Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Muzungumuze Vizuri ili Ndoa Yenu Iwe na Furaha

Muzungumuze Vizuri ili Ndoa Yenu Iwe na Furaha

‘Neno linalosemwa wakati unaofaa ni kama matunda ya mutofaa ya zahabu kwenye chombo cha feza kilichopambwa.’​—MET. 25:11.

1. Namna gani kuzungumuza vizuri kumesaidia ndoa nyingi?

 NDUGU mumoja wa Canada alisema hivi: “Ninafurahia zaidi wakati ninaopitisha na bibi yangu kuliko wakati ninaopitisha na mutu mwengine yeyote. Ninapomuelezea namna ninavyojisikia, furaha yangu inaongezeka na huzuni yangu inapunguka.” Mwanaume mumoja wa Australie aliandika hivi: “Kwa miaka 11 ambayo tumeishi pamoja, hakuna hata siku moja ambayo imepita bila mimi kuongea na bibi yangu. Mimi na bibi yangu tunatumainiana. Kuzungumuza vizuri kila mara ndilo jambo kubwa ambalo limetusaidia.” Dada mumoja wa Costa Rica alishuhudia hivi: “Kuzungumuza vizuri kumesaidia ndoa yetu iwe na furaha, kumetusaidia tumukaribie Yehova zaidi, kumetulinda na majaribu, kumetuunganisha, na kumekomalisha upendo wetu.”

2. Ni mambo gani yanayoweza kufanya iwe vigumu kwa bibi na bwana kuzungumuza vizuri?

2 Je, wewe na bibi yako munazungumuza vizuri ao munaona kwamba ni vigumu kufanya hivyo? Bila shaka, matatizo yanaweza kutokea, kwa kuwa ndoa inaunganisha watu wawili wasio wakamilifu ambao wana tabia tofauti, zinazotia ndani tabia zinazotokana na desturi za kwao na namna ambavyo walikomaa. (Rom. 3:23) Zaidi ya hayo, bibi na bwana wanaweza kuzungumuza kwa njia tofauti. Ndiyo maana John M. Gottman na Nan Silver ambao ni wanaume wawili wanaojifunza mambo ya ndoa wanasema hivi: “Ili ndoa idumu, inafaa kuwa na ujasiri, bidii na uvumilivu.”

3. Ni nini imewasaidia bibi na bwana wengi wawe na furaha katika ndoa zao?

3 Bibi na bwana wanapaswa kufanya yote wanayoweza ili ndoa yao iwe na furaha. Ikiwa wanafanya hivyo, watapata furaha nyingi. Bibi na bwana wanaopendana wanaweza kabisa kuishi pamoja kwa furaha. (Mhu. 9:9) Fikiria ndoa yenye furaha ya Isaka na Rebeka. (Mwa. 24:67) Hata kisha kuishi pamoja kwa muda fulani, hakuna jambo linaloonyesha kwamba upendo wao ulipunguka. Bibi na bwana wengi wako hivyo leo pia. Siri yao ni nini? Wamejifunza kuzungumuzia waziwazi mawazo yao na namna wanavyojisikia, lakini wanafanya hivyo kwa upole, na wanakomalisha na kuonyesha sifa ya hekima, upendo, heshima kubwa, na unyenyekevu. Kama tutakavyoona, sifa hizo za maana zinapoonyeshwa katika ndoa, mazungumuzo yanakuwa mazuri kila siku.

FAHAMU VIZURI BIBI AO BWANA YAKO

4, 5. Namna gani ufahamu unaweza kuwasaidia bibi na bwana waelewane vizuri zaidi? Toa mifano.

4 Andiko la Methali 16:20 linasema hivi: ‘Anayetumia ufahamu katika jambo atapata mema, naye anayemutegemea Yehova ni mwenye furaha.’ Maneno hayo ni ya kweli kuhusu ndoa na maisha ya familia leo. (Soma Methali 24:3.) Neno la Mungu ndilo chanzo kizuri zaidi cha ufahamu na hekima. Andiko la Mwanzo 2:18 linatuambia kwamba Mungu alimuumba bibi ili awe kikamilisho cha bwana yake, wala si mutu aliye sawa na bwana yake. Daraka la mwanamuke linaonekana katika namna yake ya kuzungumuza. Bila shaka, watu wanatofautiana, wanawake kwa ujumla wanapenda kueleza kuhusu namna wanavyojisikia, kuhusu watu na marafiki. Wanapendezwa sana na mazungumuzo ya kirafiki, yaliyo wazi, kwa sababu yanawafanya wajisikie kuwa wanapendwa. Lakini, wanaume wengi hawafurahie kueleza namna wanavyojisikia, lakini wanafurahia zaidi kuzungumuzia kazi, matatizo, na namna ya kutatua matatizo hayo. Pia, wanaume wanataka waheshimiwe.

5 Dada mumoja wa Angleterre alisema hivi: “Bwana yangu anataka kutatua matatizo haraka kuliko kunisikiliza kwanza. Hilo linaweza kuvunja moyo kabisa kwa sababu jambo kubwa ninalotamani ni ‘yeye kunisikiliza na kujitia pa nafasi yangu.’” Bwana mumoja aliandika hivi: “Mwanzoni mwa ndoa yetu, muelekeo wangu ulikuwa tu kutafuta haraka namna tatizo lolote la bibi yangu linaweza kutatuliwa. Hata hivyo, baadaye nilitambua kwamba bibi yangu alitaka kwanza nimusikilize.” (Met. 18:13; Yak. 1:19) Bwana anayemufahamu ao kumuelewa bibi yake anafikiria namna anavyojisikia na anajipatanisha na hali yake. Wakati huo huo, anamuhakikishia kwamba anahangaikia mambo yaliyo katika moyo wake. (1 Pet. 3:7) Bibi pia anajikaza kuelewa maoni ya bwana yake. Bibi na bwana wanapoelewa, wanapofurahia, na kutimiza madaraka yao waliyopewa na Mungu, ndoa yao inapendeza kabisa. Na hilo linawasaidia wachukue na kutimiza pamoja maamuzi yenye hekima na yenye kusawazika.

6, 7. (a) Namna gani kanuni iliyo katika andiko la Mhubiri 3:7 inaweza kusaidia bibi na bwana watende kwa ufahamu? (b) Bibi anaweza kutenda kwa hekima namna gani, na bwana anapaswa kujikaza kufanya nini?

6 Bibi na bwana walio na ufahamu wanajua pia kwamba kuna “wakati wa kukaa kimya na wakati wa kusema.” (Mhu. 3:1, 7) Dada mumoja ambaye ameolewa kwa miaka kumi alisema hivi: “Ninatambua sasa kwamba kuna wakati ambapo si vizuri kuzungumuzia jambo fulani. Ikiwa bwana yangu amelemewa na kazi ao madaraka mengine, ninangoja wakati upite mbele ya kuzungumuzia mambo fulani. Kwa hiyo, mazungumuzo yetu yamekuwa mazuri zaidi.” Wanawake walio na hekima wanazungumuza kwa upole, wakijua kwamba maneno mazuri ‘yanayosemwa kwa wakati unaofaa’ yanavutia na kufurahiwa.​—Soma Methali 25:11.

Mambo madogo​-madogo ni ya maana sana katika ndoa

7 Bwana Mukristo anapaswa pia kumusikiliza bibi yake na kujikaza kumuelezea waziwazi mambo yaliyo katika moyo wake. Muzee mumoja wa kutaniko ambaye amefunga ndoa kwa miaka 27 alisema hivi: “Ninapaswa kujikaza sababu si rahisi kwangu kumuelezea bibi yangu mambo yaliyo katika moyo wangu.” Ndugu mumoja ambaye amefunga ndoa kwa miaka 24 alisema hivi: “Kila mara ninanyamaza na kufikiri kwamba tatizo fulani litamalizika ikiwa silizungumuzie. Lakini nimetambua kwamba kuonyesha bibi yangu mambo yaliyo katika moyo wangu si uzaifu. Ninaposhindwa kuzungumuzia mambo yaliyo katika moyo wangu, ninasali ili nipate maneno yanayofaa na niyaseme kwa njia inayofaa. Kisha kutulia vizuri, ninaanza kuongea.” Ni vizuri pia kuchagua wakati unaofaa, labda wakati munapochunguza andiko la siku ao munaposoma Biblia ninyi wawili tu.

8. Ni mambo gani mengine yanayoweza kuwachochea bibi na bwana wafanye mazungumuzo yao yawe mazuri?

8 Bibi na bwana wanapaswa kusali na kuwa na tamaa ya kufanya mazungumuzo yao yawe mazuri. Bila shaka, si rahisi kuachana na tabia za zamani. Lakini, ikiwa bibi na bwana wanamupenda Yehova, wanamuomba roho yake, na kuona ndoa yao kuwa takatifu, mambo hayo yatawachochea kufanya mabadiliko. Lakini watu wengi hawafanye hivyo. Bibi mumoja aliye na miaka 26 aliandika hivi: “Mimi na bwana yangu tunaheshimu sana maoni ya Mungu kuhusu ndoa, kwa hiyo hatufikirie hata kidogo kuachana. Hilo linatuchochea kufanya yote tunayoweza ili kutatua matatizo yetu kwa kuyazungumuzia pamoja.” Uaminifu kama huo unamupendeza Mungu na unaletea familia baraka nyingi.​—Zab. 127:1.

KOMALISHA UPENDO WAKO

9, 10. Namna gani bibi na bwana wanaweza kukomalisha upendo wao?

9 Upendo, ambao ni “kifungo kikamilifu cha muungano,” ni sifa ya maana sana katika ndoa. (Kol. 3:14) Upendo wa kweli unakomaa kadiri bibi na bwana waaminifu wanavyofurahia pamoja maisha na kupambana na matatizo. Wanaendelea hata kuwa marafiki wa karibu zaidi na wanafurahia kuwa pamoja. Bibi na bwana hao wamefanya ndoa zao ziwe na furaha si kwa kutendeana tu mambo makubwa-makubwa, kama filme na vitabu vya ulimwengu vinaonyesha, lakini kwa kutendeana mambo madogo-madogo kama vile, kukumbatiana, kumuambia bibi ao bwana yako neno la upole, kumutendea tendo nzuri, kumuangalia na sura yenye kicheko, ao kumuuliza “ulipitisha muchana namna gani?” Mambo hayo madogo-madogo ni ya maana sana katika ndoa. Bwana mumoja ambaye amekuwa na ndoa yenye furaha kwa miaka 19 anasema kwamba yeye na bibi yake wanazungumuza kupitia telefone ao wanaandikiana ujumbe mufupi wakati wa muchana “ili tu kujua ikiwa mwenzake iko katika hali gani.”

10 Upendo unachochea pia bibi ao bwana aendelee kujifunza ili kuelewa sifa na tabia za mwenzake. (Flp. 2:4) Kumufahamu bibi ao bwana yako kunafanya umupende zaidi ijapokuwa uzaifu wake mbalimbali. Ili kuwa na furaha zaidi, bibi na bwana wanapaswa kuendelea kufanya mabadiliko. Kwa hiyo, ikiwa umefunga ndoa, unaweza kujiuliza hivi: ‘Ninamujua bibi ao bwana yangu kadiri gani? Je, ninaelewa namna anavyojisikia na mawazo yake kuhusu mambo? Ni mara ngapi ninafikiri kuhusu bibi ao bwana yangu, labda kufikiria tena sifa ambazo zilinifanya nimupende nilipovutiwa naye kwa mara ya kwanza?’

MUHESHIMIANE

11. Sababu gani ni jambo la maana bibi na bwana waheshimiane? Toa mufano.

11 Hata ndoa zenye furaha zaidi zina matatizo, na bibi na bwana wanaopendana hawawezi kuwa na maoni yenye kupatana siku zote. Abrahamu na Sara hawakukubaliana kila mara. (Mwa. 21:9-11) Hata hivyo, uhusiano wao haukuharibika kwa sababu ya kuwa na maoni tofauti. Sababu gani? Kwa sababu waliheshimiana. Kwa mufano, Abrahamu alitumia neno ‘tafazali’ alipozungumuza na Sara. (Mwa. 12:11, 13) Sara kwa upande wake, alimutii Abrahamu na alimuona kuwa “bwana” wake. (Mwa. 18:12) Bibi na bwana wanapokosa kuheshimiana, hilo linaonekana wazi katika namna yao ya kuzungumuza ao sauti zao. (Met. 12:18) Ikiwa hawazungumuzie matatizo yao, ndoa yao inaweza kuvunjika.​—Soma Yakobo 3:7-10, 17, 18.

12. Sababu gani bibi na bwana ambao ni wapya katika ndoa wanapaswa kujikaza kuzungumuza kwa heshima?

12 Bibi na bwana ambao ni wapya katika ndoa, wanapaswa kujikaza sana kuzungumuza kwa upole na kwa heshima, hilo litafanya kila mumoja wao ajisikie huru kueleza maoni yake. Bwana mumoja anakumbuka hivi: “Ijapokuwa miaka ya kwanza​-kwanza katika ndoa ni yenye furaha, matatizo yanaweza kutokea wakati fulani. Kadiri kila mumoja anavyoendelea kujua vizuri namna mwengine anavyojisikia, tabia zake, na mahitaji yake, hilo linaweza kutokeza matatizo mengine madogo madogo! Hata hivyo, jambo litakalowasaidia ni kuwa na maoni mazuri kuhusu matatizo hayo, kuwa mwenye kufanya muzaha ao kuchekesha kidogo, na kuonyesha sifa zinazosaidia ndoa iwe nguvu, ni kusema, unyenyekevu, uvumulivu na kumutegemea Yehova.” Hayo ni mashauri mazuri kabisa.

ONYESHA UNYENYEKEVU WA KWELI

13. Sababu gani unyenyekevu ni jambo la maana ili ndoa iwe yenye furaha?

13 Mazungumuzo mazuri ni kama muto unaotiririka polepole na kwa utulivu katika bustani. Kuwa “wanyenyekevu katika akili” kunasaidia sana mazungumuzo yaendelee kupendeza. (1 Pet. 3:8) Ndugu mumoja ambaye amefunga ndoa kwa miaka 11 alisema hivi: “Unyenyekevu ni njia rahisi ya kutatua matatizo kwa sababu unamuchochea mutu kuomba musamaha.” Muzee mumoja wa kutaniko ambaye amekuwa katika ndoa yenye furaha kwa miaka 20, anaeleza hivi: “Wakati fulani ni jambo la maana kusema ‘Unisamehe’ kuliko kusema ‘Ninakupenda.’” Aliongezea hivi: “Njia moja rahisi ya kupata unyenyekevu ni sala. Tunapomukaribia Yehova Mungu katika sala, mimi na bibi yangu tunakumbuka kwamba sisi ni watu wasio wakamilifu na tunahitaji fazili zisizostahiliwa za Mungu. Kukumbuka hayo kunatusaidia tutatue matatizo yetu.”

Endelea kuzungumuza vizuri na bibi ao bwana yako

14. Namna gani kiburi kinaweza kuharibu amani katika ndoa?

14 Hata hivyo, kiburi kinaharibu amani. Kinazuia mazungumuzo kwa sababu kinamufanya mutu asiwe na nia ya kuomba musamaha. Kuliko kusema kwa upole, “Nimekosea; tafazali unisamehe,” mutu mwenye kiburi anajitetea. Kuliko kutambua uzaifu wake, anaona tu makosa ya wengine. Anapoumizwa, kuliko kufanya amani, anajilipizia kisasi, labda kupitia maneno makali ao anaepuka kuongea na mutu aliyemukosea. (Mhu. 7:9) Kwa kweli, kiburi kinaweza kuua ndoa. Ni vizuri kukumbuka kwamba ‘Mungu anawapinga wenye majivuno, lakini anawapa wanyenyekevu fazili zisizostahiliwa.’​—Yak. 4:6.

15. Eleza namna gani kutumia kanuni inayopatikana katika Waefeso 4:26, 27 kunaweza kusaidia bibi na bwana watatue matatizo yao.

15 Bila shaka, tusifikiri kama hatuwezi kuwa na kiburi. Tunapaswa kutambua makosa yetu na kuyazungumuzia. Mutume Paulo aliwaambia Wakristo wenzake hivi: ‘Jua lisitue mukiwa katika hali ya kuchokozeka, wala musimupe Ibilisi nafasi.’ (Efe. 4:26, 27) Kushindwa kutumikisha mashauri ya Neno la Mungu kunaweza kuleta matatizo. Dada mumoja alilalamika hivi: “Wakati mumoja, mimi na bwana yangu hatukutumia mashauri ya andiko la Waefeso 4:26, 27. Hizo zilikuwa siku mbaya sana katika maisha yangu, sikupata usingizi wakati huo.” Bila shaka ni vizuri sana kuzungumuzia bila kuchelewa mambo yanayowasumbua mukiwa na nia ya kurudisha amani kati yenu. Kwa kweli, bibi ao bwana anapaswa kumuachia mwenzake wakati wa kutulizana mbele ya kuzungumuza naye juu ya tatizo fulani. Ni vizuri pia kumuomba Yehova amani ya akili, hilo linatia ndani pia kuwa na unyenyekevu ambao utakusaidia kufikiria tatizo, wala si kujifikiria, ili usiharibu mambo zaidi.​—Soma Wakolosai 3:12, 13.

16. Namna gani unyenyekevu unasaidia bibi ao bwana awe na maoni yanayofaa kuhusu uwezo wa pekee na sifa za mwengine?

16 Unyenyekevu na kiasi vinamusaidia kila mumoja afikirie sana sifa nzuri na uwezo mbalimbali wa bibi ao bwana yake. Kwa mufano, bibi anaweza kuwa na uwezo fulani wa pekee anaoweza kutumia ili kuisaidia familia yake. Ikiwa bwana yake ni munyenyekevu na mwenye kiasi, hatafikiri kama bibi yake anataka kumunyanganya madaraka yake ao kujionyesha, lakini atamutia moyo atumie uwezo ao zawadi yake; hilo litaonyesha kwamba bwana anamusamini na kumupenda. (Met. 31:10, 28; Efe. 5:28, 29) Vilevile, bibi munyenyekevu na mwenye kiasi hatajivuna kwa sababu ya uwezo wake mbalimbali ao kumuzarau bwana yake. Wote wawili ni ‘mwili mumoja,’ sivyo? Na jambo linaloweza kumuumiza huyu linaweza pia kumuumiza yule mwengine.​—Mt. 19:4, 5.

17. Ni nini inayoweza kusaidia ndoa za leo ziwe zenye furaha na zenye kumutukuza Yehova?

17 Bila shaka, unapenda ndoa yako iwe kama ile ya Abrahamu na Sara ao Isaka na Rebeka, ni kusema, ndoa yenye furaha ya kweli, yenye kudumu, na inayomutukuza Yehova. Ikiwa hiyo ndio tamaa yako, shikamana na maoni ya Mungu kuhusu ndoa. Tafuta hekima ya Neno lake. Onyesha upendo wa kweli, ambao ni “mwali wa moto wa Yah” kwa kufikiria zaidi sana sifa nzuri za bibi ao bwana yako. (Wim. 8:6) Jikaze kuonyesha unyenyekevu. Muheshimu bibi ao bwana yako. Ukifanya mambo hayo, ndoa yako itakuletea wewe furaha na itamutukuza Baba yetu wa mbinguni. (Met. 27:11) Kwa kweli, unaweza kuwa na maoni yanayofanana na yale ya bwana mumoja ambaye amefunga ndoa kwa miaka 27, aliyeandika hivi: “Sijue maisha yangu yanaweza kuwa namna gani ikiwa ninaishi bila bibi yangu. Ndoa yetu inaendelea kuwa yenye furaha zaidi na zaidi kila siku. Mambo yamekuwa hivyo kwa sababu tunamupenda Yehova na tunazungumuza kwa ukawaida.”