Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MKARIBIE MUNGU

“Endeleeni Kuomba, Nanyi Mtapewa”

“Endeleeni Kuomba, Nanyi Mtapewa”

“Bwana, tufundishe jinsi ya kusali.” (Luka 11:1) Yesu aliombwa hivyo na mmoja wa wanafunzi wake. Katika jibu lake, Yesu alisimulia mifano miwili inayotufundisha jinsi ya kusali na kusikilizwa na Mungu. Ikiwa umewahi kujiuliza kama Mungu husikiliza sala, utafurahi kujua jibu la Yesu.—Soma Luka 11:5-13.

Mfano wa kwanza unamkazia fikira mtu anayesali. (Luka 11:5-8) Katika hadithi hiyo, mtu fulani anatembelewa na mgeni katikati ya usiku na hana chakula cha kumpa. Kwa mwenyeji, hilo ni jambo la dharura. Ingawa ni usiku, anaenda nyumbani kwa rafiki yake ili aombe mkate. Mwanzoni, rafiki yake anasitasita kuamka kwa sababu yeye pamoja na familia yake wamelala. Lakini bila kuaibika, yule mtu anaendelea kuomba mpaka mwishowe rafiki yake anaamka na kumpa chakula. *

Mfano huo unatufundisha nini kuhusu sala? Yesu anatuambia kwamba tunahitaji kudumu, kuendelea kuomba, kutafuta, na kupiga hodi. (Luka 11:9, 10) Kwa nini? Je, Yesu anamaanisha tunaposali, ni kama tunabisha mlango wa Mungu asiyetaka kufungua? La. Yesu anamaanisha kwamba kinyume na yule rafiki anayesitasita kufungua, Mungu yuko tayari kutimiza mahitaji yanayofaa ya wale wanaosali kwa imani. Tunaonyesha imani kama hiyo kwa kudumu. Tunapoomba tena na tena, tunaonyesha kwa kweli tunahitaji kile tunachoomba na kwamba tunaamini Mungu anaweza kutupatia, ikiwa ni mapenzi yake.—Marko 11:24; 1 Yohana 5:14.

Mfano wa pili unamkazia fikira “Msikiaji wa sala,” Yehova. (Zaburi 65:2) Yesu anauliza: “Ni baba gani kati yenu ambaye, ikiwa mwana wake anaomba samaki, labda atampa nyoka badala ya samaki? Au ikiwa pia anaomba yai, atampa nge?” Jibu ni wazi, hakuna baba mwenye kujali anayeweza kuwapa watoto wake vitu vinavyoweza kuwadhuru. Kisha Yesu anafafanua mfano huo: Ikiwa baba wasio wakamilifu huwapa watoto wao “zawadi zilizo njema, je, Baba aliye mbinguni hatawapa hata zaidi roho takatifu”—zawadi bora zaidi—watoto wake walio duniani wakimwomba! *Luka 11:11-13; Mathayo 7:11.

Mungu yuko tayari kutimiza mahitaji yanayofaa ya wale wanaosali kwa imani

Mfano huo unatufundisha nini kumhusu Yehova, yule “Msikiaji wa sala”? Yesu anatuhimiza tumwone Yehova kama Baba anayejali ambaye yuko tayari kutimiza mahitaji ya watoto wake. Hivyo, waabudu wa Yehova wanaweza kujihisi huru kumwambia mahitaji ya moyo wao. Na wakijua kwamba anataka wafanikiwe, wanaweza kukubali anapojibu maombi yao, hata ikiwa si kama walivyotazamia. *

Usomaji wa Biblia Unaopendekezwa kwa Mwezi Aprili

Luka 7-21

^ fu. 4 Mfano wa Yesu unataja desturi na mazoea fulani halisi. Kwa Wayahudi, kuonyesha ukarimu kulikuwa wajibu muhimu. Familia ilioka mikate ya kutosha siku moja, hivyo watu walipoishiwa na mkate kwa kawaida waliomba. Pia, kama walikuwa maskini, familia nzima ililala sakafuni katika chumba kimoja.

^ fu. 6 Yesu alitumia maneno “hata zaidi,” akilinganisha baba wa kibinadamu na Mungu. Msomi mmoja anafafanua hivi: “Anamaanisha kwamba ‘Ikiwa wa kwanza anaweza kutimiza basi wa pili atatimiza hata zaidi.’”

^ fu. 7 Ili ujifunze mengi kuhusu jinsi ya kusali na kusikilizwa na Mungu, ona sura ya 17 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.