Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MASIMULIZI KUHUSU MAISHA YA WATU

Kumutii Yehova Kumetuletea Baraka Nyingi

Kumutii Yehova Kumetuletea Baraka Nyingi

Baba alisema hivi: “Tumejifunza somo nzuri kabisa kuhusu Noa. Noa alimutii Yehova na aliipenda familia yake, na wote waliokoka Garika kwa sababu familia yote iliingia katika safina.”

HAYO ni kati ya mambo ya kwanza kwanza ninayokumbuka kumuhusu baba yangu, mwanaume wa kawaida, mufanyakazi mwenye bidii. Alipenda sana haki, kwa hiyo ujumbe wa Biblia ulimuvutia mara moja alipousikia katika mwaka wa 1953. Kuanzia wakati huo na kuendelea, alifanya yote anayoweza ili kutufundisha mambo aliyokuwa akijifunza. Mwanzoni, mama hakutaka kuachana na desturi za dini yake ya Kikatoliki. Lakini baadaye, yeye pia alianza kuishi kulingana na mafundisho ya Biblia.

Haikuwa rahisi kwa wazazi wetu kutufundisha. Mama hakujua kusoma, na Baba alifanya kazi sana na kwa saa nyingi katika mashamba. Wakati fulani baba alikuwa amechoka sana na hakuweza kubaki macho wakati wa funzo. Hata hivyo, jitihada zake zilizaa matunda mazuri. Kwa kuwa nilikuwa mutoto wa kwanza, nilisaidia kufundisha dada yangu na ndugu zangu wawili. Mambo niliyowafundisha yalitia ndani jambo ambalo baba alizungumuzia mara nyingi, ni kusema, upendo wa Noa kwa familia yake ambao alionyesha kwa kumutii Mungu. Nilipenda sana masimulizi hayo ya Biblia! Kwa muda murefu nilikuwa nikihuzuria mikutano katika Jumba la Ufalme la Roseto degli Abruzzi, muji unaopatikana pembeni ya Bahari ya Adriatiki ya Italie.

Nilikuwa tu na miaka 11 katika mwaka wa 1955 wakati ambapo mama na mimi tulitembea juu ya milima kuelekea sehemu ya mangaribi ili kuhuzuria mukusanyiko wetu wa kwanza wa wilaya, katika Roma. Kuanzia wakati huo, nimeona mikusanyiko hiyo mikubwa kuwa sehemu nzuri sana ya maisha ya Kikristo.

Mwaka uliofuata, nilibatizwa na muda muchache baadaye nilianza utumishi wa wakati wote. Nilipokuwa na miaka 17, nilikuwa painia wa pekee katika muji wa Latina ulio kusini mwa Roma na unaopatikana umbali wa kilomita 300 na nyumbani. Kwa kuwa huo ulikuwa muji mupya kabisa, watu hawakujiuliza ikiwa wengine wangefikiri namna gani kama wanakubali ujumbe wa Biblia. Mimi na painia mwenzangu tulifurahia sana kugawanyia watu vichapo vinavyotegemea Biblia, lakini kwa kuwa nilikuwa ningali kijana, nilitamani sana kurudi nyumbani! Hata hivyo, nilitaka kufuata muongozo niliokuwa nimetolewa.

Siku ya arusi yetu

Baadaye nilitumwa katika muji wa Milan ili nisaidie kutayarisha Mukusanyiko wa Kimataifa wa mwaka wa 1963 uliokuwa na kichwa “Habari Njema za Milele.” Wakati wa mukusanyiko huo, nilifanya kazi ya kujitolea pamoja na wengine, kutia ndani Paolo Piccioli, ndugu kijana kutoka muji wa Florence. Siku ya pili ya mukusanyiko, alitoa hotuba yenye kutia moyo juu ya useja. Nakumbuka kwamba nilifikiri hivi: ‘Inaonekana wazi kwamba ndugu huyu hatafunga ndoa hata kidogo.’ Hata hivyo, tulianza kuandikiana, na ilionekana wazi tulikuwa na mambo mengi yenye kupatana​—miradi yetu, upendo wetu kwa Yehova, na tamaa yetu yenye nguvu ya kumutii Yehova. Mimi na Paolo tulifunga ndoa katika mwaka wa 1965.

MAZUNGUMUZO NA VIONGOZI WA KIDINI

Nilifanya upainia wa kawaida katika muji wa Florence kwa miaka kumi. Ilifurahisha sana kuona ongezeko katika makutaniko, zaidi sana kuona namna vijana walivyofanya maendeleo ya kiroho. Mimi na Paolo tulifurahia kupitisha wakati pamoja nao tukizungumuzia mambo ya kiroho na kujifurahisha, Paolo alifurahia kucheza mupira. Bila shaka, nilipenda kupitisha wakati pamoja na bwana yangu, lakini nilitambua kwamba vijana na familia katika kutaniko walifaidika sana na namna alivyowahangaikia, na walipenda kupitisha wakati mwingi pamoja naye.

Kukumbuka mafunzo mengi ya Biblia tuliyoongoza kungali kunaniletea furaha nyingi. Tulijifunza na Adriana, aliyeelezea familia mbili mambo aliyokuwa anajifunza. Familia hizo zilifanya mupango ili kuzungumuza pamoja na padri mumoja juu ya mafundisho kama vile Utatu na kutokufa kwa nafsi. Mapadri watatu walikuja kushiriki mazungumuzo hayo. Mafasirio yao yalipingana, wanafunzi wetu wa Biblia walitambua waziwazi hivyo walipoyalinganisha na mafundisho yaliyo wazi ya Biblia. Bila shaka, mazungumuzo hayo yalibadili sana maoni yao. Baadaye, watu 15 wa familia hizo walikubali kweli na kuwa Mashahidi.

Bila shaka, leo njia za kuhubiri zimebadilika. Wakati huo, Paolo alikuwa “fundi mukubwa” katika kuzungumuza na mapadri—na alifanya mazungumuzo mengi pamoja nao. Ninakumbuka siku moja alipozungumuza nao mbele ya watu ambao hawakuwa Mashahidi. Ilionekana wazi kwamba wapinzani walikuwa wamefanya mupango mbele ya wakati ili watu fulani kati ya wasikilizaji waulize maulizo waliyofikiri kuwa magumu. Hata hivyo, mambo yalibadilika. Mutu mumoja aliuliza ikiwa dini inapaswa kujiingiza katika siasa, kama ilivyokuwa imefanya kwa miaka mingi. Kuhusu jambo hilo, ilikuwa wazi kwamba mapadri walikuwa na shida. Kwa gafula, taa zilizimika, na mazungumuzo yakakatizwa. Miaka fulani baadaye tulitambua kwamba mipango ilikuwa imefanywa ili taa zizimwe ikiwa mazungumuzo hayataendeshwa kabisa namna mapadri walivyotaka.

MAPENDELEO MAPYA YA UTUMISHI

Kisha miaka kumi ya ndoa yetu, mimi na Paolo tulialikwa kufanya kazi ya muzunguko. Paolo alikuwa na kazi nzuri, na haikuwa rahisi kuamua. Lakini kisha kusali na kufikiria jambo hilo kwa uzito, tulikubali pendeleo hilo jipya la utumishi. Tulifurahi kupitisha wakati pamoja na familia zilizotukaribisha. Mangaribi, tulijifunza pamoja, na baadaye Paolo aliwasaidia watoto wa familia zilizotukaribisha kufanya kazi za masomo, zaidi sana ikiwa zilihusu hesabu. Zaidi ya hayo, Paolo alipenda sana kusoma vitabu na alifurahia kuelezea wengine mambo mazuri na yenye kujenga aliyosoma. Siku ya Kwanza, tulienda mara nyingi kuhubiri katika miji ambako hakuwa Mashahidi, tukiwaalika watu waje kusikia hotuba ambayo ingetolewa mangaribi.

Tulifurahia kupitisha wakati pamoja na vijana, Paolo alifurahia kucheza mupira

Kisha tu miaka miwili katika kazi ya muzunguko, tulialikwa kutumika kwenye Beteli ya Roma. Paolo alishugulikia mambo ya kisheria, na mimi nilipewa mugawo katika Idara ya Magazeti. Haikuwa rahisi kuzoea migawo yetu mipya, lakini tuliazimia kuwa watiifu. Ilifurahisha sana kuona namna Beteli ilivyopanuliwa na ongezeko kubwa katika Italie. Wakati huo, Mashahidi wa Yehova walitambuliwa kisheria katika Italie. Tulikuwa wenye furaha kabisa katika aina hiyo ya utumishi.

Paolo alipenda utumishi wake kwenye Beteli

Tulipokuwa tukitumika kwenye Beteli, watu wengi katika Italie walianza kujiuliza maulizo mengi kuhusu uamuzi wetu unaotegemea Biblia juu ya damu. Mwanzoni mwa miaka ya 1980, kulikuwa kesi moja kuhusu damu iliyowashangaza wengi. Bibi na bwana waliokuwa Mashahidi walishitakiwa kwa uongo kwamba wao ndio waliomuuisha binti yao, ijapokuwa kwa kweli alikufa kutokana na magonjwa makali ya damu ambayo watu wengi wanaoishi katika eneo la Mediterania wanariti. Ndugu na dada wa familia ya Beteli walisaidia wanasheria waliotetea wazazi hao. Kikaratasi kimoja na gazeti la pekee la Amkeni! viliwatolea watu maelezo ya kweli na kuwasaidia kuelewa vizuri yale ambayo Neno la Mungu linasema kuhusu damu. Muda wa miezi hiyo, Paolo alifanya kila mara kazi kwa saa 16 kwa siku bila kupumuzika. Nilifanya yote ninayoweza ili kumutegemeza katika kazi hiyo ya maana.

BADILIKO LINGINE KATIKA MAISHA YETU

Kisha kupitisha miaka 20 katika maisha ya ndoa, tulipatwa na jambo fulani ambalo hatukutazamia. Nilikuwa na miaka 41 na Paolo alikuwa na miaka 49 nilipomujulisha kwamba nilifikiri nilikuwa na mimba. Katika kitabu chake cha kumbukumbu, niliona maneno haya kwenye ukurasa wa siku hiyo: “Sala: Ikiwa ni kweli, utusaidie kubaki katika utumishi wa wakati wote, tusiregee kiroho, na utusaidie kuwa wazazi wazuri. Zaidi sana, unisaidie kutumikisha hata kiasi kidogo cha mambo yote ambayo nimesema kwenye jukwaa kwa miaka zaidi ya 30 iliyopita.” Ninapofikiria matokeo mazuri ambayo tumepata, ninaona kwamba Yehova amejibu kabisa sala yake na yangu.

Kuzaliwa kwa Ilaria kulileta mabadiliko makubwa katika maisha yetu. Kwa kweli, kulikuwa wakati ambapo tulivunjika moyo, kama vile Methali 24:10 inavyoonyesha: “Je, umejionyesha kuwa umevunjika moyo siku ya taabu? Nguvu zako zitakuwa chache.” Lakini tumetegemezana, tukikumbuka kwamba ni jambo la maana kutiana moyo.

Ilaria anasema bila kusita kwamba anafurahi kuwa mutoto wa Mashahidi wawili waliokuwa na mengi ya kufanya katika utumishi wa wakati wote. Hajajisikia hata siku moja kuwa hatumuhangaikie; alikomalia katika familia iliyo kabisa kama familia zingine. Wakati wa muchana, nilimushugulikia. Paolo aliporudi nyumbani mangaribi, alikuwa kila mara na kazi fulani ya kumalizia; lakini, alipitisha wakati pamoja naye, akicheza naye na kumusaidia kufanya kazi za masomo. Alifanya hivyo hata ikiwa hilo lilimuomba kutumika mupaka saa munane ao saa kenda ya usiku ili kumalizia kazi yake mwenyewe. Kila mara Ilaria alisema hivi: “Baba ndiye rafiki yangu muzuri zaidi.”

Kama unavyoweza kuwazia, tulipaswa kuwa na maoni yenye kupatana—na wakati fulani kuwa imara—ili kumusaidia Ilaria abaki katika kweli. Ninakumbuka wakati mumoja alijiendesha vibaya alipokuwa akicheza na rafiki yake. Tulimufasiria kupitia Biblia sababu gani hapaswe kufanya hivyo. Tulimuambia aombe rafiki yake musamaha mbele yetu.

Ilaria anasema kwamba anafurahia sana upendo ambao wazazi wake walionyesha kwa ajili ya utumishi. Kwa kuwa sasa ameolewa, anaelewa vizuri zaidi sababu gani ni jambo la maana kumutii Yehova na kufuata uongozi wake.

UTII HATA KATIKA NYAKATI ZA TAABU

Katika mwaka wa 2008, Paolo alitambua kwamba ana ugonjwa wa kansa. Mwanzoni ilionekana kwamba Paolo angepona, na alinitia moyo sana. Zaidi ya kutafuta mashauri mazuri ya kiganga, mimi na Ilaria tulitoa sala ndefu kwa Yehova, tukimuomba atusaidie kupambana na hali zinazoweza kutokea wakati ujao. Hata hivyo, nilimutazama mwanaume aliyekuwa na nguvu wakati fulani ambaye pole kwa pole alianza kuwa muzaifu. Kifo chake katika mwaka wa 2010 kilituumiza sana. Lakini, ninapofikiria mambo tuliyofanya miaka 45 tulipokuwa pamoja, hilo linanifariji sana. Tulimutolea Yehova kilicho bora zaidi. Ninajua kwamba kazi tuliyofanya itaendelea kuwa na samani. Na nina hamu ya kumuona Paolo wakati wa ufufuo, kulingana na maneno ya Yesu kwenye Yohana 5:28, 29.

“Katika moyo wangu, ningali yule binti mudogo mwenye kupenda sana hadisi ya Noa. Azimio langu halijabadilika”

Katika moyo wangu, ningali yule binti mudogo mwenye kupenda sana hadisi ya Noa. Azimio langu halijabadilika. Ninataka kumutii Yehova katika kila jambo. Niko hakika kwamba hata tupatwe na matatizo ya namna gani, hata tuishi maisha ya kujinyima ya namna gani, na kupoteza mambo fulani, yote hayo ni machache yanapolinganishwa na baraka nzuri ambazo Mungu wetu mwenye upendo anatutolea. Mimi mwenyewe nimejionea jambo hilo, na ninawahakikishia kwamba, kumutii Yehova kunaleta baraka nyingi.