Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wazazi na Watoto—Wasilianeni kwa Upendo

Wazazi na Watoto—Wasilianeni kwa Upendo

“Kila mtu lazima awe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu.” —YAK. 1:19.

1, 2. Kwa ujumla wazazi na watoto huwa na hisia gani kati yao, lakini nyakati nyingine wanakabili tatizo gani?

“IKIWA ungejua kwa njia fulani kwamba wazazi wako watakufa kesho, ni jambo gani ambalo ungetaka sana kuwaambia leo?” Mamia ya watoto nchini Marekani waliulizwa swali hilo. Badala ya kutaja matatizo au hali yoyote ya kutoelewana, asilimia 95 ya watoto walisema kwamba wangewaambia wazazi wao: “Pole” na “Ninakupenda sana.”—Kitabu For Parents Only, cha Shaunti Feldhahn na Lisa Rice.

2 Kwa ujumla, watoto wanawapenda wazazi wao, na wazazi wanawapenda watoto wao. Ndivyo ilivyo hasa katika familia za Kikristo. Ingawa wazazi na watoto hutamani kuwa na uhusiano wa karibu, nyakati nyingine inakuwa vigumu kwao kuwasiliana. Kwa nini wanaepuka kabisa kuzungumzia masuala fulani, hata wanapoongea kwa unyoofu na waziwazi? Ni baadhi ya mambo gani yanayozuia mawasiliano mazuri? Mnawezaje kukabiliana nayo?

Msiruhusu mambo yanayokengeusha fikira na pia kujitenga kuwazuie kuwasiliana katika familia yenu

‘NUNUENI’ WAKATI WA KUWASILIANA

3. (a) Kwa nini ni vigumu kwa familia nyingi kuwa na mawasiliano mazuri? (b) Kwa nini ilikuwa rahisi kwa familia katika Israeli kupata wakati wa kuwa pamoja?

3 Ni vigumu kwa familia nyingi kupata wakati wa kutosha wa kuwa na mawasiliano mazuri. Haikuwa hivyo zamani. Musa aliwaagiza hivi akina baba Waisraeli: “Uyakazie [maneno ya Mungu] kwa mwana wako na kuyasema unapoketi katika nyumba yako na unapotembea barabarani na unapolala na unapoamka.” (Kum. 6:6, 7) Kwa siku nzima, watoto walikaa na mama yao nyumbani au walifanya kazi na baba yao shambani au mahali pake pa kazi. Watoto na wazazi walikuwa na wakati mwingi wa kuwa pamoja na kuzungumza. Kwa hiyo, wazazi walikuwa na fursa ya kujua mahitaji,  tamaa, na utu wa watoto wao. Vivyo hivyo, watoto walikuwa na wakati wa kutosha wa kuwajua wazazi wao vizuri.

4. Kwa nini familia nyingi leo zina tatizo la kutowasiliana?

4 Maisha yamebadilika sana leo! Katika nchi fulani, watoto huanza masomo ya chekechea wakiwa na umri mdogo, nyakati nyingine wakiwa na umri wa miaka miwili tu. Akina baba na mama wengi hufanya kazi mbali na nyumbani. Badala ya wazazi na watoto kutumia muda mchache wanaokuwa pamoja ili kuwasiliana, mara nyingi wanautumia kutazama televisheni, kutumia kompyuta, na vifaa vingine vya kielektroniki. Mara nyingi, watoto na wazazi huishi kama wageni wasiofahamiana. Huenda wasiwe na mazungumzo yoyote ya maana.

5, 6. Baadhi ya wazazi ‘hununuaje’ wakati zaidi ili wawe pamoja na watoto wao?

5 Je, mnaweza ‘kununua’ wakati mnaoutumia katika mambo mengine ili muwe na wakati zaidi wa kuwa pamoja na familia yenu? (Soma Waefeso 5:15, 16.) Baadhi ya familia hukubaliana kupunguza wakati wanaotumia kutazama televisheni au kutumia kompyuta. Wengine hujitahidi kula pamoja angalau mlo mmoja kila siku. Na mpango wa ibada ya familia unawapa wazazi na watoto fursa nzuri kama nini ya kujenga uhusiano wa karibu na kuzungumzia mambo ya kiroho kwa utulivu! Kutenga saa moja hivi kila juma kwa kusudi hilo ni mwanzo mzuri, lakini muda zaidi unahitajiwa ili kuzungumzia mambo kwa undani. Ili kufanya hivyo, ni lazima familia iwasiliane kwa ukawaida na mara nyingi. Kabla mtoto wako hajaenda shuleni, mwambie jambo litakalomtia moyo, zungumzieni andiko la siku, au usali pamoja naye. Kufanya hivyo kunaweza kumsaidia sana kukabiliana na hali za siku hiyo.

6 Baadhi ya wazazi wamefaulu kubadili mtindo wao wa maisha ili kutumia wakati zaidi pamoja na watoto wao. Kwa mfano, Laura, * mama wa watoto wawili wadogo,  aliacha kazi ya kuajiriwa ya wakati wote ili apate wakati wa kuwa na watoto wake. Anasema hivi: “Asubuhi sote tulitoka haraka-haraka na kwenda kazini au shuleni. Niliporudi nyumbani jioni, niliwakuta watoto wakiwa wamelala baada ya kubembelezwa na yaya. Baada ya kuacha kazi tumelazimika kuishi maisha rahisi, lakini sasa ninahisi kwamba ninaelewa matatizo na mawazo ya watoto wangu. Wanaposali, ninasikiliza wanayosema na kuwaongoza, ninawatia moyo na kuwafundisha.”

UWE “MWEPESI KUHUSU KUSIKIA”

7. Kwa kawaida wazazi na watoto hulalamika kuhusu nini?

7 Baada ya kuwahoji vijana wengi, watungaji wa kitabu For Parents Only walitaja kizuizi kingine cha mawasiliano. Wanasema hivi: “Watoto wengi walilalamika hivi kuhusu wazazi wao, ‘Hawasikilizi.’” Si wazazi tu walio na tatizo hilo. Kwa kawaida wazazi hulalamika vivyo hivyo kuhusu watoto wao. Ili mawasiliano yawe mazuri, ni lazima washiriki wa familia wawasikilize kwa makini washiriki wenzao.—Soma Yakobo 1:19.

8. Wazazi wanawezaje kuwasikiliza kwa makini watoto wao?

8 Wazazi, je, mnawasikiliza kwa makini watoto wenu? Huenda ikawa vigumu kufanya hivyo mnapokuwa mmechoka au watoto wanapozungumzia mambo yanayoonekana kuwa madogo. Lakini huenda mambo mnayoona kuwa madogo ni muhimu sana kwa mtoto wenu. ‘Kuwa mwepesi wa kusikia’ kunamaanisha kutilia maanani mambo anayosema na pia jinsi anavyoyasema. Sauti yake na ishara za mwili zinaweza kuwasaidia kuelewa hisia za mtoto. Ni muhimu pia kuuliza maswali. Biblia inasema hivi: “Mawazo ya mtu ni kama maji katika kisima chenye kina, lakini mtu mwenye ufahamu anaweza kuyateka.” (Met. 20:5, Today’s English Version) Mnahitaji ufahamu na utambuzi mnapowachochea watoto wenu wajieleze hasa mnapozungumzia masuala mazito.

9. Kwa nini watoto wanapaswa kuwasikiliza wazazi wao?

9 Watoto, je, mnawatii wazazi wenu? Neno la Mungu linasema: “Mwanangu, sikiliza nidhamu ya baba yako, wala usiiache sheria ya mama yako.” (Met. 1:8) Kumbukeni kwamba wazazi wenu wanawapenda na wanawajali kutoka moyoni, kwa hiyo ni jambo la hekima kuwasikiliza na kuwatii. (Efe. 6:1) Ni rahisi zaidi kutii mnapokuwa na mawasiliano mazuri na wazazi wenu na mnapojua kwamba mnapendwa. Waambieni wazazi wenu jinsi mnavyohisi kuhusu mambo mbalimbali. Kufanya hivyo kutawasaidia wazazi kuwaelewa. Bila shaka, mnapaswa pia kujitahidi kuwaelewa.

10. Tunajifunza nini kutokana na simulizi la Biblia kumhusu Rehoboamu?

10 Mnahitaji kuwa waangalifu kuhusu kusikiliza mashauri ya vijana wenzenu. Wanaweza kuwaambia mambo mnayotaka kusikia, lakini huenda mashauri yao yasiwasaidie kamwe. Kwa kweli, huenda hata yakawadhuru. Kwa kuwa hawana hekima na uzoefu kama watu wazima, vijana wengi hawawezi kuona matokeo ya matendo fulani wala kutambua madhara yake. Mkumbukeni Rehoboamu, mwana wa Mfalme Sulemani. Alipotawazwa kuwa mfalme wa Israeli, angetenda kwa hekima ikiwa angefuata mashauri ya wanaume wazee. Badala yake, alifuata mashauri ya kipumbavu ya wanaume vijana aliolelewa nao. Matokeo ni kwamba raia wengi wa ufalme wake hawakuendelea kumuunga mkono. (1 Fal. 12:1-17) Badala ya kuiga mwenendo usio wa hekima wa Rehoboamu, jitahidini kuwasiliana waziwazi na wazazi wenu. Zungumzeni na wazazi wenu kuhusu mambo mnayofikiria. Faidikeni na mashauri  yao na mjifunze kutokana na hekima yao.—Met. 13:20.

11. Matokeo yanaweza kuwa nini ikiwa wazazi hawana urafiki?

11 Wazazi, ikiwa hamtaki watoto wenu watafute mashauri kutoka kwa wenzao, jitahidini kuwa wenye urafiki ili wajihisi huru kuongea nanyi. Dada mmoja tineja aliandika hivi: “Ninapotaja tu jina la mvulana, wazazi wangu hushikwa na wasiwasi. Hilo hunifanya niogope na kusita kuendelea kuongea.” Dada mwingine kijana aliandika hivi: “Matineja wengi wanataka mashauri ya wazazi wao, lakini ikiwa wazazi wanapuuza maoni yao, watamfikia mtu mwingine atakayewasikiliza, hata ikiwa hana uzoefu mwingi.” Ikiwa mko tayari kuwasikiliza watoto wenu kwa huruma wanapozungumzia jambo lolote lile, inaelekea kwamba wataongea nanyi kwa uhuru na kukubali mwongozo wenu.

‘USIWE MWEPESI WA KUSEMA’

12. Itikio la wazazi linawezaje kuwazuia kuwasiliana na watoto wao?

12 Watoto wanapowaambia wazazi mambo fulani, wazazi huzuia mawasiliano wanapoudhika na kukasirika. Ni jambo la kawaida kwa wazazi Wakristo kutaka kuwalinda watoto wao. ‘Siku hizi za mwisho’ zimejaa hatari za kiroho na hatari nyingine. (2 Tim. 3:1-5) Hata hivyo, huenda watoto wakaona kwamba wazazi wao wanawalinda kupita kiasi.

13. Kwa nini wazazi wanapaswa kuwa waangalifu kutokimbilia kutoa maoni yao?

13 Ni jambo la hekima kwa wazazi kutokimbilia kutoa maoni yao. Ni kweli kwamba si rahisi sikuzote kunyamaza watoto wenu wanapowaambia jambo fulani linaloudhi. Lakini ni muhimu kusikiliza kwa makini kabla ya kujibu. Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Yeyote anapojibu jambo kabla ya kulisikia, huo ni upumbavu na aibu kwake.” (Met. 18:13) Ukiwa mtulivu, utasikia mengi zaidi na watoto wako wataendelea kuongea. Ni lazima upate habari kamili kabla ya kuweza kuwasaidia. Huenda “mazungumzo ya ovyoovyo” yakawa yanatoka katika moyo uliovurugika. (Ayu. 6:1-3) Mkiwa wazazi wenye upendo, tumieni masikio yenu kupata uelewaji na ulimi wenu kuponya.

14. Kwa nini watoto hawapaswi kuwa wepesi wa kusema?

14 Watoto, ninyi pia ‘hampaswi kuwa wepesi wa kusema,’ hampaswi kufanya haraka kukataa mnayoambiwa na wazazi wenu, kwa kuwa Mungu amewapa wazazi jukumu la kuwalea. (Met. 22:6) Huenda wamewahi kukabili hali mnazokabili sasa. Isitoshe, wanajutia makosa waliyofanya walipokuwa vijana na wanataka kwa dhati kukulinda ili usifanye makosa kama hayo. Kwa hiyo, waone wazazi wako kuwa marafiki badala ya kuwaona kuwa maadui au wapinzani. (Soma Methali 1:5.) “Mheshimu baba yako na mama yako,” na uwaonyeshe kwamba unawapenda kama wanavyokupenda. Hilo litafanya iwe rahisi zaidi kwao ‘kukulea katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.’—Efe. 6:2, 4.

‘USIWE MWEPESI WA GHADHABU’

15. Ni nini kitakachotusaidia kuendelea kuwa na subira na kutowakasirikia wapendwa wetu?

15 Nyakati nyingine tunakosa subira tunaposhughulika na wale tunaowapenda. Alipowaandikia “watakatifu na ndugu waaminifu katika muungano na Kristo walioko Kolosai,” mtume Paulo alisema hivi: “Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu nanyi msiwakasirikie kwa uchungu. Enyi akina baba, msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, ili wasivunjike moyo.” (Kol. 1:1, 2; 3:19, 21) Paulo aliwahimiza hivi Waefeso: “Uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu.” (Efe. 4:31) Kusitawisha ustahimilivu,  upole, na kujizuia—sifa za tunda la roho ya Mungu—kutatusaidia kubaki watulivu hata chini ya hali ngumu.—Gal. 5:22, 23.

16. Yesu aliwarekebishaje wanafunzi wake, na kwa nini hilo lilikuwa jambo la pekee?

16 Fikiria mfano wa Yesu. Wazia mkazo mkubwa aliokuwa nao kwenye mlo wake wa mwisho pamoja na mitume wake. Yesu alijua kwamba baada ya saa chache angekufa kifo cha polepole na chenye maumivu makali. Kutakaswa kwa jina la Baba yake na wokovu wa wanadamu ulitegemea uaminifu wake. Hata hivyo, kwenye mlo huo, ‘kulitokea bishano kali kati [ya mitume] juu ya ni nani kati yao aliyeonekana kuwa mkuu zaidi ya wote.’ Yesu hakuwafokea kwa hasira au kuwashutumu kwa uchungu. Badala yake, alizungumza nao kwa utulivu. Yesu aliwakumbusha kwamba walikuwa wameshikamana naye katika majaribu. Ingawa Shetani alikuwa amedai kuwapepeta kama ngano, Yesu alikuwa na hakika kwamba wangebaki waaminifu. Hata alifanya agano pamoja nao.—Luka 22:24-32.

Je, unawasikiliza kwa makini watoto wako?

17. Ni nini kitakachowasaidia watoto kuwa watulivu?

17 Watoto pia wanahitaji kuwa watulivu. Wanapofikia hasa umri wa utineja, huenda wakahisi kwamba wazazi hawawaamini ndiyo sababu wanawapa mwongozo. Ingawa huenda ikaonekana hivyo nyakati nyingine, tambua kwamba wazazi wako wanakuhangaikia kwa sababu wanakupenda. Ukiwasikiliza kwa utulivu na kushirikiana nao, watakuheshimu na kukuona kuwa mtu anayewajibika. Ukijiendesha kwa njia hiyo huenda wakakupa uhuru zaidi wa kujiamulia mambo fulani maishani. Ni jambo la hekima kuwa na sifa ya kujizuia. Methali moja yenye hekima inasema hivi: “Mtu mjinga huiachilia roho yake yote, lakini mwenye hekima huituliza mpaka mwisho.”—Met. 29:11.

18. Upendo huletaje mawasiliano mazuri?

18 Kwa hiyo, wazazi na watoto wapendwa, msivunjike moyo ikiwa mawasiliano katika familia yenu si mazuri kama vile ambavyo mngependa. Endeleeni kujitahidi kuyaboresha, na mwendelee kutembea katika kweli. (3 Yoh. 4) Katika ulimwengu mpya, watu wakamilifu watakuwa na mawasiliano makamilifu, hawatakosana wala kugombana. Hata hivyo, kwa sasa, sisi sote hufanya mambo tunayojutia baadaye. Basi usisite kuomba msamaha. Samehe kwa hiari. ‘Muunganishwe pamoja kwa upatano katika upendo.’ (Kol. 2:2) Upendo una nguvu. ‘Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. Hauchokozeki. Hauweki hesabu ya ubaya. Huhimili mambo yote, huamini mambo yote, hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote.’ (1 Kor. 13:4-7) Endeleeni kusitawisha upendo, na mawasiliano yataboreka, familia yenu itapata shangwe nanyi mtamletea sifa Yehova.

^ fu. 6 Jina limebadilishwa.