Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinufaishe na Uwanufaishe Wengine kwa Kutumia Neno la Mungu

Jinufaishe na Uwanufaishe Wengine kwa Kutumia Neno la Mungu

“Nimeyaona maagizo yote juu ya mambo yote kuwa ni sawa.”—ZAB. 119:128.

1. Kwa nini tunapaswa kuwa na uhakika kabisa katika Neno la Mungu?

WAZEE wanapofikiria ikiwa mwanafunzi wa Biblia anastahili kushiriki katika huduma ya shambani, wanajiuliza hivi: ‘Je, maelezo yake yanaonyesha anaamini kwamba Biblia ni Neno la Mungu lililoandikwa kwa mwongozo wa roho takatifu?’ * Mtu anayetamani kuwa mhubiri wa Ufalme, na bila shaka watumishi wote wa Mungu, ni lazima waamini jambo hilo. Kwa nini? Uhakika wetu katika Neno la Mungu na ustadi wetu wa kulitumia katika huduma utatuwezesha kuwasaidia wengine kumjua Yehova na kupata wokovu.

2. Kwa nini tunapaswa ‘kuendelea katika mambo tuliyojifunza’?

2 Mtume Paulo alikazia umuhimu wa Neno la Mungu alipomwandikia Timotheo hivi: “Endelea katika mambo uliyojifunza na uliyoshawishiwa kuamini.” “Mambo” aliyotaja Paulo ni kweli za Biblia zilizomchochea Timotheo kuamini habari njema. Kweli hizo zimetuchochea leo kwa njia hiyohiyo, na zinaendelea kutusaidia kuwa na “hekima kwa ajili ya wokovu.” (2 Tim. 3:14, 15) Kwa kawaida tunatumia maneno yafuatayo ya Paulo kuwaonyesha wengine kwamba Mungu ndiye chanzo cha Biblia, lakini huenda tukanufaika zaidi kibinafsi kutokana na maneno hayo yanayopatikana katika 2 Timotheo 3:16. (Soma.) Acheni tuchunguze kwa undani zaidi mstari huo. Kufanya hivyo kutatusaidia kuwa na uhakika zaidi kwamba mafundisho yote ya Yehova yako “sawa.”—Zab. 119:128.

“LENYE FAIDA KWA KUFUNDISHA”

3-5. (a) Umati uliitikiaje hotuba ya Petro siku ya Pentekoste, na kwa nini? (b) Kwa nini watu wengi waliikubali kweli huko Thesalonike? (c) Leo, huenda watu wakavutiwa na nini katika huduma yetu?

3 Yesu aliliambia taifa la Israeli hivi: “Ninatuma kwenu  manabii na watu wenye hekima na wafundishaji wa watu wote.” (Mt. 23:34) Yesu alikuwa akiongea kuhusu wanafunzi wake aliowafundisha kutumia Maandiko katika huduma yao. Katika Pentekoste ya 33 W.K., mtume Petro aliyekuwa mmoja wa ‘wafundishaji hao wa watu wote,’ alihutubia umati wa watu huko Yerusalemu, na katika hotuba hiyo alinukuu sana Maandiko ya Kiebrania. Walipomsikia Petro akifafanua Maandiko hayo, wasikilizaji wengi “walichomwa moyoni.” Walitubu dhambi walizokuwa wamefanya. Watu elfu tatu hivi kati yao walitafuta msamaha wa Mungu na kuwa Wakristo.—Mdo. 2:37-41.

4 Mtume Paulo aliyekuwa pia mfundishaji wa watu wote, alihubiri habari njema mpaka maeneo ya mbali nje ya Yerusalemu. Kwa mfano, katika jiji la Thesalonike huko Makedonia, aliongea na wale waliokuwa wakiabudu katika sinagogi. Kwa Sabato tatu, Paulo ‘alijadiliana nao kwa kutumia Maandiko, akieleza na kuthibitisha kwa marejeo kwamba ilikuwa lazima Kristo ateseke na kufufuliwa kutoka kwa wafu.’ Matokeo yakawa nini? “Baadhi yao [Wayahudi] wakawa waamini,” na ndivyo na “umati mkubwa kati ya Wagiriki.”—Mdo. 17:1-4.

5 Watu wengi huvutiwa na jinsi watumishi wa Mungu wanavyotumia Biblia leo. Baada ya mwenye nyumba fulani nchini Uswisi kumsikiliza dada yetu akisoma andiko, alimuuliza hivi: “Mnamwakilisha nani?” Dada huyo akajibu: “Sisi ni Mashahidi wa Yehova.” Mwenye nyumba akasema: “Nilipaswa kujua hivyo. Ni nani wengine wanaoweza kuja nyumbani kwangu kunisomea Biblia isipokuwa Mashahidi wa Yehova?”

6, 7. (a) Wale wanaofundisha kutaniko wanawezaje kuitumia Biblia vizuri? (b) Kwa nini ni muhimu sana kutumia Maandiko vizuri tunapoongoza mafunzo ya Biblia?

6 Tunawezaje kuitumia Biblia kikamili zaidi tunapofundisha? Ikiwa una pendeleo la kufundisha kutaniko ukiwa jukwaani, taja maandiko hususa ya Biblia. Badala ya kueleza kwa maneno yako maandiko ya msingi au kusoma maandiko yaliyochapishwa kwenye karatasi au kuyasoma katika kifaa cha kielektroniki, fungua Biblia na usome maandiko hayo katika Biblia, na uwahimize wasikilizaji wafanye vivyo hivyo. Pia, chukua wakati wa kutosha kueleza maana ya maandiko hayo kwa njia inayowasaidia wasikilizaji kumkaribia Yehova zaidi. Badala ya kutumia mifano migumu na mambo yanayowachekesha tu wasikilizaji, tumia wakati kufafanua Neno la Mungu.

7 Tunahitaji kukumbuka nini tunapoongoza mafunzo ya Biblia? Tunapotumia machapisho yetu ya Kikristo, ni lazima tuwe waangalifu kutopuuza maandiko ya Biblia. Tunapaswa kumhimiza mwanafunzi asome maandiko yaliyoonyeshwa na kumsaidia kuelewa maana ya maandiko hayo. Jinsi gani? Si kwa kutoa maelezo marefu kana kwamba tunatoa mfululizo wa hotuba, bali kwa kumtia moyo mwanafunzi ajieleze. Badala ya kumwambia mambo anayopaswa kuamini au kufanya, tunaweza kwa busara kumuuliza maswali yatakayomsaidia kufikia mkataa unaofaa. *

“LENYE FAIDA . . . KWA KUKARIPIA”

8. Paulo alikuwa na pambano gani mwilini mwake?

8 Mara nyingi, tunaona “kukaripia” ni kazi ya wazee Wakristo. Ni kweli kwamba waangalizi wana jukumu la ‘kuwakaripia wenye mazoea ya kutenda dhambi.’ (1 Tim. 5:20; Tito 1:13) Lakini pia ni muhimu tujikaripie wenyewe. Paulo alikuwa mfano mzuri sana wa Mkristo aliyekuwa na dhamiri safi. (2 Tim. 1:3) Hata hivyo, aliandika hivi: “Mimi naona ndani ya viungo vyangu sheria nyingine ikipigana na sheria ya akili yangu na kunichukua mateka kwa sheria ya dhambi.” Tukichunguza muktadha wa maneno hayo, tutaelewa vizuri ni vita gani ambavyo Paulo alihitaji  kupigana ili kudhibiti mwelekeo wake wa kufanya dhambi.—Soma Waroma 7:21-25.

9, 10. (a) Huenda Paulo alihitaji kupambana na udhaifu gani? (b) Inaelekea Paulo aliendelea kupigana jinsi gani na dhambi?

9 Paulo alijitahidi kuushinda udhaifu gani? Ingawa hakuutaja waziwazi, alimwandikia Timotheo kwamba mwanzoni, yeye alikuwa “mtu mwenye dharau.” (1 Tim. 1:13) Kabla ya kuwa Mkristo, Paulo aliwachukia sana Wakristo. Kuhusu hisia zake kuelekea wafuasi wa Kristo, aliungama hivi: “Nilikuwa nimejawa na wazimu kupita kiasi juu yao.” (Mdo. 26:11) Paulo alijifunza kudhibiti hasira yake, hata hivyo, huenda mara kwa mara alipambana ili kudhibiti maneno na hisia zake. (Mdo. 15:36-39) Ni nini kilichomsaidia kufaulu?

10 Alipowaandikia Wakristo waliokuwa Korintho, Paulo alieleza mbinu aliyotumia ili kujikaripia. (Soma 1 Wakorintho 9:26, 27.) Aliupiga udhaifu wake wa kibinadamu kwa ngumi za kiroho zilizoelekezwa vizuri. Inaelekea sana kwamba alitafuta mashauri katika Maandiko, akatoa dua ili Yehova amsaidie kuyatumia, kisha akajitahidi sana kuboresha utu wake. * Tunaweza kufaidika kutokana na mfano wake kwa sababu tunapigana vita kama hivyo na mielekeo yetu ya kutokamilika.

11. Tunawezaje ‘kuendelea kujijaribu’ ili kuona ikiwa tunatembea katika njia ya ile kweli?

11 Hatupaswi kamwe kutosheka tu na ibada yetu. Badala yake, tunahitaji ‘kuendelea kujijaribu’ ili kuhakikisha kwamba kwa kweli tunatembea katika njia ya ile kweli. (2 Kor. 13:5) Tunaposoma maandiko kama vile Wakolosai 3:5-10, tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, mimi ninajitahidi kabisa kuua mielekeo yangu ya dhambi, au je, ninadhoofika kiadili? Kituo kinachoonyesha mambo mapotovu kinapofunguka wakati ninapotumia Intaneti, je, mimi hukifunga mara moja au ninatafuta vituo vya Intaneti visivyofaa?’ Kutumia kibinafsi shauri la Neno la Mungu kwa njia hiyo kutatusaidia ‘kukaa macho na kutunza akili zetu.’—1 The. 5:6-8.

“LENYE FAIDA . . . KWA KUNYOOSHA MAMBO”

12, 13. (a) Tunapaswa kuwa na kusudi gani ‘tunaponyoosha mambo,’ na tunawezaje kuiga mfano wa Yesu tunapofanya hivyo? (b) Hatupaswi kutumia maneno ya aina gani ‘tunaponyoosha mambo’ kati yetu na wengine?

12 Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “kunyoosha mambo” linamaanisha “kutengeneza vizuri, kusahihisha, kurekebisha, kurudisha katika hali nzuri.” Nyakati nyingine, ni lazima tuchukue hatua ya kunyoosha mambo kati yetu na wengine ambao hawaelewi vizuri maneno au matendo yetu. Kwa mfano, viongozi wa dini ya Kiyahudi walilalamika kwamba Yesu aliwaonyesha fadhili “wakusanya-kodi na watenda-dhambi.” Yesu aliwaambia hivi: “Watu wenye afya hawahitaji tabibu, bali wenye kuugua ndio wanaomhitaji. Nendeni, basi, mkajifunze maana ya jambo hili, ‘Ninataka rehema, wala si dhabihu.’” (Mt. 9:11-13) Kwa subira na fadhili, Yesu aliwafafanulia watu wote maneno ya Mungu. Hivyo, watu wanyenyekevu walijifunza kwamba Yehova ni “Mungu mwenye rehema na neema, si mwepesi wa hasira naye ni mwingi wa fadhili zenye upendo na kweli.” (Kut. 34:6) Kwa kuwa mwana wa Mungu alijitahidi “kunyoosha mambo,” wengi waliamini habari njema.

13 Mfano wa Yesu unatufunza jinsi tunavyopaswa kuwasaidia wengine. Mtu aliyekasirika anaweza kusema hivi kwa ukali: ‘Ninataka kunyoosha jambo fulani kati yangu na wewe.’ Lakini njia hiyo ya kushughulikia mambo haipatani na andiko la 2 Timotheo 3:16. “Andiko lote” halitupi mamlaka ya kuwakemea wengine kwa hasira. Kama “upanga  unaochoma,” mara nyingi kuwashutumu wengine vikali husababisha uchungu mwingi na kwa kawaida hakuleti faida yoyote.—Met. 12:18.

14-16. (a) Wazee wanawezaje “kunyoosha mambo” kwa njia inayowasaidia wengine kutatua matatizo yao? (b) Kwa nini ni muhimu sana “kunyoosha mambo” kwa kutumia Maandiko unapolea watoto?

14 Kwa hiyo, tunawezaje kuonyesha subira na fadhili ‘tunaponyoosha mambo’? Tuseme wenzi wa ndoa wanaogombana mara kwa mara wanamwomba mzee Mkristo awasaidie. Mzee huyo atafanya nini? Bila kumuunga mkono yeyote kati yao, anaweza kuwasaidia akitumia kanuni za Biblia, labda kanuni zilizo katika sura ya 3 ya kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia. Mzee anapozungumza nao, wenzi hao wanaweza kuona shauri ambalo kila mmoja wao anapaswa kutumia kwa ukamili zaidi. Baadaye, itakuwa vizuri ikiwa mzee huyo atawauliza kuhusu hali ya familia yao na kuwapa msaada zaidi ikiwa unahitajika.

 15 Wazazi wanawezaje “kunyoosha mambo” kwa njia inayowaimarisha kiroho watoto wao? Wazia kwamba unataka kumsaidia binti yako tineja kuepuka rafiki asiyefaa. Kwanza, unapaswa kujua mambo ya hakika kuhusu rafiki huyo. Kisha, ikiwa bado una wasiwasi, unaweza kuongea naye, labda ukitumia habari iliyo katika kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2. Baadaye, unaweza kutumia wakati zaidi pamoja naye. Pia, angalia mtazamo wake anaposhiriki katika utumishi wa shambani au tafrija ya familia. Ukionyesha subira na ukiwa mwenye fadhili, binti yako atatambua kwamba unampenda na kumjali. Inaelekea kwamba atachochewa kutumia shauri ulilompa na kuepuka madhara maishani.

16 Vivyo hivyo, tunaweza kuwatia moyo kwa subira na upendo walio na wasiwasi kuhusu afya yao, walioshuka moyo kwa sababu ya kufutwa kazi, au wale wanaotatanishwa na mafundisho fulani ya Kimaandiko.  Kutumia Neno la Mungu “kunyoosha mambo” huwanufaisha sana watu wa Yehova.

“LENYE FAIDA . . . KWA KUTIA NIDHAMU KATIKA UADILIFU”

17. Kwa nini tunapaswa kukubali na kuthamini nidhamu?

17 “Hakuna nidhamu inayoonekana kwa sasa kuwa yenye shangwe, bali ni yenye kuhuzunisha.” Hata hivyo, “baadaye kwa wale ambao wamezoezwa nayo hiyo huzaa tunda lenye kufanya amani, yaani, uadilifu.” (Ebr. 12:11) Wakristo wengi ambao sasa ni watu wazima wanakubali kwamba nidhamu waliyopewa na wazazi wao Wakristo iliwasaidia. Na kukubali nidhamu kutoka kwa Yehova inayotolewa na wazee Wakristo, hutusaidia kuendelea kutembea katika njia ya uzima.—Met. 4:13.

18, 19. (a) Kwa nini shauri la Methali 18:13 ni muhimu sana katika “kutia nidhamu katika uadilifu”? (b) Wazee wanapoonyesha upole na upendo wanaposhughulika na wakosaji, kwa kawaida matokeo huwa nini?

18 Ustadi unahitajiwa ili kutoa nidhamu kwa njia inayofaa. Yehova aliwaambia Wakristo watoe nidhamu “katika uadilifu.” (2 Tim. 3:16) Hivyo, tunapaswa kutumia kanuni za Biblia tunapotoa nidhamu. Kanuni moja inapatikana katika Methali 18:13: “Yeyote anapojibu jambo kabla ya kulisikia, huo ni upumbavu na aibu kwake.” Kwa hiyo, wazee wanapohitaji kuzungumza na mtu aliyeshtakiwa kwamba amefanya dhambi nzito, ni lazima wachunguze kwa makini sana jambo hilo ili wajue mambo yote ya hakika. (Kum. 13:14) Ni kwa njia hiyo tu ndipo wanapoweza kutoa nidhamu “katika uadilifu.”

19 Isitoshe, Neno la Mungu linawaagiza wazee Wakristo wawarekebishe wengine “kwa upole.” (Soma 2 Timotheo 2:24-26.) Ni kweli kwamba mtu anaweza kumletea Yehova suto na pia kuwaumiza wengine wasio na hatia. Lakini, mzee anapomshauri kwa hasira mtu huyo, hatamsaidia. Hata hivyo, wazee wanapoiga “sifa ya fadhili za Mungu,” wanaweza kumchochea mkosaji kutubu.—Rom. 2:4.

20. Ni kanuni zipi ambazo wazazi wanapaswa kufuata wanapowatia nidhamu watoto wao?

20 Ili wazazi wawalee watoto wao “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova,” ni lazima wafuate kanuni za Biblia. (Efe. 6:4) Baba anapaswa kuepuka kumwadhibu mwana wake kwa kutegemea tu mambo anayoambiwa kuhusu tabia ya mtoto huyo. Hasira kali haipaswi kamwe kuonyeshwa katika familia ya Kikristo. “Yehova ni mwenye upendo mwororo sana na mwenye rehema,” na wale walio na daraka la kuwatia nidhamu watoto wanapaswa kujitahidi kuonyesha sifa hizo za upendo.—Yak. 5:11.

ZAWADI YENYE THAMANI SANA TULIYOPEWA NA YEHOVA

21, 22. Ni maneno gani katika Zaburi 119:97-104 yanayofunua vizuri jinsi unavyohisi kuhusu Neno la Yehova?

21 Pindi moja, mwanamume aliyemwogopa Mungu alieleza sababu iliyomfanya aipende sheria ya Yehova. (Soma Zaburi 119:97-104.) Kwa kujifunza sheria hiyo, alipata hekima, ufahamu, na uelewaji. Kutii shauri la Mungu kulimsaidia kuepuka njia za uwongo zilizowaletea wengine maumivu ya moyo. Kujifunza Maandiko kulimpendeza na kumridhisha. Aliazimia kumtii Mungu ambaye maagizo yake yalimletea manufaa mengi maishani.

22 Je, unathamini sana “kila Andiko”? Maandiko yatakusaidia kuwa na imani kwamba Mungu atatimiza kusudi lake. Shauri lake lililoongozwa na roho hukulinda kutokana na madhara mabaya sana ya kuzoea kufanya dhambi. Unapoyafafanua kwa ustadi, unaweza kuwasaidia wengine kuipata na kuendelea kuifuata barabara inayoongoza kwenye uzima. Acheni tutumie kikamili “kila Andiko” tunapomtumikia Mungu wetu mwenye upendo na hekima yote, Yehova.

^ fu. 1 Tazama kitabu Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova, ukurasa wa 79.

^ fu. 7 Yesu alipofundisha, mara nyingi aliuliza hivi: “Mnaonaje?” Kisha, alisubiri watoe jibu.—Mt. 18:12; 21:28; 22:42.

^ fu. 10 Barua za Paulo zina mambo mengi yanayoweza kututia moyo kuishinda mielekeo ya dhambi. (Rom. 6:12; Gal. 5:16-18) Ni jambo linalopatana na akili kufikia mkataa wa kwamba yeye mwenyewe alitumia mashauri aliyowaandikia wengine.—Rom. 2:21.