Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Una “Bidii kwa Ajili ya Kazi Njema”?

Je, Una “Bidii kwa Ajili ya Kazi Njema”?

‘Kristo Yesu, alijitoa mwenyewe kwa ajili yetu ili ajisafishie mwenyewe watu walio wake kwa njia ya pekee, walio na bidii kwa ajili ya kazi njema.’—TITO 2:13, 14.

1, 2. Mashahidi wa Yehova wana pendeleo gani la pekee, na unahisije kuhusu pendeleo hilo?

WATU wengi huona kwamba ni heshima kubwa kupewa tuzo kwa sababu ya kutimiza jambo fulani kubwa. Kwa mfano, wengine wamepewa Tuzo ya Nobeli kwa kujitahidi kuleta amani kati ya vikundi vinavyozozana au vilivyotengana. Hata hivyo, ni heshima kubwa kama nini kutumwa na Mungu ukiwa balozi au mjumbe wake ili kuwasaidia watu kuwa na uhusiano wenye amani pamoja na Muumba wao!

2 Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tumepewa pendeleo hilo la pekee. Tunatii amri ya Mungu na Kristo kwa kuwasihi watu ‘wapatanishwe na Mungu.’ (2 Kor. 5:20) Yehova anatutumia kuwavuta watu kwake. Mamilioni ya watu katika nchi zaidi ya 235 wamevutwa kwa njia hiyo na kusaidiwa kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu na kuwa na tumaini la kupata uzima wa milele. (Tito 2:11) Tunajitahidi kwa moyo wote kumwalika ‘yeyote anayetaka kuchukua maji ya uzima bure.’ (Ufu. 22:17) Kwa kuwa tunathamini sana mgawo huo wa pekee na tunautimiza kwa bidii, tunaweza kwa kufaa kuitwa watu “walio na bidii kwa ajili ya kazi njema.” (Tito 2:14) Acheni sasa tuone jinsi bidii yetu kwa ajili ya kazi njema inavyotusaidia kuwavuta watu kwa Yehova. Njia moja ni kupitia kazi yetu ya kuhubiri.

IGA BIDII YA YEHOVA NA YESU

3. “Bidii ya Yehova” inatuhakikishia nini?

3 Likitaja yale ambayo utawala wa Mwana wa Mungu utatimiza, andiko la Isaya 9:7 linasema hivi: “Bidii ya Yehova wa majeshi itafanya hayo.” Maneno hayo yanakazia jinsi Baba yetu wa mbinguni anavyopendezwa sana na wokovu wa wanadamu. Kielelezo cha Yehova cha bidii kinaonyesha waziwazi kwamba tunapaswa kuunga mkono kwa moyo wetu wote kazi tuliyopewa na Mungu ya kuwa watangazaji wa Ufalme, na kuifanya kwa shauku na bidii. Tunaonyesha kwamba tunaiga bidii ya Yehova tunapokuwa na tamaa kubwa ya kuwasaidia watu wamjue Mungu.  Kwa hiyo, tukiwa wafanyakazi wenzi wa Mungu, je, sisi binafsi tumeazimia kushiriki kikamili katika kutangaza habari njema kadiri hali zetu zinavyoruhusu?—1 Kor. 3:9.

4. Yesu aliwekaje kielelezo kwa kuendelea kuhubiri kwa bidii?

4 Fikiria pia bidii ya Yesu. Aliweka kielelezo kikamilifu kwa kuendelea kuhubiri kwa bidii. Licha ya upinzani mkali, alidumisha bidii katika kazi ya kuhubiri hadi alipokufa kifo chenye maumivu makali hapa duniani. (Yoh. 18:36, 37) Wakati ulipokuwa ukikaribia wa Yesu kuuawa ili kutoa uhai wake kuwa dhabihu, aliazimia hata zaidi kuwasaidia wengine wamjue Yehova.

5. Yesu alitendaje kupatana na mfano aliotoa wa mtini?

5 Kwa mfano, katika mwaka wa 32 W.K., Yesu alitoa mfano wa mwanamume aliyekuwa na mtini katika shamba lake la mizabibu ambao haukuzaa matunda kwa miaka mitatu. Mtunza-mizabibu alipoambiwa aukate mti huo, aliomba apewe muda ili autilie mbolea. (Soma Luka 13:6-9.) Wakati huo, ni wanafunzi wachache tu ambao wangeonwa kuwa matunda ya kazi ya Yesu ya kuhubiri. Lakini kama inavyoonyeshwa na mfano huo wa mtunza-mizabibu, Yesu alitumia wakati mfupi uliobaki, yaani, miezi sita hivi, kuhubiri kwa bidii zaidi huko Yudea na Perea. Siku chache kabla ya kifo chake, Yesu alilia kwa sababu ya Wayahudi wenzake ambao ‘walimsikia bila kuitikia.’—Mt. 13:15; Luka 19:41.

6. Kwa nini tunapaswa kuongeza bidii katika kazi ya kuhubiri?

6 Kwa kuwa tunakaribia upeo wa siku za mwisho, je, si ni jambo muhimu kwetu kuongeza bidii katika kazi ya kuhubiri? (Soma Danieli 2:41-45.) Ni pendeleo zuri kama nini kuwa Mashahidi wa Yehova! Ni sisi peke yetu duniani tunaotangaza tumaini la suluhisho la kweli la matatizo ya wanadamu. Hivi karibuni, mwandishi mmoja wa gazeti alisema kwamba swali hili halina jibu: “Kwa nini watu wazuri hupatwa na mambo mabaya?” Tukiwa Wakristo, tuna wajibu na pendeleo la kuwaonyesha majibu ya Biblia ya maswali kama hayo wote walio tayari kusikiliza. Tuna kila sababu ya ‘kuwaka roho’ tunapotimiza mgawo tuliopewa na Mungu. (Rom. 12:11) Yehova atabariki bidii yetu ya kueneza injili na tutawasaidia wengine kumjua na kumpenda Yehova.

ROHO YA KUJIDHABIHU HUMLETEA HESHIMA YEHOVA

7, 8. Roho ya kujidhabihu humleteaje heshima Yehova?

7 Kama inavyoonyeshwa na mambo yaliyompata mtume Paulo, huduma yetu inaweza kutufanya ‘tukose usingizi’ na ‘nyakati nyingine kuwa bila chakula.’ (2 Kor. 6:5) Maneno hayo yanaonyesha kihalisi maana ya kuwa na roho ya kujidhabihu na huenda yakatukumbusha hali ya mapainia wanaotanguliza huduma maishani huku wakijitegemeza kifedha. Wafikirie pia wamishonari wetu wenye bidii ‘wanaojimimina kama toleo la kinywaji’ ili kuwatumikia watu katika nchi za kigeni. (Flp. 2:17) Namna gani wazee wetu wenye bidii ambao hukosa chakula au usingizi ili kutunza kondoo wa Yehova? Miongoni mwetu pia kuna wale walio na umri mkubwa na wengine walio na matatizo ya kiafya wanaojitahidi kabisa kuhudhuria mikutano ya Kikristo na kushiriki katika huduma ya shambani. Mioyo yetu hujaa uthamini tunapowafikiria watumishi hao wote wa Mungu wanaojidhabihu. Jitihada hizo huwafanya wengine wawe na maoni mazuri kuhusu huduma yetu.

8 Msomaji mmoja ambaye si Shahidi wa Yehova alisema hivi katika barua aliyoandika katika gazeti moja (Boston Target) huko Lincolnshire, Uingereza: “Watu wanapoteza imani katika dini . . . Wahudumu wa makanisa wanafanya kazi gani? Hawatembelei kamwe watu kama Kristo alivyofanya . . . Mashahidi wa Yehova ndiyo dini pekee inayoonekana kuwajali watu. Wao ndio wanaowatembelea watu na kuhubiri kweli kwa  moyo wote.” Katika ulimwengu huu unaopenda anasa, roho yetu ya kujidhabihu humletea heshima Yehova Mungu.—Rom. 12:1.

Unaposhiriki katika huduma unatoa ushahidi mkubwa kwa watazamaji

9. Ni nini kinachoweza kutuchochea tuendelee kuwa na bidii kwa ajili ya kazi njema katika huduma yetu?

9 Hata hivyo, tunaweza kufanya nini ikiwa bidii yetu katika huduma inapungua? Ni vizuri kutafakari mambo ambayo Yehova anatimiza kupitia kazi ya kuhubiri. (Soma Waroma 10:13-15.) Ili watu waokolewe ni lazima waliitie jina la Yehova kwa imani, lakini hawatafanya hivyo tusipowahubiria. Kutambua jambo hilo kunapaswa kutuchochea tuendelee kuwa na bidii kwa ajili ya kazi njema na kujitahidi kutangaza habari njema ya Ufalme.

MWENENDO MZURI HUWAVUTA WATU KWA MUNGU

Watu huona unyoofu na bidii yako

10. Kwa nini tunaweza kusema kwamba mwenendo wetu mzuri huwavuta watu kwa Yehova?

10 Bidii ni muhimu sana katika huduma, hata hivyo, bidii peke yake haitoshi kuwavuta watu kwa Mungu. Jambo la pili linalowavuta watu kwa Mungu ni mwenendo mzuri wa Kikristo. Paulo alikazia umuhimu wa mwenendo wetu alipoandika hivi: “Sisi hatutoi sababu yoyote ya kukwaza kwa njia yoyote, ili huduma yetu isilaumiwe.” (2 Kor. 6:3) Usemi na mwenendo wetu mzuri hulipamba fundisho la Mungu, na kufanya wengine wavutiwe na ibada ya Yehova. (Tito 2:10) Kwa kweli, mara nyingi tunasikia kuhusu watu wanyoofu wanaokubali kweli wanapoona mwenendo wetu ulio kama wa Kristo.

11. Kwa nini tunapaswa kusali na kufikiria matokeo ya mwenendo wetu?

11 Ingawa tunatambua kwamba matendo yetu yanaweza kuwavuta watu katika kweli, tunatambua pia kwamba yanaweza kuwafanya waikatae. Kwa hiyo, tuwe kazini, nyumbani, au shuleni, tunajitahidi sana kutompa mtu yeyote sababu ya kuilaumu huduma na mwenendo wetu. Tukizoea kutenda dhambi kimakusudi, matokeo yatakuwa mabaya  sana kwetu. (Ebr. 10:26, 27) Wazo hilo linapaswa kutuchochea kusali na kufikiria mambo tunayofanya na jinsi mtindo wetu wa maisha unavyoonwa na wengine. Kadiri viwango vya maadili vya ulimwengu huu vinavyozidi kushuka, ndivyo inavyokuwa rahisi zaidi kwa watu wanyoofu ‘kuona tofauti kati ya mtu anayemtumikia Mungu na mtu ambaye hajamtumikia.’ (Mal. 3:18) Naam, mwenendo wetu mzuri wa Kikristo unatimiza sehemu muhimu sana katika kuwapatanisha watu na Mungu.

12-14. Uvumilivu wetu tunapokabili majaribu ya imani unaweza kuwafanya wengine wawe na maoni gani kuelekea huduma yetu? Toa mfano.

12 Alipowaandikia Wakorintho, Paulo alisema kwamba alipatwa na dhiki, magumu, mapigo, na vifungo vya gerezani. (Soma 2 Wakorintho 6:4, 5.) Tukipatwa na majaribu ya imani, uvumilivu wetu unaweza kuwasaidia watazamaji kukubali kweli. Kwa mfano: Miaka kadhaa iliyopita, watu fulani walijaribu kuwakomesha Mashahidi wa Yehova katika eneo moja nchini Angola. Mashahidi wawili waliobatizwa na watu 30 wanaopendezwa waliokuwa wakihudhuria mikutano walikamatwa. Kisha, wenyeji wa eneo hilo walikusanywa ili kuwatazama watu hao wasiokuwa na hatia wakichapwa na wapinzani wao hadi wakatoka damu. Hata wanawake na watoto walichapwa kikatili. Lengo lilikuwa kuwatisha watu ili mtu yeyote asiwasikilize Mashahidi wa Yehova. Lakini baada ya Mashahidi kuchapwa hadharani, watu wengi katika eneo hilo waliwaomba Mashahidi wajifunze nao Biblia! Baadaye, kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme ilisonga mbele na kukawa na ongezeko kubwa na baraka tele.

13 Mfano huo unaonyesha kwamba tunaposhikamana kabisa na kanuni za Biblia tunaweza kuwasaidia wengi kukubali kweli. Hatujui ni wangapi waliopatanishwa na Mungu kwa sababu ya ujasiri wa Petro na mitume wengine. (Mdo. 5:17-29) Leo pia, wanafunzi wenzetu, wafanyakazi wenzetu, au washiriki wa familia zetu wanaweza kukubali kweli wakiona msimamo wetu kuelekea lililo sawa.

14 Sikuzote kumekuwa na ndugu zetu wanaoteswa katika nchi mbalimbali. Kwa mfano, nchini Armenia, angalau ndugu 40 wamefungwa gerezani kwa sababu ya kukataa utumishi wa kijeshi, na huenda wengine wengi wakafungwa katika miezi inayokuja. Nchini Eritrea, watumishi 55 wa Yehova wamefungwa gerezani, baadhi yao wana umri wa miaka zaidi ya 60. Huko Korea Kusini, Mashahidi 700 hivi wamefungwa gerezani kwa sababu ya imani yao. Hali hiyo imeendelea kwa miaka 60 sasa. Acheni tusali ili ndugu zetu wanaoteswa katika nchi mbalimbali waendelee kuwa waaminifu na hivyo kumtukuza Yehova na kuwasaidia wale wanaopenda uadilifu wajiunge na ibada ya kweli.—Zab. 76:8-10.

15. Toa mfano unaoonyesha jinsi kujiendesha kwa unyoofu kunavyoweza kuwavuta wengine katika kweli.

15 Kwa kuwa tunajiendesha kwa unyoofu, tunaweza pia kuwafanya watu wavutiwe na kweli. (Soma 2 Wakorintho 6:4, 7.) Kwa mfano, fikiria jambo hili lililoonwa: Dada mmoja alipotaka kukata tikiti ili asafiri kwa basi, rafiki yake alimwambia kwamba hakuhitaji kukata tikiti kwa sababu hakuwa akisafiri mbali. Dada huyo alimweleza kwamba ni jambo linalofaa kukata tikiti hata kama hasafiri mbali. Baadaye, rafiki huyo alishuka. Kisha, dereva wa basi alimuuliza dada huyo, “Je, wewe ni Shahidi wa Yehova?” Dada huyo akajibu, “Ndiyo, kwa nini umeniuliza swali hilo?” “Nilisikia mazungumzo yenu kuhusu kulipia nauli ya basi, na ninajua kwamba Mashahidi wa Yehova ni kati ya watu wachache sana wanaofanya hivyo na ni wanyoofu katika kila jambo.” Miezi michache baadaye, mwanamume mmoja alimfikia dada huyo katika mkutano na kumuuliza, “Unanijua? Mimi ndiye dereva wa basi uliyezungumza naye kuhusu nauli. Mwenendo  wako ulinifanya niamue kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova.” Mwenendo wetu wa unyoofu hutupendekeza kuwa wahudumu wanaotegemeka.

SIKUZOTE ONYESHA SIFA ZINAZOMLETEA HESHIMA MUNGU

16. Kwa nini sifa kama vile ustahimilivu, upendo, na fadhili hugusa mioyo ya watu? Toa mfano.

16 Tunapoonyesha sifa kama vile ustahimilivu, upendo, na fadhili, tunashiriki pia katika kuwavuta watu kwa Yehova. Baadhi ya wale wanaotutazama wanaweza kutamani kujifunza kumhusu Yehova, makusudi yake, na watu wake. Mtazamo na mwenendo wa Wakristo wa kweli ni tofauti kabisa na wonyesho wa nje wa ujitoaji-kimungu wa wale ambao ibada yao ni ya kinafiki tu. Viongozi fulani wa kidini wametajirika kwa kulaghai makundi yao, wakitumia kiasi kikubwa cha pesa hizo kununua nyumba na magari ya bei ghali, na katika kisa fulani, kiongozi wa kidini alitumia pesa hizo kumjengea mbwa wake kibanda chenye mfumo wa kusafisha hewa. Kwa kweli, wengi wanaodai kuwa wafuasi wa Kristo hawana mwelekeo wa ‘kutoa bure.’ (Mt. 10:8) Badala yake, kama makuhani waasi wa Israeli la kale, wao “hufundisha ili tu wapate malipo”—na mafundisho yao mengi hayapatani na maandiko. (Mika 3:11) Mwenendo wa kinafiki kama huo hauwezi kumpatanisha yeyote na Mungu.

17, 18. (a) Tunamleteaje heshima Yehova tunapoonyesha sifa kama zake maishani mwetu? (b) Ni nini kinachokuchochea kuendelea kufanya kazi njema?

17 Kwa upande mwingine, mafundisho ya kweli ya Kikristo na kuwatendea mema majirani hugusa mioyo ya watu. Kwa mfano, pindi moja mjane fulani aliyezeeka alimwambia painia aliyekuwa akihubiri nyumba kwa nyumba kwamba hana wakati wa kumsikiliza. Mjane huyo alisema kwamba painia huyo alipopiga kengele, alikuwa amepanda ngazi jikoni akijaribu kubadilisha taa. Painia huyo akamwambia, “Ni hatari kufanya hivyo ukiwa peke yako.” Kisha painia huyo akambadilishia taa hiyo na kuondoka. Mwana wa mjane huyo alipoelezwa jambo hilo, alivutiwa sana hivi kwamba akajitahidi kumtafuta ndugu huyo ili amshukuru. Hatimaye, mwana huyo alikubali kujifunza Biblia.

18 Kwa nini umeazimia kuendelea kufanya kazi njema? Labda ni kwa sababu unajua kwamba tukiwa na bidii kwa ajili ya huduma yetu na kufanya mambo kulingana na mapenzi ya Mungu, tunamletea heshima Yehova na huenda tukawasaidia wengine kupata wokovu. (Soma 1 Wakorintho 10:31-33.) Tamaa kubwa ya kuonyesha kwamba tunampenda Mungu na wanadamu wenzetu ndiyo inayotuchochea kuwa na bidii kwa ajili ya kazi njema kwa kuhubiri habari njema na kujiendesha kwa njia inayompendeza Mungu. (Mt. 22:37-39) Ikiwa tuna bidii kwa ajili ya kazi njema, tutathawabishwa sana kwa kuwa na shangwe na uradhi sasa. Kwa kuongezea, tunaweza kutazamia wakati ambapo wanadamu wote watakuwa wenye bidii kwa ajili ya ibada ya kweli na kumletea heshima Muumba wetu, Yehova.