Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Wazazi, Watoto—Muzungumuze kwa Upendo

Wazazi, Watoto—Muzungumuze kwa Upendo

‘Kila mutu lazima awe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa gazabu.’​—YAK. 1:19.

1, 2. Kwa kawaida wazazi na watoto wanaonyeshana sifa gani, lakini ni matatizo gani wanayopambana nayo?

 WATOTO wengi katika États-Unis waliulizwa hivi: “Ikiwa ungejua kwamba wazazi wako watakufa kesho, ni jambo gani la maana sana ambalo ungetaka kuwaambia leo?” Kuliko kufikiria tu matatizo na kutoelewana ambako labda kumetokea kati yao na wazazi wao, watoto karibu 95 kati ya 100 walisema kwamba wangefurahia kuwaambia wazazi wao hivi: “Unisamehe kwa mambo yote ambayo nimekutendea” na “Ninakupenda sana.”​—For Parents Only, kitabu kilichoandikwa na Shaunti Feldhahn na Lisa Rice.

2 Kwa kawaida, watoto wanawapenda wazazi wao, na wazazi wanawapenda watoto wao. Hilo linaonekana zaidi sana katika familia za Kikristo. Ijapokuwa wazazi na watoto wanatamani sana kuwa marafiki wa karibu, wakati fulani inakuwa vigumu kwao kuzungumuza. Hata ikiwa wanaweza kuzungumuza waziwazi, sababu gani hawataki hata kidogo kuzungumuzia mambo fulani? Ni mambo gani yanayozuia mazungumuzo mazuri? Namna gani tunaweza kuyaepuka?

Musiruhusu kujitenga na wengine na vitu vya kukengeusha akili vizuie mazungumuzo

‘NUNUA’ WAKATI WA KUZUNGUMUZA

3. (a) Sababu gani mazungumuzo yenye kujenga yanakosekana katika familia nyingi? (b) Sababu gani tunaweza kusema kwamba ilikuwa rahisi kwa familia katika taifa la Israeli kupitisha wakati pamoja?

3 Familia nyingi zinakosa wakati wa kutosha ili kuwa na mazungumuzo yenye kujenga. Lakini, mambo hayakuwa hivyo zamani. Musa aliwaagiza akina baba katika taifa la Israeli hivi: ‘Ukazie [Maneno ya Mungu] kwa mwana wako na kuyasema unapoketi katika nyumba yako na unapotembea barabarani na unapolala na unapoamuka.’ (Kum. 6:6, 7) Watoto walipitisha wakati pamoja na mama yao nyumbani ao pamoja na baba yao shambani ao mahali pake pa kazi. Wazazi na watoto walikuwa na wakati mwingi wa kuwa pamoja na kuzungumuza. Kwa hiyo, ilikuwa rahisi kwa wazazi kujua mahitaji ya watoto wao, mambo wanayopenda, na tabia zao. Pia, watoto walikuwa na wakati na nafasi nyingi za kuwajua vizuri wazazi wao.

4. Ni mambo gani yanayozuia mazungumuzo kati ya wazazi na watoto?

4 Leo, mambo yamebadilika kabisa! Katika inchi fulani, watoto wanaanza masomo wakiwa na umri mudogo, wakati mwengine wakiwa na miaka miwili tu. Baba na mama wengi wanafanya kazi mbali na nyumbani. Na hata wanapokuwa pamoja kwa wakati muchache, ordinatere, televizyo, ao vyombo vingine vya kielektroniki vinazuia mazungumuzo kati ya wazazi na watoto. Katika familia nyingi, kila mutu anahangaikia tu mambo yake. Kwa hiyo, wazazi na watoto hawafahamiane na hawazungumuze tena.

5, 6. Wazazi fulani ‘wamenunua’ wakati namna gani ili wapitishe wakati mwingi zaidi pamoja na watoto wao?

5 Je, unaweza ‘kununua’ wakati unaotumia kufanya mambo mengine ili upitishe wakati mwingi zaidi pamoja na familia yako? (Soma Waefeso 5:15, 16.) Familia fulani zimekubali kupunguza wakati wanaotumia ili kutazama televizyo ao kutumia ordinatere. Wengine wanajikaza kutumia chakula pamoja hata mara moja kwa siku. Pia, mupango kwa ajili ya ibada ya familia unawatolea wazazi na watoto nafasi nzuri ya kuwa pamoja na kuzungumuzia mambo ya kiroho kwa utulivu. Ni vizuri kupanga saa moja ao zaidi kila juma kwa ajili ya mupango huo, lakini mengi yanahitajiwa ili washiriki wa familia wajisikie huru kueleza maoni yao. Kwa hiyo, wazazi na watoto wanapaswa kuzungumuza kwa ukawaida. Mbele mutoto wako aende kwenye masomo, muambie jambo fulani lenye kutia moyo, chunguza pamoja naye andiko la siku, ao unaweza kusali pamoja naye. Kufanya hivyo kunaweza kumusaidia sana siku hiyo.

6 Wazazi fulani wamebadili namna yao ya kuishi ili kupitisha wakati mwingi zaidi pamoja na watoto wao. Kwa mufano, Laura, * mama aliye na watoto wawili wadogo, aliacha kazi iliyokuwa ikimuchukua wakati mwingi ili aweze kupitisha wakati pamoja na watoto wake. Anasema hivi: “Asubuhi, kila mutu alifanya haraka ili kuenda kwenye kazi ao kwenye masomo. Niliporudi nyumbani mangaribi, tayari watoto wangu walikuwa wamelala, mwanamuke anayelipwa ili kuwachunga watoto wangu ndiye alikuwa amewashugulikia. Nilipoacha kazi hiyo, tulihitaji kuishi na feza kidogo, lakini ninatambua kwamba sasa ninajua mawazo na matatizo ya watoto wangu. Ninasikiliza namna wanavyosali na ninaweza kuwapa mashauri, ninawatia moyo, na kuwafundisha.”

UWE “MWEPESI KUHUSU KUSIKIA”

7. Wazazi na watoto wengi wanalalamika juu ya jambo gani?

7 Kisha kuwauliza vijana wengi, waandishi wa kitabu kilichotajwa mwanzoni mwa habari hii walitambua jambo lingine linalozuia mazungumuzo. Wanasema hivi: “Lalamiko la kwanza ambalo watoto walitoa kuhusu wazazi wao lilikuwa, ‘Wazazi wetu hawatusikilize.’” Lakini si wazazi tu wasiosikiliza. Wazazi pia wamelalamika mara nyingi kwamba watoto wao hawawasikilize. Ili kila mutu ajisikie huru kuzungumuza na mwengine, kila mushiriki wa familia anapaswa kusikiliza vizuri mwenzake.​—Soma Yakobo 1:19.

8. Namna gani wazazi wanapaswa kuwasikiliza watoto wao?

8 Wazazi, je, munasikiliza kwa uangalifu watoto wenu? Labda inaweza kuwa vigumu kufanya hivyo ikiwa mumechoka ao ikiwa mazungumuzo yao yanahusu mambo yasiyo ya maana. Lakini, mambo ambayo unaweza kuona kuwa si ya maana yanaweza kuwa ya maana kwa mutoto wako. Kuwa “mwepesi kuhusu kusikia” kunamaanisha kukazia uangalifu mambo ambayo mutoto wako anasema na namna anavyoyasema. Sauti na ishara za mwili zinaweza kukusaidia kutambua namna mutoto wako anavyojisikia. Unapaswa pia kumuuliza maulizo. Biblia inasema hivi: ‘Shauri moyoni mwa mutu ni kama kilindi cha maji, lakini mwenye utambuzi ataliteka.’ (Met. 20:5) Unapaswa kuwa na utambuzi na hekima zaidi sana unapotaka kujua mawazo ya watoto wako kuhusu mambo ambayo si rahisi kuzungumuzia.

9. Sababu gani watoto wanapaswa kutii wazazi wao?

9 Watoto, je, munawatii wazazi wenu? Neno la Mungu linasema hivi: ‘Mwanangu, sikiliza nizamu ya baba yako, wala usiache sheria ya mama yako.’ (Met. 1:8) Usisahau kwamba wazazi wako wanakupenda na wanataka uwe na maisha mazuri, kwa hiyo, ni jambo la hekima kuwasikiliza na kuwatii. (Efe. 6:1) Itakuwa rahisi zaidi kwako kuwatii wazazi wako ikiwa unazungumuza nao vizuri na ikiwa unajua kwamba wanakupenda. Waelezee wazazi wako mawazo yako. Hilo litawasaidia wakuelewe. Lakini, wewe pia unapaswa kujikaza kuwaelewa.

10. Masimulizi ya Biblia kuhusu Rehoboamu yanatufundisha nini?

10 Unapaswa kuwa mwangalifu kuhusu mashauri ambayo vijana wa umri wako wanaweza kukutolea. Wanaweza kukuambia mambo unayotaka tu kusikia, lakini mashauri yao hayawezi kukusaidia. Na yanaweza hata kukuletea shida. Kwa sababu hawana hekima na hawajaona mambo mengi kama vile watu wazima, vijana hawaone mbali na labda hawawezi kutambua matokeo ya matendo fulani. Kumbuka mufano wa mwana wa Mufalme Sulemani anayeitwa Rehoboamu. Alipokuwa mufalme katika Israeli, lingekuwa jambo la hekima ikiwa angefuata mashauri ya wanaume wazee. Lakini, alifuata mashauri ya upumbavu ya wanaume vijana waliokomaa naye. Kwa hiyo, raia wengi wa ufalme wake waliasi. (1 Fal. 12:1-17) Kuliko kuiga mufano wa upumbavu wa Rehoboamu, jikaze ili mazungumuzo yabaki wazi kati yako na wazazi wako. Waelezee mawazo yako. Fuata mashauri yao, na ujifunze kutokana na hekima yao.​—Met. 13:20.

11. Mambo yanaweza kuwa namna gani ikiwa wazazi ni watu ambao si rahisi kuzungumuza nao?

11 Wazazi, ikiwa hamutaki watoto wenu waende kuomba mashauri kwa rafiki zao, mujikaze kuwa rafiki zao ili wazungumuze nanyi kwa urahisi. Dada mumoja aliye na miaka kati ya 13 na 19 alisema hivi: “Ninapotaja tu jina la kijana fulani, wazazi wangu wanakasirika mara moja. Hilo linanivunja moyo na ninashindwa kuendelea kuongea.” Dada mwengine kijana aliandika hivi: “Vijana wengi walio na miaka kati ya 13 na 19 wanapenda mashauri ya wazazi wao, lakini ikiwa wazazi wao hawawaelewe, vijana hao wanaenda kumutafuta mutu atakayewaelewa, hata ikiwa mutu huyo hana hekima nyingi.” Ikiwa unamusikiliza mutoto wako na kujitia pa nafasi yake anapozungumuzia habari yoyote, hataogopa kukuelezea mambo yaliyo katika moyo wake na atafurahia kufuata mashauri yako.

USIWE “MWEPESI WA KUSEMA”

12. Wazazi wanaweza namna gani kuzuia mazungumuzo kati yao na watoto wao?

12 Wazazi wanaweza tena kuzuia mazungumuzo kati yao na watoto wao ikiwa wanaitikia kwa njia isiyofaa kuhusu mambo ambayo watoto wanawaambia. Bila shaka, wazazi Wakristo wanataka kuwalinda watoto wao. Hizi “siku za mwisho” zinajaa hatari nyingi za kiroho na hatari zingine. (2 Tim. 3:1-5) Hata hivyo, watoto wanaweza kufikiri kwamba wazazi wao wanawanyima uhuru.

13. Sababu gani wazazi hawapaswe kutoa maoni yao haraka​-haraka?

13 Ni jambo la hekima wazazi wasitoe maoni yao haraka​-haraka. Kwa kweli, si rahisi kubaki mutulivu wakati mutoto wako anakuelezea jambo fulani lenye kusumbua akili. Lakini ni vizuri kusikiliza kwa uangalifu mbele ya kusema jambo lolote. Mufalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Yeyote anapojibu jambo kabla ya kulisikia, huo ni upumbavu na aibu kwake.” (Met. 18:13) Ikiwa unabaki mutulivu, utasikia mambo mengi na mutoto wako ataendelea kuongea. Unapaswa kuelewa mambo vizuri mbele ya kutoa mashauri. Labda utaelewa kwamba “mazungumuzo ya ovyoovyo” ya mutoto wako yanatokana na maumivu aliyo nayo moyoni. (Ayu. 6:1-3) Ikiwa unamupenda mutoto wako, unapaswa kumusikiliza ili uelewe namna mambo yalivyo na unapaswa kutumia ulimi wako ili kumuponya.

14. Sababu gani watoto hawapaswe kuwa wepesi wa kusema?

14 Watoto, hamupaswe kuwa ‘wepesi wa kusema,’ hamupaswe kupinga mara moja mambo ambayo wazazi wenu wanasema, kwa sababu Mungu amewapa daraka la kuwalea. (Met. 22:6) Labda wamekwisha kujionea mambo yanayofanana na yale munayojionea leo. Zaidi ya hayo, wanasikitikia makosa waliyofanya walipokuwa vijana na wanatamani sana kuwasaidia musifanye kama wao. Kwa hiyo, muwaone wazazi wenu kuwa marafiki, wala si maadui, muwaone kuwa washauri, wala si wapinzani. (Soma Methali 1:5.) ‘Muheshimu baba yako na mama yako,’ na uonyeshe kama unawapenda kama vile wao wanavyokupenda. Ikiwa unafanya hivyo, itakuwa rahisi kwao ‘kukulea katika nizamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.’​—Efe. 6:2, 4.

USIWE ‘MWEPESI WA GAZABU’

15. Ni nini itatusaidia tuvumilie na kubaki watulivu wakati watu tunaopenda wanatukosea?

15 Kila mara tunashindwa kuvumilia watu tunaowapenda. Mutume Paulo aliwaandikia ‘watakatifu na ndugu waaminifu walio Kolosai’ hivi: ‘Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu nanyi musiwakasirikie kwa uchungu. Enyi akina baba, musiwe mukiwakasirisha watoto wenu, ili wasivunjike moyo.’ (Kol. 1:1, 2; 3:19, 21) Mutume Paulo aliwashauri Waefeso hivi: ‘Uchungu wote wenye uovu na hasira na gazabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu.’ (Efe. 4:31) Kuonyesha ustahimilivu, upole, na kujizuia​—ambazo ni sifa za tunda la roho ya Mungu​—kutatusaidia tubaki watulivu tunapochokozwa.​—Gal. 5:22, 23.

16. Namna gani Yesu alirekebisha maoni ya wanafunzi wake, na sababu gani jambo hilo lilikuwa lenye kutia moyo sana?

16 Fikiria mufano wa Yesu. Wazia namna alivyofazaika sana alipokula chakula cha mwisho cha mangaribi pamoja na mitume wake. Yesu alijua kwamba kisha saa chache angekufa kifo chenye maumivu mengi. Kutakaswa kwa jina la Baba yake na wokovu wa wanadamu wote vilitegemea uaminifu ambao angeonyesha. Pia, wakati huo huo, ‘kulitokea bishano kali kati yao [mitume] juu ya ni nani kati yao aliyeonekana kuwa mukubwa zaidi ya wote.’ Yesu hakuwafokea ao kuwakasirikia. Lakini, alifikiri nao kwa utulivu. Yesu aliwakumbusha kama walikuwa wamebaki washikamanifu kwake wakati wa majaribu. Na kwamba ijapokuwa Shetani alikuwa akitafuta kuwapepeta kama ngano, alikuwa hakika kwamba watabaki waaminifu. Alifanya hata agano pamoja nao.​—Lu. 22:24-32.

Je, unawasikiliza watoto wako kwa uangalifu?

17. Vijana, ni nini itawasaidia mubaki watulivu?

17 Vijana pia wanapaswa kubaki watulivu. Zaidi sana wanapokuwa na miaka kati ya 13 na 19, wanaweza kufikiri kwamba wazazi wao wanawatolea mashauri kwa sababu hawawaaminie. Hata ikiwa wakati fulani inaweza kuonekana hivyo, mujue kama wazazi wenu wanawatolea mashauri kwa sababu wanawapenda. Mukiwasikiliza kwa utulivu na kuwaunga mukono, watawaheshimu na watawaona kama watu wenye kutumainiwa. Kutenda hivyo kunaweza kuwafanya wakutolee uhuru zaidi katika mambo mengine. Ni jambo la hekima kujizuia. Mezali moja inasema: ‘Mutu mujinga anaachilia roho yake yote, lakini mwenye hekima anaituliza mupaka mwisho.’​—Met. 29:11.

18. Namna gani upendo unafanya mazungumuzo yawe mazuri katika familia?

18 Kwa hiyo, vijana na wazazi, musivunjike moyo ikiwa mazungumuzo yenu si mazuri kama vile munavyotazamia. Muendelee kufanya mazungumuzo yenu yawe mazuri na muendelee kutembea katika kweli. (3 Yoh. 4) Katika ulimwengu mupya, mambo yanayozuia mazungumuzo mazuri hayatakuwa tena, hakutakuwa kutoelewana. Lakini, leo, sisi wote tunasema mambo tunayosikitikia baadaye. Kwa hiyo, usisite kuomba musamaha. Na ikiwa unaombwa musamaha, uwe tayari kusamehe. Acheni ‘tuunganishwe pamoja kwa upendo.’ (Kol. 2:2) Upendo una nguvu. ‘Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fazili. Hauchokozeki. Hauweki hesabu ya ubaya. Huhimili mambo yote, huamini mambo yote, hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote.’ (1 Kor. 13:4-7) Tuendelee kukomalisha upendo, hilo litafanya namna yetu ya kuzungumuza iwe nzuri, na familia yetu itakuwa na furaha na itamutukuza Yehova.

^ Majina yamebadilishwa.