Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Liheshimu Jina Kuu la Yehova

Liheshimu Jina Kuu la Yehova

“Nitalitukuza jina lako mpaka wakati usio na kipimo.”—ZAB. 86:12.

1, 2. Tofauti na makanisa mengi yanayodai kuwa ya Kikristo, Mashahidi wa Yehova wanalionaje jina la Mungu?

KWA ujumla, makanisa yanayodai kuwa ya Kikristo hayataki kutumia jina la Mungu. Kwa mfano, utangulizi wa tafsiri ya Revised Standard Version unasema hivi: ‘Haifai kamwe kutumia jina la kibinafsi la Mungu mmoja wa pekee katika imani ya ulimwenguni pote ya Kanisa la Kikristo.’

2 Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova wanajivunia kuitwa kwa jina la Mungu na kulitukuza. (Soma Zaburi 86:12; Isaya 43:10.) Kwa kuongezea, tunaliona kuwa pendeleo kuelewa maana ya jina hilo na suala la ulimwengu wote linalohusu kutakaswa kwa jina hilo. (Mt. 6:9) Hata hivyo, hatupaswi kamwe kupuuza pendeleo hilo. Kuhusiana na hilo, acheni tuchunguze maswali matatu muhimu: Kulijua jina la Mungu kunamaanisha nini? Ni katika njia gani Yehova ametenda kulingana na jina lake kuu na hivyo kuongeza utukufu wa jina hilo? Na tunawezaje kutembea katika jina la Yehova?

MAANA YA KULIJUA JINA LA MUNGU

3. Kulijua jina la Mungu kunamaanisha nini?

3 Kulijua jina la Mungu kunahusisha mengi zaidi ya kujua tu neno “Yehova.” Kunatia ndani kuzijua sifa nzuri za Yehova, makusudi yake, na utendaji wake unaofunuliwa katika Biblia, kama vile jinsi alivyoshughulika na watumishi wake. Bila shaka, Yehova anatupatia ufahamu huo hatua kwa hatua, kulingana na utimizo wa kusudi lake. (Met. 4:18) Yehova aliwafunulia wanadamu wawili wa kwanza jina lake; ndiyo sababu Hawa alilitumia baada ya kumzaa Kaini. (Mwa. 4:1) Wazee wa ukoo waaminifu Noa, Abrahamu, Isaka, na Yakobo walilijua jina la Mungu. Zaidi ya hilo, walilithamini hata zaidi Yehova alipowabariki, alipowatunza, na kuwafunulia mambo mbalimbali yanayohusiana na kusudi lake. Musa alipewa ufahamu wa pekee kuhusu jina la Mungu.

Musa alijua maana ya jina la Mungu, na hilo lilitia nguvu imani yake

4. Kwa nini Musa alimuuliza Mungu jina lake, na kwa nini alikuwa na sababu nzuri za kuuliza swali hilo?

 4 Soma Kutoka 3:10-15. Musa alipokuwa na umri wa miaka 80, Mungu alimpa amri hii nzito: “Uwatoe watu wangu wana wa Israeli kutoka Misri.” Kwa heshima, Musa alimuuliza swali muhimu sana. Ni kana kwamba Musa aliuliza hivi: ‘Jina lako ni nani?’ Kwa kuwa jina la Mungu lilijulikana tangu zamani, kwa nini Musa aliuliza swali hilo? Bila shaka, Musa alitaka kujua mengi zaidi kuhusu yule aliyewakilishwa na jina hilo, yaani, mambo hakika ambayo yangewasadikishia watu wa Mungu kwamba kwa kweli Angewakomboa. Musa alikuwa na sababu nzuri ya kuuliza swali hilo kwa sababu Waisraeli walikuwa watumwa kwa muda mrefu. Inaelekea kwamba wangekuwa na shaka ikiwa Mungu wa mababu zao angeweza kuwaokoa. Isitoshe, baadhi ya Waisraeli walikuwa wameanza kuabudu miungu ya Wamisri!—Eze. 20:7, 8.

5. Yehova aliendeleaje kufunua maana ya jina lake alipomjibu Musa?

5 Yehova alijibuje swali la Musa? Kwa sehemu, alisema hivi: “Hivi ndivyo utakavyowaambia wana wa Israeli, ‘NITAKUWA amenituma kwenu.’” * Kisha akaongeza hivi: “Yehova Mungu wa mababu zenu . . . amenituma kwenu.” Mungu alifunua kwamba atakuwa chochote anachochagua kuwa ili kutimiza kusudi lake, na kwamba sikuzote atatimiza ahadi yake. Ndiyo sababu katika mstari wa 15 tunasoma kwamba Yehova mwenyewe alisema hivi: “Hilo ndilo jina langu mpaka wakati usio na kipimo, na huo ndio ukumbusho wangu kwa kizazi baada ya kizazi.” Bila shaka jambo hilo lilimstaajabisha sana Musa na kuitia nguvu imani yake!

YEHOVA ALITENDA KULINGANA NA JINA LAKE

6, 7. Yehova alitendaje kikamili kulingana na jina lake kuu?

6 Muda mfupi baada ya kumtuma Musa, Yehova alitenda kikamili kulingana na jina lake kwa ‘kuthibitika kuwa’ Mkombozi wa Israeli. Aliwaaibisha Wamisri kwa mapigo kumi yenye kuangamiza, na wakati huohuo akaonyesha wazi kwamba miungu ya Misri, kutia ndani Farao, haina nguvu. (Kut. 12:12) Kisha Yehova akaitenganisha Bahari Nyekundu, akawaongoza Waisraeli kuivuka, na kumzamisha Farao na majeshi yake. (Zab. 136:13-15) Katika ‘nyika yote iliyo kuu na yenye kutia woga,’ Yehova alithibitika kuwa Mhifadhi wa uhai kwa kuwapa chakula na maji watu wake ambao huenda idadi yao  ilikuwa kuanzia milioni mbili mpaka milioni tatu au zaidi! Hata alihakikisha kwamba mavazi yao na viatu vyao havichakai. (Kum. 1:19; 29:5) Ndiyo, hakuna kinachoweza kumzuia Yehova kutenda kulingana na jina lake lisilo na kifani. Baadaye, Yehova alimwambia Isaya hivi: “Mimi—mimi ni Yehova, na zaidi ya mimi hakuna mwokozi.”—Isa. 43:11.

7 Yoshua, mrithi wa Musa, alishuhudia pia matendo ya Yehova yenye kuogopesha huko Misri na nyikani. Kwa hiyo, alipokaribia kufa, Yoshua aliwaambia hivi Waisraeli wenzake kwa usadikisho kutoka moyoni: “Nanyi mnajua vema kwa mioyo yenu yote na kwa nafsi zenu zote kwamba halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi. Yote yametimia kwenu. Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya hayo.” (Yos. 23:14) Ndiyo, kwa njia iliyo wazi kabisa, Yehova alitimiza neno lake, ‘alijithibitisha kuwa.’

8. Yehova anatenda kulingana na jina lake kwa njia gani leo?

8 Leo pia, Yehova ‘anathibitika kuwa.’ Kupitia Mwana wake, alitabiri kwamba katika siku za mwisho, ujumbe wa Ufalme ungehubiriwa “katika dunia yote inayokaliwa.” (Mt. 24:14) Ni nani mwingine isipokuwa Mungu Mweza-yote, angeweza kutabiri kuhusu kazi hiyo, kuhakikisha kwamba inafanywa, na kuwatumia watu wengi “wasio na elimu na wa kawaida tu” ili kuitimiza? (Mdo. 4:13) Kwa hiyo, tunaposhiriki katika kazi hii, kwa kweli tunashiriki kutimiza unabii wa Biblia. Tunamheshimu Baba yetu na kuonyesha hivyo kwa kusali hivi: “Jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”—Mt. 6:9, 10.

JINA LAKE NI KUU

Farao alikataa kutambua kwamba Yehova ni Mungu

9, 10. Yehova aliendeleaje kufunua maana ya jina lake aliposhughulika na Waisraeli, na matokeo yalikuwa nini?

9 Muda mfupi baada ya Waisraeli kutoka Misri, Yehova alitimiza jukumu jipya kuelekea watu wake. Kwa msingi wa agano la Sheria, Yehova akawa “mume” wao, na hivyo akachukua majukumu yote yanayohusu daraka hilo. (Yer. 3:14) Na hivyo Waisraeli wakawa mke wake wa mfano, watu walioitwa kwa jina lake. (Isa. 54:5, 6) Kadiri walivyojitiisha kwake kwa hiari na kushika amri zake, ndivyo alivyothibitika kuwa ‘Mume’ mkamilifu. Angewabariki, angewatunza, na kuwapa amani. (Hes. 6:22-27) Hivyo, jina kuu la Yehova lingetukuzwa kati ya mataifa. (Soma Kumbukumbu la Torati 4:5-8; Zaburi 86:7-10.) Kwa kweli, katika historia yote ya taifa la Israeli, wageni wengi walivutiwa na kujiunga na ibada ya kweli. Ni kana kwamba walisema maneno haya ambayo Ruthu Mmoabu alimwambia Naomi:  “Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako Mungu wangu.”—Rut. 1:16.

10 Kwa miaka 1,500 hivi ambayo Yehova alishughulika na Waisraeli, alifunua sifa nyingi ambazo hawakuwa wamejua. Licha ya uasi wa taifa hilo, Yehova alithibitisha tena na tena kuwa yeye ni “Mungu mwenye rehema” na “si mwepesi wa hasira.” Alikuwa Mungu mwenye ustahimilivu na subira isiyo ya kawaida. (Kut. 34:5-7) Hata hivyo, subira ya Yehova ilikuwa na mipaka, na ilifikia mwisho wakati taifa hilo la Wayahudi lilipomkataa na kumuua Mwana wake. (Mt. 23:37, 38) Wazao wa kimwili wa taifa la Israeli hawakuitwa tena kwa jina la Mungu. Kwa ujumla, walikufa kiroho, kama mti uliokauka. (Luka 23:31) Jambo hilo liliathirije mtazamo wao kuelekea jina la Mungu?

11. Jina la Mungu liliachaje kuhusianishwa na Wayahudi?

11 Historia inaonyesha kwamba, baada ya muda,Wayahudi walianza kuwa na maoni ya kishirikina kuelekea jina la Mungu, wakiona kwamba halipaswi kutajwa. (Kut. 20:7) Pole kwa pole, jina la Mungu halikuhusianishwa tena na dini ya Kiyahudi. Bila shaka Yehova alihuzunika kuona jina lake likikosewa sana heshima. (Zab. 78:40, 41) Hata hivyo, ni wazi kwamba Mungu, “ambaye jina lake ni Wivu,” asingeendelea milele kuwaita kwa jina hilo watu waliomkataa na aliowakataa. (Kut. 34:14) Jambo hilo linapaswa kutusaidia kuona umuhimu wa kuliheshimu sana jina la Muumba wetu.

TAIFA JIPYA LINALOITWA KWA JINA LA MUNGU

12. Yehova alianzishaje taifa alilotabiri kwamba lingeitwa kwa jina lake?

12 Yehova alifunua kupitia Yeremia kusudi lake la kufanya “agano jipya” na taifa jipya, Israeli la kiroho. Yeremia alitabiri kwamba washiriki wote wa taifa hilo, ‘kuanzia yule aliye mdogo zaidi kati yao mpaka yule aliye mkubwa zaidi, wangemjua Yehova.’ (Yer. 31:31, 33, 34) Unabii huo ulianza kutimizwa katika Pentekoste ya 33 W.K. Mungu alipoanzisha agano jipya. Taifa jipya, “Israeli wa Mungu,” lililotia ndani Wayahudi na watu wasio Wayahudi, likawa “watu kwa ajili ya jina [la Mungu],” au “watu wanaoitwa kwa jina langu,” akasema Yehova.—Gal. 6:16; soma Matendo 15:14-17; Mt. 21:43.

13. (a) Je, Wakristo wa mapema walilitumia jina la Mungu? Eleza. (b) Unalionaje pendeleo la kulitumia jina la Yehova unapohubiri?

13 Wakiwa ‘watu wanaoitwa kwa jina la Mungu,’ washiriki wa taifa hilo la kiroho walilitumia jina la Mungu, na bila shaka walifanya hivyo waliponukuu Maandiko ya Kiebrania. * Kwa hiyo, mtume Petro alipowahutubia wasikilizaji Wayahudi na wageuzwa-imani kutoka mataifa mbalimbali katika Pentekoste ya 33 W.K., alilitumia jina la Mungu mara kadhaa. (Mdo. 2:14, 20, 21, 25, 34) Wakristo wa mapema walimheshimu Yehova, naye akabariki jitihada zao katika kazi ya kuhubiri. Leo pia, Yehova anabariki utumishi wetu tunapojivunia kutangaza jina lake na kuwaonyesha wanaopendezwa katika Biblia zao wenyewe inapowezekana. Kwa njia hiyo, tunawasaidia kumjua Mungu wa kweli. Hilo ni pendeleo kubwa kama nini kwao na kwetu! Jambo hilo linaweza kuwasaidia baadhi yao kuanza kusitawisha uhusiano mzuri ajabu na Yehova utakaozidi kuimarika na kudumu kwa umilele wote.

14, 15. Licha ya kuenea kwa uasi-imani, Yehova amefanya nini kuhusu jina lake kuu?

14 Baadaye uasi-imani ulianza kuathiri kutaniko la Kikristo la mapema, hasa baada ya mitume kufa. (2 The. 2:3-7) Hata walimu wa uwongo walianza kufuata mapokeo ya Wayahudi ya kutolitumia jina la Mungu.  Lakini, je, Yehova angeruhusu jina lake kuu lifutiliwe mbali? Hangeruhusu kamwe! Ni kweli kwamba leo hatujui kwa uhakika jina hilo lilivyotamkwa, lakini limedumu. Kwa muda mrefu, limetumiwa katika tafsiri mbalimbali za Biblia na pia katika maandishi ya wasomi wa Biblia. Kwa mfano, katika mwaka wa 1757, Charles Peters aliandika kwamba jina “Yehova,” tofauti na majina mengi ya Mungu ya cheo, “linaonekana ndilo linalofunua vizuri zaidi utu wake.” Katika kitabu alichoandika mwaka wa 1797 kuhusu ibada ya Mungu, Hopton Haynes alianza sura ya 7 ya kitabu chake kwa maneno haya: “Jina la kibinafsi la MUNGU walilotumia Wayahudi ni YEHOVA; walimwabudu yeye peke yake; kama alivyofanya Kristo na Mitume wake.” Henry Grew (1781-1862) hakutumia tu jina la Mungu bali pia alitambua kwamba jina hilo limeletewa suto na ni lazima litakaswe. Vivyo hivyo, George Storrs (1796-1879), aliyeshirikiana kwa ukaribu na Charles T. Russell, alilitumia jina la Mungu, sawa tu na alivyofanya Russell.

15 Mwaka wa 1931 ulikuwa muhimu sana, kwa kuwa katika mwaka huo Wanafunzi wa Biblia, kama watu wa Mungu walivyoitwa wakati huo, walianza kutumia jina la Kimaandiko, Mashahidi wa Yehova. (Isa. 43:10-12) Hivyo, wakatangaza ulimwenguni pote kwamba wanajivunia kuwa watumishi wa Mungu wa pekee wa kweli, wakiwa “watu kwa ajili ya jina lake,” wanaolisifu jina hilo. (Mdo. 15:14) Maendeleo hayo yanatukumbusha maneno ya Yehova yanayopatikana katika Malaki 1:11: “Tangu kuchomoza kwa jua mpaka kutua kwake jina langu litakuwa kuu kati ya mataifa.”

TEMBEA KATIKA JINA LA YEHOVA

16. Kwa nini tunapaswa kuona kwamba ni jambo la heshima kutembea katika jina la Yehova?

16 Nabii Mika aliandika hivi: “Vikundi vyote vya watu vitatembea kila kimoja katika jina la mungu wake; bali sisi tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele.” (Mika 4:5) Yehova alipowaruhusu Wanafunzi wa Biblia walitumie jina lake hakuwapa tu heshima isiyo na kifani, bali pia aliwahakikishia kwamba amewakubali. (Soma Malaki 3:16-18.) Vipi wewe? Je, unajitahidi kabisa ‘kutembea katika jina la Yehova’? Je, unajua kutembea katika jina hilo kunahusisha nini?

17. Kutembea katika jina la Mungu kunahusisha nini?

17 Kutembea katika jina la Mungu kunahusisha angalau mambo matatu hivi. Kwanza, ni lazima tuwatangazie wengine jina hilo tukitambua kwamba ni wale tu ‘wanatakaoliitia jina la Yehova ndio wataokolewa.’ (Rom. 10:13) Pili, tunahitaji kuonyesha sifa za Yehova hasa upendo wake. Na tatu, tunatembea katika jina la Mungu tunapotii kwa shangwe viwango vyake vya uadilifu, ili tusililetee suto jina takatifu la Baba yetu. (1 Yoh. 4:8; 5:3) Je, umeazimia ‘kutembea katika jina la Yehova Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo’?

18. Kwa nini wote wanaoliheshimu jina kuu la Yehova wanaweza kutazamia wakati ujao wakiwa na uhakika?

18 Hivi karibuni wote wanaompuuza au kumdharau Yehova watalazimika kumtambua. (Eze. 38:23) Wanatia ndani watu walio kama Farao aliyesema hivi: “Yehova ni nani, hivi kwamba mimi niitii sauti yake?” Punde si punde, alimtambua! (Kut. 5:1, 2; 9:16; 12:29) Hata hivyo, sisi tumeamua kwa hiari kumjua Yehova. Tunajivunia kuitwa kwa jina lake na kumtii tukiwa watu wake. Kwa hiyo, tunatazamia wakati ujao tukiwa na uhakika katika ahadi hii iliyoandikwa kwenye Zaburi 9:10: “Wale wanaolijua jina lako watakutegemea, kwa maana hakika hutawaacha wale wanaokutafuta, Ee Yehova.”

^ fu. 5 Jina la Mungu linatokana na kitenzi cha Kiebrania kinachomaanisha “kuwa.” Kwa hiyo, “Yehova” linamaanisha “Yeye Husababisha Kuwa.”—Mwa. 2:4.

^ fu. 13 Maandiko ya Kiebrania yaliyotumiwa na Wakristo wa mapema yalikuwa na herufi za Tetragramatoni. Ushahidi unaonyesha kwamba ndivyo ilivyokuwa katika nakala za mapema za Septuajinti, yaani, tafsiri ya Kigiriki ya Maandiko ya Kiebrania.