Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Linda Urithi Wako kwa Kufanya Maamuzi ya Hekima

Linda Urithi Wako kwa Kufanya Maamuzi ya Hekima

“Chukieni maovu, shikamaneni na mema.”—ROM. 12:9.

1, 2. (a) Uliamua jinsi gani kumtumikia Mungu? (b) Ni maswali gani tunayoweza kuuliza kuhusu urithi wetu wa kiroho?

MAMILIONI wamefanya uamuzi wa hekima wa kumtumikia Yehova Mungu na kufuata kwa ukaribu hatua za Yesu Kristo. (Mt. 16:24; 1 Pet. 2:21) Tunauchukua kwa uzito wakfu wetu kwa Mungu. Uamuzi wetu haukutegemea ujuzi wa kijuujuu tu wa maandiko machache, bali ulitegemea funzo lenye kina la Neno la Mungu. Kupitia funzo hilo, tulijifunza mambo mengi yenye kujenga imani kuhusu urithi ambao Yehova amewaahidi wale ‘wanaopata ujuzi juu yake na juu ya yule aliyemtuma, Yesu Kristo.’—Yoh. 17:3; Rom. 12:2.

2 Ili kudumisha msimamo wetu tukiwa Wakristo, ni lazima tufanye maamuzi yanayompendeza Baba yetu wa mbinguni. Hivyo, makala hii itajibu maswali haya muhimu: Urithi wetu ni nini? Tunapaswa kuuonaje? Tunawezaje kuhakikisha kwamba tunapata urithi wetu? Ni nini kitakachotusaidia kufanya maamuzi ya hekima?

URITHI WETU NI NINI?

3. Ni urithi gani unaowangojea (a) watiwa-mafuta na (b) “kondoo wengine”?

3 Idadi ndogo ya Wakristo wanatarajia kupata “urithi usioharibika na usiotiwa unajisi na usiofifia,” yaani, pendeleo lenye thamani sana la kutawala pamoja na Kristo mbinguni. (1 Pet. 1:3, 4) Ili kupata urithi huo, ni lazima kila mmoja wao ‘azaliwe tena.’ (Yoh. 3:1-3) Ni urithi gani watakaopata mamilioni ya “kondoo wengine” wa Yesu, wanaoshirikiana na wafuasi wake watiwa-mafuta katika kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu? (Yoh. 10:16) Kondoo wengine watapokea urithi ambao Adamu na Hawa waliotenda dhambi  hawakupata kamwe, yaani, uzima wa milele katika dunia paradiso ambayo haitakuwa tena na kuteseka, kifo, au maombolezo. (Ufu. 21:1-4) Ndiyo sababu Yesu alimwahidi hivi mtenda-maovu aliyekufa pamoja naye: “Kwa kweli mimi nakuambia leo, Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.”—Luka 23:43.

4. Tunafurahia baraka gani sasa?

4 Hata sasa, tunafurahia mambo fulani ya urithi wetu. Kwa sababu tunadhihirisha imani katika “fidia ambayo Kristo Yesu alilipa,” tuna amani ya akili na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. (Rom. 3:23-25) Tuna uelewaji ulio wazi wa ahadi zenye thamani zilizo katika Neno la Mungu. Isitoshe, tunapata shangwe nyingi sana kwa sababu ya kuwa sehemu ya undugu wa ulimwenguni pote wenye upendo. Na ni pendeleo kubwa kama nini kuwa Shahidi wa Yehova! Ndiyo sababu tunathamini sana urithi wetu!

5. Shetani amejaribu kuwafanya nini watu wa Mungu, na ni nini kitakachotusaidia kubaki imara dhidi ya hila zake?

5 Hata hivyo, ili tushikilie kabisa urithi wetu mzuri ajabu, ni lazima tuwe macho kutambua mbinu za Shetani. Nyakati zote Shetani hujaribu kuwashawishi watu wa Mungu wafanye maamuzi yanayoweza kuwafanya wapoteze urithi wao. (Hes. 25:1-3, 9) Akijua kwamba mwisho wake unakaribia, Shetani amezidisha jitihada zake za kutupotosha. (Soma Ufunuo 12:12, 17.) Ili tuendelee “kusimama imara na kupinga hila za Ibilisi,” ni lazima tuendelee kuthamini sana urithi wetu. (Efe. 6:11) Kuhusiana na jambo hilo, kielelezo cha kuonya cha Esau, mwana wa mzee wa ukoo, Isaka, kinatufundisha mambo tunayopaswa kuchukua kwa uzito.

USIWE KAMA ESAU

6, 7. Esau alikuwa nani, naye angepata urithi gani?

6 Miaka 4,000 hivi iliyopita, Isaka na Rebeka, walipata watoto wawili, Esau na ndugu yake pacha, Yakobo. Mapacha hao walipozidi kukua, walikuwa na nyutu tofauti na walipenda mambo tofauti. “Esau akawa mwanamume anayejua jinsi ya kuwinda, mwanamume wa mbugani,” naye “Yakobo akawa mwanamume asiye na lawama, akikaa katika mahema.” (Mwa. 25:27) Mtafsiri wa Biblia, Robert Alter, anasema kwamba neno la Kiebrania linalotafsiriwa “asiye na lawama,” “linaonyesha utimilifu au hata kutokuwa na hatia.”

7 Esau na Yakobo walipokuwa na umri wa miaka 15, Abrahamu, babu yao alikufa, lakini Yehova hakusahau ahadi aliyompa Abrahamu. Baadaye, Yehova alirudia ahadi hiyo alipozungumza na Isaka, akisema kwamba mataifa yote ya dunia yangejibariki kupitia uzao wa Abrahamu. (Soma Mwanzo 26:3-5.) Ahadi hiyo ilifunua kwamba Masihi, yaani, ‘mzao’ mwaminifu anayetajwa katika Mwanzo 3:15, angetokea kupitia uzao wa Abrahamu. Akiwa mwana wa kwanza wa Isaka, Esau alikuwa na haki ya kisheria ya kutimiza ahadi hiyo. Esau angepata urithi mzuri ajabu kama nini! Je, aliuthamini urithi huo?

Usihatarishe urithi wako wa kiroho

8, 9. (a) Esau aliamua kufanya nini na urithi wake? (b) Miaka mingi baadaye, Esau aligundua nini kuhusu uamuzi wake, naye akatendaje?

8 Siku moja Esau alipotoka mbugani, alimkuta Yakobo ‘akitokosa mchuzi.’ Esau akasema hivi: “Haraka, tafadhali, nipe nimeze chekundu—chekundu hicho, kwa maana nimechoka!” Yakobo akamjibu hivi: “Niuzie, kwanza kabisa, haki yako ya mzaliwa wa kwanza!” Esau alichagua nini? Kwa kushangaza, alisema: “Haki ya kuzaliwa ina faida gani kwangu?” Naam, Esau alichagua bakuli la mchuzi badala ya haki yake ya kuzaliwa! Ili kufanya badilishano hilo la haki ya kuzaliwa liwe halali, Yakobo alisisitiza hivi: “Niapie kwanza  kabisa!” Bila kusita, Esau akampa haki yake ya kuzaliwa. Baada ya kufanya hivyo, “Yakobo akampa Esau mkate na mchuzi wa dengu, naye akala na kunywa. Kisha akaondoka akaenda zake. Kwa hiyo Esau aliidharau haki ya kuzaliwa.”—Mwa. 25:29-34.

9 Miaka mingi baadaye, Isaka alipojua kwamba anakaribia kufa, Rebeka alifanya mipango ili kuhakikisha kwamba Yakobo anapokea haki ya kuzaliwa iliyopotezwa na Esau. Naye Esau alipogundua kwa kuchelewa kuhusu uamuzi wake wa kipumbavu, alimsihi Isaka hivi: “Nibariki mimi, hata mimi pia, baba yangu! . . . Je, hukuniachia baraka yoyote?” Isaka aliposema kwamba hawezi kumnyang’anya Yakobo baraka aliyompa, “Esau akapaaza sauti yake na kuanza kulia machozi.”—Mwa. 27:30-38.

10. Yehova aliwaonaje Esau na Yakobo, na kwa nini?

10 Maandiko yanaonyesha nini waziwazi kuhusu mtazamo wa Esau? Alionyesha kwamba jambo muhimu zaidi kwake lilikuwa kutosheleza tamaa za kimwili kuliko kupata baraka za wakati ujao ambazo zingetokana na urithi wake. Esau hakuthamini haki yake ya kuzaliwa na hivyo akaonyesha wazi kwamba hakumpenda Mungu kikweli. Zaidi ya hayo, Esau hakujali jinsi ambavyo uamuzi wake ungewaathiri wazao wake. Tofauti na Esau, Yakobo alithamini sana urithi wake. Kwa mfano, Yakobo alifuata maagizo ya wazazi wake alipochagua mke. (Mwa. 27:46–28:3) Kwa sababu Yakobo alifanya uamuzi huo uliomlazimu kuwa na subira na kujidhabihu, alikuja kuwa babu ya Masihi. Mungu aliwaonaje Esau na Yakobo? Kupitia nabii Malaki, Yehova alisema hivi: “Nilimpenda Yakobo, naye Esau nikamchukia.”—Mal. 1:2, 3.

11. (a) Kwa nini mfano wa Esau unatuhusu sisi Wakristo? (b) Kwa nini Paulo alitaja uasherati alipozungumzia kile alichofanya Esau?

11 Je, yale ambayo Biblia inasema kumhusu Esau yanawahusu Wakristo leo? Bila shaka. Mtume Paulo aliwaonya waamini wenzake kuwa waangalifu ili kwamba “kusiwe na mwasherati wala yeyote asiyethamini mambo matakatifu, kama Esau, ambaye alitoa haki zake za kuwa mzaliwa wa kwanza kwa kubadilishana na mlo mmoja.” (Ebr. 12:16) Onyo hilo bado linawahusu Wakristo. Ni lazima tudumishe uthamini wetu wa mambo matakatifu ili tusishindwe na tamaa za mwili na hivyo kupoteza urithi wetu wa kiroho. Hata hivyo, kwa nini Paulo alitaja uasherati alipozungumzia kile alichofanya Esau? Ni kwa sababu inaelekea sana kwamba mtu mwenye mtazamo wa kimwili kama wa Esau ataachilia mbali mambo matakatifu ili kufurahia matendo haramu, kama vile uasherati.

 TAYARISHA MOYO WAKO SASA

12. (a) Shetani anatushawishi kwa njia gani? (b) Toa mifano ya Kimaandiko inayoweza kutusaidia tunapohitaji kufanya maamuzi mazito.

12 Tukiwa watumishi wa Yehova, bila shaka hatutafuti kimakusudi hali zenye kushawishi zinazoweza kutuongoza kwenye mwenendo mpotovu kingono. Badala yake, tunasali ili Yehova Mungu atusaidie tusishindwe tunaposhawishiwa na mtu fulani kutomtii Yeye. (Mt. 6:13) Hata hivyo, Shetani hujaribu daima kudhoofisha hali yetu ya kiroho tunapojitahidi kudumisha utimilifu wetu katika ulimwengu huu uliopotoka. (Efe. 6:12) Akiwa mungu wa mfumo huu mwovu wa mambo, Ibilisi anajua jinsi ya kutumia vibaya tamaa za mwili wetu usio mkamilifu kwa kujaribu kutunasa kwa vishawishi vinavyowapata wanadamu wasio wakamilifu. (1 Kor. 10:8, 13) Kwa mfano, wazia ukiwa katika hali inayokupa fursa ya kutosheleza tamaa fulani kwa njia iliyopotoka. Utafanya uamuzi gani? Je, utakuwa kama Esau na kusema hivi: ‘Haraka! Nipe!’ Au utapinga kishawishi na kukimbia kama alivyofanya Yosefu, mwana wa Yakobo, aliyeshawishiwa na mke wa Potifa?—Soma Mwanzo 39:10-12.

13. (a) Wengi wametendaje leo kama Yosefu, lakini wengine wametendaje kama Esau? (b) Mifano ya wale waliotenda kama Esau inatukumbusha uhitaji gani wa lazima?

13 Wengi wa ndugu na dada zetu walijikuta katika hali zilizowalazimisha kuamua kutenda kama Esau au kama Yosefu. Wengi wametenda kwa hekima na hivyo kuufurahisha moyo wa Yehova. (Met. 27:11) Hata hivyo, baadhi ya waamini wenzetu waliposhawishiwa, walichagua kutenda kama Esau na hivyo kuhatarisha urithi wao wa kiroho. Kwa kweli, watu wengi huchukuliwa hatua za kihukumu na kutengwa na ushirika kila mwaka kwa sababu ya maadili mapotovu ya kingono. Kwa hiyo, ni jambo muhimu kama nini kwetu kuutayarisha moyo wetu sasa kabla ya kujikuta katika hali zitakazojaribu utimilifu wetu! (Zab. 78:8) Tunaweza kuchukua hatua mbili hivi zitakazotulinda kama ukuta dhidi ya kishawishi na kutusaidia kufanya maamuzi ya hekima baadaye.

TAFAKARI NA UJIIMARISHE

Tunaimarisha ulinzi wetu wa kiroho kwa kutafuta hekima ya Yehova

14. Ni maswali gani ya kutafakari yatakayotusaidia ‘kuchukia maovu’ na ‘kushikamana na mema’?

14 Hatua ya kwanza inahusisha kutafakari matokeo ya matendo yetu. Kina cha uthamini wa urithi wetu wa kiroho kinategemea sana kina cha upendo wetu kwa Yehova, Mpaji wa urithi huo. Tukimpenda mtu, hatutaki kuumiza hisia zake. Badala yake, tunajitahidi sana kukubaliwa naye. Hivyo, kabla ya kujitumbukiza katika tamaa chafu za kimwili, ni vizuri kutafakari jinsi matendo hayo yatakavyotuathiri na kuwaathiri wengine. Tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Matendo yangu ya kichoyo yataathirije uhusiano wangu na Yehova? Matendo yangu yasiyofaa yataiathirije familia yangu? Jambo hilo litawaathirije ndugu na dada zangu kutanikoni? Je, nitawakwaza wengine?’ (Flp. 1:10) Tunaweza pia kujiuliza hivi: ‘Je, ni jambo la busara kupata maumivu ya moyo kwa sababu tu ya uamuzi usiofaa wa kufurahia dhambi kwa muda? Je, kweli ninataka kulia kwa uchungu kama Esau ninapotambua kile nilichotenda?’ (Ebr. 12:17) Kutafakari maswali kama hayo kutatusaidia ‘kuchukia maovu’ na ‘kushikamana na mema.’ (Rom. 12:9) Upendo wetu kwa Yehova utatusaidia hasa kushikamana na urithi wetu.—Zab. 73:28.

15. Ni nini kitakachoimarisha ulinzi wetu wa kiroho ili tupambane na hali zinazohatarisha hali yetu ya kiroho?

15 Hatua ya pili inatia ndani kuimarisha ulinzi wetu wa kiroho. Yehova ametupa maandalizi mengi ya kuimarisha ulinzi wetu wa  kiroho ili tupambane na hali za ulimwengu huu zinazohatarisha hali yetu ya kiroho. Maandalizi yake yanatia ndani kujifunza Biblia, mikutano ya Kikristo, huduma ya shambani, na sala. (1 Kor. 15:58) Kila mara tunapomwambia Yehova yaliyo moyoni mwetu kupitia sala na kila mara tunaposhiriki kikamili katika huduma ya Kikristo, ni kana kwamba tunaimarisha ukuta wetu wa kuzuia vishawishi. (Soma 1 Timotheo 6:12, 19.) Kwa kadiri fulani, ukuta wetu wa kiroho unategemea jitihada zetu wenyewe. (Gal. 6:7) Jambo hilo limekaziwa katika sura ya pili ya kitabu cha Methali.

“ENDELEA KUUTAFUTA”

16, 17. Tunawezaje kufanikiwa kupata uwezo wa kufanya maamuzi ya hekima?

16 Methali sura ya 2 inatutia moyo tujipatie hekima na uwezo wa kufikiri. Zawadi hizo zinatuwezesha kuchagua kati ya jema na baya, kati ya kujitia nidhamu na kutosheleza tamaa za mwili. Hata hivyo, tutafanikiwa ikiwa tuko tayari kujitahidi. Biblia inakazia kweli hiyo ya msingi kwa kusema hivi: “Mwanangu, ikiwa utapokea maneno yangu na kujiwekea amri zangu kama hazina, ili kwa sikio lako usikilize hekima kwa makini, ili uelekeze moyo wako kwenye utambuzi, ikiwa utaita uelewaji na kupaaza sauti yako uite utambuzi, ikiwa utaendelea kuutafuta kama fedha, na kuendelea kuutafuta kama hazina zilizofichika, ndipo utakapoelewa kumwogopa Yehova, nawe utapata kumjua Mungu. Kwa maana Yehova mwenyewe anatoa hekima; kinywani mwake hutoka ujuzi na utambuzi.”—Met. 2:1-6.

17 Ni wazi kwamba ili tufanikiwe kupata uwezo unaohitajiwa wa kufanya maamuzi ya hekima, ni lazima tutimize masharti yaliyotajwa katika kitabu cha Methali. Tunaweza kufanikiwa kubaki imara dhidi ya vishawishi ikiwa tutaruhusu maneno ya Yehova yafinyange utu wetu wa ndani, ikiwa tutaendelea kusali ili tupate mwongozo wa Mungu, na ikiwa tutaendelea kutafuta ujuzi kumhusu Mungu kama hazina zilizofichika.

18. Umeazimia kuendelea kufanya nini, na kwa nini?

18 Yehova huwapa ujuzi, uelewaji, utambuzi, na hekima wale wanaojitahidi kutafuta zawadi hizo. Kadiri tunavyozitafuta na kuzitumia, ndivyo tutakavyomkaribia zaidi Yehova, Mpaji wa zawadi hizo. Hivyo, uhusiano wetu wa karibu sana pamoja na Yehova Mungu utatulinda tunaposhawishiwa. Kumkaribia Yehova na kuwa na hofu inayofaa kumwelekea kutatulinda ili tusitende dhambi. (Zab. 25:14; Yak. 4:8) Acheni shangwe ya kuwa rafiki za Yehova na kutumia hekima yake ituchochee sote kuendelea kufanya maamuzi yatakayoufurahisha moyo wa Yehova na kuulinda urithi wetu.