Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tumetakaswa

Tumetakaswa

‘Mumeoshwa mukawa safi, . . . mumetakaswa.’​—1 KOR. 6:11.

1. Ni mambo gani yenye kuhuzunisha ambayo Nehemia alijionea aliporudi Yerusalemu? (Ona picha mwanzoni mwa habari hii.)

 WAKAAJI wa Yerusalemu wanazungumuza. Mugeni mwenye sifa mbaya anaishi katika chumba cha hekalu. Walawi wameacha mugawo wao. Wazee wanafanya biashara siku ya Sabato kuliko kuongoza mambo ya ibada. Waisraeli wengi wameoa wanawake wageni. Hayo ni mambo fulani yenye kuhuzunisha ambayo Nehemia alikuta aliporudi Yerusalemu kisha mwaka wa 443 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu.​—Neh. 13:6.

2. Namna gani Waisraeli walifikia kuwa taifa lililotakaswa?

2 Israeli lilikuwa taifa lililojitoa kwa Mungu. Katika mwaka wa 1513 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, Waisraeli walikubali kwa furaha kufanya mapenzi ya Yehova. Walisema hivi: “Maneno yote ambayo Yehova amesema tuko tayari kuyafanya.” (Kut. 24:3) Kwa hiyo, Mungu aliwatakasa ao aliwaweka kando kuwa watu wake waliochaguliwa. Hilo lilikuwa pendeleo nzuri kabisa! Kisha miaka makumi ine, Musa aliwakumbusha hivi: ‘Ninyi ni watu watakatifu kwa Yehova Mungu wenu. Ni ninyi ambao Yehova Mungu amewachagua muwe watu wake, mali ya pekee, kutoka kati ya vikundi vyote vya watu vilivyo kwenye uso wa inchi.’​—Kum. 7:6.

3. Wayahudi walikuwa katika hali gani ya kiroho Nehemia alipofika Yerusalemu kwa mara ya pili?

3 Mwanzoni Waisraeli walifurahia pendeleo lao la kuwa taifa takatifu, lakini jambo la kuhuzunisha ni kwamba hawakuendelea kufanya hivyo. Ijapokuwa kila mara kulikuwa watu fulani waliomutumikia Mungu, Wayahudi kwa ujumla walihangaikia sana kuonekana kuwa watakatifu kuliko kuhangaikia kufanya mapenzi ya Mungu. Wakati Nehemia alifika Yerusalemu kwa mara ya pili, kulikuwa kumepita miaka mia moja hivi tangu mabaki ya Wayahudi waaminifu watoke Babiloni ili kurudisha ibada ya kweli. Mara nyingine tena, bidii ya taifa hilo kwa ajili ya mambo ya kiroho ilikuwa imepunguka sana.

4. Tutachunguza mambo gani ambayo yatatusaidia tubaki watu waliotakaswa?

4 Kama Waisraeli, leo pia Mashahidi wa Yehova kwa ujumla wametakaswa na Mungu. Wakristo watiwa​-mafuta na wale wa ‘mukutano mukubwa’ ni watakatifu, ni kusema, wamewekwa kando kwa ajili ya utumishi mutakatifu. (Ufu. 7:9, 14, 15; 1 Kor. 6:11) Hakuna yeyote kati yetu anayependa kupoteza pendeleo hilo kama Waisraeli walivyofanya. Ni nini kinachoweza kutusaidia tusipoteze pendeleo hilo ili tubaki watakatifu na kuendelea kufanya kazi ya Yehova? Katika habari hii, tutachunguza mambo mane yanayozungumuziwa katika Nehemia sura ya 13: (1) Kuepuka marafiki wabaya; (2) Kuunga mukono mipango ya kiteokrasi; (3) Kutia mambo ya kiroho pa nafasi ya kwanza; na (4) Kulinda utambulisho wako wa Kikristo. Acheni sasa tuchunguze jambo moja-moja.

KUEPUKA MARAFIKI WABAYA

Namna gani Nehemia alionyesha uaminifu wake kwa Yehova? (Ona fungu la 5 na la 6)

5, 6. Eliashibu na Tobia walikuwa nani, na labda ni kwa sababu gani Eliashibu alijiacha achochewe na Tobia?

5 Soma Nehemia 13:4-9. Si rahisi kwetu kubaki watakatifu kwa sababu tunazungukwa na watu wabaya. Tufikirie mufano wa Eliashibu na Tobia. Eliashibu alikuwa kuhani mukubwa, na Tobia alikuwa Mwamoni na labda alikuwa wa cheo cha chini katika utawala wa Waperse huko Yudea. Tobia na marafiki wake walipinga jitihada za Nehemia za kujenga upya kuta za Yerusalemu. (Neh. 2:10) Waamoni walikatazwa kuingia katika viwanja vya hekalu. (Kum. 23:3) Namna gani basi kuhani mukubwa angemupatia mutu kama Tobia nafasi katika chumba kimoja cha kulia chakula cha hekalu?

6 Tobia alikuwa rafiki wa karibu wa Eliashibu. Tobia na mwana wake Yehohanani walioa wanawake Wayahudi, na Wayahudi wengi walimusifu sana Tobia. (Neh. 6:17-19) Mumoja wa wajukuu wa Eliashibu alioa binti wa Sanbalati, aliyekuwa gavana wa Samaria, ambaye alikuwa mumoja wa marafiki wa karibu wa Tobia. (Neh. 13:28) Uhusiano huo unaweza kutusaidia kuelewa kwa nini Kuhani Mukubwa Eliashibu alijiacha achochewe na mutu asiyeamini na mupinzani kama huyo. Lakini Nehemia alionyesha ushikamanifu kwa Yehova kwa kutupa inje vitu vyote vya Tobia.

7. Namna gani wazee na watumishi wengine wa Yehova wanaepukamambo yanayoweza kuwachafua?

7 Kwa kuwa sisi ni watu waliojitoa kwa Mungu, siku zote tunapaswa kwanza kuwa washikamanifu kwa Yehova. Tusiposhika kanuni zake za haki, hatuwezi kubaki watakatifu mbele yake. Tusiache uhusiano wa familia utufanye tuzarau kanuni za Biblia. Wazee Wakristo pia wanaongozwa na mawazo ya Yehova, wala si maoni ao mapendezi yao wenyewe. (1 Tim. 5:21) Wazee wanapaswa kuwa waangalifu ili kuepuka jambo lolote linaloweza kuwafanya wakose uaminifu kwa Mungu.​—1 Tim. 2:8.

8. Ni jambo gani ambalo watumishi wote wa Yehova waliojitoa kwake wanapaswa kukumbuka kuhusiana na marafiki wao?

8 Ni vizuri tukumbuke kwamba ‘mashirika mabaya yanaharibu tabia nzuri.’ (1 Kor. 15:33) Labda watu fulani wa jamaa yetu hawatatuchochea kufanya mambo mazuri katika maisha yetu. Eliashibu alikuwa mufano muzuri kwa Wayahudi kwa kumuunga kabisa Nehemia mukono katika kazi ya kujenga upya kuta za Yerusalemu. (Neh. 3:1) Lakini, inaonekana kwamba baadaye, Tobia na wengine walimuchochea Eliashibu kufanya mambo machafu mbele za Yehova. Marafiki wazuri wanatutia moyo tufuatie miradi ya kiroho, kama vile kusoma Biblia, kukusanyika, na kuhubiri. Tunawapenda na kuwasamini sana washiriki wa familia yetu wanaotutia moyo kufanya mambo mazuri.

KUUNGA MUKONO MIPANGO YA KITEOKRASI

9. Sababu gani Walawi hawakutimiza migawo yao, na Nehemia alilaumu nani?

9 Soma Nehemia 13:10-13. Inaonekana kwamba michango kwa ajili ya hekalu ilikuwa haifanyike tena wakati Nehemia alirudi Yerusalemu. Kwa kuwa michango hiyo iliyokuwa ikitegemeza Walawi haikutolewa tena, Walawi waliacha migawo yao na kuenda kutumika katika mashamba yao. Nehemia aliwalaumu watawala wasaidizi kwa sababu ya hali hiyo. Inaonekana kwamba hawakufanya kazi yao kama ilivyostahili. Labda hawakukusanya sehemu za kumi kutoka kwa watu ao hawakuzipeleka kwenye hekalu kama walivyoombwa kufanya. (Neh. 12:44) Kwa hiyo, Nehemia alifanya mipango ili sehemu za kumi zikusanywe. Alichagua wanaume wenye kutumainika ili wasimamie depo za hekalu na ugawaji wa sehemu za kumi.

10, 11. Watu wa Mungu wana pendeleo gani wanapotegemeza ibada ya kweli?

10 Je, hali hiyo inatufundisha somo fulani? Ndiyo, Biblia inatukumbusha kwamba tuna pendeleo la kumuheshimu Yehova kwa vitu vyetu vyenye samani. (Met. 3:9) Tunapotoa michango ili kutegemeza kazi ya Yehova, tunamutolea tu Yehova vitu vyake. (1 Nya. 29:14-16) Tunaweza kuwaza kama hatuna kitu cha kumutolea Yehova, lakini ikiwa tuna nia, sisi wote tunaweza kutoa.​—2 Kor. 8:12.

11 Kwa miaka mingi, familia moja ya watu wengi ilialika mara moja kila juma ndugu mumoja na bibi yake wenye kuzeeka, waliokuwa mapainia wa pekee, ili kutumia chakula pamoja nao. Hata ikiwa familia hiyo ilikuwa na watoto munane, mama alikuwa akisema hivi: “Sahani mbili ya zaidi ni nini?” Labda familia hiyo iliona kuwatolea mapainia hao chakula mara moja kwa juma kuwa jambo ndogo, lakini mapainia hao walishukuru sana familia hiyo kwa kuwaonyesha ukaribishaji! Nao walikuwa baraka kwa familia iliyowakaribisha. Maneno yao yenye kutia moyo na kuzungumuzia mambo waliojionea kulisaidia watoto katika familia hiyo wajiwekee miradi ya kiroho. Baadaye, watoto wote katika familia hiyo walianza utumishi wa wakati wote.

12. Ni mufano gani muzuri ambao wanaume wenye madaraka wanatuwekea katika kutaniko?

12 Jambo lingine tunalojifunza ni hili: Kama Nehemia, wanaume walio na madaraka leo wanapaswa kuwa wa kwanza katika kutegemeza mipango ya kiteokrasi. Wengine katika kutaniko wanafuata mufano wao. Kwa kufanya hivyo, wazee pia wanafuata mufano wa mutume Paulo. Yeye alitegemeza ibada ya kweli na alitoa muongozo unaofaa. Kwa mufano, alitoa maagizo yanayofaa kuhusu namna ya kutoa michango.​—1 Kor. 16:1-3; 2 Kor. 9:5-7.

KUTIA MAMBO YA KIROHO PA NAFASI YA KWANZA

13. Namna gani Wayahudi fulani hawakuwa wakiheshimu Sabato?

13 Soma Nehemia 13:15-21. Ikiwa tunahangaikia sana vitu vya kimwili, hali yetu ya kiroho inaweza kuwa zaifu pole kwa pole. Kulingana na Kutoka 31:13, Sabato ya kila juma ilikuwa ikiwakumbusha Waisraeli kwamba walikuwa watu waliotakaswa. Siku ya Sabato ilipaswa kutumiwa kwa ajili ya ibada ya familia, sala, na kutafakari Sheria ya Mungu. Lakini, kwa watu fulani wa siku za Nehemia, siku ya Sabato ilikuwa imegeuka kuwa siku ya kufanya kazi kama tu siku zingine. Walipuuza kabisa ibada ya Yehova. Alipoona hivyo, Nehemia aliamuru milango ya muji ifungwe mangaribi siku ya sita, na alifukuza wafanya-biashara wageni mbele ya Sabato kuanza.

14, 15. (a) Tunaweza kupatwa na nini ikiwa tunahangaikia sana mambo ya biashara? (b) Namna gani tunaweza kuingia katika pumuziko la Mungu?

14 Mufano wa Nehemia unatufundisha nini? Tunajifunza kwamba hatupaswe kutia mambo ya biashara pa nafasi ya kwanza. Tukifanya hivyo, tunaweza kukengeushwa kwa urahisi—ao hata tunaweza kuwa na moyo wenye kugawanyika​—zaidi sana ikiwa tunapenda kazi yetu ya kimwili kupita kiasi. Kumbuka shauri la Yesu kuhusu kutumikia mabwana wawili. (Soma Mathayo 6:24.) Nehemia alikuwa na mali, lakini namna gani alitumia wakati wake huko Yerusalemu? (Neh. 5:14-18) Kuliko kufuatia mambo ya biashara na Watiro ao watu wengine, Nehemia alijitoa ili kusaidia ndugu zake na alifanya mambo yaliyosaidia kutakasa jina la Yehova. Leo pia, wazee na watumishi wa huduma wanahangaikia sana mambo yanayoweza kufaidi kutaniko; kwa hiyo ndugu na dada wanawapenda kwa sababu ya roho wanayoonyesha. Hilo linafanya kuwe upendo, amani, na usalama kati ya watu wa Mungu.​—Eze. 34:25, 28.

15 Hata ikiwa Wakristo hawaombwe kushika Sabato ya kila juma, mutume Paulo anatuambia kwamba ‘bado limebaki pumuziko la sabato kwa ajili ya watu wa Mungu.’ Aliongeza hivi: ‘Mutu ambaye ameingia katika pumuziko la Mungu yeye mwenyewe pia amepumuzika kutokana na kazi zake mwenyewe.’ (Ebr. 4:9, 10) Sisi Wakristo, tunaweza kuingia katika pumuziko la Mungu kwa kutenda kwa unyenyekevu kulingana na kusudi lake. Je, wewe na washiriki wa familia yako munatia ibada ya familia, kuhuzuria mikutano, na kazi ya kuhubiri pa nafasi ya kwanza katika maisha yenu? Tunapaswa kuazimia kuheshimu programe zetu za kiroho wakati mukubwa wetu wa kazi ao wale tunaofanya nao biashara wanatafuta kuzivuruga. Kufanya hivyo ni kama vile ‘kufunga milango ya muji na kufukuza Watiro’ ili kuhangaikia vizuri mambo matakatifu na kuyatia pa nafasi ya kwanza. Kwa kuwa tumetakaswa, ni vizuri tujiulize hivi: ‘Je, maisha yangu yanaonyesha kwamba nimewekwa kando kwa ajili ya kazi ya Yehova?’​—Mt. 6:33.

KULINDA UTAMBULISHO WAKO WA KIKRISTO

16. Namna gani Waisraeli walikuwa karibu kupoteza pendeleo lao la kuwa watu wa Mungu waliotakaswa katika siku za Nehemia?

16 Soma Nehemia 13:23-27. Katika siku za Nehemia, wanaume Waisraeli walioa wanawake wageni. Alipokuja mara ya kwanza Yerusalemu, Nehemia alilazimisha wanaume wazee wote watie sinyatire kwenye kikaratasi kinachohakikisha kwamba hawataoa wanawake wapagani. (Neh. 9:38; 10:30) Lakini, miaka michache baadaye, alitambua kwamba wanaume hao Wayahudi walijichukulia wanawake wageni na walikuwa karibu kupoteza pendeleo lao la kuwa watu wa Mungu waliotakaswa! Watoto wa wanawake hao wageni hawakujua kusoma wala kuzungumuza Kiebrania. Walipokomaa, je, wangeweza kusema kwamba wao ni Waisraeli? Ao kwamba wao ni Waashdodi, Waamoni, ao Wamoabu? Kwa kuwa hawakujua Kiebrania, je, wangeweza kuelewa Sheria ya Mungu? Namna gani wangefikia kumujua Yehova na kuamua kumutumikia kuliko kutumikia miungu ya uongo ambayo mama zao walikuwa wakiabudu? Iliomba kuchukua hatua bila kuchelewa ili kutengeneza mambo, na Nehemia alifanya hivyo.​—Neh. 13:28.

Wasaidie watoto wako wawe na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova (Ona fungu la 17, 18)

17. Namna gani wazazi wanaweza kuwasaidia watoto wao wawe na uhusiano wa pekee pamoja na Yehova?

17 Leo, tunapaswa kuchukua hatua ili kusaidia watoto wetu wapate utambulisho wa Kikristo. Wazazi, mujiulize hivi: “Je, watoto wangu wanazungumuza vizuri ‘luga safi’ ya kweli za Biblia? (Zef. 3:9) Je, mazungumuzo ya watoto wangu yanaonyesha kwamba wanaongozwa na roho ya Mungu ao roho ya ulimwengu?” Usivunjike moyo haraka ikiwa unatambua kwamba watoto wako wanahitaji kufanya mabadiliko fulani. Inachukua wakati ili kujifunza luga fulani, zaidi sana ikiwa tunazungukwa na mambo yanayoweza kutukengeusha. Watoto wako wanapambana na hali ngumu zinazoweza kuwachochea wapoteze utambulisho wao wa Kikristo. Kwa hiyo, mutumie vipindi vya Ibada ya Familia na nafasi zingine ili kuwasaidia kwa uvumilivu watoto wenu wawe na uhusiano muzuri pamoja na Yehova. (Kum. 6:6-9) Muwaonyeshe faida za kuwa tofauti na ulimwengu wa Shetani. (Yoh. 17:15-17) Na mujikaze kugusa mioyo yao.

18. Sababu gani wazazi Wakristo ndio wanastahili kuwasaidia watoto wao wajitoe kwa Yehova?

18 Mwishowe, kila mutoto ataamua mwenyewe ikiwa atamutumikia Mungu ao hapana. Lakini, kuna mambo mengi ambayo wazazi wanaweza kufanya. Mambo hayo yanatia ndani kuwawekea watoto mufano muzuri, kuwatilia mipaka iliyo wazi, na kuzungumuza nao kuhusu matokeo ya maamuzi yao. Wazazi, ni ninyi tu munaostahili kuwasaidia watoto wenu wajitoe kwa Yehova. Wanahitaji musaada wenu ili wapate na kulinda utambulisho wao wa Kikristo. Bila shaka, sisi wote tunahitaji kuwa waangalifu ili tusipoteze ‘mavazi [yetu] ya inje,’ ni kusema, sifa na kanuni zinazotutambulisha kuwa wafuasi wa Kristo.​—Ufu. 3:4, 5; 16:15

KUKUMBUKWA “KWA AJILI YA WEMA”

19, 20. Namna gani tunaweza kukumbukwa na Yehova “kwa ajili ya wema”?

19 Nabii Malaki, aliyeishi katika siku za Nehemia, alionyesha kwamba ‘kitabu cha kumbukumbu kilianza kuandikwa kwa ajili ya wale wenye kumuogopa Yehova na kwa ajili ya wale wanaolifikiria jina lake.’ (Mal. 3:16, 17) Mungu hatawasahau hata kidogo wale wanaomuogopa na kumuheshimu na wanaolipenda jina lake.​—Ebr. 6:10.

20 Nehemia alisali hivi: “Unikumbuke kwa ajili ya wema, Ee Mungu wangu.” (Neh. 13:31) Kama Nehemia, majina yetu yataandikwa katika kitabu cha kumbukumbu cha Mungu ikiwa tutaendelea kuepuka marafiki wabaya, ikiwa tutategemeza mipango ya kiteokrasi, ikiwa tutatia mambo ya kiroho pa nafasi ya kwanza, na kulinda utambulisho wetu wa Kikristo. Acheni ‘tuendelee kujijaribu ikiwa tuko katika imani.’ (2 Kor. 13:5) Ikiwa tutaendelea kuchunga uhusiano wetu mutakatifu pamoja na Yehova, atatukumbuka “kwa ajili ya wema.”