Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Vikumbusho vya Yehova Ni Vyenye Kutegemeka

Vikumbusho vya Yehova Ni Vyenye Kutegemeka

‘Kikumbusho cha Yehova ni chenye kutegemeka, kinamufanya asiye na uzoefu awe na hekima.’​—ZAB. 19:7.

1. Ni habari gani ambazo tunajifunza kwa ukawaida, na kuzirudilia kunatuletea faida gani?

 ‘MBONA tumekwisha kujifunza habari hii wakati uliopita?’ Labda umekwisha kujiuliza ulizo hilo ulipokuwa ukitayarisha habari ya kujifunza katika Munara wa Mulinzi. Ikiwa umekuwa katika kutaniko la Kikristo kwa muda fulani, labda umetambua kwamba habari fulani zinazungumuziwa mara kwa mara. Ufalme wa Mungu, zabihu ya ukombozi, kazi ya kufanya wanafunzi, na sifa mbalimbali kama vile upendo na imani ni habari tunazojifunza kwa ukawaida. Kurudilia habari hizo, kunatusaidia tuwe na imani yenye nguvu na ‘tuwe watendaji wa neno, na si wasikiaji tu.’​—Yak. 1:22.

2. (a) Mara nyingi neno “kikumbusho” linamaanisha nini? (b) Namna gani vikumbusho vya Mungu vinatofautiana na sheria za wanadamu?

2 Mara nyingi neno la Kiebrania linalotafsiriwa “kikumbusho” linamaanisha sheria, amri, na masharti ambayo Mungu anawatolea watu wake. Tofauti na sheria za wanadamu, ambazo kila mara zinahitaji kusahihishwa ao kubadilishwa, sheria na masharti ya Yehova ni yenye kutegemeka nyakati zote. Mungu anaweza kutoa sheria fulani kwa ajili ya kipindi ao hali fulani tu. Lakini hilo halimaanishe kwamba sheria hizo ni zenye makosa ao ni zenye kupungukiwa na kitu fulani. Mutunga​-zaburi alisema hivi: ‘Uadilifu wa vikumbusho vyako ni wa mupaka wakati usio na kipimo.’​—Zab. 119:144.

3, 4. (a) Vikumbusho vya Yehova vinaweza kutia ndani nini? (b) Waisraeli wangepata faida gani ikiwa wangetii vikumbusho hivyo?

3 Pengine umekwisha kutambua kwamba wakati fulani vikumbusho vya Yehova vilitia ndani ujumbe wa kuonya watu. Mara kwa mara Mungu alitolea taifa la Israeli maonyo kupitia manabii wake. Kwa mufano, muda kidogo mbele Waisraeli waingie katika Inchi ya Ahadi, Musa aliwaonya hivi: ‘Jiangalieni mioyo yenu isije ikashawishiwa, nanyi mugeuke kando na kuabudu miungu mingine na kuiinamia, na hasira ya Yehova iwake juu yenu.’ (Kum. 11:16, 17) Biblia inaonyesha kwamba Mungu aliwatolea watu wake vikumbusho vingi vya maana.

4 Nyakati nyingine, Yehova aliwasihi Waisraeli wamuogope, wasikilize sauti yake, na kulitakasa jina lake. (Kum. 4:29-31; 5:28, 29) Ikiwa wangetii vikumbusho hivyo, hakika wangepata baraka nyingi.​—Law. 26:3-6; Kum. 28:1-4.

WAISRAELI WALIITIKIA NAMNA GANI VIKUMBUSHO VYA MUNGU?

5. Sababu gani Yehova alimupigania Mufalme Hezekia?

5 Katika kipindi chote chenye kujaa misukosuko cha historia ya Waisraeli, Mungu hakukosa kutimiza ahadi yake. Kwa mufano, Mufalme wa Asiria Senakeribu alipoivamia Yuda na kuonyesha kwamba angepindua Ufalme wa Hezekia, Yehova alimusaidia kwa kumutuma malaika. Katika usiku mumoja tu, malaika wa Mungu aliangamiza ‘kila shujaa, mwanaume mwenye nguvu’ katika jeshi la Asiria, kwa hiyo, Senakeribu alirudi akiwa na haya. (2 Nya. 32:21; 2 Fal. 19:35) Sababu gani Mungu alimupigania Mufalme Hezekia? Alifanya hivyo kwa sababu ‘[Hezekia] aliendelea kushikamana na Yehova. Hakugeuka kando na kuacha kumufuata, bali aliendelea kuzishika amri zake ambazo Yehova alimuamuru.’​—2 Fal. 18:1, 5, 6.

Vikumbusho vya Yehova vilimuchochea Yosia kutetea ibada ya kweli (Ona fungu la 6)

6. Namna gani Mufalme Yosia alionyesha kwamba alimutumainia Yehova?

6 Mufano mwingine wa mutu ambaye alitii amri za Yehova ni Mufalme Yosia. Kuanzia umri mudogo wa miaka munane, ‘alifanya yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova . . . Hakugeuka kando upande wa kuume wala wa kushoto.’ (2 Nya. 34:1, 2) Yosia alionyesha kwamba anamutumainia Yehova kwa kuondoa ibada ya sanamu katika inchi na kurudisha ibada ya kweli. Kwa kufanya hivyo, Yosia alibarikiwa na aliletea taifa lote baraka.​—Soma 2 Mambo ya Nyakati 34:31-33.

7. Waisraeli walipozarau vikumbusho vya Yehova, walipatwa na nini?

7 Hata hivyo, jambo la kuhuzunisha ni kwamba, kila mara watu wa Mungu hawakutegemea kikamili vikumbusho vya Yehova. Wakati fulani walimutii Mungu na wakati mwingine hawakumutii. Imani yao ilipopunguka, ‘walirushwa huku na huku kama kwa mawimbi na kuchukuliwa huku na huku na kila upepo wa fundisho,’ kulingana na maneno ya mutume Paulo. (Efe. 4:13, 14) Na kama ilivyotabiriwa, wakati ambapo hawakutia tumaini lao katika vikumbusho vya Mungu, walipatwa na magumu.​—Law. 26:23-25; Yer. 5:23-25.

8. Mufano wa Waisraeli unatufundisha nini?

8 Tunaweza kujifunza nini kutokana na mufano wa Waisraeli? Kama wao, leo sisi pia tunapata mashauri na nizamu. (2 Pet. 1:12) Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake linaweza kuwa kikumbusho kwetu kila wakati ambapo tunalisoma. Kwa kuwa tuna uhuru wa kuchagua, tunaweza kuchagua ikiwa tutatii muongozo wa Yehova ao ikiwa tutafuatilia mambo yanayoonekana kuwa mazuri machoni petu. (Met. 14:12) Acheni tuzungumuzie sababu fulani zinazoweza kutufanya tutumainie vikumbusho vya Yehova na namna gani tunaweza kufaidika tunapotenda kulingana na vikumbusho hivyo.

UMUTII MUNGU ILI UOKOLEWE

9. Waisraeli walipokuwa katika jangwa, namna gani Yehova alionyesha kwamba alikuwa akiwaongoza?

9 Waisraeli walipoanza safari yao ya miaka 40 katika nyika [ao jangwa] “kubwa yenye kuogopesha,” Yehova hakuwatolea mafasirio fulani mbele ya wakati kuhusu namna ambavyo angewaongoza, kuwalinda, na kuwatunza. Hata hivyo, aliwaambia tena na tena kwamba walipaswa kumutegemea yeye na kufuata maagizo yake. Yehova alitumia nguzo ya wingu wakati wa muchana na nguzo ya moto wakati wa usiku ili kuwakumbusha Waisraeli kwamba alikuwa akiwategemeza muda wote aliokuwa akiwaongoza katika jangwa hiyo ya hatari. (Kum. 1:19; Kut. 40:36-38) Yehova aliwatimizia pia mahitaji yao ya lazima. “Mavazi yao hayakuchakaa, wala miguu yao haikuvimba.” Bila shaka, “hawakukosa chochote.”​—Neh. 9:19-21.

10. Namna gani Yehova anawaongoza watumishi wake leo?

10 Leo watumishi wa Mungu wanakaribia kuingia katika ulimwengu mupya wenye haki. Je, tunatumaini kwamba Yehova atatutolea yale tunayohitaji ili tuokoke ‘ziki kubwa’ inayokuja? (Mt. 24:21, 22; Zab. 119:40, 41) Ni kweli kwamba leo Yehova hatumie nguzo ya wingu ao nguzo ya moto ili kutuongoza katika ulimwengu mupya. Lakini anatumia tengenezo lake ili kutusaidia tubaki macho. Kwa mufano, tumekumbushwa mara kwa mara umaana wa kutia nguvu hali yetu ya kiroho kupitia usomaji wa Biblia, Ibada ya Familia ya mangaribi, na vilevile kwa kuhuzuria mikutano na kuhubiri kwa ukawaida. Je, umefanya mabadiliko ili ufuate maagizo hayo? Kufanya hivyo kutatuwezesha kuwa na imani ambayo itatusaidia tuokoke na kuingia katika ulimwengu mupya.

Kutumia vikumbusho vya Yehova kunatusaidia kulinda Jumba letu la Ufalme likiwa mahali salama na ambapo watu wanaweza kufika kwa urahisi (Ona fungu la 11)

11. Ni katika njia gani Mungu anaonyesha kwamba anatuhangaikia?

11 Zaidi ya kutusaidia tubaki macho kiroho, Yehova ametutolea maagizo yanayotusaidia katika shuguli zetu za kila siku. Maagizo hayo yanatia ndani kuwa na maoni yanayofaa kuhusu vitu vya kimwili na kuwa na jicho rahisi ili kupunguza mahangaiko. Pia, tumefaidika na maagizo yanayohusu kuvaa na kujipamba, kujiburudisha kwa njia inayofaa, na kuwa na maoni yanayofaa kuhusu elimu ya juu. Fikiria pia vikumbusho kuhusu namna ya kulinda usalama nyumbani, kwenye Jumba la Ufalme, tunapoendesha gari ao pikipiki, na namna ya kujitayarisha ili kupambana na hali zisizotazamiwa. Mashauri hayo yanaonyesha kwamba Mungu anahangaikia usalama wetu.

VIKUMBUSHO VILIWASAIDIA WAKRISTO WA KWANZA​-KWANZA KUBAKI WAAMINIFU

12. (a) Ni jambo gani ambalo Yesu alizungumuzia mara kwa mara na wanafunzi wake? (b) Ni tendo gani la unyenyekevu ambalo Petro hangesahau, na linatuchochea kufanya nini?

12 Watumishi wa Mungu wa wakati wa mitume walipata vikumbusho kwa ukawaida. Mara kwa mara, Yesu aliwakumbusha wanafunzi wake uhitaji wa kuonyesha unyenyekevu. Hata hivyo, zaidi ya kuwafasiria wanafunzi wake maana ya kuwa munyenyekevu, Yesu aliwaonyesha mufano. Usiku wa mwisho mbele ya kifo chake, Yesu aliwakusanya mitume wake kwa ajili ya Pasaka. Mitume wake walipokuwa wakila, Yesu aliacha kula na akaanza kunawisha mitume wake miguu​—tendo ambalo kwa kawaida lilifanywa na mutumwa. (Yoh. 13:1-17) Mitume hawangesahau hata kidogo tendo hilo la unyenyekevu. Miaka 30 hivi baadaye, mutume Petro, aliyekuwa hapo, aliwatolea waamini wenzake mashauri kuhusu unyenyekevu. (1 Pet. 5:5) Mufano wa Yesu unapaswa kuchochea kila mumoja wetu kuwa munyenyekevu katika uhusiano wake pamoja na wengine.​—Flp. 2:5-8.

13. Yesu aliwakumbusha wanafunzi wake uhitaji wa kuwa na sifa gani ya maana?

13 Kila mara Yesu alizungumuza pia na wanafunzi wake kuhusu uhitaji wa kuwa na imani yenye nguvu. Kisha kushindwa kumufukuza roho muovu aliyekuwa katika kijana fulani, wanafunzi wake walimuuliza hivi: ‘Kwa nini sisi hatukuweza kumufukuza?’ Yesu aliwajibu: ‘Ni kwa sababu ya imani yenu kidogo, kwa maana kwa kweli ninawaambia, mukiwa na imani inayotoshana na mbegu ya haradali, . . . hakuna jambo litakalowashinda.’ (Mt. 17:14-20) Muda wote wa huduma yake, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kwamba imani ni sifa ya lazima. (Soma Mathayo 21:18-22.) Je, tunafaidika na nafasi tulizonazo ili kutia imani yetu nguvu kupitia mafundisho yenye kujenga tunayopata kwenye mikusanyiko, na mikutano ya Kikristo? Mikusanyiko na mikutano yetu si vipindi vinavyotuletea furaha tu; lakini inatutolea pia nafasi ya kuonyesha kwamba tunamutumaini Yehova.

14. Sababu gani ni jambo la lazima tuonyeshe upendo kama ule wa Kristo leo?

14 Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanajaa vikumbusho kuhusu umaana wa kuonyeshana upendo. Yesu alisema kwamba amri ya pili iliyo kubwa zaidi ni ‘kumupenda jirani yako kama wewe mwenyewe.’ (Mt. 22:39) Vivyo hivyo, Yakobo, ndugu​-nusu ya Yesu, aliuita upendo “sheria ya kifalme.” (Yak. 2:8) Mutume Yohana aliandika hivi: ‘Wapendwa, ninawaandikia ninyi, si amri mupya, bali amri ya zamani ambayo mumekuwa nayo tangu mwanzo.’ (1 Yoh. 2:7, 8) Yohana alikuwa akizungumuzia nini alipotumia maneno “amri ya zamani”? Alikuwa akizungumuzia amri hiyo ya upendo. Amri hiyo ilikuwa “ya zamani” katika maana ya kwamba Yesu alikuwa ameitoa “kutoka mwanzoni,” ni kusema, miaka mingi hapo mbele. Lakini pia amri hiyo ilikuwa ‘mupya’ katika maana ya kwamba wanafunzi walipaswa kuwa tayari kuwapenda wengine na hata kufikia kufa kwa ajili yao. Wanafunzi walipaswa kuonyesha roho hiyo ili kupambana na hali ambazo zingetokea baadaye. Kwa kuwa sisi ni wanafunzi wa Kristo, je, tunasamini mashauri yanayotusaidia tuepuke roho ya kujipenda wenyewe ambayo watu wengi katika ulimwengu wanaonyesha, na ambayo inaweza kupunguza upendo wetu kwa jirani?

15. Ni nini iliyokuwa kazi kubwa ya Yesu duniani?

15 Yesu aliwahangaikia sana watu. Tunaona namna alivyowahangaikia watu kwa upendo alipowaponyesha wagonjwa na walemavu na alipofufua wafu. Hata hivyo, kazi kubwa ya Yesu haikuwa kuponyesha watu kimwili. Kazi yake ya kuhubiri na kufundisha iliwaletea watu faida nyingi na zenye kudumu. Sababu gani tunasema hivyo? Kwa mufano, tunajua kwamba, wale ambao Yesu aliponyesha na kufufua wakati wa mitume, walizeeka na kufa baadaye, lakini wale waliosikiliza ujumbe wake walipata tumaini la uzima wa milele.​—Yoh. 11:25, 26.

16. Ni nini inayoonyesha kwamba kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi inafanywa kwa njia kubwa sana leo?

16 Kazi ya kuhubiri ambayo Yesu alianzisha wakati wa mitume inafanywa kwa njia kubwa sana leo. Yesu aliwapa wanafunzi wake amri hii: ‘Kwa hiyo nendeni mukafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ (Mt. 28:19) Kwa kweli walifanya hivyo, sisi pia tunaweza kusema kwamba tunafanya hivyo! Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni saba wanatangaza Ufalme wa Mungu kwa bidii katika inchi zaidi ya 230, na wanafundisha mamilioni ya watu Biblia kwa ukawaida. Kazi hiyo ya kuhubiri inaonyesha kwamba tunaishi katika siku za mwisho.

ENDELEA KUMUTUMAINIA YEHOVA

17. Ni mashauri gani ambayo mutume Paulo na Petro walitoa?

17 Bila shaka, vikumbusho vilisaidia Wakristo wa kwanza-kwanza kuendelea kuwa na imani yenye nguvu. Fikiria namna Timotheo alivyotiwa moyo mutume Paulo, aliyekuwa mufungwa huko Roma wakati huo, alipomuambia hivi: “Endelea kushika kielelezo cha maneno yenye afya aliyosikia kutoka kwangu.” (2 Tim. 1:13) Kisha kuwatia moyo Wakristo wasitawishe sifa kama vile uvumilivu, upendo wa kindugu, na kujizuia, mutume Petro aliongeza hivi: ‘Nitakuwa na mwelekeo wa kuwakumbusha ninyi kuhusu mambo haya, ijapokuwa munayajua hayo na mumewekwa imara katika kweli.’​—2 Pet. 1:5-8, 12.

18. Wakristo wa kwanza​-kwanza walikuwa na maoni gani kuhusu vikumbusho walivyopokea?

18 Bila shaka, barua ambazo Paulo na Petro waliandika zilikuwa na “maneno yaliyosemwa hapo zamani na manabii watakatifu.” (2 Pet. 3:2) Je, ndugu zetu wa wakati wa mitume walinungunika kisha kupokea muongozo huo? Hapana, kwa kuwa muongozo huo ulionyesha kwamba Mungu aliwapenda, na uliwasaidia ‘waendelee kukua katika fazili zisizostahiliwa na ujuzi juu ya Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo.’​—2 Pet. 3:18.

19, 20. Sababu gani tunapaswa kutegemea vikumbusho vya Yehova, na namna gani tunafaidika kwa kufanya hivyo?

19 Leo, tuna sababu nyingi za kutegemea vikumbusho vya Yehova vinavyopatikana katika Neno lake linalosema kweli siku zote, Biblia. (Soma Yoshua 23:14.) Biblia inasimulia namna Mungu alivyoshugulika na wanadamu wasio wakamilifu kwa muda wa miaka mingi. Masimulizi hayo yaliandikwa kwa faida yetu. (Rom. 15:4; 1 Kor. 10:11) Tumejionea utimizo mbalimbali wa unabii wa Biblia. Unabii unaweza kufananishwa na vikumbusho vilivyotolewa mbele ya wakati. Kwa mufano, mamilioni ya watu wamekuja kwenye ibada safi ya Yehova. Unabii ulionyesha kwamba hilo lingetokea “katika siku za mwisho.” (Isa. 2:2, 3) Hali za ulimwengu zinazoendelea kuharibika zinatimiza pia unabii wa Biblia. Zaidi ya hilo, kampanye kubwa ya kuhubiri inayofanywa leo ulimwenguni pote inatimiza kabisa-kabisa maneno ya Yesu.​—Mt. 24:14.

20 Muumbaji wetu amefanya mambo mengi yanayotuchochea tumutumainie. Je, tunafaidika na mambo hayo? Tunapaswa kuamini vikumbusho vyake. Hilo ndilo jambo ambalo dada Rosellen alifanya. Yeye anasema hivi: “Nilipoanza kumutumainia kabisa Yehova, nilianza kuona waziwazi zaidi namna anavyonitegemeza kwa upendo na kunitia nguvu.” Acheni basi sisi pia tufaidike na vikumbusho vya Yehova.