Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vikumbusho vya Yehova Ni Vyenye Kutegemeka

Vikumbusho vya Yehova Ni Vyenye Kutegemeka

“Kikumbusho cha Yehova ni chenye kutegemeka, humfanya asiye na uzoefu awe na hekima.”ZAB. 19:7..

1. Ni habari gani zinazozungumziwa kwa ukawaida na watu wa Mungu, na tunafaidikaje kwa kuzirudia?

UNAPOTAYARISHA makala ya Funzo la Mnara wa Mlinzi, huenda umewahi kusema hivi: ‘Nafikiri tumewahi kujifunza habari hii.’ Ikiwa umeshirikiana na kutaniko la Kikristo kwa muda fulani, inaelekea umeona kwamba baadhi ya habari huzungumziwa tena na tena. Kujifunza kuhusu Ufalme wa Mungu, fidia, kazi ya kufanya wanafunzi na sifa kama vile upendo na imani ni sehemu ya kawaida ya chakula chetu cha kiroho. Kurudia mambo hayo kunatusaidia kuendelea kuwa wenye afya katika imani na ‘kuwa watendaji wa neno, na si wasikiaji tu.’Yak. 1:22.

2. (a) Mara nyingi vikumbusho vya Mungu hurejelea nini? (b) Vikumbusho vya Mungu vinatofautianaje na vya wanadamu?

2 Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “kikumbusho,” mara nyingi hurejelea sheria, amri, na masharti ambayo Mungu huwapa watu wake. Masharti na sheria za Yehova zinategemeka sikuzote, tofauti na sheria za wanadamu ambazo mara nyingi zinahitaji kurekebishwa au kusahihishwa. Ingawa baadhi ya sheria hizo hutolewa kwa ajili ya wakati au hali fulani hususa, ni kamilifu na haziwezi kamwe kuwa na kasoro yoyote. Mtunga-zaburi alisema hivi: “Uadilifu wa vikumbusho vyako ni wa mpaka wakati usio na kipimo.”Zab. 119:144.

3, 4. (a) Vikumbusho vya Yehova huenda vikatia ndani nini? (b) Waisraeli wangefaidikaje kwa kuvitii?

3 Huenda umeona kwamba nyakati nyingine vikumbusho vya Yehova vinatia ndani maonyo. Taifa la Israeli lilipokea kwa ukawaida maonyo kupitia manabii wa Mungu. Kwa mfano, muda mfupi kabla ya Waisraeli kuingia katika Nchi ya Ahadi, Musa aliwaonya hivi: “Jiangalieni mioyo yenu isije ikashawishiwa,  nanyi mgeuke kando na kuabudu miungu mingine na kuiinamia, na hasira ya Yehova iwake juu yenu.” (Kum. 11:16, 17) Biblia inaonyesha kwamba Mungu aliwapa watu wake vikumbusho vingi vilivyowasaidia.

4 Katika pindi nyingine nyingi, Yehova aliwahimiza Waisraeli wamwogope, waisikilize sauti yake, na kulitakasa jina lake. (Kum. 4:29-31; 5:28, 29) Bila shaka wangepokea baraka nyingi ikiwa wangetii vikumbusho hivyo.Law. 26:3-6; Kum. 28:1-4.

JINSI WAISRAELI WALIVYOITIKIA VIKUMBUSHO VYA MUNGU

5. Kwa nini Yehova alimpigania Mfalme Hezekia?

5 Katika historia yote yenye msukosuko ya taifa la Israeli, Mungu alitimiza ahadi yake. Kwa mfano, Mfalme Senakeribu wa Ashuru alipovamia Yuda na kutishia kumpindua Mfalme Hezekia, Yehova aliingilia kati kwa kumtuma malaika. Kwa usiku mmoja tu, malaika wa Mungu aliangamiza ‘kila shujaa na mwanamume mwenye nguvu’ wa jeshi la Ashuru hivi kwamba Senakeribu akalazimika kurudi nyumbani akiwa ameaibika. (2 Nya. 32:21; 2 Fal. 19:35) Kwa nini Mungu alimpigania Mfalme Hezekia? Kwa sababu ‘Hezekia aliendelea kushikamana na Yehova. Hakugeuka kando na kuacha kumfuata, bali aliendelea kuzishika amri zake.’2 Fal. 18:1, 5, 6.

Vikumbusho vya Yehova vilimchochea Yosia kutetea ibada ya kweli (Tazama fungu la 6)

6. Mfalme Yosia alimtegemeaje Yehova?

6 Mfalme Yosia aliweka pia mfano katika kutii amri za Yehova. Tangu alipokuwa na umri wa miaka minane, ‘alifanya yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova. Hakugeuka kando upande wa kuume wala wa kushoto.’ (2 Nya. 34:1, 2) Yosia alionyesha kwamba anamtegemea Yehova kwa kuondoa sanamu zote na kurudisha ibada ya kweli. Yosia alibarikiwa alipofanya hivyo na taifa zima pia.Soma 2 Mambo ya Nyakati 34:31-33.

7. Waisraeli walipatwa na nini walipopuuza vikumbusho vya Yehova?

7 Hata hivyo, inasikitisha kwamba watu wa Mungu hawakuendelea kuvitegemea kikamili vikumbusho vya Yehova. Kwa karne nyingi, hawakumtii kikamili. Imani yao ilipopungua walianza “kuchukuliwa huku na huku na kila upepo wa fundisho,” kama mtume Paulo alivyotaja. (Efe. 4:13, 14) Na kama ilivyotabiriwa, walipokosa kutegemea vikumbusho vya Mungu, walipatwa na matokeo mabaya sana.Law. 26:23-25; Yer. 5:23-25.

8. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Waisraeli?

8 Tunajifunza nini kutokana na mfano  wa Waisraeli? Leo, watumishi wa Mungu wanashauriwa na kutiwa nidhamu kama Waisraeli. (2 Pet. 1:12) Neno la Mungu lililoongozwa na roho linaweza kuwa kikumbusho kila mara tunapolisoma. Kwa kuwa tuna uhuru wa kuchagua, tunaweza kuamua kutii miongozo ya Yehova au kufuatilia kinachoonekana kuwa sawa machoni petu. (Met. 14:12) Acheni tuchunguze baadhi ya sababu zinazoonyesha kwa nini tunapaswa kutegemea vikumbusho vya Yehova na jinsi tunavyonufaika tunapovitii.

JITIISHE KWA MUNGU ILI UISHI

9. Yehova aliwahakikishiaje Waisraeli kwamba alikuwa akiwategemeza nyikani?

9 Waisraeli walipoanza safari iliyowachukua miaka 40 katika ‘nyika yenye kutia woga,’ Yehova hakuwaambia waziwazi jinsi ambavyo angewaongoza, angewalinda, na kuwatunza. Hata hivyo, aliwathibitishia tena na tena kwamba wangeweza kumtegemea na kutegemea maagizo yake. Akitumia nguzo ya wingu mchana na nguzo ya moto usiku, Yehova aliwakumbusha Waisraeli kwamba alikuwa akiwategemeza alipowaongoza nyikani. (Kum. 1:19; Kut. 40:36-38) Aliwaandalia pia mahitaji yao ya msingi. “Mavazi yao hayakuchakaa, wala miguu yao haikuvimba.” Kwa kweli, “hawakukosa chochote.”Neh. 9:19-21.

10. Yehova anawaongoza watu wake jinsi gani leo?

10 Leo, watumishi wa Mungu wako karibu sana kuingia katika ulimwengu mpya wenye uadilifu. Je, tunaamini kwamba Yehova atatuandalia tunachohitaji ili kuokoka “dhiki kuu” inayokuja? (Mt. 24:21, 22; Zab. 119:40, 41) Ni kweli kwamba Yehova hatumii nguzo ya wingu au ya moto kutuongoza kuingia katika ulimwengu mpya. Lakini anatumia tengenezo lake kutusaidia kuendelea kukesha. Kwa mfano, tunahimizwa sana tuimarishe hali yetu ya kiroho kwa kusoma Biblia kibinafsi, kuwa na jioni ya Ibada ya Familia, na pia kuhubiri na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. Je, tumefanya marekebisho ili kufuata miongozo hiyo? Tukifanya hivyo tutajenga imani itakayotusaidia kuokoka na kuingia katika ulimwengu mpya.

Kutii vikumbusho vya Yehova hutusaidia kulitunza ifaavyo Jumba la Ufalme (Tazama fungu la 11)

11. Mungu anaonyesha kwa njia gani kwamba anatujali?

11 Mbali na kutusaidia kuendelea kukesha kiroho, maagizo tunayopokea yanatusaidia katika maisha yetu ya kila siku. Kwa mfano, yanatusaidia kuendelea kuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu vitu vya kimwili na kuendelea kuwa na jicho rahisi ili kupunguza mahangaiko. Tumepokea pia mwongozo ambao umetusaidia kuhusu mavazi na mapambo, kuchagua burudani inayofaa, na kuamua kiwango cha elimu kinachofaa. Fikiria pia vikumbusho tulivyopokea kuhusu kudumisha usalama katika Jumba la Ufalme, nyumbani, magari yetu, na kuwa tayari kwa ajili ya hali za dharura. Mashauri hayo yanaonyesha kwamba Mungu anatujali.

VIKUMBUSHO VILIWASAIDIA WAKRISTO WA MAPEMA KUBAKI WAAMINIFU

12. (a) Yesu aliwakumbusha wanafunzi wake tena na tena kuhusu nini? (b) Petro alikumbuka kwa muda mrefu tendo gani la unyenyekevu, na linapaswa kutuchocheaje?

12 Katika karne ya kwanza, watu wa Mungu walipewa vikumbusho kwa ukawaida. Yesu aliwakumbusha wanafunzi wake tena na tena kwamba walihitaji kusitawisha unyenyekevu. Hata hivyo, hakuwaambia tu maana ya unyenyekevu, aliwaonyesha kwa matendo. Katika siku yake ya mwisho duniani, Yesu aliwakusanya mitume wake kwa ajili ya Pasaka. Mitume walipokuwa wakila, Yesu alisimama kutoka kwenye mlo na kuosha miguu  yao, kazi ambayo kwa kawaida ilifanywa na mtumishi. (Yoh. 13:1-17) Walikumbuka kwa muda mrefu tendo hilo la unyenyekevu. Miaka 30 hivi baadaye, mtume Petro aliyekuwa katika mlo huo, aliwashauri waamini wenzake kuhusu unyenyekevu. (1 Pet. 5:5) Mfano wa Yesu unapaswa kutuchochea sote kuwa wanyenyekevu tunaposhughulika na wengine.Flp. 2:5-8.

13. Yesu aliwakumbusha wanafunzi wake kwamba walihitaji kusitawisha sifa gani muhimu?

13 Yesu pia aliwakumbusha mara nyingi wanafunzi wake kwamba walihitaji kuwa na imani yenye nguvu. Baada ya wanafunzi kushindwa kumfukuza roho mwovu, walimuuliza Yesu hivi: “Kwa nini sisi hatukuweza kumfukuza?” Yesu akawajibu: “Ni kwa sababu ya imani yenu kidogo. Kwa maana kwa kweli ninawaambia, Mkiwa na imani inayotoshana na mbegu ya haradali, . . . hakuna jambo litakalowashinda.” (Mt. 17:14-20) Katika huduma yake yote, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kwamba imani ni sifa muhimu. (Soma Mathayo 21:18-22.) Je, tunahudhuria makusanyiko na mikutano ya Kikristo na kutumia mafundisho yanayoimarisha imani tunayopata? Hizo si pindi zinazoleta shangwe tu bali pia ni pindi za kuonyesha kwamba tunamtegemea Yehova.

14. Kwa nini ni muhimu leo kusitawisha upendo kama wa Kristo?

14 Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yana vikumbusho vingi vinavyotuhimiza tupendane. Yesu alisema kwamba amri ya pili iliyo kuu ni hii: “Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” (Mt. 22:39) Naye Yakobo, ndugu wa kambo wa Yesu, alisema kwamba upendo ni “sheria ya kifalme.” (Yak. 2:8) Mtume Yohana aliandika hivi: “Wapendwa, ninawaandikia ninyi, si amri mpya, bali amri ya zamani ambayo mmekuwa nayo tangu mwanzo.” (1 Yoh. 2:7, 8) Yohana alimaanisha nini alipotaja “amri ya zamani”? Alimaanisha amri ya kuwa na upendo. Amri hiyo ilikuwa ya “zamani” katika maana ya kwamba Yesu aliitoa miaka mingi iliyopita, yaani, “tangu mwanzo.” Hata hivyo, ilikuwa pia “mpya” katika maana ya kwamba walipaswa kuwa na upendo wa kujidhabihu, sifa ambayo huenda wangehitaji ili kukabiliana na hali mpya. Tukiwa wanafunzi wa Kristo, je, hatuthamini maonyo yanayotusaidia kujilinda ili tusisitawishe roho ya ubinafsi ya ulimwengu huu, inayoweza kutuzuia kuwapenda jirani zetu?

15. Ni kazi gani kuu aliyofanya Yesu duniani?

15 Yesu alipendezwa kibinafsi na watu. Tunaona hangaiko lake lenye upendo alipowaponya wagonjwa, walemavu, na kufufua  wafu. Hata hivyo, kazi kuu ya Yesu haikuwa kuponya watu kihalisi. Kazi yake ya kuhubiri na kufundisha ilibadili kabisa maisha ya watu. Jinsi gani? Tunajua kwamba watu walioponywa na kufufuliwa na Yesu katika karne ya kwanza walizeeka na kufa baadaye, lakini waliokubali ujumbe aliohubiri walipata tumaini la kuishi milele.Yoh. 11:25, 26.

16. Kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi inatimizwa kwa kadiri gani leo?

16 Kazi ya kuhubiri habari njema aliyoanzisha Yesu katika karne ya kwanza inatimizwa kwa kiwango kikubwa zaidi leo. Ndiyo, Yesu aliwaagiza hivi wanafunzi wake: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” (Mt. 28:19) Kwa kweli wamefanya hivyo, na tunaweza kusema kwamba tumefanya hivyo pia! Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni saba wanatangaza kwa bidii kuhusu Ufalme wa Mungu katika nchi zaidi ya 230, nao hujifunza Biblia kwa ukawaida na mamilioni ya watu. Kazi hii ya kuhubiri inathibitisha kwamba tunaishi katika siku za mwisho.

MTEGEMEE YEHOVA

17. Paulo na Petro walitoa mashauri gani?

17 Ni wazi kwamba vikumbusho viliwasaidia Wakristo wa mapema kubaki imara katika imani. Wazia jinsi Timotheo alivyotiwa moyo alipoambiwa hivi na mtume Paulo, aliyekuwa mfungwa huko Roma wakati huo: “Endelea kushika kielelezo cha maneno yenye afya uliyosikia kutoka kwangu.” (2 Tim. 1:13) Baada ya kuwatia moyo Wakristo wenzake wasitawishe sifa kama vile uvumilivu, upendo wa kindugu, na kujizuia, mtume Petro alisema hivi: “Sikuzote nitakuwa na mwelekeo wa kuwakumbusha ninyi kuhusu mambo haya, ijapokuwa mnayajua hayo na mmewekwa imara katika kweli.”2 Pet. 1:5-8, 12.

18. Wakristo wa karne ya kwanza walikuwa na maoni gani kuhusu vikumbusho?

18 Naam, barua ambazo Paulo na Petro waliandika zina “maneno yaliyosemwa hapo zamani na manabii watakatifu.” (2 Pet. 3:2) Je, ndugu zetu katika karne ya kwanza walikasirika waliposhauriwa? Hapana, kwa kuwa mashauri hayo yalithibitisha kwamba Mungu anawapenda na yaliwasaidia ‘kuendelea kukua katika fadhili zisizostahiliwa na ujuzi juu ya Bwana na Mwokozi wao Yesu Kristo.’2 Pet. 3:18.

19, 20. Kwa nini tunapaswa kutegemea vikumbusho vya Yehova, na tunanufaikaje kwa kufanya hivyo?

19 Leo, tuna sababu nyingi za kutegemea vikumbusho vya Yehova vinavyopatikana katika Neno lake linalotegemeka, yaani, Biblia. (Soma Yoshua 23:14.) Tunapoisoma tunaona jinsi Mungu alivyoshughulika na wanadamu wasio wakamilifu kwa maelfu ya miaka. Mambo hayo yaliandikwa kwa faida yetu. (Rom. 15:4; 1 Kor. 10:11) Tumejionea unabii wa Biblia ukitimia. Unabii unaweza kufananishwa na vikumbusho vinavyosemwa mapema. Kwa mfano, mamilioni wamemiminika katika ibada safi ya Yehova katika “siku za mwisho,” kama ilivyotabiriwa. (Isa. 2:2, 3) Hali zinazozidi kuzorota za ulimwengu zinatimiza pia unabii wa Biblia. Na kama tulivyotaja, kampeni kubwa ya kuhubiri inayoendelea ulimwenguni pote inatimiza moja kwa moja maneno ya Yesu.Mt. 24:14.

20 Muumba wetu ametuonyesha wazi kwamba tunaweza kumtegemea. Je, tunanufaika na jambo hilo? Tunahitaji kuamini vikumbusho vyake. Rosellen alifanya hivyo. Anasema hivi: “Nilipoanza kumtegemea Yehova kikamili, nilianza kuona vizuri zaidi mkono wake wenye upendo ukiniimarisha na kunitegemeza.” Acheni tunufaike kwa kuendelea kutii vikumbusho vya Yehova.