Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Timiza Jukumu Lako Ukiwa Mweneza-Injili

Timiza Jukumu Lako Ukiwa Mweneza-Injili

“Fanya kazi ya mweneza-injili, timiza kwa ukamili huduma yako.”—2 TIM. 4:5.

1. Kwa nini Yehova anaweza kuitwa Mweneza-injili wa kwanza aliye mkuu zaidi?

MWENEZA-INJILI ni mtu anayetangaza habari njema. Yehova Mungu ndiye Mweneza-injili wa kwanza aliye mkuu zaidi. Mara tu baada ya wazazi wetu wa kwanza kuasi, Yehova alitangaza habari njema ya kwamba nyoka, yaani, Shetani Ibilisi, ataharibiwa. (Mwa. 3:15) Kwa karne nyingi, Yehova aliwaongoza kwa roho takatifu wanaume waaminifu kuandika mambo mengi kuhusu jinsi jina lake litakavyoondolewa suto, jinsi madhara yaliyosababishwa na Shetani yatakavyoondolewa, na jinsi wanadamu wanavyoweza kupata tena baraka zilizopotezwa na Adamu na Hawa.

2. (a) Malaika hutimiza jukumu gani katika kazi ya kueneza injili? (b) Yesu aliwawekea wanadamu wanaoeneza injili kielelezo gani?

2 Malaika pia ni waeneza-injili. Wanatangaza habari njema na kuwasaidia wengine kueneza habari njema. (Luka 1:19; 2:10; Mdo. 8:26, 27, 35; Ufu. 14:6) Namna gani Mikaeli, yule malaika mkuu? Alipokuwa duniani aliitwa Yesu, na aliwawekea kielelezo bora wanadamu wanaoeneza injili. Kwa kweli, Yesu alitumia maisha yake yote kueneza habari njema!—Luka 4:16-21.

3. (a) Ni habari gani njema tunayoeneza? (b) Ni maswali gani tunayopaswa kuchunguza tukiwa waeneza-injili?

3 Yesu aliwaamuru wanafunzi wake wawe waeneza-injili. (Mt. 28:19, 20; Mdo. 1:8) Mtume Paulo alimhimiza hivi Timotheo, mfanyakazi mwenzake: “Fanya kazi ya mweneza-injili, timiza kwa ukamili huduma yako.” (2 Tim. 4:5) Ni habari gani njema tunayoeneza tukiwa wafuasi wa Yesu? Inatia ndani ukweli unaotia moyo wa kwamba Baba yetu wa mbinguni, Yehova, anatupenda. (Yoh. 3:16; 1 Pet. 5:7) Njia kuu ambayo Yehova Mungu hutuonyesha upendo ni kupitia Ufalme wake. Kwa hiyo, tunawaambia wengine kwa furaha kwamba wote wanaojitiisha chini ya utawala wa Ufalme, wanaomtii Mungu, na kutenda uadilifu wanaweza kuwa na  uhusiano naye wakiwa rafiki zake. (Zab. 15:1, 2) Ukweli ni kwamba Yehova anakusudia kuondoa mateso yote yanayosababishwa na ukosefu wa haki. Ataondoa pia maumivu yanayosababishwa na kumbukumbu ya mateso ya wakati uliopita. Hizo ni habari njema kama nini! (Isa. 65:17) Kwa kuwa sisi ni waeneza-injili, acheni tuchunguze majibu ya maswali haya mawili muhimu: Kwa nini ni muhimu sana watu wasikie habari njema leo? Na tunawezaje kutimiza kwa mafanikio jukumu letu tukiwa waeneza-injili?

KWA NINI WATU WANAHITAJI KUSIKIA HABARI NJEMA?

Maswali yanayoulizwa kwa ustadi huwasaidia watu kueleza sababu zinazowafanya waamini mambo fulani

4. Watu huambiwa hadithi gani za uwongo kumhusu Mungu?

4 Wazia ukiambiwa kwamba baba yako amekuacha na kuiacha familia yenu yote. Tuseme kwamba wale wanaodai walimfahamu wanasema alijitenga na watu, alifanya mambo yake kwa siri, na alikuwa mkatili. Huenda hata wengine wakakusadikisha kwamba hakuna haja ya kujaribu kumtafuta baba yako kwa sababu amekufa. Watu wengi wanaambiwa hadithi kama hizo kumhusu Mungu. Wanafundishwa kwamba Mungu ni fumbo, hawezi kujulikana, au ni mkatili. Kwa mfano, viongozi fulani wa kidini wanadai kwamba Mungu atawaadhibu watu wabaya kwa kuwatesa milele katika moto. Wengine husema kwamba Mungu ndiye anayewatesa watu kupitia misiba ya asili. Ingawa matukio hayo huwaangamiza watu wazuri na wabaya, inasemekana kwamba ni adhabu kutoka kwa Mungu.

Maswali hufungua akili na moyo wao ili wakubali kweli

5, 6. Nadharia ya mageuzi na mafundisho ya uwongo yameathirije watu?

5 Wengine wanadai kwamba hakuna Mungu. Kwa mfano, fikiria nadharia ya mageuzi. Wengi wanaoitetea nadharia hiyo wanasema kwamba uhai ulijitokeza bila mwongozo wa mtu fulani mwenye akili. Wanadai kwamba hakuna Muumba. Hata baadhi yao wamesema kwamba mwanadamu ni mnyama tu, basi haishangazi anapotenda kama mnyama. Wanadai kwamba watu wenye nguvu wanaowakandamiza kikatili walio dhaifu wanafuata tu zile zinazoitwa sheria za asili. Basi haishangazi kwamba wengi huamini kuwa ukosefu wa haki utaendelea kuwapo. Kwa hiyo, wale wanaoamini mageuzi hawana tumaini la kweli.

6 Bila shaka, nadharia ya mageuzi na mafundisho ya uwongo yamechangia mateso yanayowakumba wanadamu katika siku hizi za mwisho. (Rom. 1:28-31; 2 Tim. 3:1-5) Mafundisho hayo ya wanadamu si habari njema za kweli zinazodumu. Badala yake, kama mtume Paulo anavyosema, yamewaacha watu ‘katika giza kiakili, wakiwa wametenganishwa mbali na uzima ambao ni wa Mungu.’ (Efe. 4:17-19) Kwa kuongezea, nadharia ya mageuzi na mafundisho ya uwongo yamewazuia watu wasikubali habari njema zinazotoka kwa Mungu.—Soma Waefeso 2:11-13.

Maswali huwasaidia kufikiri ili wafikie mkataa unaofaa

7, 8. Watu wanaweza tu kuelewa kikamili habari njema kwa kufanya nini?

7 Ili wapatanishwe na Mungu, ni lazima kwanza watu wasadiki kwamba Yehova yupo na kwamba kuna sababu nzuri za kumkaribia. Tunaweza kuwasaidia kupata ujuzi huo kwa kuwatia moyo wachunguze uumbaji. Watu wanapochunguza uumbaji wakiwa na mtazamo unaofaa, wanajifunza kwamba Mungu ana hekima na nguvu. (Rom. 1:19, 20) Ili kuwasaidia watu kusitawisha hofu na heshima wanapokazia fikira mambo ambayo Muumba Mkuu ametimiza, tunaweza kutumia broshua hizi mbili: Uhai—Ulitokana na Muumba? na Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai. Hata hivyo, wale wanaojifunza kwa kuuchunguza uumbaji peke yake hawatapata majibu ya maswali yenye kutatanisha sana maishani kama vile, Kwa nini Mungu anaruhusu wanadamu wateseke? Mungu ana kusudi gani kwa ajili ya dunia? Je, Mungu ananijali mimi binafsi?

 8 Watu wanaweza tu kuelewa kikamili habari njema kumhusu Mungu na makusudi yake kwa kujifunza Biblia. Tuna pendeleo kubwa kama nini la kuwasaidia watu kupata majibu ya maswali yao! Hata hivyo, ili tuguse mioyo ya wasikilizaji wetu, tunahitaji kufanya mengi zaidi kuliko tu kuwajulisha mambo ya hakika; ni lazima tuwashawishi. (2 Tim. 3:14) Tunaweza kuwashawishi zaidi tukiiga mfano wa Yesu. Kwa nini alifanikiwa sana katika kufanya hivyo? Sababu moja ni kwamba alitumia maswali kwa ustadi. Tunaweza kumwiga jinsi gani?

WAENEZA-INJILI WENYE MATOKEO HUTUMIA MASWALI KWA USTADI

9. Ni lazima tufanye nini ili tuwasaidie watu kiroho?

9 Kama Yesu, kwa nini tunapaswa kutumia maswali tunapoeneza injili? Fikiria hali hii: Daktari wako anakuambia kwamba ana habari njema. Anaweza kutibu ugonjwa wako akikufanyia upasuaji mkubwa. Huenda ukamwamini. Lakini namna gani akitoa ahadi hiyo hata kabla ya kukuuliza swali lolote kuhusu afya yako? Inaelekea kwamba hutamwamini. Hata kama daktari huyo ni stadi kadiri gani, anapaswa kukuuliza maswali na kukusikiliza unapomweleza kuhusu ugonjwa wako kabla ya kukutibu. Vivyo hivyo, ili tuwasaidie watu wakubali habari njema ya Ufalme ni lazima tujifunze kuuliza maswali kwa ustadi. Tunaweza kuwasaidia tu baada ya kuelewa vizuri hali yao ya kiroho.

Ili tuguse mioyo ya wasikilizaji wetu, ni lazima tuwashawishi

10, 11. Tunaweza kutimiza nini kwa kuiga njia ya Yesu ya kufundisha?

10 Yesu alijua kwamba maswali yanayochaguliwa vizuri humsaidia mwalimu kumwelewa mwanafunzi na pia humchochea mwanafunzi kushiriki katika mazungumzo. Kwa mfano, Yesu alipotaka kuwafundisha wanafunzi wake somo kuhusu unyenyekevu, alianza kwa kuwauliza swali lililowachochea kufikiri. (Marko 9:33) Ili kumfundisha Petro kutumia kanuni, Yesu alimuuliza maswali kadhaa. (Mt. 17:24-26) Pindi nyingine, Yesu alipotaka kuwachochea wanafunzi wake waeleze yaliyo moyoni mwao, aliwauliza maswali kadhaa ya maoni. (Soma Mathayo 16:13-17.) Kwa kutumia maswali na kufafanua mambo, Yesu alitimiza mengi zaidi kuliko kufundisha tu mambo ya hakika. Aligusa mioyo na kuwachochea watu kutenda kupatana na habari njema.

11 Tunapomwiga Yesu kwa kutumia maswali kwa ustadi, tunatimiza angalau mambo matatu. Tunajifunza njia bora zaidi ya kuwasaidia watu, tunashinda vizuia-mazungumzo vinavyoweza kutokea, na tunawafundisha watu wanyenyekevu jinsi ya kujinufaisha wenyewe. Fikiria hali tatu zinazoonyesha jinsi tunavyoweza kutumia maswali kwa ustadi.

12-14. Unaweza kumsaidiaje mtoto kuhubiri habari njema kwa uhakika zaidi? Toa mfano.

12 Hali ya Kwanza: Ukiwa mzazi, ungefanya nini ikiwa mtoto wako tineja angekwambia kwamba hajui jinsi ya kutetea imani yake katika uumbaji anapoongea na mwanafunzi mwenzake? Bila shaka, ungetaka kumsaidia kuwa na uhakika anapowahubiria wengine habari njema. Kwa hiyo, badala ya kumshutumu au kuanza kumshauri, kwa nini usiige mfano wa Yesu kwa kumuuliza maswali ili ujue maoni yake? Utafanyaje hivyo?

13 Baada ya kusoma mafungu fulani katika broshua Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai pamoja na mtoto wako, unaweza kumwomba akueleze ni mawazo gani yanayompendeza zaidi. Mtie moyo  aeleze sababu zinazomfanya aamini kwamba kuna Muumba na kwa nini anataka kufanya mapenzi ya Mungu. (Rom. 12:2) Mweleze mtoto wako kwamba si lazima awe na sababu kama zako za kumwamini Mungu.

14 Mwambie mtoto wako kwamba anapozungumza na mwanafunzi mwenzake anaweza kutumia njia uliyomwonyesha. Yaani, anaweza kumwonyesha mambo fulani ya hakika na kumuuliza maswali ya maoni au ya kumsaidia kuelewa. Kwa mfano, anaweza kumwambia mwanafunzi mwenzake asome sanduku kwenye ukurasa wa 21 wa broshua Chanzo cha Uhai. Kisha, mtoto wako anaweza kumuuliza, “Je, ni kweli kwamba DNA inahifadhi habari nyingi kuliko kompyuta yoyote leo?” Inaelekea kwamba mwanafunzi huyo atajibu ndiyo. Kisha mtoto wako anaweza kuuliza, “Ikiwa wataalamu wa kompyuta hawawezi kubuni kompyuta yenye uwezo mkubwa kama huo, inawezekanaje kwamba DNA ilijitokeza yenyewe?” Ili kumsaidia mtoto wako kutoogopa kuzungumza na wengine kuhusu imani yake, mnaweza kuwa na vipindi vya kawaida vya kufanya mazoezi hayo. Ukimzoeza kutumia maswali kwa ustadi, utamsaidia kutimiza jukumu lake akiwa mweneza-injili.

15. Tunaweza kutumiaje maswali kumsaidia mtu asiyeamini kuwapo kwa Mungu?

15 Hali ya Pili: Katika kazi yetu ya kuhubiri tunakutana na watu wanaotilia shaka kuwapo kwa Mungu. Kwa mfano, huenda mtu akatuambia kwamba haamini kuna Mungu. Badala ya kukatiza mazungumzo, tunaweza kumuuliza kwa heshima amekuwa akiamini hivyo kwa muda gani na kwa nini anafikiri hivyo. Baada ya kusikiliza majibu yake na kumpongeza kwa kufikiria jambo hilo kwa uzito, tunaweza kumuuliza ikiwa atapenda kusoma habari inayothibitisha kwamba uhai uliumbwa. Ikiwa mwenye nyumba yuko tayari kukusikiliza, inaelekea  atasema si jambo la busara kutochunguza uthibitisho huo. Kisha, tunaweza kumpa broshua Uhai—Ulitokana na Muumba? au broshua Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai. Maswali yanapoulizwa kwa busara na kwa fadhili yanaweza kuwa kama ufunguo unaofungua moyo wa mtu ili akubali habari njema.

16. Kwa nini tusitosheke mwanafunzi wa Biblia akisoma majibu katika kitabu cha kujifunzia Biblia?

16 Hali ya Tatu: Tunapoongoza funzo la Biblia, ni rahisi kumwacha mwanafunzi asome majibu yaliyo katika kitabu cha kujifunzia Biblia. Hata hivyo, kufanya hivyo kutamzuia mwanafunzi kukua kiroho. Kwa nini? Kwa sababu inaelekea kwamba mwanafunzi anayesoma tu majibu bila kutafakari hatakuwa na mizizi ya kiroho yenye kina. Anapokabili upinzani, mwanafunzi huyo anaweza kunyauka kwa urahisi kama mmea katika joto kali. (Mt. 13:20, 21) Ili kuepuka hali hiyo, tunahitaji kumuuliza mwanafunzi jinsi anavyohisi kuhusu anayojifunza. Jaribu kuona ikiwa anakubaliana na mafundisho hayo. Na jambo muhimu zaidi, mwombe aeleze kwa nini anakubali au hakubali jambo fulani. Kisha tumia Maandiko kumsaidia kufikiri ili hatimaye afikie mkataa unaofaa. (Ebr. 5:14) Tukitumia maswali kwa ustadi, inaelekea kwamba watu tunaojifunza nao watatia mizizi thabiti katika imani nao wataweza kushinda jitihada za wapinzani au wale wanaotaka kuwapotosha. (Kol. 2:6-8) Tunaweza kufanya nini kingine ili tutimize jukumu letu tukiwa waeneza-injili?

WAENEZA-INJILI WENYE MAFANIKIO HUSAIDIANA

17, 18. Tunapohubiri na Mkristo mwenzetu, tunawezaje kusaidiana?

17 Yesu aliwatuma wanafunzi wake wawili-wawili kuhubiri. (Marko 6:7; Luka 10:1) Baadaye, mtume Paulo alitaja ‘wafanyakazi wenzake’ waliokuwa ‘wamekazana pamoja naye katika habari njema.’ (Flp. 4:3) Kwa kufuata mfano huo ulio katika Maandiko, katika mwaka wa 1953, wahubiri wa Ufalme walianza mpango wa kuwazoeza wengine katika huduma.

18 Unapohubiri na Mkristo mwenzako, mnawezaje kusaidiana? (Soma 1 Wakorintho 3:6-9.) Fungua Biblia yako na usome Maandiko ambayo mhubiri mwenzako anasoma. Mtazame mhubiri mwenzako au mwenye nyumba anapoongea. Sikiliza mazungumzo kwa makini na ikihitajika, msaidie mhubiri mwenzako kujibu swali analoulizwa. (Mhu. 4:12) Hata hivyo, unapaswa kuwa mwangalifu kuhusu jambo hili: Usimkatize mhubiri mwenzako anapotoa hoja fulani za kumsadikisha mwenye nyumba. Ukimkatiza mhubiri mwenzako, unaweza kumvunja moyo na kumfanya mwenye nyumba achanganyikiwe. Nyakati nyingine, huenda ikafaa kuchangia mazungumzo. Lakini ukiamua kufanya hivyo, toa maelezo mafupi mara moja au mbili. Kisha, mwache mhubiri mwenzako aendeleze mazungumzo.

19. Ni vizuri tukumbuke jambo gani, na kwa nini?

19 Kabla ya kuhubiri nyumba inayofuata, unawezaje kusaidiana na mhubiri mwenzako? Kwa nini msitumie wakati huo kuzungumzia njia za kuboresha utangulizi wenu? Muwe waangalifu kutozungumzia mambo yenye kuvunja moyo kuhusu wenye nyumba. Vivyo hivyo, epukeni mtego wa kuwachambua-chambua waeneza-injili wenzetu. (Met. 18:24) Ni vizuri tukumbuke kwamba sisi ni vyombo vya udongo. Yehova ametuonyesha fadhili za pekee sana kwa kutukabidhi hazina ya kutangaza habari njema. (Soma 2 Wakorintho 4:1, 7.) Basi, acheni sote tuonyeshe kwamba tunathamini hazina hiyo kwa kufanya yote tuwezayo ili kutimiza jukumu letu tukiwa waeneza-injili.