Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

‘Tusichoke Kabisa’

‘Tusichoke Kabisa’

“Tusife moyo katika kufanya yaliyo mema.”​—GAL. 6:9.

1, 2. Namna gani kufikiria tengenezo la Yehova kunatia nguvu tumaini letu?

 KUJUA kwamba sisi ni sehemu ya tengenezo la Mungu kunatufanya tumuheshimu zaidi. Maono yaliyoandikwa katika sura ya 1 ya kitabu cha Ezekieli na sura ya 7 ya kitabu cha Danieli yanaonyesha waziwazi namna Yehova anavyoongoza mambo mupaka mwisho. Yesu anaongoza sehemu inayoonekana ya tengenezo la Yehova hapa duniani ili ikazie uangalifu zaidi kazi ya kuhubiri habari njema, kuwatunza wale wanaofanya kazi hiyo, na kuendeleza ibada ya kweli ya Yehova. Hilo linatufanya tutumaini tengenezo la Yehova kabisa.​—Mt. 24:45.

2 Je, sisi wenyewe tunatembea bega kwa bega na tengenezo hilo la ajabu? Je, bidii yetu katika kweli imeongezeka ao imepunguka? Kisha kufikiria maulizo hayo, labda tutatambua kwamba tumeanza kuchoka ao labda tumepoteza bidii yetu kwa kiasi fulani. Jambo hilo linaweza kutokea. Wakati wa mitume, Paulo aliwatia moyo Wakristo wenzake waige bidii ambayo Yesu alionyesha. Mutume Paulo alisema kwamba kufanya hivyo kungewasaidia ‘wasichoke na kuzimia katika nafsi zao.’ (Ebr. 12:3) Vivyo hivyo, tunatumaini kwamba habari iliyotangulia, ambayo ilionyesha mambo ambayo Yehova anatimiza kupitia tengenezo lake, imetuchochea tuendelee kuwa na bidii na uvumilivu.

3. Tunapaswa kufanya nini ili tusichoke kabisa, na tutazungumuzia nini katika habari hii?

3 Hata hivyo, mutume Paulo alionyesha kwamba mambo mengine yanahitajiwa ili tusichoke kabisa. Alisema kwamba hatupaswe kuacha “kufanya yaliyo mema.” (Gal. 6:9) Kwa hiyo, tunapaswa kufanya mambo fulani. Acheni tuzungumuzie mambo matano yatakayotusaidia kubaki imara na kuendelea kutembea bega kwa bega na tengenezo la Yehova. Kisha tunaweza kujiuliza wenyewe ikiwa kuna mambo fulani ambayo sisi ao familia zetu tunahitaji kufikiria zaidi.

TUKUSANYIKE ILI KUABUDU YEHOVA NA KUTIWA MOYO

4. Sababu gani tunaweza kusema kwamba kukusanyika ni sehemu ya maana sana ya ibada ya kweli?

4 Tangu zamani, watumishi wa Yehova wameona kukusanyika kuwa jambo la maana sana. Huko mbinguni, kuna wakati ambapo malaika wanaalikwa ili kukusanyika mbele ya Yehova. (1 Fal. 22:19; Ayu. 1:6; 2:1; Dan. 7:10) Waisraeli wa zamani walipaswa kukusanyika “ili wasikilize na ili wajifunze.” (Kum. 31:10-12) Wayahudi wa siku za mitume walizoea kwenda kwenye masinagogi ili wasome Maandiko. (Lu. 4:16; Mdo. 15:21) Kukusanyika pamoja kuliendelea kuwa jambo la maana sana wakati kutaniko la Kikristo lilianzishwa, na hata leo jambo hilo linaendelea kuwa sehemu ya maana sana katika ibada yetu. Wakristo wa kweli ‘wanafikiriana ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri.’ Tunapaswa kuendelea ‘kutiana moyo na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri tunavyoona siku ile kuwa inakaribia.’​—Ebr. 10:24, 25.

5. Namna gani tunaweza kutiana moyo kwenye mikutano?

5 Njia moja ya maana ya kutiana moyo ni kutoa majibu ao maelezo kwenye mikutano. Tunaweza kutangaza imani yetu mbele ya wengine kwa kujibu maulizo yanayopatikana katika kichapo tunachojifunza, kwa kuonyesha namna tunavyoweza kutumia andiko fulani, kwa kueleza jambo fulani ambalo ndugu walikutana nalo linaloonyesha faida ya kutumikisha kanuni za Biblia, ao kwa kutumia njia nyingine. (Zab. 22:22; 40:9) Bila shaka, unakubali kwamba hata ikiwa tumekusanyika kwa miaka mingi, tunaendelea kutiwa moyo kwenye mikusanyiko tunaposikiliza maelezo yenye kutoka moyoni ya ndugu na dada, vijana ao wazee.

6. Namna gani mikutano na mikusanyiko yetu inatusaidia tuendelee kumutumikia Yehova kwa bidii?

6 Ni kwa sababu gani zengine Mungu anatuomba tukusanyike kwa ukawaida? Mikutano na mikusanyiko yetu inatufundisha namna ya kuhubiri bila woga na namna ya kushinda upinzani ao kutopendezwa kwa watu wa eneo letu. (Mdo. 4:23, 31) Habari mbalimbali zinazotegemea Maandiko zinatia imani yetu nguvu. (Mdo. 15:32; Rom. 1:11, 12) Mafundisho na vitia moyo tunavyopata kwenye mikutano vinatutolea furaha ya kweli na ‘utulivu siku za musiba.’ (Zab. 94:12, 13) Ni Halmashauri ya Ufundishaji ya Baraza Linaloongoza ndio inasimamia utayarishaji wa chakula chote cha kiroho kwa ajili ya mafundisho yote ya watu wa Yehova duniani kote. Bila shaka tunapaswa kuwa wenye shukrani kwa ajili ya mipango inayofanywa ili tupate mafundisho yenye kujenga kwenye mikutano ya kila juma.

7, 8. (a) Ni nini kusudi kubwa la mikutano yetu? (b) Mikutano inakusaidia namna gani?

7 Hata hivyo, kuna jambo lingine la maana sana kuliko faida tunazopata kwenye mikutano yetu. Kusudi kubwa la mikutano ni kumuabudu Yehova. (Soma Zaburi 95:6.) Ni pendeleo kubwa kabisa kumusifu Mungu wetu wa ajabu! (Kol. 3:16) Yehova anastahili kuabudiwa kwa ukawaida kupitia kuhuzuria kwetu na kutoa kwetu maelezo kwenye mikutano. (Ufu. 4:11) Ndio sababu tunatiwa moyo ‘tusiache kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi.’​—Ebr. 10:25.

8 Je, tunaamini kwamba mikutano yetu ya Kikristo ni mupango unaotusaidia kuvumilia mupaka wakati Yehova atauharibu ulimwengu huu muovu? Ikiwa tunaamini hivyo, mikutano itakuwa kati ya “mambo yaliyo ya maana zaidi” ambayo tutatia pa nafasi ya kwanza katika maisha yetu yenye kujaa mambo mengi. (Flp. 1:10) Ikiwa tunakosa kukusanyika ili kumuabudu Yehova pamoja na ndugu na dada zetu, kunapaswa kuwa na sababu fulani ya lazima kabisa.

TUTAFUTE WALE WANAOSTAHILI

9. Ni nini inayoonyesha kwamba kazi ya kuhubiri ni ya maana?

9 Kufanya mengi katika kazi ya kuhubiri kunatusaidia pia kuendelea kutembea bega kwa bega na tengenezo la Yehova. Yesu alianzisha kazi hiyo alipokuwa hapa duniani. (Mt. 28:19, 20) Kuanzia wakati huo, tengenezo la Yehova limetia kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi pa nafasi ya kwanza. Leo ndugu na dada wamekutana na mambo mengi yanayoonyesha kwamba malaika wanategemeza kazi yetu na kutuongoza kwa ‘wale walio na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele.’ (Mdo. 13:48; Ufu. 14:6, 7) Leo, sehemu yenye kuonekana ya tengenezo la Yehova hapa duniani inafanya kazi hiyo ya lazima sana na kuitegemeza. Je, sisi pia tunatia kazi ya kuhubiri pa nafasi ya kwanza katika maisha yetu?

10. (a) Toa mufano unaoonyesha namna tunavyoweza kuendelea kuifurahia kweli. (b) Namna gani kazi ya kuhubiri imekusaidia ili usichoke?

10 Kuhubiri kwa bidii kunatusaidia tuendelee kuifurahia kweli. Fikiria maneno ya ndugu Mitchel, muzee na painia wa kawaida wa muda murefu. Anasema hivi: “Ninafurahia kuelezea wengine ile kweli. Ninafikiria kila mara habari mupya iliyo katika Munara wa Mulinzi ao Amkeni! na kuvutiwa mara moja na hekima na maelezo yenye kusawazika yanayopatikana katika kila gazeti. Ninakuwa na hamu ya kwenda katika mahubiri ili nione namna gani watu wataitikia, namna ninavyoweza kuamusha kupendezwa kwao. Kazi ya kuhubiri inanisaidia nibaki imara. Ninapanga mambo ili jambo lolote lisivuruge programe yangu ya mahubiri.” Vivyo hivyo, kufanya mengi katika kazi yetu ya kuhubiri kunatusaidia tubaki imara katika siku hizi za mwisho.​—Soma 1 Wakorintho 15:58.

TUKULE CHAKULA CHA KIROHO

11. Sababu gani tunapaswa kukula chakula chote cha kiroho ambacho Yehova anatutolea?

11 Yehova ametutolea kwa uwingi chakula cha kiroho kinachopatikana katika vichapo vyetu ili kututia nguvu. Labda siku moja ulipomaliza kusoma kichapo fulani uliwaza hivi: ‘Hii ndiyo habari niliyohitaji kabisa! Ni kama vile Yehova aliandikisha habari hii kwa ajili yangu!’ Usiwaze kama hilo lilitokea hivi tu. Yehova anatufundisha na kutuongoza kupitia vichapo hivyo. Yehova anasema hivi : “Nitakufanya uwe na ufahamu na kukufundisha katika njia unayopaswa kuiendea.” (Zab. 32:8) Je, tunajikaza kukula chakula chote cha kiroho tunachopokea na kutafakari juu yacho? Kufanya hivyo kutatusaidia tuendelee kuzaa matunda na kubaki nguvu kiroho katika siku hizi za mwisho.​—Soma Zaburi 1:1-3; 35:28; 119:97.

12. Nini nini inayoweza kutusaidia ili tusamini kabisa chakula cha kiroho?

12 Ni vizuri tufikirie kazi inayofanywa ili tupate kwa ukawaida chakula kizuri cha kiroho. Halmashauri ya Uandikaji ya Baraza Linaloongoza inasimamia kazi ya kutafuta habari, kuandika, kusahihisha, kutia picha, kutafsiri na kuchapisha vichapo vyetu na vilevile habari zinazotiwa kwenye adresi yetu ya Internete. Beteli zinazochapisha vichapo zinavituma kwenye makutaniko ya karibu na ya mbali. Sababu gani kazi yote hiyo inafanywa? Kazi hiyo inafanywa ili kuwalisha vizuri kiroho watu wa Yehova. (Isa. 65:13) Kwa hiyo, acheni basi tukule chakula chote cha kiroho tunachopokea kupitia tengenezo la Yehova.​—Zab. 119:27.

TUTEGEMEZE MIPANGO INAYOCHUKULIWA NA TENGENEZO

13, 14. Ni nani wanaotegemeza mipango ya Yehova huko mbinguni, na namna gani tunaweza kuwaiga?

13 Mutume Yohana alimuona Yesu katika maono akiwa juu ya farasi mweupe ili kuharibu wale wanaomupinga Yehova. (Ufu. 19:11-15) Inatia moyo sana kujua kwamba Yesu anafanya kazi na malaika waaminifu na watiwa-mafuta walioshinda hapa duniani, na ambao tayari wamepewa zawadi yao huko mbinguni! (Ufu. 2:26, 27) Wanatutolea mufano muzuri kabisa wa kutegemeza mipango ya Yehova.

14 Vivyo hivyo, mukutano mukubwa unategemeza kikamili kazi ya ndugu za Kristo waliotiwa mafuta ambao wangali hapa duniani na wanaoongoza mambo katika tengenezo la Mungu leo. (Soma Zekaria 8:23.) Namna gani kila mumoja wetu anaweza pia kutegemeza mipango ya tengenezo la Yehova? Njia moja ni kutii wale wanaotuongoza. (Ebr. 13:7, 17) Hilo linaanzia kwanza katika kutaniko letu. Je, maneno yetu yanawafanya wengine waheshimu wazee na kuheshimu daraka lao la kusimamia kutaniko? Je, tunawatia moyo watoto wetu waheshimu wanaume hao waaminifu na kuwaomba mashauri? Zaidi ya hayo, je, tunazungumuzia katika familia zetu namna tunavyoweza kutumia feza zetu ili kutoa michango ya kutegemeza kazi ya kuhubiri duniani pote? (Met. 3:9; 1 Kor. 16:2; 2 Kor. 8:12) Je, tunaona jambo la kulinda Jumba la Ufalme katika hali nzuri kuwa pendeleo la maana? Katika kutaniko ambamo muna heshima na umoja kama huo, roho ya Yehova inamiminika kwa uwingi. Kupitia roho hiyo, Yehova anaendelea kutusaidia ili tusichoke kabisa katika siku hizi za mwisho.​—Isa. 40:29-31.

TUISHI KULINGANA NA YALE TUNAYOFUNDISHA

15. Sababu gani tunapaswa kuendelea kupigana vita ili tuishi kulingana na kusudi nzuri la Yehova?

15 Mwishowe, ili tuvumilie na kuendelea kutembea bega kwa bega na tengenezo la Yehova, tunapaswa kupatanisha maisha yetu na ujumbe tunaohubiri kwa “kuhakikisha lile linalokubalika kwa Bwana.” (Efe. 5:10, 11) Kila siku tunapigana na mawazo ya kufanya mambo mabaya kwa sababu ya mwili wetu wenye zambi, Shetani na ulimwengu muovu. Wengine kati ya ndugu na dada zako wanapigana vita kila siku kama wewe ili kulinda uhusiano wao pamoja na Yehova. Hilo linamufanya Yehova awapende sana. Tusichoke! Kuishi kulingana na kusudi la Yehova kutatuletea furaha kubwa na kutatupatia uhakika kwamba kumuabudu Yehova si kazi bure.​—1 Kor. 9:24-27.

16, 17. (a) Tunapaswa kufanya nini ikiwa tunafanya zambi nzito? (b) Mufano wa dada yetu Ana unatufundisha nini?

16 Hata hivyo, unapaswa kufanya nini ikiwa unafanya zambi nzito? Tafuta musaada haraka iwezekanavyo. Kuficha zambi kutaharibu mambo zaidi. Kumbuka kwamba, Daudi alisema kwamba alipoficha zambi zake, ‘mifupa yake ilichakaa kwa sababu ya kuugua kwake muchana kutwa.’ (Zab. 32:3) Bila shaka, kuficha zambi kutakuchokesha kiakili na kuharibu hali yako ya kiroho, lakini ‘yule anayeungama na kuiacha ataonyeshwa rehema.’​—Met. 28:13.

17 Fikiria mufano wa dada yetu Ana. * Alikuwa painia wa kawaida alipokuwa kijana. Lakini, alianza kuishi maisha ya unafiki. Hilo lilimuletea matatizo mengi. Anasema hivi: “Zamiri yangu iliendelea kunisumbua. Sikuwa na furaha na nilikuwa mwenye kuvunjika moyo kila wakati.” Alifanya nini basi? Anasema kwamba siku moja kwenye mikutano walizungumuzia andiko la Yakobo 5:14, 15. Ana alitambua kwamba alihitaji musaada na alienda kuwaona wazee. Anapofikiria wakati huo, anasema hivi: “Maandiko ni dawa ambayo Yehova ametutolea ili afya yetu ya kiroho iwe nzuri. Si kwepesi kumeza dawa hiyo, lakini inaponyesha. Nilitumikisha mashauri niliyopewa kupitia maandiko hayo, na yalinisaidia sana.” Miaka fulani baadaye, Ana amepata nguvu mupya na anaendelea kumutumikia Yehova kwa bidii na zamiri safi.

18. Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

18 Ni pendeleo kuishi katika siku hizi za mwisho na kuwa katika tengenezo la ajabu la Yehova! Kwa hiyo, acheni tusizarau hata kidogo pendeleo hilo. Badala yake, sisi wote kwa umoja tukusanyike kwa ukawaida na kutaniko letu, tutafute kwa bidii na kwa moyo wote wale wanaostahili walio katika eneo letu, na tufurahie chakula cha kiroho ambacho Yehova anatutolea kwa ukawaida. Acheni pia tutegemeze wale wanaotuongoza na kuishi kulingana na ujumbe tunaohubiri. Tukifanya hivyo, tutaendelea kutembea bega kwa bega na tengenezo la Yehova na hatutachoka kabisa kutenda yaliyo mema.

^ Jina limebadilishwa.