Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova ‘Hunibebea Mzigo Wangu Kila Siku’

Yehova ‘Hunibebea Mzigo Wangu Kila Siku’

Ingawa afya yangu ni mbaya na ilionekana si rahisi kuvumilia, nimetegemezwa kwa upendo na Baba yetu mpendwa wa mbinguni maishani. Na kwa zaidi ya miaka 20 iliyopita nimepata shangwe ya pekee ya kumtumikia Yehova nikiwa painia.

Nilizaliwa mwaka wa 1956 nikiwa na ugonjwa wa spina bifida unaosababishwa na kutoziba kabisa kwa mrija wa neva katika uti wa mgongo. Tatizo hilo la neva limefanya iwe vigumu kwangu kutembea na limesababisha matatizo mengine makubwa ya afya.

Muda fulani kabla sijazaliwa, wazazi wangu walianza kufundishwa Biblia na wamishonari ambao ni Mashahidi wa Yehova. Nilipokuwa mtoto, kulikuwa na wahubiri wachache tu walioishi sehemu mbalimbali katika mji wetu wa Usakos, Namibia. Kwa hiyo, tulizungumzia habari za mikutano tukiwa familia. Nilipokuwa na umri wa miaka saba, nilifanyiwa upasuaji na kuwekewa mrija wa kupitishia mkojo. Nilipokuwa na umri wa miaka 14, niliugua kifafa. Kwa kuwa shule ya sekondari ilikuwa mbali sana na nilihitaji kutunzwa kwa njia ya pekee na wazazi wangu, singeweza kumaliza masomo yangu katika shule hiyo.

Hata hivyo, niliamua kujiimarisha kiroho. Wakati huo, machapisho yetu mengi ya Kikristo hayakupatikana katika lugha yetu ya Kiafrikana. Kwa hiyo, nilijifunza kusoma Kiingereza ili nijifunze vitabu vyetu vingi. Nikawa mhubiri wa Ufalme na kubatizwa nikiwa na umri wa miaka 19. Kwa miaka minne iliyofuata, nilipatwa na matatizo mengi ya kiafya na ya kihisia. Zaidi ya hayo, nilishindwa kushiriki kwa bidii katika huduma kwa sababu ya kuhofu wanadamu na ushirikiano wa karibu sana wa jamii yetu.

Nilipokuwa na umri wa miaka 20 hivi, tulihama Namibia na kwenda Afrika Kusini, na niliweza kushirikiana na kutaniko kwa mara ya kwanza nikiwa huko. Hilo lilikuwa jambo bora kama nini! Hata hivyo, nilihitaji kufanyiwa upasuaji mwingine, wakati huu niliwekewa utumbo mpana wa bandia.

Wakati fulani baadaye, nilimsikia mwangalizi wa mzunguko akizungumzia upainia. Maneno yake yaligusa moyo wangu. Nilijua kwamba afya yangu haikuwa nzuri, lakini nilijionea jinsi Yehova alivyonisaidia kupambana na matatizo mengi. Hivyo, niliomba kuwa painia wa kawaida. Hata hivyo, wazee walisita kukubali ombi langu kwa sababu ya matatizo yangu ya kiafya.

Hata hivyo, niliamua kufanya yote niwezayo katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme. Kwa msaada wa mama yangu na wengine, nilifaulu kutimiza saa za painia katika huduma kwa zaidi ya miezi sita. Hilo lilithibitisha azimio langu la kufanya upainia na kuonyesha kwamba matatizo yangu ya kiafya si kikwazo. Nilijaza tena ombi, wakati huu likakubaliwa. Hivyo, nikawa painia wa kawaida Septemba 1, 1988.

Nikiwa painia, Yehova amenitegemeza daima. Kuwafundisha wapya kweli badala ya kukazia fikira hali zangu kumenilinda, kumeniimarisha, na kunisaidia kukua kiroho. Nimepata shangwe kubwa sana kwa kuwasaidia watu kadhaa kufikia wakfu na ubatizo.

Afya yangu bado inanisumbua. Lakini Yehova ‘hunibebea mzigo wangu kila siku.’ (Zab. 68:19) Anafanya mengi zaidi mbali na kunisaidia kuvumilia; ananifanya nifurahie kuwa hai!