Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Acha Nizamu ya Yehova Ikufinyange

Acha Nizamu ya Yehova Ikufinyange

“Utaniongoza kwa shauri lako, na baadaye utanipeleka kwenye utukufu.”​—ZAB. 73:24.

1, 2. (a) Ni mambo gani yanayoweza kutusaidia kuwa na uhusiano muzuri pamoja na Yehova? (b) Tutapata faida gani kwa kujifunza masimulizi ya Biblia kuhusu namna watu walivyoitikia nizamu ya Mungu?

 ‘LAKINI mimi, kumukaribia Mungu ni kwema kwangu. Nimeweka kimbilio langu katika Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.’ (Zab. 73:28) Kupitia maneno hayo, mutunga-zaburi alionyesha kwamba alitumainia Mungu. Ni hali gani zilizomufanya aseme maneno hayo mazito? Alipoona namna waovu walivyoishi kwa amani, hapo hapo mutunga-zaburi aliumia moyoni. Kwa hiyo, alinungunika hivi: “Nimeusafisha moyo wangu bure na kuiosha mikono yangu katika kutokuwa na hatia.” (Zab. 73:2, 3, 13, 21) Lakini, alipoingia ‘katika patakatifu pakubwa pa Mungu,’ alianza kuona mambo kama vile Yehova anavyoyaona na aliendelea kuwa na uhusiano wa karibu na Mungu. (Zab. 73:16-18) Kuingia mahali patakatifu pa Mungu kulimufundisha mutumishi huyo wa Mungu somo hili la maana: Kuwa kati ya watu wa Mungu, kukubali mashauri yake, na kuyatumikisha ni jambo la maana ili kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova.​—Zab. 73:24.

2 Sisi pia tunatamani kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu wa kweli na aliye hai. Ili kufikia muradi huo, ni jambo la maana kuacha mashauri ao nizamu yake itufinyange ili tuwe watu wanaomupendeza. Zamani, Mungu alionyesha mutu mumoja mumoja na mataifa mazima rehema kwa kuwatolea nafasi za kukubali ao kukataa nizamu yake. Masimulizi kuhusu watu waliokubali ao kukataa nizamu ya Yehova yameandikwa katika Biblia ili “kutufundisha sisi” na ni “onyo kwetu sisi ambao tumefikiwa na miisho ya mifumo ya mambo.” (Rom. 15:4; 1 Kor. 10:11) Kujifunza masimulizi hayo kwa uangalifu kutatusaidia kuelewa sifa za Yehova na kutatuonyesha namna tunaweza kufaidika na nizamu yake.

NAMNA YEHOVA ANAVYOTUMIA MAMLAKA YAKE

3. Namna gani maandiko ya Isaya 64:8 na Yeremia 18:1-6 yanazungumuzia kwa njia ya mufano mamlaka ya Yehova juu ya watu? (Ona picha mwanzoni mwa habari hii.)

3 Ili kuzungumuzia kwa njia ya mufano mamlaka ya Yehova juu ya mutu mumoja mumoja na mataifa mazima, andiko la Isaya 64:8 linasema hivi: ‘Ee Yehova, wewe ni Baba yetu. Sisi ni udongo, nawe ni Mufinyanzi wetu; nasi sote ni kazi ya mukono wako.’ Mufinyanzi ana mamlaka yote juu ya udongo anaofinyanga, anaweza kuutumia ili kutengeneza chombo anachotaka. Udongo hauwezi kumuambia kitu. Ndivyo ilivyo kati ya mwanadamu na Mungu. Mwanadamu hana haki ya kubishana na Mungu kama vile udongo hauwezi kubishana na mufinyanzi anayetumia mikono yake ili kuufinyanga namna anavyopenda.​—Soma Yeremia 18:1-6.

4. Je, Yehova anawafinyanga watu fulani ao mataifa ovyoovyo? Eleza.

4 Yehova alionyesha taifa la Israeli kwamba ana uwezo wa kuwatendea kama vile mufinyanzi anavyoutendea udongo. Lakini kuna tofauti moja kubwa. Mufinyanzi anaweza kutumia udongo alio nao ili kufanya chombo cha aina yoyote. Je, hilo linamaanisha kwamba Yehova anawafinyanga watu ovyoovyo, akiwafanya wengine kuwa wazuri na wengine kuwa wabaya? Biblia haiseme hivyo. Yehova amewapa wanadamu zawadi ya maana sana​—uhuru wa kuchagua. Ijapokuwa yeye ndiye Mutawala Mukubwa wa Ulimwengu Wote, yeye hatumie mamlaka yake ili kuwalazimisha watu. Kila mwanadamu anapaswa kuchagua kufinyangwa na Yehova.​—Soma Yeremia 18:7-10.

5. Yehova anatumia mamlaka yake namna gani wakati wanadamu wanakataa awafinyange?

5 Namna gani Yehova, Mufinyanzi Mukubwa, anatumia mamlaka yake wakati wanadamu wanakataa kwa kiburi kufinyangwa naye? Fikiria jambo linaloweza kutokea ikiwa udongo haufae kwa ajili ya kutengeneza chombo fulani. Labda mufinyanzi anaweza kutumia udongo huo ili kutengeneza chombo kingine ao anaweza tu kuutupa. Kwa kawaida udongo unaweza kuwa usiofaa ikiwa mufinyanzi hakuufinyanga vizuri. Lakini, Mufinyanzi wetu hawezi kukosea hata kidogo. (Kum. 32:4) Wakati mutu anakataa kufinyangwa na Yehova, kosa ni la mutu huyo tu. Yehova anabadili namna yake ya kuwafinyanga wanadamu kulingana na jinsi wanavyokubali ao kukataa nizamu yake. Wale wanaokubali kufinyangwa naye wanakuwa watu wa maana kwake. Kwa mufano, Wakristo watiwa​-mafuta ni “vyombo vya rehema” ambavyo vimefanywa kuwa ‘vyombo kwa matumizi yenye kuheshimika.’ Kwa upande mwengine, wale wanaokataa kwa kiburi kufinyangwa na Mungu wanakuwa ‘vyombo vya gazabu vilivyofanywa kuwa vyenye kufaa kwa ajili ya uharibifu.’​—Rom. 9:19-23.

6, 7. Namna gani Mufalme Daudi na Mufalme Sauli wanatofautiana katika namna yao ya kukubali mashauri ya Yehova?

 6 Njia moja ambayo Yehova anatumia ili kuwafinyanga watu ni kuwatolea mashauri ao nizamu. Tunaweza kuona namna anavyotumia mamlaka yake juu ya wale anaowafinyanga kwa kufikiria mifano ya wafalme wawili wa kwanza wa Israeli, Sauli na Daudi. Mufalme Daudi alipofanya uzinifu na Bath-sheba, matendo yake yalimuumiza yeye na yaliwaumiza wengine sana. Hata ikiwa Daudi alikuwa mufalme, Yehova hakujizuia kumutolea nizamu kali. Mungu alimutuma nabii Nathani aende kumutolea Daudi ujumbe muzito. (2 Sam. 12:1-12) Daudi aliitikia namna gani? Alisikitikia sana makosa yake na akatubu. Daudi alifaidika na rehema ya Mungu.​—Soma 2 Samweli 12:13.

 7 Lakini, Mufalme Sauli aliyemutangulia Daudi, hakukubali mashauri. Kupitia nabii Samweli, Yehova alimutolea Mufalme Sauli amri hii iliyo wazi: Haribu Waamaleki wote na mifugo yao. Sauli hakutii amri hiyo ya Mungu. Hakumuua mufalme Agagi na hakuwaua wanyama walio wanono. Sababu gani? Kwanza ilikuwa kwa sababu alitaka kujitafutia sifa. (1 Sam. 15:1-3, 7-9, 12) Aliposhauriwa, Sauli alipaswa kujiacha afinyangwe na Mufinyanzi Mukubwa kwa kusikiliza na kukubali mashauri. Lakini, Sauli alikataa kufinyangwa. Alijitetea kwa kusema kwamba jambo alilofanya halikuwa kosa kwa sababu wanyama aliochukua wangetolewa kuwa zabihu kwa Yehova, na alizarau mashauri ya Samweli. Yehova alimukataa Sauli asiwe tena mufalme, na kuanzia wakati huo, Sauli hakuwa tena na uhusiano muzuri pamoja na Mungu wa kweli.​—Soma 1 Samweli 15:13-15, 20-23.

Sauli alizarau na kutupilia mbali shauri. Alikataa kufinyangwa! (Ona  fungu la 7)

Daudi alisikitikia sana makosa yake na alikubali shauri. Alikubali Mungu amufinyange. Je, wewe pia unaitikia hivyo? (Ona  fungu la 6)

MUNGU HANA UBAGUZI

8. Namna ambavyo taifa la Israeli liliitikia nizamu ya Yehova inatufundisha nini?

8 Yehova anatolea mutu mumoja mumoja na mataifa nafasi ya kukubali ao kukataa kufinyangwa naye. Katika mwaka wa 1513, Waisraeli walikombolewa katika utumwa wa Misri na kuingia katika uhusiano wa pekee pamoja na Mungu. Waisraeli walikuwa taifa lililochaguliwa la Yehova na walikuwa na pendeleo la kufinyangwa. Lakini, waliendelea kufanya mabaya machoni pa Yehova, na hata waliabudu miungu ya mataifa yaliyowazunguka. Mara kwa mara, Yehova aliwatumia manabii ili wawaonye, lakini hawakuwasikiliza. (Yer. 35:12-15) Kwa sababu ya kuonyesha shingo ngumu, Waisraeli walipaswa kupewa nizamu kali. Kwa sababu walikuwa kama chombo kinachostahili kuharibiwa, ufalme wa kaskazini wa makabila kumi uliharibiwa na Asiria na ule wa kusini wa makabila mawili uliharibiwa na Wababiloni. Mufano wao unaweza kutufundisha jambo la maana sana! Tutafaidika na nizamu ya Yehova ikiwa tu tunaikubali.

9, 10. Wakaaji wa Ninawi walitenda namna gani walipotolewa onyo?

9 Yehova aliwatolea pia watu wa Ninawi, muji mukubwa wa Asiria, nafasi ya kutii ao kutotii onyo lake. Yehova alimuambia Yona hivi: “Ondoka, uende Ninawi lile jiji kubwa, ukalitangazie kwamba ubaya wao umefika mbele zangu.” Muji wa Ninawi ulistahili kabisa kuharibiwa.​—Yona 1:1, 2; 3:1-4.

10 Lakini, Yona alipotangaza ujumbe wa hukumu, ‘watu wa Ninawi walianza kumwamini Mungu, ndipo wakatangaza kufunga na kuvaa nguo za magunia, kutoka aliye mukubwa zaidi kati yao mupaka aliye mudogo zaidi.’ Mufalme wao ‘alisimama kutoka kwenye kiti chake cha ufalme, akavua vazi lake rasmi na kujifunika nguo za magunia na kuketi katika majivu.’ Wakaaji wa Ninawi walikubali Yehova awafinyange na walitubu. Kwa hiyo, Yehova hakuwaharibu tena.​—Yona 3:5-10.

11. Ni sifa gani ya Yehova ambayo tunajifunza kutokana na namna alivyowatendea Waisraeli na wakaaji wa Ninawi?

11 Hata ikiwa Waisraeli walikuwa taifa la pekee la Mungu, Yehova hakujizuia kuwatolea nizamu. Kwa upande mwengine, wakaaji wa Ninawi hawakuwa na uhusiano wa pekee na Mungu. Hata hivyo, Yehova alituma nabii wake awatangazie ujumbe wake wa hukumu na aliwaonyesha rehema walipokubali awafinyange. Mifano hiyo miwili inatuonyesha waziwazi kwamba Yehova ‘hamutendee yeyote kwa upendeleo’!​—Kum. 10:17.

YEHOVA ANABADILI MAAMUZI YAKE KULINGANA NA HALI

12, 13. (a) Sababu gani Yehova anabadili maamuzi yake wakati watu wanakubali awafinyange? (b) Ni katika maana gani Yehova alijuta kuhusiana na Sauli na wakaaji wa Ninawi?

12 Anapotufinyanga, Yehova iko tayari kubadili maamuzi yake kulingana na hali. Hilo linaonekana waziwazi katika masimulizi yanayoonyesha namna Yehova alivyokuwa tayari kuharibu watu fulani lakini baadaye alibadili uamuzi wake kwa sababu watu hao walitubu. Kuhusu mufalme wa kwanza wa Israeli, Maandiko yanaonyesha kwamba Yehova ‘alijuta kwamba amemufanya Sauli kuwa mufalme.’ (1 Sam. 15:11) Watu wa Ninawi walipotubu na kuacha kufanya mabaya, Biblia inasema kwamba ‘Mungu wa kweli alijuta juu ya musiba ambao alikuwa amesema ataleta juu yao; naye hakuuleta.’​—Yona 3:10.

13 Maneno ya Kiebrania yanayotafsiriwa “akajuta” yanahusiana na kubadili mutazamo ao nia. Yehova alimuchagua Sauli awe mufalme, na baadaye alimukataa. Yehova alibadili maoni yake, si kwa sababu alikosea alipomuchagua awe mufalme, lakini kwa sababu Sauli alikosa imani na hakuendelea kuwa mutiifu. Mungu wa kweli alijuta kuhusiana na wakaaji wa Ninawi katika maana ya kwamba alibadili uamuzi ambao alikuwa amechukua juu yao. Inafariji sana kujua kwamba Mufinyanzi wetu, Yehova, mwenye neema na rehema, iko tayari kubadili maamuzi yake wakati waovu wanapofanya mabadiliko!

TUSIZARAU NIZAMU YA YEHOVA

14. (a) Namna gani Yehova anatufinyanga leo? (b) Tunapaswa kuitikia namna gani Yehova anapotufinyanga?

14 Leo, Yehova anatufinyanga zaidi sana kupitia neno lake, Biblia, na tengenezo lake. (2 Tim. 3:16, 17) Tunapaswa kukubali shauri lolote ao nizamu yoyote ambayo tunapata kupitia njia hizo. Hata ikiwa miaka mingi imepita tangu tulipobatizwa ao tumepata mapendeleo mengi katika tengenezo la Yehova, tunapaswa kuendelea kukubali mashauri ya Yehova, kuruhusu yatufinyange ili tuwe vyombo kwa ajili ya matumizi yenye kuheshimika.

15, 16. (a) Mutu anaweza kujisikia namna gani kisha kupoteza madaraka katika kutaniko? Toa mufano. (b) Ni nini inaweza kutusaidia tusiendelee kujisikia kuwa hatufae?

15 Yehova anaweza kututolea nizamu fulani kwa kutufundisha ao kutukaripia. Lakini nyakati fulani, tunaweza kupewa nizamu kwa sababu tumekosea. Nizamu hiyo inaweza kufanya tupoteze madaraka fulani. Fikiria mufano wa ndugu Dennis * aliyekuwa muzee wa kutaniko. Alipewa karipio kwa sababu hakuchukua maamuzi mazuri katika mambo ya biashara. Dennis alijisikia namna gani usiku ambao tangazo lilitolewa katika kutaniko kwamba yeye haiko tena muzee? Dennis anasema hivi: “Nilijisikia kuwa mutu asiyefaa. Kwa miaka zaidi ya 30, nilikuwa nimepata madaraka mengi. Nilikuwa nimefanya upainia wa kawaida, nilitumika kwenye Beteli, nilikuwa nimewekwa kuwa mutumishi wa huduma na baadaye muzee wa kutaniko. Nilikuwa tu nimetoa hotuba ya kwanza kwenye mukusanyiko wa wilaya. Lakini, nilipoteza yote hayo kwa gafula. Zaidi ya kusikia haya na kushangaa, nilifikiri kwamba mimi si mutu wa maana tena katika kutaniko.”

16 Dennis alipaswa kubadilika kwa kuacha makosa ambayo yalifanya akaripiwe. Lakini ni nini ilimusaidia asiendelee kujisikia kuwa mutu asiyefaa? Anaeleza hivi: “Niliazimia kuendelea kuwa na mazoea mazuri ya kiroho. Na jambo la maana ni kwamba ndugu na dada walinitegemeza na nilipata vitia-moyo katika vichapo vyetu. Habari iliyotolewa katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 8, 2009, yenye kichwa ‘Umewahi Kuwa na Mapendeleo? Je, Unaweza Kutumikia Tena?’ ilikuwa jibu kwa sala zangu. Katika habari hiyo, nilifurahia zaidi sana shauri hili: ‘Kwa kuwa sasa hauna madaraka mengi katika kutaniko, jikaze kufanya hali yako ya kiroho iwe nzuri.’” Namna gani Dennis alifaidika na nizamu hiyo? Kisha miaka fulani, anasema hivi: “Yehova amenibariki tena kwa kunipa pendeleo la kuwa mutumishi wa huduma.”

17. Kutengwa na kutaniko kunaweza kumusaidia mutenda-zambi namna gani? Toa mufano.

17 Kutengwa na kutaniko ni njia nyingine ambayo Yehova anatumia ili kututolea nizamu. Nizamu hiyo inasaidia washiriki wa kutaniko wasiambukizwe na matendo mabaya ya mutenda-zambi na inamusaidia mutenda​-zambi huyo amurudilie Yehova. (1 Kor. 5:6, 7, 11) Robert alitengwa na kutaniko kwa muda wa miaka 16. Muda wote huo, wazazi wake na ndugu zake walitumia kwa ushikamanifu muongozo wa Neno la Mungu wa kuepuka kuchangamana na watenda​-zambi, na hata kuwasalimu. Robert amerudishwa katika kutaniko kumepita miaka fulani sasa na anafanya maendeleo mazuri ya kiroho. Alipoulizwa kile kilichomuchochea amurudilie Yehova na kurudia katika kutaniko kisha muda murefu kama huo, alijibu kwamba ni musimamo wa familia yake ndio uliomuchochea. Alisema hivi: “Ikiwa watu wa familia yangu wangekuwa na uhusiano pamoja nami hata kwa kiasi kidogo, singeona tofauti kubwa kabisa na singekuwa na tamaa ya kumurudilia Mungu.”

18. Tunapaswa kuwa aina gani ya udongo katika mikono ya Mufinyanzi Mukubwa?

18 Labda hatuhitaji nizamu kama hiyo, lakini sisi tutakuwa udongo wa aina gani katika mikono ya Mufinyanzi Mukubwa? Je, tutaikubali nizamu ao tutaikataa? Je, tutakuwa kama Daudi ao Sauli? Mufinyanzi Mukubwa ni Baba yetu. Usisahau hata siku moja kwamba ‘yeye ambaye Yehova anamupenda, anamukaripia, kama vile baba anavyomukaripia mwana anayemufurahia.’ Kwa hiyo, ‘usikatae nizamu ya Yehova, na usichukie karipio lake.’​—Met. 3:11, 12.

^ Majina yamebadilishwa.