Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 KICHWA KIKUU: JE, UNAWEZA KUWA NA MAISHA YENYE KUSUDI

Je, Unaweza Kuwa na Maisha Yenye

Je, Unaweza Kuwa na Maisha Yenye Kusudi?
Kusudi?

“Miaka ya kuishi ni sabini, au tukiwa wenye afya, themanini; lakini yote ni shida na taabu!” —Zaburi 90:10, Biblia Habari Njema.

MANENO hayo ni ya kweli kabisa! Maisha katika ulimwengu huu yamejaa “shida na taabu.” Huenda umejiuliza, ‘Je, ninaweza kuwa na maisha yenye kusudi?’

Kwa mfano, mfikirie Maria. Alikuwa mtu mwenye nguvu na shughuli nyingi, lakini sasa, ana umri wa miaka 84, na hawezi kutoka nyumbani bila msaada. Ingawa akili yake inafanya kazi vizuri, mwili wake hauna nguvu kama zamani. Je, kweli maisha yake yana kusudi?

Namna gani wewe? Huenda wakati mwingine umejiuliza ikiwa maisha yako yana kusudi. Huenda unafanya kazi ileile, inayochosha, na usiyofurahia. Huenda wengine wasitambue jitihada zako. Hata kama sasa umefanikiwa huenda una wasiwasi kuhusu wakati ujao. Nyakati nyingine, unaweza pia kuhisi upweke au hata kushuka moyo. Huenda familia yako imejaa mizozo na matatizo. Labda umefiwa na mpendwa wako. Mwanamume anayeitwa André alimpenda sana baba yake, ambaye aliugua ghafla na kufa. Hilo lilikuwa pigo kubwa sana kwa André, ambaye anahisi hawezi kushinda hali hiyo yenye kuvunja moyo.

Hata tukikabili matatizo gani, tunahitaji kujua jambo fulani: Je, tunaweza kuwa na maisha yenye kusudi? Tunaweza kupata jibu kwa kuchunguza maisha ya mtu aliyeishi duniani miaka 2,000 hivi iliyopita—Yesu Kristo. Licha ya matatizo aliyokabili, Yesu alikuwa na maisha yenye kusudi. Sisi pia tunaweza kuwa na maisha yenye kusudi tukiiga mfano wake.