Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 WAFUNDISHE WATOTO WAKO

Tunajifunza Nini Kutoka kwa Mhalifu?

Tunajifunza Nini Kutoka kwa Mhalifu?

Mhalifu tutakayejifunza kumhusu ni yule anayezungumza na Yesu kwenye picha. Mhalifu huyo anajuta kwa sababu ya uhalifu wake. Anamwomba Yesu: “Unikumbuke utakapoingia katika ufalme wako.” Kama unavyoona kwenye picha, sasa Yesu anazungumza na mhalifu huyo. Unajua Yesu anamwambia nini? * Yesu anamwahidi: “Kwa kweli mimi nakuambia leo, utakuwa pamoja nami katika Paradiso.”

Unafikiri Paradiso hiyo itakuwaje?— Ili tuelewe vizuri, acheni tuzungumzie Paradiso ambayo Mungu aliumba kwa ajili ya mwanamume na mwanamke wa kwanza, Adamu na Hawa. Paradiso hiyo ilikuwa wapi? Je, ilikuwa mbinguni, au duniani?

Ni kweli kwamba ilikuwa duniani. Basi, tunapomfikiria yule mhalifu akiwa “katika Paradiso,” ni wakati dunia hii itageuzwa na kuwa paradiso. Paradiso hiyo itakuwaje?— Acheni tuone.

Baada ya Yehova Mungu kuwaumba Adamu na Hawa, Biblia inasema kwamba aliwaweka katika paradiso iliyokuwa hapa duniani. Iliitwa “bustani katika Edeni.” Unaweza kuwazia jinsi “bustani katika Edeni” ilivyokuwa maridadi?— Bila shaka, ilikuwa maridadi na bora kuliko bustani tunazoona leo!

Una maoni gani? Je, Yesu atakuwa hapa duniani pamoja na yule mhalifu aliyejutia dhambi zake?— Hapana, Yesu atakuwa mbinguni akitawala akiwa Mfalme juu ya dunia Paradiso. Basi, Yesu atakuwa na mhalifu huyo kwa maana ya kwamba atamfufua kutoka kwa wafu na kuhakikisha ametunzwa akiwa katika Paradiso duniani. Lakini kwa nini Yesu atamruhusu mwanamume aliyekuwa mhalifu aishi katika Paradiso?— Acheni tuzungumzie jambo hilo.

 Ni kweli kwamba mhalifu huyo alifanya mambo mabaya sana. Lakini pia mabilioni ya watu wengine walioishi duniani walifanya mabaya. Hata hivyo, wengi walifanya mambo mabaya kwa sababu hawakufundishwa kamwe kumhusu Yehova na mambo aliyotaka wafanye.

Basi, watu kama hao, kutia ndani mhalifu ambaye Yesu alizungumza naye akiwa mtini, watafufuliwa ili waishi katika Paradiso itakayokuwa hapa duniani. Watafundishwa mapenzi ya Mungu. Kisha watathibitisha kama wanampenda Yehova.

Je, unajua jinsi wanavyoweza kuthibitisha hilo?— Ni kwa kufanya yale ambayo Mungu anataka wafanye. Itafurahisha kama nini kuishi katika Paradiso hiyo na sikuzote kuwa pamoja na watu wanaompenda Yehova na wanaopendana pia!

Soma Katika Biblia Yako

^ fu. 3 Kama unasoma sehemu hii pamoja na mtoto, unapoona kistari kama hiki (—), tua na umtie moyo mtoto atoe maoni yake.