Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Timiza Daraka Lako la Mweneza-injili

Timiza Daraka Lako la Mweneza-injili

“Fanya kazi ya mweneza-injili, timiza kwa ukamili huduma yako.”​—2 TIM. 4:5.

1. Sababu gani Yehova anaweza kuitwa Mweneza-injili mukubwa na wa kwanza?

 MWENEZA​-INJILI ni mutu anayetangaza habari njema. Yehova ndiye Mweneza-injili mukubwa na wa kwanza. Kisha tu wazazi wetu wa kwanza kuasi, Yehova alitangaza habari njema iliyoonyesha kwamba yule joka, ni kusema, Shetani Ibilisi ataharibiwa. (Mwa. 3:15) Kwa maelfu ya miaka, Yehova aliwaongoza watumishi wake waaminifu waandike habari zilizoonyesha namna ambavyo jina lake litatakaswa, namna matatizo ambayo Shetani alitokeza yataondolewa, na namna wanadamu wanaweza kupata tena maisha mazuri ambayo Adamu na Eva walipoteza.

2. (a) Malaika wanatimiza daraka gani katika kazi ya kueneza injili? (b) Yesu aliwaachia waeneza-injili wote mufano gani?

2 Malaika pia ni waeneza​-injili. Wanatangaza habari njema, na wanatusaidia kueneza habari hiyo. (Lu. 1:19; 2:10; Mdo. 8:26, 27, 35; Ufu. 14:6) Tuseme nini basi kuhusu Mikaeli, malaika mukubwa? Alipokuwa duniani, Yesu aliwaachia waeneza-injili wote mufano. Namna gani? Kwa kutumia maisha yake yote ili kutangaza habari njema!​—Lu. 4:16-21.

3. (a) Ni habari njema gani ambayo tunatangaza? (b) Tutazungumuzia maulizo gani?

3 Yesu aliwaamuru wanafunzi wake wafanye kazi ya kueneza injili. (Mt. 28:19, 20; Mdo. 1:8) Mutume Paulo alimutia moyo mufanyakazi mwenzake Timotheo hivi: “Fanya kazi ya mweneza-injili, timiza kwa ukamili huduma yako.” (2 Tim. 4:5) Ni habari njema gani ambayo sisi wafuasi wa Yesu tunatangaza? Habari njema hiyo inatia ndani kweli hii yenye kufariji: Yehova, Baba yetu wa mbinguni, anatupenda. (Yoh. 3:16; 1 Pet. 5:7) Njia moja kubwa inayoonyesha kwamba Yehova anatupenda ni mupango aliochukua wa kusimamisha Ufalme wake. Kwa hiyo, tunawaambia wengine kwa furaha kwamba wote wanaokubali Ufalme huo, wanaotii Mungu, na kutenda mema wanaweza kuwa marafiki wake. (Zab. 15:1, 2) Bila shaka, kusudi la Yehova ni kumaliza mateso yote. Ataondoa pia huzuni tunayokuwa nayo tunapokumbuka mambo mabaya yaliyotupata zamani. Hiyo ni habari njema kabisa. (Isa. 65:17) Kwa kuwa sisi ni waeneza​-injili, acheni tuzungumuzie maulizo haya mawili ya maana sana: Sababu gani watu wanahitaji kusikia habari njema? Na namna gani tunaweza kutimiza vizuri daraka letu la kueneza injili?

SABABU GANI WATU WANAHITAJI KUSIKIA HABARI NJEMA?

Maulizo yanayoulizwa kwa ufundi . . . yanasaidia watu wavumbue sababu zinazowafanya waamini mambo fulani

4. Watu wamefundishwa habari gani za uongo kumuhusu Mungu?

4 Wazia unaambiwa kwamba baba yako amekuacha wewe na watu wengine wa familia yako. Wazia wale wanaodai kwamba walimujua baba yako wanakuambia kwamba hakuwa anawahangaikia, alikuwa mwenye kuficha mambo yake, na hakuwa na huruma. Wengine wanaweza hata kukusadikisha kwamba si lazima ujaribu kuanzisha tena uhusiano na baba yako kwa kuwa amekwisha kufa. Kwa kweli, watu wengi wameambiwa habari kama hizo kumuhusu Mungu. Wamefundishwa kwamba Mungu ni mutu anayeficha mambo yake, kwamba hajulikane, ao kwamba yeye hana huruma. Kwa mufano, viongozi fulani wa dini wanadai kwamba Mungu ataazibu watu wabaya katika moto wa milele. Wengine wanasema kwamba Mungu ndiye analeta misiba ya asili. Hata ikiwa misiba hiyo inawaua watu wabaya na watu wazuri pia, viongozi wanasema kwamba misiba hiyo ni malipizi ya Mungu.

yanafungua akili na mioyo ya watu ili wakubali ukweli

5, 6. Fundisho la mageuzi na mafundisho mengine ya uongo yamekuwa na matokeo gani juu ya watu?

5 Watu wengine wanasema kama hakuna Mungu. Fikiria kwa mufano fundisho la mageuzi. Wengi wanaotetea fundisho hilo wanasema kama uzima ulijitokeza wenyewe. Wanadai kama hakuna Muumba. Wengine hata wamesema kwamba mutu ni aina nyingine tu ya munyama, kwa hiyo haingepaswa kushangaza kuona mutu anayetenda kama munyama. Wanasema kwamba watu wenye mamlaka wanaowakandamiza watu wa hali ya chini, wanafanya hivyo tu kwa sababu wanafuata sheria inayoitwa eti ya asili. Haishangaze kwamba wengi wanafikiri kwamba ukosefu wa haki hautakuwa na mwisho. Kwa hiyo, wale wanaoamini mageuzi wanakosa tumaini katika maisha.

6 Bila shaka, fundisho la mageuzi na mafundisho mengine ya uongo ni kati ya mambo yanayofanya matatizo yaongezeke katika siku hizi za mwisho. (Rom. 1:28-31; 2 Tim. 3:1-5) Mafundisho hayo si habari njema ya kweli na yenye kudumu. Tofauti na hilo, kama vile mutume Paulo alivyoonyesha, mafundisho hayo yamewatia watu ‘katika giza kiakili, na kuwatenganisha mbali na uzima ambao ni wa Mungu.’ (Efe. 4:17-19) Zaidi ya hayo, fundisho la mageuzi na mafundisho mengine ya uwongo yamewazuia watu wasisikie habari njema inayotoka kwa Mungu.—Soma Waefeso 2:11-13.

yanawasaidia wafikiri ili wafikie uamuzi muzuri

7, 8. Ni njia gani moja tu inayoweza kusaidia watu waelewe vizuri habari njema?

7 Ili kuwa marafiki wa Mungu, watu wanapaswa kusadiki kwamba yeye yuko na kwamba kuna sababu nzuri zinazopaswa kuwachochea wanadamu wamukaribie. Tunaweza kuwasaidia wapate ujuzi huo kwa kuwatia moyo wachunguze uumbaji. Watu wanapochunguza uumbaji wakiwa na maoni mazuri, wataona hekima na nguvu ya Mungu. (Rom. 1:19, 20) Ili kusaidia watu wamuogope Mungu wanapofikiria mambo aliyoumba, tunaweza kutumia broshua Uhai—Ulitokana na Muumba? na Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai. Hata hivyo, kuchunguza tu uumbaji hakutamusaidia mutu apate majibu ya maulizo yanayosumbua sana watu kama vile: Kwa nini Mungu anaacha watu wateseke? Kwa nini Mungu aliumba dunia? Je, Mungu ananihangaikia mimi?

8 Njia moja tu inayoweza kusaidia watu waelewe vizuri habari njema kumuhusu Mungu na makusudi yake ni kujifunza Biblia. Tuna pendeleo kubwa kabisa la kusaidia watu wapate majibu ya maulizo yao! Ili tuguse mioyo ya wasikilizaji wetu, hatupaswe tu kuwafasiria mambo, tunapaswa pia kuwasadikisha. (2 Tim. 3:14) Tunaweza kusadikisha watu vizuri zaidi kwa kufuata mufano wa Yesu. Sababu gani Yesu alipata matokeo mazuri? Sababu moja ni kwamba alitumia maulizo kwa ufundi. Namna gani tunaweza kumuiga?

WAENEZA​-INJILI WAZURI WANATUMIA MAULIZO KWA UFUNDI

9. Ikiwa tunataka kusaidia watu kiroho, tunapaswa kufanya nini?

9 Kwa nini tunapaswa kutumia maulizo katika kazi yetu ya kueneza injili, kama Yesu alivyofanya? Tufikirie hali hii: Muganga wako anakuambia kwamba ana habari njema kwa ajili yako. Anakuambia kwamba anaweza kukuponyesha ikiwa utakubali upasuaji hatari. Labda unaweza kumuamini. Lakini, namna gani ikiwa anakuahidi hivyo mbele hata ya kukuuliza maulizo fulani ili ajue hali ya afya yako? Inawezekana kwamba hautamuamini. Hata muganga huyo awe na ufundi wa namna gani, anapaswa kwanza kukuuliza maulizo kuhusu ugonjwa wako na kukusikiliza mbele ya kutoa matunzo yoyote yatakayokusaidia. Vivyo hivyo, ikiwa tunataka kusaidia watu wakubali habari njema ya Ufalme, tunapaswa kuwa na ufundi wa kuuliza maulizo. Ni kisha tu kuelewa vizuri hali yao ya kiroho, ndipo tunaweza kuwatolea musaada.

Ili tuguse mioyo ya wasikilizaji wetu, tunapaswa kuwasadikisha

10, 11. Tunaweza kutimiza mambo gani ikiwa tunaiga namna ya Yesu ya kufundisha?

10 Yesu alijua kwamba maulizo yaliyochaguliwa vizuri yanasaidia mwalimu ajue maoni ya mwanafunzi na yanafanya musikilizaji ashiriki katika mazungumuzo. Kwa mufano, Yesu alipotaka kufundisha wanafunzi wake somo la unyenyekevu, alitumia kwanza ulizo ambalo liliwafanya wafikiri. (Mk. 9:33) Ili kumusaidia Petro afikiri juu ya kanuni, Yesu alimuuliza ulizo ambalo lilimutolea nafasi ya kuchagua jibu la kweli. (Mt. 17:24-26) Wakati mwingine, Yesu alipotaka kujua yale yaliyokuwa katika mioyo ya wanafunzi wake, alitumia maulizo mengi yanayomufanya mutu atoe maoni yake. (Soma Mathayo 16:13-17.) Kwa kutumia maulizo na kufasiria mambo, Yesu hakuwa tu akifundisha habari za kweli, lakini pia aligusa mioyo, na aliwachochea watu ili watende kulingana na habari njema.

11 Tunapomuiga Yesu kwa kutumia maulizo kwa ufundi, tunatimiza mambo matatu hivi. Tunavumbua namna tunavyoweza kusaidia watu kwa njia nzuri zaidi, tunashinda vizuia-mazungumuzo, na tunafundisha wapole namna wanavyoweza kufaidika na mambo wanayojifunza. Acheni tuzungumuzie hali tatu zinazoonyesha namna tunavyoweza kutumia maulizo kwa ufundi.

12-14. Namna gani unaweza kumusaidia mutoto wako atangaze habari njema bila woga? Toa mufano.

12 Hali ya 1: Muzazi, unaweza kufanya nini ikiwa mutoto wako anaogopa kutetea mambo anayoamini kuhusu uumbaji anapozungumuza na wanafunzi wenzake? Bila shaka, utapenda kumusaidia atangaze habari njema bila woga. Kwa hiyo, kuliko kumuchambua ao kumutolea mashauri mara moja, kwa nini usimuige Yesu kwa kumuuliza maulizo yatakayomufanya atoe maoni yake? Unaweza kufanya hivyo namna gani?

13 Kisha kusoma pamoja na mutoto wako sehemu fulani za broshua Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai, unaweza kumuuliza mawazo ambayo anaona kwamba yanaweza kumufanya mutu afikiri. Umutie moyo atafute sababu zake mwenyewe zinazomufanya aamini kwamba kuna Muumba na kwa nini anapenda kufanya mapenzi ya Mungu. (Rom. 12:2) Umusaidie ajue kwamba sababu zake na zako zinaweza kutofautiana.

14 Elezea mutoto wako kwamba anapozungumuza na wanafunzi wenzake, anaweza kuiga namna ulivyofanya. Hivyo, anaweza kuwaelezea habari fulani za kweli na kuwauliza maulizo yatakayowafanya watoe maoni yao. Kwa mufano, anaweza kumuomba mwanafunzi mwenzake asome kisanduku kwenye ukurasa wa 21 wa broshua Chanzo cha Uhai. Kisha mutoto wako anaweza kuuliza hivi: “Ni kweli kwamba chembe za uriti za ADN zina uwezo mukubwa wa kuchunga habari kuliko ordinatere yoyote leo?” Labda mwanafunzi mwenzake atajibu ndiyo. Kisha mutoto wako anaweza tena kuuliza hivi: “Ikiwa watengenezaji wa ordinatere hawana ordinatere inayoweza kuchunga habari hivyo, je, kitu kisichokuwa na akili kinaweza kufanya hivyo chenyewe?” Ili kumusaidia mutoto wako asiogope anapozungumuza na wenzake kuhusu mambo anayoamini, unaweza kufanya naye mazoezi kwa ukawaida. Ikiwa unamuzoeza kutumia maulizo kwa ufundi, utamusaidia kutimiza daraka lake la kueneza injili.

15. Namna gani tunaweza kutumia maulizo ili kusaidia mutu asiyeamini kwamba kuna Mungu?

15 Hali ya 2: Katika kazi yetu ya kutoa ushahidi, tunakutana na watu walio na mashaka kwamba kuna Mungu. Kwa mufano, mutu fulani anaweza kutuambia kwamba haamini kama kuna Mungu. Kuliko kuacha kuzungumuza naye kwa sababu tu ametuambia hivyo, tunaweza kumuuliza kwa heshima kama amekuwa na mawazo hayo tangu wakati gani. Kisha kusikiliza majibu yake na kumushukuru kwa kuwa amekwisha kufikiria sana jambo hilo, tunaweza kumuuliza ikiwa atafurahia tumuonyeshe kichapo kinachozungumuzia sababu zinazotusadikisha kwamba uzima uliumbwa. Ikiwa musikilizaji huyo iko tayari kusikiliza maoni ya wengine, labda anaweza kusema kwamba kukataa sababu hizo ni kukosewa akili. Kisha, tunaweza kumutolea broshua Uhai—Ulitokana na Muumba? ao broshua Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai. Maulizo yanayoulizwa kwa ufundi na busara, yanaweza kuwa kama ufunguo unaoweza kufungua moyo wa mutu ili akubali habari njema.

16. Sababu gani si vizuri kumuomba mwanafunzi asome tu majibu katika kitabu cha funzo?

16 Hali ya 3: Tunapoongoza funzo la Biblia, labda tunazoea tu kumuambia mwanafunzi asome majibu yanayoandikwa katika kitabu cha funzo. Lakini tukifanya hivyo, tunaweza kuzuia mwanafunzi huyo kukomaa kiroho. Sababu gani? Kwa sababu mwanafunzi anayesoma tu majibu katika kitabu bila kutafakari hatakuwa na mizizi ya kiroho. Kama vile mumea unaokauka haraka kwa sababu ya joto, mwanafunzi huyo anaweza kushindwa kuvumilia upinzani. (Mt. 13:20, 21) Ili jambo hilo lisitokee, tunapaswa kumuuliza mwanafunzi namna anavyoona mambo anayojifunza. Tafuta kujua ikiwa anakubaliana na mambo hayo. Jambo la lazima zaidi ni kumuacha aseme kwa nini anakubaliana na mambo hayo ao kwa nini hakubaliane nayo. Kisha umuonyeshe namna ya kufikiri juu ya Maandiko ili mwishowe yeye mwenyewe afikie maamuzi mazuri. (Ebr. 5:14) Ikiwa tunatumia maulizo kwa ufundi, watu tunaofundisha watakuwa na imani yenye nguvu na wataweza kushindana na watu wanaojitahidi kuwapinga ao kuwadanganya. (Kol. 2:6-8) Ni jambo gani lingine tunaloweza kufanya ili kutimiza daraka letu la kueneza injili?

WAENEZA-INJILI WAZURI WANASAIDIANA

17, 18. Unapomusindikiza muhubiri mwenzako, namna gani munaweza kuungana mukono?

17 Yesu alituma wanafunzi wake katika kazi ya kuhubiri wakiwa wawili-wawili. (Mk. 6:7; Lu. 10:1) Baadaye, mutume Paulo alizungumuzia ‘wafanyakazi wenzake waliokazana pamoja naye katika habari njema.’ (Flp. 4:3) Kwa kuiga wahubiri hao wa wakati wa mitume, katika mwaka wa 1953, Mashahidi wa Yehova, walianzisha programe ya kuwazoeza wengine katika mahubiri.

18 Unapomusindikiza muhubiri mwenzako katika mahubiri, namna gani munaweza kuungana mukono? (Soma 1 Wakorintho 3:6-9.) Muhubiri mwenzako anaposoma maandiko fulani, wewe pia uyatafute katika Biblia yako. Sikiliza vizuri yale ambayo muhubiri mwenzako ao musikilizaji anasema. Kufuata mazungumuzo kwa uangalifu kutakusaidia kujua wakati gani unaweza kumusaidia muhubiri mwenzako kujibu ulizo fulani ngumu ao kushinda tatizo lingine. (Mhu. 4:12) Lakini angalisho: Epuka kumukatiza-katiza muhubiri mwenzako anapojaribu kufikiri vizuri pamoja na musikilizaji. Ukimukatiza-katiza, hilo linaweza kumuvunja moyo na kuvuruga musikilizaji. Wakati mwengine, inaweza kuwa vizuri kushiriki katika mazungumuzo. Lakini, ukipenda kusema jambo fulani, toa maelezo mafupi mara moja ao mara mbili. Kisha umuache muhubiri mwenzako aendelee na mazungumuzo.

19. Ni vizuri tukumbuke nini, na sababu gani?

19 Namna gani munaweza kusaidiana munapotoka kwenye mulango mumoja mupaka mulango mwengine? Munaweza kutumia wakati huo ili kuzungumuzia namna ya kufanya utangulizi wenu uwe muzuri zaidi. Muwe waangalifu ili mazungumuzo yenu kuhusu watu wa eneo lenu yasiwe yenye kuvunja moyo. Pia, muepuke kuongea-ongea juu ya uzaifu wa wahubiri wengine. (Met. 18:24) Ni vizuri tukumbuke kwamba sisi ni vyombo vya udongo. Yehova ametuonyesha wema mukubwa kwa kututolea hazina ya kuhubiri habari njema. (Soma 2 Wakorintho 4:1, 7.) Kwa hiyo, acheni sote tupendezwe sana na hazina hiyo kwa kufanya yote tunayoweza ili kutimiza daraka letu la kueneza injili.