaweza kumuletea shida gani?

13 Yesu alisema: ‘Mawazo mabaya yanatoka moyoni, mauaji, uzinzi, uasherati, wizi, ushuhuda wa uongo, makufuru.’ (Mt. 15:19) Ni kweli kwamba, ikiwa moyo mugumu wa ndugu unamusukuma kufanya uasherati ao uzinifu na hatubu, anaweza kupoteza uhusiano wake pamoja na Mungu milele. Hata mutu ambaye hakufanya uasherati ao uzinifu anaweza kuruhusu tamaa mbaya zikomae katika moyo wake. (Soma Mathayo 5:27, 28.) Ndio sababu kuchunguza moyo wetu ni kwa lazima sana. Unapochunguza moyo wako kwa uangalifu, labda utavumbua kwamba una mawazo mabaya kuelekea mwanaume ao mwanamuke asiyekuwa bibi ao bwana yako, tamaa zenye kujificha ambazo Mungu haruhusu na ambazo unapaswa kuondoa katika moyo wako.

14 Ao ndugu ambaye hajafanya “mauaji” anaweza kuacha moyo wake uweke kinyongo hivi kwamba anafikia kuchukia Mukristo mwenzake. (Law. 19:17) Ikiwa ni hivyo anapaswa kujikaza kutupilia mbali mawazo hayo mabaya yanayoweza kufanya moyo wake uwe mugumu, sivyo?​—Mt. 5:21, 22.

15, 16. (a) Toa mufano unaoonyesha namna Mukristo anaweza kuwa na ‘moyo usiotahiriwa.’ (b) Sababu gani unafikiri kama ‘moyo usiotahiriwa’ haumupendeze Yehova?

15 Jambo lenye kufurahisha ni kwamba, Wakristo wengi hawana moyo kama huo. Yesu pia alizungumuzia “mawazo mabaya.” Mawazo hayo ni maoni ao mielekeo inayoweza kugusa hali mbalimbali za maisha. Kwa mufano, mutu anaweza kushikamana na watu wa jamaa yake kwa njia isiyofaa. Bila shaka, Wakristo wana “upendo wa asili” kuelekea watu wa jamaa yao, si kama wengi wanaokosa upendo kama huo katika hizi “siku za mwisho.” (2 Tim. 3:1, 3) Hata hivyo inawezekana kuvuka mipaka katika kuonyesha upendo huo. Watu wengi wanaamini kwamba “damu ya mutu ni damu ya mutu.” Kwa hiyo, wanatetea watu wa jamaa yao hata ikiwa kufanya hivyo kutavunja sheria ya Mungu. Fikiria yale ambayo ndugu wa Dina walifanya kwa sababu ya upendo wenye kuvuka mipaka. (Mwa. 34:13, 25-30) Wazia chuki iliyokuwa katika moyo wa Absalomu, iliyomuongoza kufanya mipango ya kumuuwisha ndugu yake Amnoni. (2 Sam. 13:1-30) Je, hauone kwamba watu hao wamefanya hivyo kwa sababu wameongozwa na “mawazo mabaya”?

16 Ni kweli kwamba Wakristo wa kweli hawauane. Lakini, je, wanaweza kuendelea kukasirikia ndugu ao dada ambaye alisema ao kumutendea isivyofaa mumoja wa watu wa jamaa yao ao kwa sababu wanawazia tu kwamba alifanya hivyo? Wanaweza kukataa ukaribishaji wa ndugu ambaye wanawazia kwamba alitendea vibaya mutu wa jamaa yao, ao wanaweza kuamua kutokumukaribisha. (Ebr. 13:1, 2) Mawazo mabaya kama hayo na kukosa ukaribishaji haviwezi kukubaliwa hata kidogo kwa sababu vinaonyesha kama mutu hana upendo. Ndiyo, Yehova anayechunguza moyo anaweza kuona kwamba moyo kama huo ni ‘moyo usiotahiriwa.’ (Yer. 9:25, 26) Kumbuka wale ambao Yehova alishauri hivi: ‘Muondoe magovi ya mioyo yenu.’​—Yer. 4:4.

JINSI YA KUPATA NA KULINDA ‘MOYO WA KUMUJUA’ MUNGU

17. Namna gani kumuogopa Yehova kunaweza kutusaidia tuwe na moyo uliyo tayari kukubali mashauri?

17 Utafanya nini ikiwa unajichunguza na kutambua kwamba moyo wako wa mufano haukubali tena mashauri ya Yehova na kwamba kwa kiasi fulani ‘haukutahiriwa’? Labda unatambua kama katika moyo wako muna woga wa mwanadamu, upendo wa vitu vya kimwili, kiburi ao kupenda uhuru. Usifikiri kwamba ni wewe mutu wa kwanza kupatwa na hali hiyo. (Yer. 7:24; 11:8) Yeremia aliandika kwamba Wayahudi wasio waaminifu wa siku zake walikuwa na ‘moyo mugumu na wenye kuasi.’ Aliongeza hivi: “Hawakusema moyoni mwao: ‘Sasa, na tumuogope Yehova Mungu wetu, Yeye anayenyesha mvua kubwa na mvua ya vuli.’” (Yer. 5:23, 24) Ikiwa tunamuogopa Yehova na kusamini yale ambayo ametufanyia, hilo litatusaidia tuondoe ‘govi la moyo,’ sivyo? Woga kama huo unaofaa unaweza kusaidia kila mumoja wetu awe na moyo ulio tayari kutenda yale ambayo Mungu anapenda tufanye.

18. Yehova aliwaahidi nini wale walio katika agano jipya?

18 Na kwa kuwa Yehova ametupatia ‘moyo wa kumujua’ tunaweza kuwa watu wake. Hivyo ndivyo aliahidi Wakristo watiwa-mafuta walio katika agano jipya, aliposema hivi: “Nitaitia sheria yangu ndani yao, nami nitaiandika katika moyo wao. Nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu.” Na alisema nini kuhusu kumujua kabisa? Anaongeza hivi: “Hawatafundishana tena kila mutu na mwenzake wala kila mutu na ndugu yake, wakisema, ‘Mumujue Yehova!’ kwa maana wote watanijua mimi, kuanzia yule aliye mudogo zaidi kati yao mupaka yule aliye mukubwa zaidi kati yao. Kwa maana nitalisamehe kosa lao, na zambi yao sitaikumbuka tena.”​—Yer. 31:31-34. *

19. Wakristo wa kweli wana tumaini gani nzuri ajabu?

19 Iwe utafaidika na baraka zinazotokana na ile agano jipya duniani ao mbinguni, unapaswa kumujua Yehova na kuwa sehemu ya watu wake. Ili ufaidike na baraka hizo, ni lazima zambi zako zisamehewe kwa musingi wa zabihu ya ukombozi ambayo Kristo alitoa. Kujua tu kama unaweza kusamehewa, hilo linapaswa kukuchochea kusamehe wengine, hata wale wanaofanya mambo yanayokuchukiza, sivyo? Ikiwa uko tayari kuondoa katika moyo wako mawazo mabaya kuelekea wengine, utakuwa umetendea moyo wako jambo nzuri. Hilo litaonyesha kama unapenda kumutumikia Yehova na kwamba unamujua vizuri. Utakuwa kama wale ambao Yehova alizungumuzia kupitia Yeremia, aliposema: ‘Nanyi kwa kweli mutanitafuta na kunipata, kwa maana mutanitafuta kwa moyo wenu wote. Nami nitajiacha munipate.’​—Yer. 29:13, 14.

^ Agano jipya linazungumuziwa katika sura ya 14 ya kitabu Mungu Anasema Nasi Kupitia Yeremia.