Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Acha Nidhamu ya Yehova Ikufinyange

Acha Nidhamu ya Yehova Ikufinyange

“Utaniongoza kwa shauri lako, na baadaye utanipeleka kwenye utukufu.”ZAB. 73:24.

1, 2. (a) Ni muhimu tufanye nini ili tuwe na uhusiano mzuri pamoja na Yehova? (b) Tutanufaikaje tukichunguza masimulizi ya Kimaandiko yanayoonyesha jinsi watu walivyoitikia nidhamu ya Mungu?

“KUMKARIBIA Mungu ni kwema kwangu. Nimeweka kimbilio langu katika Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.” (Zab. 73:28) Katika andiko hilo, mtunga-zaburi alieleza uhakika wake katika Mungu. Ni hali gani zilizomwongoza kufikia mkataa huo muhimu? Alipoona amani ya watu waovu, mwanzoni mtunga-zaburi aliumia sana moyoni. Alilalamika hivi: “Nimeusafisha moyo wangu bure na kuiosha mikono yangu katika kutokuwa na hatia.” (Zab. 73:2, 3, 13, 21) Hata hivyo, alipoingia “patakatifu pakuu pa Mungu,” alikuwa katika mazingira yaliyomsaidia kubadili fikira zake na kuendelea kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. (Zab. 73:16-18) Jambo hilo lilimfundisha somo muhimu sana mwanamume huyo aliyemwogopa Mungu: Ili kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova, ni muhimu tuwe miongoni mwa watu wa Mungu, tukubali, na kutumia mashauri yake.Zab. 73:24.

2 Sisi pia tunatamani kuwa na uhusiano wa karibu sana pamoja na Mungu wa kweli aliye hai. Ili kutimiza lengo hilo, ni muhimu turuhusu mashauri au nidhamu yake itufinyange, ili tuwe watu wanaompendeza. Nyakati za kale, Mungu aliwapa kwa rehema watu na mataifa mbalimbali nafasi za kukubali nidhamu yake. Masimulizi yanayoonyesha jinsi walivyoitikia nidhamu yake yameandikwa katika Biblia “ili kutufundisha sisi” na “kuwa onyo kwetu sisi ambao tumefikiwa na miisho ya mifumo ya mambo.” (Rom. 15:4; 1 Kor. 10:11) Kuchunguza masimulizi hayo kwa undani kutatusaidia kuelewa zaidi utu wa Yehova na kutuonyesha jinsi tunavyoweza kunufaika tukikubali atufinyange.

 JINSI MFINYANZI ANAVYOTUMIA MAMLAKA YAKE

3. Andiko la Isaya 64:8 na Yeremia 18:1-6 yanaonyesha nini kuhusu mamlaka ya Yehova juu ya watu? (Tazama picha iliyo kwenye ukurasa wa 24.)

3 Andiko la Isaya 64:8 linasema hivi kwa njia ya mfano kuhusu mamlaka ambayo Yehova anayo juu ya mtu mmoja-mmoja na juu ya mataifa: “Ee Yehova, wewe ni Baba yetu. Sisi ni udongo, nawe ni Mfinyanzi wetu; nasi sote ni kazi ya mkono wako.” Mfinyanzi ana mamlaka kamili ya kuufinyanga udongo na kutengeneza chombo anachotaka. Udongo hauna mamlaka yoyote katika jambo hilo. Ndivyo ilivyo kati ya mwanadamu na Mungu. Mwanadamu hana haki ya kubishana na Mungu kama vile tu udongo usivyoweza kubishana na mfinyanzi anayeufinyanga kwa mikono yake.Soma Yeremia 18:1-6.

4. Je, Mungu huwafinyanga watu au mataifa kwa lazima? Eleza.

4 Yehova aliposhughulika na taifa la kale la Israeli, alionyesha uwezo wake wa kuwafinyanga kama mfinyanzi anavyoufinyanga udongo. Hata hivyo, Yehova ni tofauti kwa njia fulani kubwa. Mfinyanzi anaweza kufinyanga chombo cha aina yoyote kutokana na udongo. Je, Yehova huwafinyanga kwa lazima watu au mataifa, akiwafanya wengine kuwa wema na wengine wabaya? Jibu la Biblia ni hapana. Yehova amewapa wanadamu zawadi yenye thamani sana, yaani, zawadi ya uhuru wa kuchagua. Akiwa mwenye enzi kuu, hatumii mamlaka yake kwa njia inayowazuia wanadamu kutumia zawadi hiyo. Ni lazima wanadamu wakubali kufinyangwa na Muumba, Yehova.Soma Yeremia 18:7-10.

5. Wanadamu wanapokataa kufinyangwa na Yehova, anatumiaje mamlaka yake juu yao?

5 Vipi wanadamu wakikataa kwa ukaidi kufinyangwa na yule Mfinyanzi Mkuu? Anatumiaje mamlaka yake akiwa Mungu? Fikiria inavyokuwa kwa udongo usiofaa kutumiwa kwa kusudi fulani hususa. Mfinyanzi anaweza kuutumia udongo huo kufinyanga chombo kingine au kuutupa! Hata hivyo, kwa kawaida udongo usipofaa, ni kosa la mfinyanzi. Lakini Mfinyanzi wetu hawezi kamwe kukosea. (Kum. 32:4) Mtu asipokubali kufinyangwa na Yehova, ni kosa la mtu huyo. Yehova hutumia mamlaka yake kama ya mfinyanzi kuwafinyanga wanadamu ikitegemea jinsi wanavyoitikia jitihada zake za kuwafinyanga. Wale wanaoitikia ifaavyo wanafinyangwa kwa njia yenye manufaa. Kwa mfano, Wakristo watiwa-mafuta ni “vyombo vya rehema” ambavyo vimefinyangwa na kuwa ‘vyombo kwa matumizi yenye kuheshimika.’ Kwa upande mwingine, wale wanaompinga Mungu kwa ukaidi wanakuwa “vyombo vya ghadhabu vilivyofanywa kuwa vyenye kufaa kwa ajili ya uharibifu.”Rom. 9:19-23.

6, 7. Mfalme Daudi na Mfalme Sauli waliitikia mashauri ya Yehova kwa njia gani tofauti?

 6 Njia moja anayotumia Yehova kuwafinyanga watu ni kupitia mashauri au nidhamu. Tukichunguza wafalme wawili wa kwanza wa Israeli, yaani, Sauli na Daudi, tunaweza kuona jinsi anavyotumia mamlaka yake juu ya wale anaowafinyanga. Mfalme Daudi alipofanya uzinzi na Bath-sheba, matendo yake yalimwathiri sana yeye na wengine. Hata ingawa Daudi alikuwa mfalme, Yehova hakusita kumtia nidhamu kali. Mungu alimtuma Nathani, nabii wake, kumpa Daudi ujumbe mkali. (2 Sam. 12:1-12) Daudi aliitikiaje? Alichomwa sana moyoni naye akatubu. Daudi alionyeshwa rehema na Mungu.Soma 2 Samweli 12:13.

 7 Kinyume chake, Mfalme Sauli aliyetawala kabla ya Daudi, hakuitikia vyema aliposhauriwa. Yehova alimpa Sauli amri ya moja kwa moja kupitia nabii Samweli: Waangamize Waamaleki wote na mifugo yao. Sauli hakutii amri hiyo ya Mungu. Hakumwangamiza Mfalme Agagi na mifugo yao  bora zaidi. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba alitaka aheshimiwe. (1 Sam. 15:1-3, 7-9, 12) Aliposhauriwa, Sauli hakupaswa kuufanya moyo wake uwe mgumu, alipaswa kukubali kufinyangwa na yule Mfinyanzi Mkuu. Hata hivyo, Sauli alikataa kufinyangwa. Aliutetea mwenendo wake. Alitoa kisingizio kwamba jambo alilofanya lilikubalika kwa sababu mifugo ingetolewa dhabihu, na hivyo akapunguza uzito wa shauri la Samweli. Yehova alikataa Sauli asiendelee kuwa mfalme, naye Sauli hakuwa tena na uhusiano mzuri pamoja na Mungu wa kweli.Soma 1 Samweli 15:13-15, 20-23.

Sauli alikataa na kupunguza uzito wa shauri. Alikataa kufinyangwa! (Tazama fungu la 7)

Daudi alichomwa moyoni naye akakubali shauri. Alikubali Mungu amfinyange. Je, wewe hukubali? (Tazama fungu la 6)

MUNGU HANA UPENDELEO

8. Tunajifunza somo gani kutokana na jinsi taifa la Israeli lilivyoitikia lilipofinyangwa na Yehova?

8 Yehova humpa mtu mmoja-mmoja na pia mataifa mbalimbali nafasi ya kukubali awafinyange. Katika mwaka wa 1513 K.W.K., wana wa Israeli waliwekwa huru kutoka katika utumwa huko Misri na kufanya agano pamoja na Mungu. Waisraeli walikuwa taifa lake alilolichagua na walikuwa na pendeleo la kufinyangwa naye, kana kwamba juu ya gurudumu la yule Mfinyanzi Mkuu. Hata hivyo, watu hao walizidi kufanya mabaya machoni pa Yehova, hata wakaanza kuabudu miungu ya mataifa yaliyowazunguka. Yehova aliwatuma manabii tena na tena ili wawachochee kutubu, lakini Waisraeli hawakusikiliza. (Yer. 35:12-15) Waisraeli walitiwa nidhamu kali kwa sababu ya kujiendesha kwa ukaidi. Kama chombo kinachostahili kuharibiwa, ufalme wa kaskazini wa makabila kumi ulishindwa na Waashuru na ufalme wa kusini wa makabila mawili ulishindwa na Wababiloni. Jambo hilo linapaswa kutufundisha  somo muhimu kama nini! Yehova anaweza kutufinyanga na kutusaidia ikiwa tu tutaitikia ifaavyo.

9, 10. Waninawi waliitikiaje onyo la Mungu?

9 Pia, Yehova aliwapa watu wa Ninawi, mji mkuu wa Ashuru, nafasi ya kutii onyo lake. Neno lake lilimjia Yona, na kusema: “Ondoka, uende Ninawi lile jiji kubwa, ukalitangazie kwamba ubaya wao umefika mbele zangu.” Ninawi lilionwa kuwa linastahili uharibifu.Yona 1:1, 2; 3:1-4.

10 Hata hivyo, Yona alipotangaza ujumbe wa maangamizi, “watu wa Ninawi wakaanza kumwamini Mungu, ndipo wakatangaza kufunga na kuvaa nguo za magunia, kutoka aliye mkubwa zaidi kati yao mpaka aliye mdogo zaidi.” Mfalme wao “akasimama kutoka kwenye kiti chake cha ufalme, akavua vazi lake rasmi na kujifunika nguo za magunia na kuketi katika majivu.” Waninawi walikubali kufinyangwa na Yehova nao wakatubu. Kwa hiyo, Yehova hakuleta msiba.Yona 3:5-10.

11. Yehova alionyesha wazi sifa gani aliposhughulika na Waisraeli na Waninawi?

11 Yehova hakukosa kuwatia nidhamu Waisraeli hata ingawa walikuwa taifa alilolichagua. Kwa upande mwingine, Waninawi hawakuwa wamefanya agano pamoja na Mungu. Hata hivyo, Yehova aliagiza watangaziwe ujumbe wake wa hukumu naye aliwaonyesha rehema walipobadilika na kuwa kama udongo laini mikononi mwake. Mifano hiyo miwili inaonyesha waziwazi kwamba Yehova Mungu wetu ‘hamtendei yeyote kwa upendeleo.’Kum. 10:17.

YEHOVA NI MWENYE USAWAZIKO NAYE HUNYUMBULIKA

12, 13. (a) Kwa nini Mungu hubadili uamuzi wake watu wanapokubali awafinyange? (b) ‘Kujuta’ kwa Yehova kulimaanisha nini kuhusiana na Sauli? Na kuhusiana na Ninawi?

12 Utayari wa Mungu wa kutufinyanga unaonyesha kwamba ana usawaziko na ananyumbulika. Hilo linathibitishwa na hali zinazomfanya Yehova aamue kuwachukulia watu hatua ikitegemea hukumu yake ya haki, kisha anabadili uamuzi huo kwa sababu ya itikio lao. Kuhusu mfalme wa kwanza wa Israeli, Maandiko yanasema kwamba Yehova ‘alijuta kwamba alimfanya Sauli kuwa mfalme.’ (1 Sam. 15:11) Watu wa Ninawi walipotubu, walipogeuka, na kuacha njia zao mbaya, Biblia inasema: “Mungu wa kweli akajuta juu ya msiba ambao alikuwa amesema ataleta juu yao; naye hakuuleta.”Yona 3:10.

13 Kwa kweli, neno la Kiebrania lililotafsiriwa “akajuta” linamaanisha kubadili mtazamo au nia. Ingawa Yehova alimchagua Sauli kuwa mfalme, alibadili mtazamo Wake na kumkataa. Yehova hakubadili mtazamo wake eti kwa sababu alikosea kumchagua Sauli, aliubadili kwa sababu Sauli alitenda bila imani naye hakumtii. Mungu wa kweli alijuta aliposhughulika na Waninawi; yaani, alibadili nia yake kuwaelekea. Inafariji kama nini kujua kwamba Yehova, Mfinyanzi wetu, ni mwenye usawaziko, ananyumbulika, ni mwenye neema na rehema, na yuko tayari kubadili uamuzi wake ikiwa wakosaji wanafanya mabadiliko yafaayo!

TUSIKATAE NIDHAMU YA YEHOVA

14. (a) Yehova hutufinyanga jinsi gani leo? (b) Tunapaswa kuitikiaje tunapofinyangwa na Mungu?

14 Leo, Yehova hutufinyanga akitumia hasa Neno lake, Biblia, na tengenezo lake. (2 Tim. 3:16, 17) Je, hatupaswi kukubali shauri au nidhamu yoyote tunayopokea kupitia njia hizo? Hata kama muda mrefu kadiri gani umepita tangu tubatizwe au tuna mapendeleo mengi kadiri gani, tunapaswa kuendelea kukubali mashauri ya Yehova, na kuyaruhusu yatufinyange ili tuwe vyombo vya matumizi yenye kuheshimika.

15, 16. (a) Mtu anaweza kuwa na hisia gani zisizofaa anapotiwa nidhamu inayohusisha kupoteza mapendeleo? Toa mfano. (b) Ni nini kinachoweza kutusaidia kukabiliana na hisia zisizofaa zinazotokana na kutiwa nidhamu?

 15 Huenda tukatiwa nidhamu kwa kurekebishwa au kufundishwa. Hata hivyo, huenda nyakati nyingine tukahitaji kutiwa nidhamu tusipofanya jambo linalofaa. Nidhamu hiyo inaweza kuhusisha kupoteza mapendeleo. Fikiria mfano wa Dennis * aliyekuwa akitumikia akiwa mzee. Alitenda dhambi kwa sababu ya kufanya uamuzi usiofaa katika masuala ya kibiashara, na hivyo akakaripiwa faraghani. Dennis alihisije usiku ambao kutaniko lilitangaziwa kwamba hatumikii tena akiwa mzee? Anasema hivi: “Nilihisi kwamba sifai hata kidogo. Kwa miaka 30 nilikuwa na mapendeleo mengi. Nilikuwa painia wa kawaida, nilitumikia Betheli, niliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa huduma na kisha mzee. Nilikuwa pia nimetoa tu hotuba yangu ya kwanza katika kusanyiko la wilaya. Kwa ghafla, nilipoteza mapendeleo yote. Licha ya kwamba niliaibika na kuona haya, nilihisi sistahili tena kuwa katika tengenezo.”

16 Dennis alihitaji kubadili mwenendo wake na kuacha makosa yaliyofanya atiwe nidhamu. Lakini ni nini kilichomsaidia kukabiliana na hisia zisizofaa? Anaeleza hivi: “Niliazimia kudumisha mazoea mazuri ya kiroho. Nilisaidiwa vilevile na utegemezo niliopata kutoka kwa undugu wetu wa Kikristo na kitia-moyo kutoka katika machapisho yetu. Makala yenye kichwa ‘Umewahi Kuwa na Mapendeleo ya Utumishi? Je, Unaweza Kutumikia Tena?’ katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 15, 2009, ilikuwa kama barua ya kibinafsi iliyojibu sala zangu. Nilithamini zaidi shauri hili: ‘Kwa kuwa sasa huna madaraka mengi katika kutaniko, jitahidi kuboresha hali yako ya kiroho.’” Nidhamu imemnufaishaje Dennis? Baada ya miaka kadhaa, anasema hivi: “Yehova amenibariki tena kwa kunipa pendeleo la kutumikia nikiwa mtumishi wa huduma.”

17. Kutenga na ushirika kunaweza kumsaidiaje mtenda-dhambi kutubu? Toa mfano.

17 Kutenga na ushirika ni aina nyingine ya nidhamu kutoka kwa Yehova. Hatua hiyo inalilinda kutaniko kutokana na uvutano mbaya na inaweza kumsaidia mtenda-dhambi kutubu. (1 Kor. 5:6, 7, 11) Robert alitengwa na ushirika kwa miaka karibu 16. Wakati huo, wazazi wake na ndugu zake walifuata kwa ushikamanifu mwongozo wa Neno la Mungu wa kutoshirikiana na hata kutowasalimu wakosaji. Miaka kadhaa imepita tangu Robert aliporudishwa kutanikoni, na sasa anaendelea vizuri kiroho. Alipoulizwa kilichomchochea amrudie Yehova na watu Wake baada ya kukaa nje kwa muda mrefu hivyo, alisema kwamba alichochewa na msimamo wa familia yake. “Kama familia yangu ingeshirikiana nami hata kidogo, labda kwa kunijulia hali, ningetosheka na ushirika huo mdogo na inaelekea kwamba singechochewa kumrudia Mungu kwa sababu ya kutamani ushirika wao.”

18. Tunapaswa kuwa udongo wa aina gani mikononi mwa yule Mfinyanzi Mkuu?

18 Huenda tusihitaji nidhamu ya aina hiyo, lakini tutakuwa udongo wa aina gani mikononi mwa yule Mfinyanzi Mkuu? Tutaitikiaje tukitiwa nidhamu? Je, tutakuwa kama Daudi au kama Sauli? Yule Mfinyanzi Mkuu ni Baba yetu. Usisahau kamwe kwamba “yeye ambaye Yehova anampenda, humkaripia, kama vile baba anavyomkaripia mwana anayemfurahia.” Kwa hiyo, “usikatae nidhamu ya Yehova; wala usichukie karipio lake.”Met. 3:11, 12.

^ fu. 15 Majina yamebadilishwa.