Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tuliheshimu Jina Kubwa la Mungu

Tuliheshimu Jina Kubwa la Mungu

‘Nami nitalitukuza jina lako kwa wakati usio na kipimo.’​—ZAB. 86:12.

1, 2. Tofauti na dini zinazojiita kuwa za Kikristo, Mashahidi wa Yehova wanaliona jina la Mungu namna gani?

 KWA ujumla, dini zote zinazojiita kuwa za Kikristo hazihangaikie jina la Mungu. Kwa mufano, tafsiri ya Revised Standard Version inasema hivi katika maneno yake ya utangulizi: “Kutumia jina lolote la pekee ili kutaja Mungu wa kweli . . . ni jambo lisilofaa kabisa kwa waamini wote wa Kanisa la Kikristo.”

2 Lakini, Mashahidi wa Yehova wanaona kuwa pendeleo kuitwa kwa jina la Mungu na kulitukuza. (Soma Zaburi 86:12; Isaya 43:10.) Zaidi ya hayo, tunaona kuwa pendeleo kuelewa maana ya jina la Mungu na kuelewa sababu gani jina hilo linapaswa kutakaswa. (Mt. 6:9) Hata hivyo, inatuomba kuchukua pendeleo hilo kwa uzito. Kwa hiyo, acheni tuzungumuzie maulizo matatu ya maana: Kujua jina la Mungu kunamaanisha nini? Yehova anatenda kulingana na maana ya jina lake, namna gani kufanya hivyo kunaongezea jina hilo utukufu? Namna gani tunaweza kutembea katika jina la Mungu?

KUJUA JINA LA MUNGU

3. Kujua jina la Mungu kunamaanisha nini?

3 Kujua jina la Mungu hakumaanishe tu kujua kwamba Mungu anaitwa “Yehova.” Kujua jina la Mungu kunamaanisha kujua sifa zake, kusudi lake, na kazi zake kama inavyoonyeshwa katika Biblia; namna alivyotendea watumishi wake zamani. Bila shaka, Yehova anawasaidia watumishi wake kuelewa mambo hayo hatua kwa hatua, kulingana na kutimizwa kwa mapenzi yake. (Met. 4:18) Yehova aliwajulisha Adamu na Eva jina lake; ndio sababu, Eva alilitumia alipozaa Kaini. (Mwa. 4:1) Wazee waaminifu wa zamani kama vile Noa, Abrahamu, Isaka, na Yakobo walilijua jina la Mungu. Tena, kadiri walivyoona kwamba Yehova anawabariki, anawahangaikia, na kuwafunulia sehemu mbalimbali za kusudi lake, waliliheshimu jina hilo zaidi. Musa alipewa pendeleo la pekee la kuelewa jina la Mungu.

Musa alijua maana ya jina la Mungu, na hilo lilitia nguvu imani yake

4. Sababu gani Musa alimuuliza Mungu jina lake, na sababu gani alikuwa na haki ya kufanya hivyo?

4 Soma Kutoka 3:10-15. Musa alipokuwa na miaka 80, Mungu alimupa daraka nzito, alimuamuru hivi: “Uwatoe watu wangu wana wa Israeli kutoka Misri.” Kwa heshima, Musa alikubali, lakini alimuuliza Mungu ulizo fulani lenye maana sana. Alimuuliza hivi: ‘Jina lako nani?’ Kwa kuwa jina la Mungu lilijulikana tangu zamani, Musa alitaka kujua nini kabisa? Ni wazi kwamba, Musa alitaka kujua mengi kuhusu mutu anayeitwa kwa jina hilo, jambo ambalo lingesadikisha watu wake kwamba kwa kweli Mungu angewakomboa. Musa alikuwa na haki ya kuuliza hivyo kwa sababu Waisraeli walikuwa wamepitisha miaka mingi katika utumwa. Bila shaka wangeweza kujiuliza ikiwa kweli Mungu wa mababu zao angewakomboa. Lakini pia, Waisraeli fulani walikuwa hata wameanza kuabudu miungu ya Wamisri.​—Eze. 20:7, 8.

5. Alipomujibu Musa, namna gani Yehova alielewesha zaidi maana ya jina lake?

5 Yehova alimujibu Musa namna gani? Alimujibu hivi: “Hivi ndivyo utakavyowaambia wana wa Israeli, ‘NITAKUWA amenituma kwenu.’” * Kisha akaongeza hivi: “Yehova Mungu wa mababu zenu . . . amenituma kwenu.” Mungu alifunua kwamba atakuwa namna yoyote anayopenda kuwa ili kutimiza kusudi lake, ni kusema, hakuna siku atakosa kutimiza neno lake. Kwa hiyo, kwenye mustari wa 15 tunasoma maneno haya ya Yehova: ‘Hilo ndilo jina langu kwa wakati usio na kipimo, na huo ndio ukumbusho wangu kwa kizazi baada ya kizazi.’ Bila shaka maneno hayo yalimufanya Musa amuheshimu Mungu tena zaidi na yalitia nguvu imani yake.

YEHOVA ANATENDA KULINGANA NA MAANA YA JINA LAKE

6, 7. Namna gani Yehova alitenda kabisa kulingana na maana ya jina lake kubwa?

6 Muda mufupi baada ya kumupa Musa daraka la kukomboa Waisraeli kutoka Misri, Yehova alitenda kabisa kulingana na maana ya jina lake, alijifanya ‘kuwa’ Mukombozi wa Israeli. Aliwanyenyekeza Wamisri kupitia mapigo kumi, na hivyo akaonyesha kwamba miungu ya Wamisri, na Farao mwenyewe, hawana nguvu. (Kut. 12:12) Ndipo Yehova alifungua Bahari Nyekundu, akawavukisha wana wa Israeli, na kuzamisha Farao na jeshi lake. (Zab. 136:13-15) Katika ile ‘nyika [ao jangwa] iliyo kubwa na yenye kutia woga,’ Yehova alijifanya kuwa Mulindaji wa maisha kwa kuwapatia watu wake chakula na maji; watu hao walikadiriwa kuwa milioni mbili ao tatu ao zaidi! Alifanya hata mavazi yao na viatu vyao visichakae. (Kum. 1:19; 29:5) Ndiyo, hakuna kitu kinachoweza kumuzuia Yehova kutenda kulingana na jina lake kubwa. Baadaye Yehova alimuambia nabii Isaya hivi: “Mimi—mimi ni Yehova, na zaidi yangu hakuna mwokozi.”​—Isa. 43:11.

7 Yoshua, ambaye alichukua nafasi ya Musa, alijionea pia matendo ya ajabu ya Yehova huko Misri na katika jangwa. Kwa sababu hiyo, Yoshua alipokaribia kufa aliwaambia Waisraeli wenzake hivi kwa moyo wenye usadikisho: ‘Munajua vema kwa mioyo yenu yote na kwa nafsi zenu zote kwamba halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi. Yote yametimia kwenu. Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya hayo.’ (Yos. 23:14) Ni kweli kwamba, Yehova alitimiza waziwazi ahadi zake, ‘alikuwa kile alichopenda kuwa.’

8. Namna gani Yehova ametenda kulingana na maana ya jina lake leo?

8 Leo pia, Yehova anaendelea ‘kuwa kile anachopenda kuwa.’ Kupitia Mwana wake, Yehova alitabiri kwamba katika siku za mwisho, habari njema ya Ufalme ingehubiriwa “katika dunia yote inayokaliwa.” (Mt. 24:14) Ni Mungu Mweza Yote tu ndiye angeweza kutabiri kwamba kazi kama hiyo itafanywa, na pia kutumia watu wengi “wasio na elimu na wa kawaida” ili kuifanya, sivyo? (Mdo. 4:13) Kwa hiyo, tunapohubiri, tunashiriki katika utimizo wa unabii wa Biblia. Tunamuheshimu Baba yetu na kuonyesha kwamba jina hilo ni la maana sana tunaposali hivi: “Jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”​—Mt. 6:9, 10.

JINA LA MUNGU NI KUBWA

Farao alikataa kutambua mamlaka ya Yehova Mungu

9, 10. Namna Yehova alivyowatendea Waisraeli inatufundisha nini?

9 Muda muchache tu kisha kukombolewa kutoka Misri, Yehova alianzisha uhusiano wa pekee pamoja na watu wake. Kupitia Agano la Sheria, Mungu alikuwa ‘Bwana’ yao, aliyekuwa tayari kutimiza madaraka yake. (Yer. 3:14) Waisraeli, kwa upande mwengine walikuwa, bibi yake wa mufano, watu walioitwa kwa jina lake. (Isa. 54:5, 6) Ikiwa wangejitiisha kwake na kushika amri zake, yeye angekuwa kabisa ‘Bwana’ muzuri kwao. Yehova angewabariki, angewalinda, na angewapa amani. (Hes. 6:22-27) Hilo lingefanya jina kubwa la Yehova litukuzwe katikati ya mataifa. (Soma Kumbukumbu la Torati 4:5-8; Zaburi 86:7-10.) Kwa miaka mingi ya historia ya Waisraeli, wageni wengi walivutiwa na ibada safi. Ni kama vile wageni hao walisema maneno ambayo mwanamuke wa Moabu, Ruthu alimuambia Naomi: “Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako atakuwa Mungu wangu.”​—Rut 1:16.

10 Kwa miaka karibu 1500, mambo ambayo Yehova aliwatendea Waisraeli yalionyesha yeye ni Mungu wa namna gani. Hata ikiwa taifa liliasi mara kwa mara, Yehova alijionyesha kuwa “Mungu mwenye rehema” ‘asiye mwepesi wa hasira.’ Alikuwa Mungu mwenye uvumilivu mukubwa. (Kut. 34:5-7) Hata hivyo, uvumilivu wa Mungu ulikuwa na mwisho, na ulifikia mwisho wakati taifa la Wayahudi lilipomukataa Mwana wake na kumuua. (Mt. 23:37, 38) Wazao wa Waisraeli wa kimwili hawakuwa tena taifa lililoitwa kwa jina la Mungu. Kwa hiyo, walikufa kiroho, kama vile muti ambao umekauka. (Lu. 23:31) Jambo hilo liliwafanya walione jina la Mungu namna gani?

11. Namna gani Wayahudi waliacha kutumia jina la Mungu?

11 Historia inaonyesha kwamba, kisha muda fulani, Wayahudi walianza kuwa na mawazo ya kiuchawi kuhusu jina la Mungu, walianza kufikiri kwamba ni vibaya kulitaja. (Kut. 20:7) Polepole Wayahudi waliacha kulitumia jina la Mungu. Bila shaka, Yehova aliumia sana moyoni alipoona namna walivyokosa kuheshimu jina lake. (Zab. 78:40, 41) Hata hivyo, Mungu, “ambaye jina lake ni wivu,” hangevumilia milele watu hao waendelee kuitwa kwa jina lake; watu ambao wamemukataa na yeye amekataa. (Kut. 34:14) Jambo hilo linatufundisha kwamba tunapaswa kuliheshimu sana jina la Muumbaji wetu.

TAIFA JIPYA LINALOITWA KWA JINA LA MUNGU

12. Namna gani Yehova alitokeza watu kwa ajili ya jina lake?

12 Kupitia nabii Yeremia, Yehova alionyesha kusudi lake la kufanya “agano jipya” pamoja na taifa jipya, Israeli la kiroho. Yeremia alisema kwamba washiriki wote wa Israeli la kiroho, ‘kuanzia yule aliye mudogo zaidi kati yao mupaka yule aliye mukubwa kati yao,’ ‘wangemujua Yehova.’ (Yer. 31:31, 33, 34) Unabii huo ulianza kutimia kuanzia Pentekoste ya mwaka wa 33, Mungu alipofanya agano jipya. Taifa jipya, “Israeli wa Mungu,” linalotia ndani Wayahudi na Watu Wasiokuwa Wayahudi, wamekuwa “watu kwa ajili ya jina [la Mungu],” ao “watu wanaoitwa kwa jina langu,” asema Yehova.​—Gal. 6:16; soma Matendo 15:14-17; Mt. 21:43.

13. (a) Je, Wakristo wa kwanza-kwanza walilitumia jina la Mungu? Eleza. (b) Unaona namna gani pendeleo la kutumia jina Yehova katika kazi yako ya kuhubiri?

13 Kwa kuwa wao ni “watu wanaoitwa kwa jina [la Mungu],” washiriki wa taifa hilo la kiroho walitumia jina la Mungu, walifanya hivyo walipokuwa wakitaja Maandiko ya Kiebrania. * Kwa mufano, mutume Petro alipotoa hotuba mbele ya Wayahudi na watu waliokubali dini ya Kiyahudi kutoka mahali mbalimbali siku ya Pentekoste mwaka wa 33, alitumia jina la Mungu mara nyingi. (Mdo. 2:14, 20, 21, 25, 34) Wakristo wa kwanza-kwanza walimuheshimu Yehova, kwa hiyo, alibariki kazi yao ya kuhubiri. Leo pia, Yehova anabariki kazi yetu ya kuhubiri wakati tunatangaza kwa furaha jina lake na kulionyesha wale wanaopendezwa katika Biblia zao, ikiwezekana. Kwa kufanya hivyo tunawasaidia wamujue Mungu wa kweli. Hilo ni pendeleo kubwa kwetu na kwao pia. Kujua hivyo jina la Mungu kunaweza kumusaidia mutu aanze kuwa na urafiki muzuri pamoja na Yehova, urafiki ambao utaendelea kuwa na nguvu na kudumu milele.

14, 15. Hata ikiwa uasi-imani ulienea, Yehova alifanya nini kwa ajili ya jina lake kubwa?

14 Uasi-imani uliotokea baadaye, ulichafua Kutaniko la Kikristo, zaidi sana kisha kifo cha mitume. (2 Thes. 2:3-7) Waalimu wa uongo walikubali hata desturi ya Wayahudi ya kutolitumia jina la Mungu. Lakini, je, Yehova angeruhusu jina lake lipotee? Hapana hata kidogo! Kwa kweli, haiwezekane kabisa kujua namna jina la Mungu lilivyokuwa likitamkwa, hata hivyo jina hilo limedumu. Mara nyingi, jina hilo limeonekana katika tafsiri mbalimbali za Biblia, na vilevile katika maandishi ya watu wenye elimu ya mambo ya Biblia. Kwa mufano, katika mwaka wa 1757, Charles Peters aliandika kwamba “tofauti na majina mengine ya cheo, Yehova ndilo jina linaloonyesha waziwazi namna Mungu alivyo.” Katika kitabu cha mwaka wa 1797 kuhusu kumuabudu Mungu, Hopton Haynes aliandika hivi katika sura ya 7: “YEHOVA ndilo jina la pekee la MUNGU wa Wayahudi; yeye pekee ndiye waliabudu; na hivyo ndivyo Kristo na Mitume walivyofanya.” Henry Grew (1781-1862) hakutumia tu jina la Mungu, lakini alitambua pia kwamba jina hilo limechafuliwa na linapaswa kutakaswa. Vivyo hivyo, George Storrs (1796-1879), aliyeshirikiana sana na ndugu Charles T. Russell, alitumia jina la Mungu, kama vile Russell alivyofanya.

15 Mwaka wa 1931 ulikuwa wa maana sana, kwa sababu ni katika mwaka huo ndio watu wa Mungu, waliokuwa wakiitwa Wanafunzi wa Biblia, walianza kuitwa kwa jina la Kimaandiko Mashahidi wa Yehova. (Isa. 43:10-12) Kwa kufanya hivyo, walitangazia ulimwengu kwamba walifurahia kuwa watumishi wa Mungu wa pekee wa kweli, walifurahia kuwa “watu kwa ajili ya jina lake,” watu wanaosifu jina hilo. (Mdo. 15:14) Habari hizo zinatukumbusha maneno ya Yehova kwenye Malaki 1:11: ‘Tangu kuchomozwa kwa jua mupaka kutua kwake jina langu litakuwa kubwa kati ya mataifa.’

TUTEMBEE KATIKA JINA LA MUNGU

16. Sababu gani tunapaswa kuona kutembea katika jina la Mungu kuwa pendeleo?

16 Nabii Mika aliandika hivi: ‘Vikundi vyote vya watu vitatembea kila kimoja katika jina la mungu wake; bali sisi tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu kwa wakati usio na kipimo, ndiyo, milele.’ (Mk. 4:5) Yehova aliwaheshimu sana Wanafunzi wa Biblia zaidi kwa kuwaruhusu waitwe kwa jina lake. Hilo lilionyesha pia kwamba anawakubali kuwa watumishi wake. (Soma Malaki 3:16-18.) Lakini, namna gani wewe? Je, unajikaza ili “kutembea katika jina la Yehova”? Je, unaishi kulingana na jina hilo?

17. Kutembea katika jina la Mungu kunamaanisha nini?

17 Kutembea katika jina la Mungu kunamaanisha mambo matatu hivi. Kwanza, tunapaswa kuwatangazia wengine jina hilo, tukitambua kwamba ni wale tu ‘wanaoliitia jina la Yehova ndio wataokolewa.’ (Rom. 10:13) Pili, tunapaswa kuonyesha sifa za Mungu, zaidi sana upendo wake. Na tatu, tunatembea katika jina la Mungu tunapotii kwa furaha kanuni zake za haki ili tusichafue jina takatifu la Baba yetu. (1 Yoh. 4:8; 5:3) Je, umeazimia ‘kutembea katika jina la Yehova Mungu wetu kwa wakati usio na kipimo’?

18. Sababu gani wale wote wanaoheshimu jina kubwa la Mungu wanangojea wakati ujao bila woga?

18 Karibuni wale wote wanaomuzarau Yehova watalazimika kumujua. (Eze. 38:23) Hao ni watu walio kama Farao, aliyesema hivi: “Yehova ni nani, hivi kwamba mimi nitii sauti yake?” Muda muchache tu alilazimika kumujua Yehova. (Kut. 5:1, 2; 9:16; 12:29) Lakini, sisi tumeamua kumujua Yehova. Tunafurahia sana pendeleo letu la kuitwa kwa jina lake na kuwa watu wake wanaomutii. Kwa hiyo, tunangojea kwa uhakika utimizo wa ahadi hii inayopatikana katika andiko la Zaburi 9:10: ‘Wale wanaolijua jina lako watakutegemea, kwa maana hakika hautawaacha wale wanaokutafuta, Ee Yehova.’

^ Jina la Mungu linatoka katika tendo la Kiebrania linalomaanisha “kuwa.” Kwa hiyo, jina “Yehova” linamaanisha “Anafanya iwe.”​—Mwa. 2:4.

^ Tetragrame (herufi ine zinazofanyiza jina la Mungu ao YHWH) ilikuwa katika maandishi ya Kiebrania ambayo Wakristo wa kwanza-kwanza walitumia. Inaonekana kwamba tetragrame ilikuwa pia katika tafsiri ya Kigiriki ya Maandiko ya Kiebrania ya Septante.