Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Imarisha Ndoa Yako Kupitia Mawasiliano Mazuri

Imarisha Ndoa Yako Kupitia Mawasiliano Mazuri

“Neno linalosemwa wakati unaofaa ni kama matunda ya mtofaa ya dhahabu kwenye chombo cha fedha kilichopambwa.” —MET. 25:11.

1. Mawasiliano mazuri yameboreshaje ndoa?

NDUGU mmoja nchini Kanada alisema hivi: “Ni afadhali nitumie wakati pamoja na mke wangu kuliko kuwa na mtu mwingine. Ninapokuwa naye furaha inaongezeka maishani na uchungu wowote nilio nao unapungua.” Mume mmoja nchini Australia aliandika hivi: “Katika miaka 11 ambayo tumeishi pamoja, sijakosa kuzungumza na mke wangu hata siku moja. Mimi na mke wangu hatuna wasiwasi wala shaka kuhusu uthabiti wa ndoa yetu. Sababu kuu ni kwamba tuna mawasiliano mazuri sana ya kawaida.” Dada mmoja nchini Kosta Rika alisema hivi: “Mbali na kuboresha ndoa yetu, mawasiliano mazuri yametusaidia kumkaribia zaidi Yehova, yametulinda kutokana na vishawishi, yametuunganisha tukiwa mume na mke, na kufanya upendo wetu usitawi.”

2. Ni mambo gani yanayoweza kuzuia mawasiliano mazuri?

2 Je, wewe na mwenzi wako wa ndoa mna mawasiliano mazuri, au mnashindwa kufanya hivyo? Bila shaka, matatizo yanaweza kutokea kwa kuwa ndoa inawaunganisha watu wawili wasio wakamilifu, wenye nyutu na tabia tofauti zinazotegemea utamaduni na malezi yao. (Rom. 3:23) Isitoshe, huenda njia ya mume ya kuwasiliana ikawa tofauti na ya mke wake. Ndiyo sababu watafiti wa ndoa John M. Gottman na Nan Silver wanasema hivi: “Wenzi wa ndoa wanahitaji kuazimia, kuwa na ujasiri na uvumilivu ili kuwa na uhusiano wenye kudumu.”

3. Ni nini ambacho kimewasaidia wenzi wa ndoa kuimarisha ndoa yao?

3 Uhakika ni kwamba jitihada kubwa zinahitajiwa ili kuwa na ndoa yenye mafanikio. Lakini jitihada hizo huleta furaha isiyo na kifani. Kwa kweli, wenzi wa ndoa wanaopendana wanaweza kufurahia maisha yao ya ndoa. (Mhu. 9:9) Fikiria ndoa yenye upendo ya Isaka na Rebeka. (Mwa. 24:67) Hata baada ya kukaa pamoja kwa  kipindi fulani wakiwa mume na mke, hakuna jambo linaloonyesha kwamba upendo wao ulipungua. Ndivyo ilivyo kuhusu wenzi wengi wa ndoa leo. Siri ni nini? Wamejifunza kuzungumzia mawazo na hisia zao waziwazi lakini kwa fadhili, wamesitawisha ufahamu, upendo, heshima kubwa, na unyenyekevu. Kama tutakavyoona, wenzi wa ndoa wanapoonyesha sifa hizo za msingi, wanakuwa na mawasiliano mazuri.

TUMIA UFAHAMU

4, 5. Ufahamu unaweza kumsaidiaje mume na mke kuelewana vizuri zaidi? Toa mifano.

4 Andiko la Methali 16:20 linasema: “Anayetumia ufahamu katika jambo atapata mema.” Bila shaka, maneno hayo yanahusu ndoa na maisha ya familia. (Soma Methali 24:3.) Neno la Mungu ndicho chanzo bora zaidi cha ufahamu na hekima. Andiko la Mwanzo 2:18 linatuambia kwamba Mungu alimuumba mwanamke ili awe kikamilisho cha mwanamume, hakutaka wafanane, ndiyo sababu mke huwasiliana kwa njia tofauti na mume wake. Bila shaka, watu hutofautiana, lakini kwa ujumla wanawake hupenda kuongea kuhusu hisia zao, watu, na mahusiano. Wanathamini mawasiliano machangamfu yanayotoka moyoni kwa kuwa yanawahakikishia kwamba wanapendwa. Kwa upande mwingine, wanaume wengi hawapendi sana kuzungumza kuhusu hisia zao, inaelekea wanapenda kuongea kuhusu kazi, matatizo, na jinsi ya kuyasuluhisha. Na wanaume hupenda kuheshimiwa.

5 Dada mmoja nchini Uingereza alisema hivi: “Mume wangu hutaka kusuluhisha matatizo haraka badala ya kunisikiliza. Hilo linaweza kuvunja moyo sana, hasa wakati ambapo ninahitaji tu ‘kikombe cha chai na kuhurumiwa.’” Mume fulani aliandika hivi: “Tulipofunga ndoa, nilizoea kutafuta suluhisho la haraka kwa tatizo lolote ambalo mke wangu alikuwa nalo. Lakini, baada ya muda nilijifunza kwamba alihitaji tu kusikilizwa.” (Met. 18:13; Yak. 1:19) Mume mwenye ufahamu anazingatia hisia za mke wake na kujitahidi kumtendea kwa ufikirio. Wakati huohuo, anamhakikishia mke wake kwamba maoni na hisia zake ni muhimu. (1 Pet. 3:7) Naye mke anajitahidi kuelewa maoni ya mume wake. Mume na mke wanapoelewa, kuthamini, na kutimiza majukumu yao ya Kimaandiko, muungano wao unavutia sana. Isitoshe, wanaweza kushirikiana kufanya maamuzi yenye hekima na yenye usawaziko na kisha kuyatekeleza.

6, 7. (a) Kanuni iliyo katika Mhubiri 3:7 inawezaje kuwasaidia wenzi wa ndoa kutumia ufahamu? (b) Mke anaweza kuonyeshaje utambuzi, na mume anapaswa kujitahidi kufanya nini?

6 Pia, mume na mke wenye ufahamu wanajua kwamba kuna “wakati wa kukaa kimya na wakati wa kusema.” (Mhu. 3:1, 7) Dada ambaye ameolewa kwa miaka kumi alisema hivi: “Sasa ninatambua kwamba kuna wakati usiofaa wa kuuliza mambo fulani. Ikiwa mume wangu ana kazi au majukumu mengi sana, ninaruhusu wakati upite kabla ya kumuuliza mambo fulani. Hilo limetusaidia kuwa na mawasiliano mazuri zaidi.” Wake wenye utambuzi huongea kwa fadhili pia, wakitambua kwamba neno linalochaguliwa vizuri na ‘kusemwa wakati unaofaa’ linavutia na linathaminiwa.—Soma Methali 25:11.

Mambo madogo-madogo huboresha sana ndoa

7 Mume Mkristo anapaswa kutimiza sehemu yake kwa kumsikiliza mke wake na kujitahidi pia kueleza hisia zake waziwazi. Mzee ambaye ameoa kwa miaka 27 alisema: “Ni lazima nijitahidi sana kumwambia mke wangu mambo yaliyo moyoni mwangu.” Ndugu ambaye ameoa kwa miaka 24 alisema hivi: “Nina mwelekeo wa kutosema jinsi ninavyohisi nikifikiri kwamba ‘nisipoongea kuhusu jambo hilo, litasahaulika.’ Hata hivyo, nimetambua kwamba kueleza hisia zangu hakuonyeshi kwamba mimi ni dhaifu. Ninaposhindwa kujieleza, ninasali ili nipate maneno yanayofaa ya kusema na ili niyaseme kwa njia inayofaa. Kisha ninavuta pumzi kwa nguvu na kuanza kuongea.” Pia kuna faida kwa wenzi wa ndoa kuwasiliana wakiwa  katika kikao kinachofaa, labda wanapokuwa peke yao wakizungumzia andiko la siku au wanaposoma Biblia pamoja.

8. Wenzi wa ndoa Wakristo wanachochewa na sababu gani nyingine kufanikisha ndoa yao?

8 Ni muhimu kwa mume na mke kusali na kutamani sana kuboresha ustadi wao wa kuwasiliana. Ni kweli kwamba inaweza kuwa vigumu kuacha mazoea ya zamani. Lakini mume na mke wanapompenda Yehova, wanapomwomba awape roho yake, na kuona muungano wao kuwa mtakatifu, wanachochewa zaidi kufanya mabadiliko na hivyo wanakuwa tofauti na wenzi wengi wa ndoa. Mke aliyeolewa kwa miaka 26 aliandika hivi: “Mimi na mume wangu tunachukua kwa uzito maoni ya Yehova kuhusu ndoa, kwa hiyo hatufikirii kamwe kutengana. Hilo linatufanya tujitahidi zaidi kutatua matatizo kwa kuyazungumzia pamoja.” Ushikamanifu na ujitoaji huo wa kimungu humpendeza Mungu na huleta baraka nyingi.—Zab. 127:1.

KUENI KATIKA UPENDO

9, 10. Ni katika njia zipi mume na mke wanaweza kuimarisha kifungo chao cha ndoa?

9 Upendo, “kifungo kikamilifu cha muungano,” ndiyo sifa muhimu zaidi katika ndoa. (Kol. 3:14) Upendo wa kweli hukua kati ya wenzi wa ndoa washikamanifu kadiri wanavyoendelea kuishi pamoja, kukabiliana na matatizo, na kufurahia baraka pamoja. Urafiki wao unakuwa wa karibu hata zaidi na wanafurahia sana kuwa pamoja. Ndoa za aina hiyo hazijengwi kwa matendo machache tu ya pekee kama inavyoonyeshwa katika vyombo vya habari, badala yake zinajengwa kwa matendo mengi sana madogo-madogo, kama vile kukumbatia, kusema neno la fadhili, tendo linaloonyesha unajali, tabasamu changamfu, au kuuliza hivi kwa unyoofu, “umeshindaje?” Mambo hayo madogo-madogo yanaweza kuboresha sana ndoa. Mume na mke ambao wamekuwa na ndoa yenye furaha kwa miaka 19 hupigiana simu au kutumiana ujumbe mfupi ili “kujuliana hali,” akasema mume.

10 Upendo humchochea pia mume au mke kuendelea kumjua mwenzi wake. (Flp. 2:4) Ujuzi huo hufanya upendo wao uimarike hata zaidi licha ya kutokamilika kwao. Ndoa yenye mafanikio haibaki palepale, badala yake inakua na kuimarika zaidi kadiri wakati unavyopita. Kwa hiyo, ikiwa umefunga ndoa, jiulize: ‘Ninamjua vyema kadiri gani mwenzi wangu? Je, ninaelewa hisia na maoni yake kuhusu mambo? Mimi humfikiria mwenzi wangu mara nyingi kadiri gani, labda nikitafakari sifa zake zilizonivutia mwanzoni?’

 SITAWISHA HESHIMA

11. Ili ndoa ifanikiwe, kwa nini heshima ni muhimu sana? Toa mfano.

11 Hata ndoa zenye furaha zaidi si kamilifu, na mume na mke wanaopendana hukosa kuelewana nyakati nyingine. Abrahamu na Sara hawakukubaliana kila mara. (Mwa. 21:9-11) Hata hivyo, tofauti hizo hazikuwatenganisha. Kwa nini? Walitendeana kwa staha na heshima. Kwa mfano, Abrahamu alimwambia Sara “tafadhali.” (Mwa. 12:11, 13) Naye Sara alimtii Abrahamu na kumwona kuwa “bwana” wake. (Mwa. 18:12) Ikiwa mume na mke hawaheshimiani, kwa kawaida hilo litaonekana wazi kupitia maneno au sauti yao. (Met. 12:18) Wasipotatua tatizo lenyewe, huenda ndoa yao ikawa hatarini.—Soma Yakobo 3:7-10, 17, 18.

12. Kwa nini mume na mke waliofunga ndoa karibuni wanapaswa hasa kujitahidi kuongea kwa heshima?

12 Wale waliofunga ndoa karibuni wanapaswa hasa kujitahidi kuzungumza kwa fadhili na heshima ili iwe rahisi kwao kuwasiliana waziwazi na kwa unyoofu. Mume mmoja anakumbuka hivi: “Ingawa miaka ya kwanza ya ndoa ni yenye shangwe, nyakati nyingine inaweza kuvunja moyo. Unapojaribu kuelewa hisia, tabia, na mahitaji ya mke wako, na mke wako anapojaribu kukuelewa, mambo yanaweza kuwa magumu! Hata hivyo, mambo yanaweza kuwa rahisi zaidi mkiwa na usawaziko, ucheshi, na sifa zinazoimarisha ndoa, yaani, unyenyekevu, subira, na kumtegemea Yehova.” Hilo ni jambo la kweli kabisa!

ONYESHA UNYENYEKEVU WA KWELI

13. Kwa nini unyenyekevu ni muhimu ili ndoa ifanikiwe na iwe na furaha?

13 Mawasiliano mazuri katika ndoa ni kama kijito cha maji kinachotiririka polepole kwa utulivu kwenye bustani. Ili kijito hicho kiendelee kutiririka, ni muhimu sana kuwa “wanyenyekevu katika akili.” (1 Pet. 3:8) Ndugu mmoja ambaye ameoa kwa miaka 11 alisema hivi: “Unyenyekevu ndiyo njia ya haraka zaidi ya kusuluhisha hali ya kutoelewana kwa kuwa unyenyekevu unakuchochea kusema, ‘Pole.’” Mzee mmoja ambaye kwa miaka 20 amekuwa na ndoa yenye furaha alisema: “Nyakati nyingine neno ‘Pole’ ni muhimu zaidi kuliko neno ‘Ninakupenda.’” Aliongezea hivi: “Sala ni kati ya njia za haraka zaidi zinazomsaidia mtu kusitawisha unyenyekevu. Mimi na mke wangu  tunapomfikia Yehova pamoja katika sala, tunakumbuka hali yetu ya kutokamilika na fadhili zisizostahiliwa za Mungu. Kukumbuka mambo hayo muhimu hunisaidia kuwa na maoni yanayofaa.”

Dumisheni mawasiliano mazuri katika ndoa yenu

14. Kiburi kinaweza kuathirije ndoa?

14 Hata hivyo, kiburi huwazuia wenzi wa ndoa kusuluhisha matatizo yao. Kiburi huzuia mawasiliano kwa sababu mtu mwenye kiburi hana nia wala ujasiri wa kuomba msamaha. Mtu mwenye kiburi hutoa visingizio badala ya kusema hivi kwa unyenyekevu: “Pole; nisamehe tafadhali.” Badala ya kukubali kwa ujasiri udhaifu wake, yeye husema kuhusu udhaifu wa mwenzi wake. Anapokosewa, badala ya kufuatilia amani, anaudhika, na huenda akalipiza kisasi kwa kumnyamazia kabisa aliyemkosea au kumshambulia kwa maneno makali. (Mhu. 7:9) Kwa kweli, kiburi kinaweza kuiharibu kabisa ndoa. Ni vizuri kukumbuka kwamba “Mungu huwapinga wenye majivuno, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili zisizostahiliwa.”—Yak. 4:6.

15. Eleza jinsi kufuata kanuni ya Waefeso 4:26, 27 kunavyoweza kumsaidia mume na mke kushughulikia hali ya kutoelewana.

15 Bila shaka, ni upumbavu kufikiri kwamba hatuwezi kamwe kuwa na kiburi. Tunahitaji kutambua sifa hiyo mbaya na kuing’oa haraka. Paulo aliwaambia hivi Wakristo wenzake: “Jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka, wala msimpe Ibilisi nafasi.” (Efe. 4:26, 27) Kutofuata Neno la Mungu kunaweza kusababisha maumivu yasiyo ya lazima. Dada mmoja alisema hivi kwa huzuni: “Pindi fulani, mimi na mume wangu hatukufuata shauri la Waefeso 4:26, 27. Katika pindi hizo, ilikuwa vigumu sana kwangu kulala usiku!” Ni afadhali zaidi kuzungumzia mambo mara moja mkiwa na lengo la kusuluhisha tatizo! Bila shaka, huenda mume au mke akahitaji kumpa mwenzi wake muda kidogo wa kutulia. Pia, ni jambo linalofaa kusali ili Yehova awasaidie kuwa na mtazamo unaofaa. Mtazamo huo unatia ndani kuwa na roho ya unyenyekevu, ambayo itakusaidia kukazia fikira tatizo, badala ya kujifikiria tu na hivyo kufanya hali iwe mbaya zaidi.—Soma Wakolosai 3:12, 13.

16. Unyenyekevu unawezaje kuwasaidia wenzi wa ndoa kuwa na maoni yanayofaa kuhusu sifa zao nzuri?

16 Unyenyekevu na kiasi humsaidia mtu aliyefunga ndoa kukazia fikira sifa nzuri za mwenzi wake wa ndoa. Kwa mfano: Huenda mke akawa na uwezo wa pekee anaotumia kwa faida ya familia. Ikiwa mume ni mnyenyekevu na ni mwenye kiasi, hatahisi kwamba mke anataka kunyakua ukichwa wake, badala yake atamtia moyo atumie uwezo wake, na hivyo mume anaonyesha kwamba anamthamini na kumpenda sana. (Met. 31:10, 28; Efe. 5:28, 29) Naye mke mnyenyekevu na mwenye kiasi hatajigamba kwa sababu ya uwezo wake wala kumdharau mume wake. Kwa kweli, wawili hao ni “mwili mmoja,” na linalomuumiza mmoja linamuumiza mwingine.—Mt. 19:4, 5.

17. Ni nini kinachoweza kuwasaidia wenzi wa ndoa leo kuwa na furaha na kumletea sifa Mungu?

17 Bila shaka ungependa ndoa yako iwe kama ya Abrahamu na Sara au ya Isaka na Rebeka, yaani, ndoa yenye furaha ya kweli, yenye kudumu, na inayomletea sifa Yehova. Ikiwa ndivyo, fuata kabisa maoni ya Mungu kuhusu ndoa. Tegemea Neno lake ili upate ufahamu na hekima. Sitawisha upendo wa kweli, yaani, “mwali wa moto wa Yah,” kwa kumfikiria na kumthamini mwenzi wako. (Wim. 8:6) Jitahidi kabisa kusitawisha unyenyekevu. Mtendee kwa heshima mwenzi wako wa ndoa. Ukifanya mambo hayo, ndoa yako itakuletea shangwe na kumletea shangwe Baba yako wa mbinguni. (Met. 27:11) Kwa kweli, unaweza kuhisi kama yule mume aliyeoa kwa miaka 27, aliyeandika hivi: “Sijui maisha yangekuwaje bila mke wangu. Ndoa yetu inazidi kuimarika kila siku kwa sababu tunampenda Yehova na tunawasiliana kwa ukawaida.”