Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Hukumu za Mungu—Je, Zilikuwa Bila Huruma?

Hukumu za Mungu—Je, Zilikuwa Bila Huruma?

ILI kujibu ulizo hilo, acheni tuzungumuzie kwa kifupi mifano miwili ya hukumu za Mungu zinazozungumuziwa katika Biblia: Garika ya siku za Noa na kuangamizwa kwa Wakanaani.

GARIKA YA SIKU ZA NOA

MAMBO AMBAYO WATU WANASEMA: “Mungu hakuwa na huruma alipoleta garika iliyoharibu wanadamu wote isipokuwa tu Noa na familia yake.”

MAMBO AMBAYO BIBLIA INASEMA: Mungu alisema hivi: ‘Ninapendezwa, si na kifo cha muovu, bali kwamba mutu muovu ageuke na kuiacha njia yake na kwa kweli aendelee kuishi. Geukeni, geukeni muziache njia zenu mbaya, maana kwa nini mufe, Ee nyumba ya Israeli?’ (Ezekieli 33:11) Hilo linaonyesha kama uharibifu wa watu waovu katika siku za Noa haukumufurahisha Mungu hata kidogo. Sasa, sababu gani aliwaharibu?

Biblia inajibu kwamba Mungu alipoleta hukumu kama hizo juu ya watu wasiomuogopa wakati wa zamani, alikuwa ‘akiweka kielelezo [ao mufano] kwa watu wasiomuogopa juu ya mambo yatakayokuja.’ (2 Petro 2:5, 6) Mungu aliweka mufano gani?

Kwanza, Mungu alionyesha kwamba hata ikiwa aliumizwa moyoni kwa kuwaharibu watu, anaona watu wasio na huruma wanaoleta mateso na inaomba watoe hesabu kwake kwa ajili ya matendo yao. Mwishowe, Mungu atamaliza ukosefu wa haki na mateso yote.

Pili, mufano wa hukumu za Mungu za wakati wa zamani unaonyesha kama Mungu aliwaonya watu kwa upendo mbele ya kuleta hukumu. Noa alikuwa muhubiri wa haki, lakini watu wengi hawakumusikiliza. Biblia inasema hivi: ‘hawakujali mupaka garika ikaja na kuwafagilia mbali wote.’​—Mathayo 24:39.

Je, Mungu anaendelea kuweka mufano huo? Ndiyo. Kwa mufano, aliwaonya watu wake Waisraeli kwamba ikiwa wanafanya mabaya kama mataifa yaliyowazunguka, angewaacha maadui wavamie inchi; waharibu Yerusalemu muji wao mukubwa, na kuwahamishia katika inchi nyingine. Waisraeli walianza kufanya mabaya​—hata kuwatoa watoto wao kuwa zabihu. Je, Yehova alitenda? Ndiyo, lakini alitenda tu kisha kuwatuma manabii ili kuwaonya watu wake, tena na tena, ili warekebishe njia zao bila kuchelewa. Na hata alisema hivi: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hatafanya lolote isipokuwa awe amewafunulia watumishi wake manabii jambo lake la siri.”​—Amosi 3:7

NAMNA GANI ULIZO HILO LINAKUHUSU WEWE: Mufano ambao tunaona katika hukumu za Yehova za wakati wa zamani unatutolea tumaini. Tunaweza kungojea kwa uhakika hukumu ya Mungu juu ya wale ambao wanaleta mateso kwa sababu ya kukosa huruma. Biblia inasema hivi: “Watenda-maovu watakatiliwa mbali . . . Bali wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.” (Zaburi 37:9-11) Unawaza nini juu ya hukumu ambayo inaondolea wanadamu mateso? Je, ni hukumu ya huruma, ao hukumu isiyo na huruma?

KUANGAMIZWA KWA WAKANAANI

MAMBO AMBAYO WATU WANASEMA: “Uharibifu wa Wakanaani ilikuwa vita ya mauaji makali inayofanana na mauaji ya watu wengi kwa mara moja yanayofanywa leo.”

MAMBO AMBAYO BIBLIA INASEMA: “Njia [za Mungu] zote ni haki. [Yeye ni] Mungu wa uaminifu, ambaye hana ukosefu wowote wa haki.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Hukumu ya haki ya Mungu haifanane na vita ya wanadamu. Sababu gani? Kwa sababu, Mungu ana uwezo wa kusoma mioyo, ni kusema, namna mutu alivyo ndani.

Kwa mufano, Mungu alipohukumu miji ya Sodoma na Gomora na kuamua kuiharibu, Abrahamu, mwanaume mwaminifu alipenda kuhakikisha ikiwa uamuzi wa Mungu ulikuwa wa haki. Hangeweza kuwazia kwamba Mungu wake mwenye haki ‘angefagilia mbali mwadilifu pamoja na muovu.’ Kwa uvumilivu, Mungu alimuhakikishia kwamba ikiwa angepata hata watu kumi wenye haki katika muji wa Sodoma, hangeharibu muji huo kwa sababu yao. (Mwanzo 18:20-33) Ni wazi kwamba Mungu alichunguza mioyo ya watu hao na aliona kama uovu wao ulikuwa mwingi.​—1 Mambo ya Nyakati 28:9.

Vilevile, Mungu alihukumu Wakanaani na kwa haki, akaamua kuwaharibu. Wakanaani walijulikana kuwa watu wasio na huruma, matendo yao yalitia ndani kuunguza watoto wakiwa wazima katika moto wa zabihu. * (2 Wafalme 16:3) Wakanaani walijua kwamba Yehova aliwaamuru Waisraeli wariti inchi yao yote. Wakaanani ambao waliamua kubakia ili kupigana na Waisraeli, walikuwa wanawapinga Waisraeli na pia Yehova, ambaye alikuwa amefanya mambo mengi ili kuonyesha kwamba alikuwa pamoja na watu wake.

Zaidi ya hilo, Mungu aliwahurumia Wakanaani ambao waliacha uovu wao na kukubali kanuni za juu za Yehova za mwenendo safi. Kwa mufano, Rahabu, mwanamuke Mukanaani aliyekuwa kahaba, aliokolewa pamoja na familia yake. Tena, wakati wakaaji wa muji wa Kanaani unaoitwa Gibeoni waliomba huruma, wote waliokolewa pamoja na watoto wao.​—Yoshua 6:25; 9:3, 24-26.

NAMNA GANI ULIZO HILO LINAKUHUSU WEWE: Tunaweza kujifunza jambo la maana kutokana na hukumu ya Mungu juu ya Wakanaani. Tunakaribia sana ‘siku ya hukumu na ya kuangamizwa kwa watu wasiomuogopa Mungu’ iliyotabiriwa. (2 Petro 3:7) Ikiwa tunamupenda Yehova, tutafaidika wakati ataondoa duniani mateso ya wanadamu kwa kuharibu wale wanaokataa utawala wake wa haki.

Wakanaani walijulikana kuwa watu wasio na huruma, na walimupinga Mungu kimakusudi na watu wake

Yehova anatukumbusha kwa upendo kwamba maamuzi ya wazazi yanaweza kuwa na matokeo fulani juu ya watoto wao. Neno la Mungu linasema hivi: ‘Lazima uchague uzima ili uendelee kuwa hai, wewe na uzao wako, kwa kumupenda Yehova Mungu wako, kwa kuisikiliza sauti yake na kwa kushikamana naye.’ (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20) Je, hayo ni maneno ya Mungu asiye na huruma ao ya Mungu anayependa watu na anayetaka wafanye uamuzi muzuri?

^ Wachunguzi wa vitu vya zamani wamevumbua vitu vinavyoonyesha kama ibada ya Wakanaani ilitia ndani kutoa watoto kuwa zabihu.