Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mmetakaswa

Mmetakaswa

“Mmeoshwa mkawa safi, . . . mmetakaswa.”1 KOR. 6:11.

1. Ni mambo gani yenye kuhuzunisha aliyogundua Nehemia aliporudi Yerusalemu? (Tazama picha iliyo kwenye ukurasa huu.)

WAKAAJI wa Yerusalemu wananung’unika kuhusu mgeni mwenye sifa mbaya anayeishi katika chumba cha hekalu. Walawi wanaacha mgawo wao. Badala ya kuongoza katika ibada, wazee wanafanya biashara siku ya Sabato. Waisraeli wengi wanaoa wanawake wasio Wayahudi. Hayo ni baadhi tu ya mambo yenye kuhuzunisha anayogundua Nehemia anaporudi Yerusalemu muda fulani baada ya mwaka wa 443 K.W.K.Neh. 13:6.

2. Israeli lilikujaje kuwa taifa lililotakaswa?

2 Israeli lilikuwa taifa lililo wakfu kwa Mungu. Katika mwaka wa 1513 K.W.K., Waisraeli walitamani kuishi kupatana na mapenzi ya Yehova. Walisema hivi: “Maneno yote ambayo Yehova amesema tuko tayari kuyafanya.” (Kut. 24:3) Kwa hiyo, Mungu aliwatakasa au kuwaweka kando kuwa watu wake waliochaguliwa. Hilo lilikuwa pendeleo kubwa kama nini! Miaka arobaini baadaye, Musa aliwakumbusha hivi: “Ninyi ni watu watakatifu kwa Yehova Mungu wenu. Ni ninyi ambao Yehova Mungu amewachagua ninyi muwe watu wake, mali ya pekee, kutoka kati ya vikundi vyote vya watu vilivyo kwenye uso wa nchi.”Kum. 7:6.

3. Hali ya kiroho ya Wayahudi ilikuwaje Nehemia alipofika Yerusalemu kwa mara ya pili?

3 Inasikitisha kwamba msisimuko ambao Waisraeli walikuwa nao mwanzoni, wa kuwa taifa takatifu haukudumu. Ingawa siku zote kulikuwa na watu mmoja-mmoja waliomtumikia Mungu, mara nyingi Wayahudi kwa ujumla walihangaikia zaidi kuonekana kuwa watakatifu au watu wenye kujitoa kidini, badala ya kufanya mapenzi ya Mungu. Nehemia alipofika Yerusalemu kwa mara ya pili, miaka mia moja hivi ilikuwa imepita tangu mabaki waaminifu waliporudi kutoka Babiloni ili kurudisha ibada ya kweli. Kwa mara nyingine, bidii ya taifa hilo kwa ajili ya mambo ya kiroho ilikuwa ikififia.

4. Tutachunguza mambo gani yanayoweza kutusaidia kuendelea kuwa watu waliotakaswa?

4 Kama Waisraeli, leo kwa ujumla Mashahidi wa  Yehova wametakaswa na Mungu. Wakristo watiwa-mafuta na washiriki wa “umati mkubwa” ni watakatifu, wamewekwa kando kwa ajili ya utumishi mtakatifu. (Ufu. 7:9, 14, 15; 1 Kor. 6:11) Hakuna yeyote kati yetu anayetaka kupoteza msimamo wake mtakatifu mbele za Mungu kama Waisraeli walivyofanya. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuepuka jambo hilo ili kuendelea kubaki tukiwa watakatifu na kumtumikia Yehova kwa njia inayofaa? Katika funzo hili, tutachunguza mambo manne yanayokaziwa katika Nehemia sura ya 13: (1) Epuka mashirika mabaya; (2) unga mkono mipango ya kitheokrasi; (3) tanguliza mambo ya kiroho; na (4) tunza utambulisho wako wa Kikristo. Acheni tuchunguze kila moja ya mambo hayo.

EPUKA MASHIRIKA MABAYA

Nehemia alionyeshaje ushikamanifu wake kwa Yehova? (Tazama fungu la 5 na 6)

5, 6. Eliashibu na Tobia walikuwa nani, na huenda ni kwa nini Eliashibu alishirikiana na Tobia?

5 Soma Nehemia 13:4-9. Tumezungukwa na uvutano usio safi, hivyo si rahisi kwetu kuendelea kuwa watakatifu. Mfikirie Eliashibu na Tobia. Eliashibu alikuwa kuhani mkuu, na inaelekea kwamba Tobia alikuwa Mwamoni na ofisa wa cheo cha chini katika utawala wa Uajemi huko Yudea. Tobia na wenzake walipinga jitihada za Nehemia za kujenga upya kuta za Yerusalemu. (Neh. 2:10) Waamoni hawakuruhusiwa kuingia katika uwanja wa hekalu. (Kum. 23:3) Basi, kwa nini kuhani mkuu alimruhusu Tobia akae katika jumba la kulia chakula la hekalu?

6 Tobia alikuwa rafiki wa karibu wa Eliashibu. Tobia na Yehohanani, mwana wake, walioa wanawake Wayahudi, na Wayahudi wengi walimsifu sana Tobia. (Neh. 6:17-19) Mmoja wa wajukuu wa Eliashibu alimwoa binti ya Sanbalati, gavana wa Samaria aliyekuwa mmoja wa rafiki wa karibu sana wa Tobia. (Neh. 13:28) Mahusiano hayo yanaweza kutusaidia kuelewa ni kwa nini Kuhani Mkuu Eliashibu aliruhusu mtu asiye mwamini na aliye mpinzani amwongoze vibaya. Hata hivyo, Nehemia alionyesha ushikamanifu kwa Yehova kwa kutupa fanicha za Tobia nje ya jumba la kulia chakula.

7. Wazee na Wakristo wengine huepukaje kuchafua msimamo wao mtakatifu mbele za Yehova?

7 Tukiwa watu waliojiweka wakfu kwa Mungu, ni lazima kwanza tuwe washikamanifu kwa Yehova sikuzote. Tusiposhikamana na viwango vyake vya uadilifu, hatutabaki watakatifu mbele zake. Hatupaswi kuruhusu mahusiano ya kifamilia yatufanye tupuuze kanuni za Biblia. Wazee Wakristo wanaongozwa na maoni ya Yehova badala ya hisia au maoni yao. (1 Tim. 5:21) Wazee hujitahidi kabisa kuepuka kufanya jambo lolote linaloweza kuwafanya walegeze msimamo wao kwa Mungu.1 Tim. 2:8.

8. Watumishi wote wa Yehova waliojiweka wakfu wanapaswa kukumbuka nini kuhusu watu wanaoshirikiana nao?

8 Tunapaswa kukumbuka kwamba “mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.” (1 Kor. 15:33) Huenda baadhi ya watu wetu wa ukoo wakawa mashirika mabaya. Eliashibu aliwawekea wengine mfano mzuri kwa kumuunga mkono kikamili Nehemia katika kujenga upya kuta za Yerusalemu. (Neh. 3:1) Hata hivyo, inaonekana kwamba uvutano mbaya wa Tobia na watu wengine ulimchochea Eliashibu kufanya mambo yaliyomfanya kuwa mchafu mbele za Yehova. Mashirika mazuri hututia moyo kufuatilia mambo ya Kikristo yenye kujenga kama vile kusoma Biblia, kuhudhuria mikutano ya Kikristo, na kushiriki katika utumishi wa shambani. Tunawapenda na kuwathamini sana washiriki wa familia wanaotuchochea kufanya yaliyo sawa.

UNGA MKONO MIPANGO YA KITHEOKRASI

9. Kwa nini mipango ya hekalu ilivurugika, naye Nehemia alimlaumu nani kwa jambo hilo?

9 Soma Nehemia 13:10-13. Inaonekana kwamba watu walikuwa wameacha kutoa michango hekaluni Nehemia aliporudi Yerusalemu. Walawi walipokosa kutegemezwa  kwa njia hiyo, waliacha migawo yao na kwenda kufanya kazi katika mashamba yao. Nehemia aliwalaumu watawala-wasaidizi kwa sababu ya hali hiyo. Kwa kweli, hawakuwa wakitimiza majukumu yao. Huenda hawakuwa wakikusanya mafungu ya kumi kutoka kwa watu au kuyapeleka hekaluni, kama walivyoagizwa. (Neh. 12:44) Kwa hiyo, Nehemia alichukua hatua ili mafungu ya kumi yakusanywe. Aliwaweka wanaume wenye kutegemeka kusimamia maghala ya hekalu na kazi ya kugawa mafungu ya kumi.

10, 11. Watu wa Mungu wana pendeleo gani la kutegemeza ibada ya kweli?

10 Je, tunajifunza jambo lolote? Ndiyo, kwa kuwa tunakumbushwa kwamba tuna pendeleo la kumheshimu Yehova kwa vitu vyetu vyenye thamani. (Met. 3:9) Tunapotoa michango ya kutegemeza kazi yake, tunamrudishia tu Yehova vitu ambavyo tayari ni vyake. (1 Nya. 29:14-16) Huenda tukafikiri kwamba hatuna vitu vingi vya kutoa, lakini ikiwa nia ipo, sote tunaweza kushiriki kutoa.2 Kor. 8:12.

11 Kwa miaka mingi, familia moja kubwa iliwaalika wenzi waliozeeka ambao ni mapainia wa pekee ili wale chakula pamoja nao mara moja kila juma. Ingawa wazazi hao walikuwa na watoto wanane, mama yao alisema hivi mara nyingi, “Si jambo kubwa kuongeza sahani mbili zaidi katika meza iliyoandaliwa watu kumi.” Huenda kufanya hivyo mara moja kila juma kusionekane kuwa jambo kubwa, lakini mapainia hao walishukuru kama nini kwa ajili ya ukarimu walioonyeshwa! Na mapainia hao walikuwa baraka kwa familia hiyo. Maneno na mambo yaliyoonwa yenye kutia moyo yaliyosimuliwa na wenzi hao yaliwachochea watoto kufanya maendeleo ya kiroho. Baadaye, wote walianza utumishi wa wakati wote.

12. Wanaume waliowekwa rasmi kutanikoni wanaweka mfano gani mzuri?

12 Jambo lingine tunalojifunza ni hili: Kama Nehemia, wanaume waliowekwa rasmi leo wanaongoza katika kuunga mkono mipango ya kitheokrasi. Wengine kutanikoni hunufaika kutokana na mfano wao. Wazee wanamwiga mtume Paulo katika jambo hilo. Aliunga mkono ibada ya kweli na kutoa mwongozo wenye manufaa. Kwa mfano, alitoa mashauri kadhaa yanayofaa kuhusu jinsi ya kutoa michango.1 Kor. 16:1-3; 2 Kor. 9:5-7.

TANGULIZA MAMBO YA KIROHO

13. Ni katika njia gani baadhi ya Wayahudi hawakuiheshimu Sabato?

13 Soma Nehemia 13:15-21. Tukijiruhusu kufuatilia sana vitu vya kimwili, hali yetu ya kiroho inaweza kudhoofika hatua kwa hatua. Kulingana na andiko  la Kutoka 31:13, Sabato ya kila juma ilipaswa kuwakumbusha Waisraeli kwamba wao ni watu waliotakaswa. Siku ya Sabato ilipaswa kutengwa kwa ajili ya ibada ya familia, sala, na kutafakari Sheria ya Mungu. Hata hivyo, baadhi ya watu katika siku za Nehemia waliiona Sabato kama siku nyingine yoyote. Waliendelea na shughuli zao. Hawakuiona ibada kuwa muhimu. Alipoona hilo, Nehemia aliagiza malango ya jiji yafungwe jioni, siku ya sita, na hivyo kuwafukuza wafanyabiashara wa kigeni kabla ya Sabato.

14, 15. (a) Ni nini kinachoweza kutupata tukitumia wakati mwingi kupita kiasi katika shughuli zetu za kimwili? (b) Tunawezaje kuingia katika pumziko la Mungu?

14 Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Nehemia? Jambo moja ni kwamba hatupaswi kutumia wakati mwingi kupita kiasi katika shughuli za kimwili. Tukifanya hivyo, tunaweza kukengeushwa kwa urahisi au hata kuwa na moyo uliogawanyika, hasa ikiwa tunapenda kazi yetu ya kimwili. Kumbuka onyo alilotoa Yesu kuhusu kutumikia mabwana wawili. (Soma Mathayo 6:24.) Ingawa Nehemia alikuwa na mali, alitumiaje wakati wake alipokuwa Yerusalemu? (Neh. 5:14-18) Badala ya kufuatilia shughuli za kibiashara pamoja na Watiro au watu wengine, alijitoa kabisa kuwasaidia ndugu zake na kufanya mambo yaliyochangia kutakaswa kwa jina la Yehova. Leo pia, wazee Wakristo na watumishi wa huduma hujitahidi kufanya mambo kwa faida ya kutaniko, na waamini wenzao wanawapenda kwa sababu ya roho hiyo. Hivyo, kuna upendo, amani, na usalama miongoni mwa watu wa Mungu.Eze. 34:25, 28.

15 Ingawa Wakristo hawako chini ya amri ya kushika Sabato ya kila juma, Paulo anatuambia kwamba “bado limebaki pumziko la sabato kwa ajili ya watu wa Mungu.” Akaongezea hivi: “Mtu ambaye ameingia katika pumziko la Mungu yeye mwenyewe pia amepumzika kutokana na kazi zake mwenyewe, kama Mungu alivyopumzika kutokana na kazi zake mwenyewe.” (Ebr. 4:9, 10) Tukiwa Wakristo, tunaweza kuingia katika pumziko la Mungu kwa kutii na kutenda kupatana na kusudi lake linaloendelea kutimizwa. Je, wewe na wapendwa wako mnatanguliza ibada ya familia, kuhudhuria mikutano, na huduma ya shambani maishani mwenu? Huenda tukahitaji kuwa thabiti tunaposhughulika na mwajiri wetu au wafanyakazi wenzetu, hasa ikiwa hawaheshimu mambo ya kitheokrasi tunayotanguliza. Huenda tukahitaji ‘kufunga malango ya jiji na kufukuza Watiro’ kwa njia ya mfano ili tutangulize na kukazia fikira ifaavyo mambo matakatifu. Kwa kuwa tumetakaswa, tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, maisha yangu yanaonyesha kwamba nimewekwa kando kwa ajili ya utumishi wa Yehova?’Mt. 6:33.

TUNZA UTAMBULISHO WAKO WA KIKRISTO

16. Utambulisho wa taifa lililotakaswa ulihatarishwa kwa njia gani katika siku za Nehemia?

16 Soma Nehemia 13:23-27. Katika siku za Nehemia, wanaume Waisraeli walikuwa wakioa wanawake wa kigeni. Alipozuru Yerusalemu mara ya kwanza, Nehemia aliwaagiza wanaume wote wazee watie sahihi hati ya makubaliano wakiapa kwamba hawataoa wapagani. (Neh. 9:38; 10:30) Hata hivyo, miaka michache baadaye, aligundua kwamba mbali na kuoa wanawake wa kigeni, wanaume hao Wayahudi walikuwa karibu kupoteza utambulisho wao wakiwa watu waliotakaswa na Mungu! Watoto wa wanawake hao wa kigeni hawakujua kusoma wala kuzungumza Kiebrania. Je, wakiwa watu wazima wangeweza kujitambulisha kwamba wao ni Waisraeli? Au wangejiona kuwa Waashdodi, Waamoni, au Wamoabu? Je, wangeweza kuelewa Sheria ya Mungu bila kujua Kiebrania? Wangemjuaje Yehova na kuchagua kumtumikia badala ya kuitumikia miungu ya uwongo ambayo mama zao waliabudu? Hatua thabiti ilihitaji  kuchukuliwa upesi, na Nehemia alichukua hatua hiyo.Neh. 13:28.

Wasaidie watoto wako wasitawishe uhusiano wa karibu pamoja na Yehova (Tazama fungu la 17 na 18)

17. Wazazi wanaweza kuwasaidia jinsi gani watoto wao kuwa na uhusiano wa kibinafsi pamoja na Yehova?

17 Leo, tunahitaji kuchukua hatua inayofaa ili kuwasaidia watoto wetu kupata utambulisho wa Kikristo. Wazazi, jiulizeni, ‘Watoto wangu wanaongea vizuri kadiri gani “lugha safi” ya kweli ya Kimaandiko? (Sef. 3:9) Je, mazungumzo ya watoto wangu yanaonyesha kwamba wanaongozwa na roho ya Mungu au ya ulimwengu?’ Usikate tamaa haraka ukiona kwamba kuna mambo mengi wanayohitaji kufanyia kazi. Inachukua muda kujifunza lugha, hasa ikiwa kuna mambo yanayotukengeusha fikira. Watoto wako wanashinikizwa sana kutomtii Mungu. Hivyo, uwe na subira na utumie vipindi vya Ibada yenu ya Familia na fursa nyingine unazopata kuwasaidia watoto wako kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. (Kum. 6:6-9) Kazia faida za kuwa tofauti na ulimwengu wa Shetani. (Yoh. 17:15-17) Na ujitahidi kugusa mioyo yao.

18. Kwa nini wazazi Wakristo ndio wanaoweza kuwatayarisha vizuri zaidi watoto wao ili wajiweke wakfu kwa Yehova?

18 Ukweli ni kwamba kila mtoto atafanya uamuzi wake mwenyewe wa kumtumikia Mungu au la. Hata hivyo, wazazi wanaweza kuwasaidia sana. Hilo linatia ndani kuwawekea mfano unaofaa, kuweka mipaka iliyo wazi, na kuzungumza na watoto wao kuhusu matokeo ya maamuzi wanayofanya. Wazazi, hakuna mtu mwingine yeyote isipokuwa ninyi, anayeweza kuwatayarisha watoto wenu kwa njia nzuri zaidi ili wajiweke wakfu kwa Yehova. Wanahitaji msaada wenu ili wapate na kutunza utambulisho wao wa Kikristo. Bila shaka, sote tunapaswa kuwa macho ili tusipoteze ‘mavazi yetu ya nje’ ya mfano, yaani, sifa na viwango vinavyotutambulisha kuwa wafuasi wa Kristo.Ufu. 3:4, 5; 16:15.

ALIKUMBUKWA “KWA AJILI YA WEMA”

19, 20. Yehova anawezaje kutukumbuka “kwa ajili ya wema”?

19 Nabii Malaki aliyeishi katika siku za Nehemia alifunua kwamba ‘kitabu cha kumbukumbu kilianza kuandikwa kwa ajili ya wale wenye kumwogopa Yehova na kwa ajili ya wale wanaolifikiria jina lake.’ (Mal. 3:16, 17) Mungu hatawasahau kamwe wale wanaomheshimu, kumwogopa na kulipenda jina lake.Ebr. 6:10.

20 Nehemia alisali hivi: “Unikumbuke kwa ajili ya wema, Ee Mungu wangu.” (Neh. 13:31) Kama Nehemia, majina yetu yatakuwa katika kitabu cha Mungu cha kumbukumbu ikiwa tutaendelea kuepuka mashirika mabaya, kuunga mkono mipango ya kitheokrasi, kutanguliza mambo ya kiroho, na kulinda utambulisho wetu wa Kikristo. Acheni ‘tuendelee kujijaribu ikiwa sisi tuko katika imani.’ (2 Kor. 13:5) Tukidumisha uhusiano wetu mtakatifu pamoja na Yehova, atatukumbuka “kwa ajili ya wema.”