Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hukumu za Mungu—Je, Zilikuwa za Kikatili?

Hukumu za Mungu—Je, Zilikuwa za Kikatili?

ILI kujibu swali hilo, acheni tuchunguze kifupi mifano miwili ya hukumu za Mungu iliyoandikwa katika Biblia—Gharika ya siku za Noa na kuangamizwa kwa Wakanaani.

GHARIKA YA SIKU ZA NOA

WENGINE HUSEMA: “Mungu alitenda kikatili alipoleta gharika iliyoangamiza wanadamu wote isipokuwa Noa na familia yake.”

BIBLIA INASEMA NINI? Mungu alisema: “Ninapendezwa, si na kifo cha mwovu, bali kwamba mtu mwovu ageuke na kuiacha njia yake na kwa kweli aendelee kuishi.” (Ezekieli 33:11) Hivyo, Mungu hakufurahia hata kidogo watu waovu walipoangamia katika siku za Noa. Basi, kwa nini aliwaangamiza?

Biblia inasema kwamba Mungu alipowaangamiza watu waovu zamani, alikuwa “akiweka kielelezo kwa watu wasiomwogopa Mungu juu ya mambo yatakayokuja.” (2 Petro 2:5, 6) Mungu aliweka kielelezo gani?

Kwanza, Mungu alionyesha kwamba ingawa hafurahii kuangamiza waovu, anaona watu wakatili wanaosababisha mateso na mbele zake wana hatia kwa sababu ya matendo yao. Hivi karibuni, ataondoa ukosefu wa haki na mateso yote.

Pili, matendo ya zamani ya Mungu yanaonyesha kwamba kwa upendo Mungu huwaonya watu kabla ya kuleta uharibifu. Noa alikuwa mhubiri wa uadilifu, lakini watu wengi walimpuuza. Biblia inasema: “Hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote.”—Mathayo 24:39.

Je, bado Mungu anafuata kielelezo hicho? Ndiyo. Kwa mfano, aliwaonya Waisraeli kwamba ikiwa wangetenda maovu kama mataifa yaliyowazunguka, angeruhusu adui zao wavamie nchi yao; waharibu jiji lao kuu la Yerusalemu; na kuwapeleka utekwani. Baadaye, Waisraeli walitenda maovu, hata walitoa watoto kama dhabihu. Je, Yehova alichukua hatua? Ndiyo, lakini kwanza aliwatuma manabii, tena na tena, ili waonye watu wake wabadili njia zao kabla hawajachelewa. Hata alisema: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hatafanya lolote isipokuwa awe amewafunulia watumishi wake manabii jambo lake la siri.”—Amosi 3:7.

JINSI UNAVYOHUSIKA: Kielelezo tunachoona katika hukumu za kale za Yehova, kinatupatia  tumaini. Kwa hakika, tunaweza kutazamia hukumu ya Mungu dhidi ya wale ambao kwa ukatili wanasababisha mateso mengi. Biblia inasema: “Watenda-maovu watakatiliwa mbali . . . Bali wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.” (Zaburi 37:9-11) Unaonaje hukumu ambayo itawaondolea wanadamu mateso? Je, ni ya kikatili, au ni ya huruma?

KUANGAMIZWA KWA WAKANAANI

WENGINE HUSEMA: “Kuangamizwa kwa Wakanaani kulikuwa hatia mbaya ya vita vya kikatili sawa na mauaji ya kisasa ya jamii nzima.”

BIBLIA INASEMA NINI? “Njia zake [Mungu] zote ni haki. [Yeye ni] Mungu wa uaminifu, ambaye hana ukosefu wowote wa haki.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Hukumu ya Mungu haiwezi kulinganishwa na vita vya wanadamu. Kwa nini? Kwa sababu, tofauti na wanadamu, Mungu anaweza kusoma mioyo, yaani, kuona jinsi wanadamu walivyo kwa ndani.

Kwa mfano, Mungu alipohukumu majiji ya Sodoma na Gomora na akaazimia kuyaharibu, mwanamume mwadilifu, Abrahamu, alitaka kuhakikisha hukumu ya Mungu ingekuwa ya haki. Hakuamini kwamba Mungu mwenye haki ‘angefagilia mbali mwadilifu pamoja na mwovu.’ Kwa subira, Mungu alimhakikishia kwamba hata kama kungekuwa na watu kumi waadilifu huko Sodoma, Hangeharibu jiji hilo kwa sababu yao. (Mwanzo 18:20-33) Bila shaka, Mungu alichunguza mioyo yao na akaona jinsi walivyokuwa waovu.—1 Mambo ya Nyakati 28:9.

Vivyo hivyo, Mungu aliwahukumu Wakanaani na kwa haki akaagiza waangamizwe. Wakanaani walikuwa wakatili sana, hata walichoma watoto katika moto wa dhabihu. * (2 Wafalme 16:3) Wakanaani walijua kwamba Mungu alikuwa amewaagiza Waisraeli wachukue nchi yote. Wale waliobaki na kupigana walikuwa wakiwapinga kimakusudi Waisraeli na vilevile Yehova, ambaye alikuwa amethibitisha kwa nguvu kwamba alikuwa pamoja na watu wake.

Zaidi ya hayo, Mungu aliwaonyesha rehema Wakanaani walioacha uovu na kukubali viwango vya juu vya Yehova kuhusu maadili. Kwa mfano, kahaba Mkanaani, Rahabu, aliokolewa pamoja na familia yake. Pia, wakaaji wa jiji la Wakanaani la Gibeoni walipotafuta rehema, wao pamoja na watoto wao hawakuangamizwa.—Yoshua 6:25; 9:3, 24-26.

JINSI UNAVYOHUSIKA: Tunajifunza somo muhimu kutokana na hukumu dhidi ya Wakanaani. “Siku ya hukumu na ya kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu” inakaribia haraka sana. (2 Petro 3:7) Ikiwa tunampenda Yehova, tutafaidika atakapoondoa mateso yanayowapata wanadamu kwa kuwaangamiza wale wanaokataa utawala wake wenye haki.

Wakanaani walikuwa wakatili sana, na walimpinga Mungu na watu wake kimakusudi

Kwa upendo Yehova anatukumbusha kwamba maamuzi ambayo wazazi hufanya yanaathiri watoto wao. Neno la Mungu linasema: “Lazima uchague uzima ili uendelee kuwa hai, wewe na uzao wako, kwa kumpenda Yehova Mungu wako, kwa kuisikiliza sauti yake na kwa kushikamana naye.” (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20) Je, maneno hayo ni ya Mungu mkatili au ni ya Mungu anayewapenda watu na anayetaka wafanye uamuzi unaofaa?

^ fu. 15 Wataalamu wamefukua uthibitisho unaoonyesha kwamba ibada ya Wakanaani ilitia ndani kuwatoa watoto dhabihu.