Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Umegeuzwa?

Je, Umegeuzwa?

“Mgeuzwe kwa kufanya upya akili yenu.”ROM. 12:2.

1, 2. Mazingira na malezi yetu hutuathirije?

SOTE huathiriwa sana na mazingira na malezi yetu. Tunavalia kwa njia fulani; tunapenda vyakula fulani; tunajiendesha kwa njia fulani. Kwa nini? Kwa kadiri fulani, ni kwa sababu ya hali zetu maishani na uvutano wa watu wanaotuzunguka.

2 Hata hivyo, kuna mambo muhimu zaidi kuliko vyakula na mitindo ya mavazi tunayopenda. Kwa mfano, malezi yetu hutufanya tuone mambo fulani kuwa sawa na yanayokubalika, lakini tunakataa mambo mengine kwa sababu tunayaona kuwa si sawa na yasiyokubalika. Mengi ya mambo hayo ni ya kibinafsi na kila mtu ana maoni tofauti kuyahusu. Huenda maamuzi tunayofanya yakaonyesha jinsi dhamiri yetu inavyotuongoza. Biblia inasema kwamba mara nyingi ‘watu wa mataifa wasio na sheria hufanya kwa asili mambo ya sheria.’ (Rom. 2:14) Lakini je, hilo linamaanisha kwamba ikiwa hakuna sheria ya moja kwa moja katika Biblia, tunaweza kufuata tu njia na viwango tulivyozoea au vinavyofuatwa na wengi katika eneo letu?

3. Ni sababu gani mbili zinazofanya Wakristo wasifuate njia na viwango vinavyokubaliwa na wengi?

3 Kuna sababu mbili muhimu kwa nini Wakristo hawapaswi kufanya hivyo. Kwanza, Biblia inatukumbusha hivi: “Kuna njia ambayo imenyooka mbele ya mwanadamu, lakini njia za kifo ndizo mwisho wake baadaye.” (Met. 16:25) Kwa sababu ya hali yetu ya kutokamilika, hatuwezi kuongoza hatua zetu kikamilifu. (Met. 28:26; Yer. 10:23) Pili, Biblia inaonyesha kwamba mitindo na viwango vya ulimwengu vinadhibitiwa na kuongozwa kwa ujanja na Shetani, “mungu wa mfumo huu wa mambo.” (2 Kor. 4:4; 1 Yoh. 5:19) Kwa hiyo, ikiwa tunataka Yehova atukubali na kutubariki, tunahitaji kutii himizo lililo katika Waroma 12:2.Soma.

4. Tutachunguza nini katika makala hii?

 4 Kuna mambo kadhaa muhimu katika Waroma 12:2 tunayopaswa kufikiria kwa uzito. (1) Kwa nini tunahitaji ‘kugeuzwa’? (2) Kugeuzwa kunahusisha nini? na (3) Tunaweza kugeuzwa jinsi gani? Acheni tuchunguze maswali hayo.

KWA NINI TUNAHITAJI KUGEUZWA?

5. Maneno ya Paulo katika Waroma 12:2 yaliwahusu nani hasa?

5 Mtume Paulo aliwaandikia Wakristo wenzake watiwa-mafuta barua kwa Waroma, hakuwaandikia watu wasio waamini au watu wengine kwa ujumla. (Rom. 1:7) Aliwahimiza wageuzwe na ‘kuacha kufanyizwa kulingana na mfumo huu wa mambo.’ Kwa Wakristo walioishi Roma wakati huo, yaani, mwaka wa 56 W.K. hivi, “mfumo wa mambo” ulitia ndani viwango, desturi, tabia, na mitindo ya Waroma. Paulo anatumia neno “acheni” kudokeza kwamba baadhi yao waliathiriwa na mfumo huo wa mambo. Mfumo huo uliwaathiri jinsi gani ndugu na dada zetu wakati huo?

6, 7. Katika siku za Paulo, hali ya kijamii na ya kidini ya Roma ilifanyaje maisha ya Wakristo yawe magumu?

6 Leo, watalii wanaotembelea Roma huona magofu ya mahekalu, makaburi, minara ya ukumbusho, viwanja, majumba ya maonyesho, na kadhalika. Baadhi ya vitu hivyo ni vya tangu karne ya kwanza. Mabaki hayo ya vitu vya kale yanatusaidia kuelewa hali ya kijamii na ya kidini katika jiji la kale la Roma. Vitabu vya historia vinaeleza pia kuhusu michezo ya jeuri, mashindano ya magari ya kukokotwa, michezo ya kuigiza, muziki uliohusu mambo mbalimbali, baadhi yake yakiwa mambo mapotovu. Jiji la Roma lilikuwa pia kituo kikuu cha kibiashara, kwa hiyo ilikuwa rahisi sana kujikusanyia vitu vingi vya kimwili.Rom. 6:21; 1 Pet. 4:3, 4.

7 Licha ya kwamba Waroma walikuwa na mahekalu na miungu mingi, hawakuwa na uhusiano wowote wa kibinafsi na miungu waliyoabudu. Dini ya Waroma ilihusisha hasa sherehe za kidesturi, kama vile sherehe za kuzaliwa, za harusi, na za mazishi ambazo zilikuwa sehemu ya kawaida ya maisha yao. Unaweza kuwazia jinsi mambo hayo yote yalivyofanya maisha ya Wakristo walioishi Roma yawe magumu. Wengi wao walilelewa katika mazingira hayo, na bila shaka walihitaji kugeuzwa ili wawe Wakristo wa kweli, nao wangeendelea kugeuzwa hata baada ya kubatizwa.

8. Leo, ulimwengu ni hatari kwa Wakristo wa kweli jinsi gani?

8 Leo, ulimwengu ni hatari kwa Wakristo waliojiweka wakfu kama ulivyokuwa kwa Wakristo huko Roma. Kwa nini? Kwa sababu roho ya ulimwengu inadhihirishwa katika njia nyingi. (Soma Waefeso 2:2, 3; 1 Yohana 2:16.) Kila siku tunakabili hatari kwa sababu ya tamaa, mawazo,  viwango, na maadili ya ulimwengu. Kwa hiyo, tuna sababu za kutosha za kutii himizo lililoongozwa na roho takatifu la ‘kuacha kufanyizwa kulingana na mfumo huu wa mambo’ na ‘kugeuzwa.’ Ni lazima tufanye nini?

NI NINI KINACHOHITAJI KUGEUZWA?

9. Wengi wamefanya mabadiliko gani kabla ya kustahili kubatizwa?

9 Kadiri mtu anavyojifunza na kutumia kweli ya Biblia maishani mwake, ndivyo anavyoanza kufanya maendeleo ya kiroho. Anaonyesha kwamba anafanya maendeleo ya kiroho kwa kufanya mabadiliko katika maisha yake na kuishi kupatana na mambo aliyojifunza. Anaacha mazoea ya dini ya uwongo na tabia zisizofaa za zamani na kusitawisha utu kama wa Kristo. (Efe. 4:22-24) Tunafurahi kuona mamia ya maelfu ya watu wakifanya maendeleo kila mwaka na kustahili kubatizwa ili kuonyesha kwamba wamejiweka wakfu kwa Yehova Mungu. Kwa kweli, jambo hilo huufanya moyo wa Yehova ushangilie. (Met. 27:11) Hata hivyo, ni vizuri tujiulize hivi: Je, mabadiliko hayo yanatosha?

Watu wengi wanahitaji kutoka katika ulimwengu wa Shetani na kugeuzwa (Tazama fungu la 9)

10. Kuna tofauti gani kati ya kugeuzwa na kufanya maendeleo?

10 Kwa kweli, kugeuzwa huhusisha mengi zaidi ya kufanya mabadiliko au maendeleo. Huenda ikatangazwa kwamba bidhaa fulani “imeboreshwa,” lakini kwa kweli ni bidhaa ileile. Huenda imeboreshwa kidogo tu na kuwekwa katika pakiti maridadi zaidi. Kuhusu neno “mgeuzwe,” kamusi moja (Vine’s Expository Dictionary) inasema hivi: ‘Andiko la Waroma 12:2 linaonyesha tofauti kati ya kufuata mambo ya mfumo huu wa mambo na kugeuzwa (au kubadilishwa umbo) kwa ndani na kufanywa upya kiakili kupitia nguvu ya Roho Takatifu.’ Basi, Mkristo hageuzwi tu kwa kuacha tabia zinazodhuru, maneno machafu, na mwenendo mpotovu. Watu fulani wasio na ujuzi wa Biblia hujitahidi kutofanya mambo hayo. Basi, kugeuzwa kwa Wakristo kunahusisha nini?

11. Paulo alionyesha kwamba watu hugeuzwa kwa njia gani?

11 Paulo aliandika hivi: “Mgeuzwe kwa kufanya upya akili yenu.” “Akili” inahusiana na uwezo wetu wa kufikiri. Lakini neno hilo linatumiwa katika Biblia kurejelea mtazamo, mwelekeo wetu wa akili, na nguvu zetu za kufikiri. Katika barua aliyowaandikia Waroma, Paulo alieleza kuhusu watu waliokuwa na “hali ya akili iliyokataliwa.” Watu hao walifuatilia ‘ukosefu wa uadilifu, uovu, tamaa, ubaya, wakiwa wamejaa wivu, uuaji, mizozo, udanganyifu,’ na mambo mengine mabaya. (Rom. 1:28-31) Hilo linatusaidia kuelewa ni kwa nini Paulo aliwahimiza Wakristo walioishi katika mazingira hayo ‘wageuzwe’ na ‘kufanya upya akili yao.’

“Hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu.”Efe. 4:31

12. Kwa ujumla, watu leo wana mtazamo gani, na unawezaje kuwa hatari kwa Wakristo?

12 Inasikitisha kwamba katika ulimwengu  huu, tumezungukwa na watu wenye tabia zinazotajwa na Paulo. Inaelekea wanafikiri kwamba ni jambo la zamani au lisilofaa kusisitiza watu waishi kupatana na viwango na kanuni. Walimu na wazazi wengi huwaruhusu watoto wafanye jambo lolote watakalo. Wanafundisha kwamba kila mtu ana uhuru wa kujiamulia linalofaa na lisilofaa. Hata wengi wanaodai kuwa watu wa dini wanahisi kwamba wana uhuru wa kufanya kile wanachofikiri kuwa sawa, bila wajibu wowote wa kumtii Mungu na amri zake. (Zab. 14:1) Mtazamo huo unaweza kuwa hatari sana kwa Wakristo wa kweli. Wale wasio waangalifu wanaweza kuanza kusitawisha mtazamo huo kuelekea mipango ya kitheokrasi. Huenda wakakataa kufuata utaratibu kutanikoni na hata kulalamika kuhusu jambo lolote wasilopenda. Au, wanaweza kutilia shaka mashauri ya Biblia kuhusu burudani, kutumia Intaneti, na kufuatilia elimu ya juu.

13. Kwa nini tunapaswa kujichunguza kwa unyoofu?

13 Ili tusifanyizwe au kufinyangwa tena na ulimwengu, tunahitaji kuchunguza kwa unyoofu mitazamo na hisia zetu za ndani, miradi yetu, na maadili yetu. Huenda wengine wasitambue hali yetu. Huenda wakatuambia kwamba hatuna tatizo. Hata hivyo, sisi wenyewe ndio tunaojua ikiwa tumeruhusu yale tuliyojifunza katika Biblia yatugeuze na ikiwa yanaendelea kutugeuza katika sehemu hizo muhimu sana.Soma Yakobo 1:23-25.

JINSI TUNAVYOGEUZWA

14. Ni nini kinachoweza kutusaidia kufanya mabadiliko yanayohitajiwa?

14 Ili tugeuzwe tunahitaji kubadili hali yetu ya ndani, hivyo, tunahitaji kitu kinachoweza kupenya ndani kabisa ya mioyo yetu. Ni nini kitakachotusaidia kufanya hivyo? Tunapojifunza mambo ambayo Yehova anataka tufanye kupatana na kusudi lake lililoandikwa katika Biblia, itikio letu huonyesha yaliyo moyoni mwetu na marekebisho tunayopaswa kufanya ili tutende kupatana na ‘mapenzi ya Mungu yaliyo makamilifu.’Rom. 12:2; Ebr. 4:12.

15. Yehova anapotufinyanga, tunageuzwa kwa njia gani?

15 Soma Isaya 64:8. Mfano aliotumia nabii Isaya una jambo fulani muhimu tunalopaswa kufikiria. Yehova, Mfinyanzi wetu, hutufinyanga kama udongo jinsi gani? Kwa kweli, hatubadilishi kihalisi, labda kwa kutufanya tuwe na sura au umbo lenye kuvutia zaidi. Yehova hutuzoeza kiroho wala si kimwili. Tukimruhusu atufinyange, tutageuzwa kwa ndani au kwa njia ya kiroho. Na hilo ndilo tunalohitaji hasa ili kushinda uvutano wa ulimwengu. Ufinyanzi hufanywaje?

16, 17. (a) Eleza jinsi mfinyanzi anavyoutayarisha udongo ili afinyange chombo kizuri. (b) Neno la Mungu linatusaidiaje kugeuzwa na kuwa vyombo vyenye thamani machoni pa Yehova?

16 Ili afinyange chungu kizuri, mfinyanzi hutumia udongo mzuri sana. Hata hivyo, anahitaji kufanya mambo mawili. Kwanza, ni lazima asafishe udongo huo ili kuondoa madini au uchafu. Kisha, ni lazima auchanganye kwa ustadi na kiasi kinachofaa cha maji ili aweze kuufinyanga kwa urahisi.

17 Ona kwamba mfinyanzi hutumia maji kuusafisha udongo na kuulainisha ili iwe rahisi kwake kufinyanga chombo chochote kile. Hivyo ndivyo Neno la Mungu linavyoweza kutusaidia maishani mwetu. Linaweza kutusaidia kuacha njia ya kufikiri tuliyokuwa nayo zamani kabla ya kumjua Mungu, na kugeuzwa kuwa vyombo vyenye thamani machoni pake. (Efe. 5:26)  Fikiria jinsi tunavyohimizwa tena na tena kusoma Biblia kila siku na kuhudhuria mikutano ya Kikristo ili kufundishwa Neno la Mungu. Kwa nini tunatiwa moyo kufanya mambo hayo? Tunapofanya mambo hayo, tunakubali kufinyangwa na Yehova.Zab. 1:2; Mdo. 17:11; Ebr. 10:24, 25.

Kugeuzwa na Neno la Mungu kutawasaidia kutatua matatizo kwa njia bora kuliko zamani (Tazama fungu la 18)

18. (a) Ikiwa tunataka Neno la Mungu lituchochee na kutugeuza, kwa nini ni muhimu tutafakari? (b) Ni maswali gani yanayoweza kutusaidia?

18 Ili Neno la Mungu litugeuze, tunahitaji kuanza kusoma na kujifunza Biblia kwa ukawaida. Watu wengi husoma Biblia mara kwa mara na hivyo wanajua mambo mengi yaliyomo. Huenda umekutana na watu hao unapohubiri. Wengine hata wanakumbuka mistari fulani ya Biblia. * Lakini huenda wasibadili mwenendo au njia yao ya kufikiri. Kwa nini? Ili Neno la Mungu limchochee mtu na kumgeuza, ni lazima akubali liguse moyo wake. (Gal. 6:6) Kwa hiyo, tunahitaji kutumia wakati kutafakari mambo tunayojifunza. Ni vizuri tujiulize hivi: ‘Je, ninasadiki kwamba hili si fundisho la kidini tu? Je, nimejithibitishia kwamba hii ndiyo kweli? Isitoshe, je, ninaona jinsi ninavyoweza kutumia maishani mwangu mambo ninayojifunza badala ya kufikiria tu jinsi nitakavyoyatumia kuwafundisha wengine? Je, ninahisi kwamba Yehova anazungumza nami?’ Kufikiria na kutafakari maswali hayo kunaweza kutusaidia kumpenda Yehova zaidi kutoka moyoni. Na upendo huo utasitawi. Mambo tunayojifunza yanapogusa moyo wetu, tutachochewa kufanya mabadiliko yanayofaa.Met. 4:23; Luka 6:45.

19, 20. Tutanufaika kikweli tukitii shauri gani la Biblia?

19 Kusoma Neno la Mungu kwa ukawaida na kulitafakari kutatuchochea kuendelea kufanya jambo hili ambalo inaelekea tumekuwa tukifanya kwa kadiri fulani: “Uvueni utu wa zamani pamoja na mazoea yake, na mjivike utu mpya, ambao kupitia ujuzi sahihi unafanywa kuwa mpya.” (Kol. 3:9, 10) Naam, tunaweza kuendelea kufanikiwa kufanya hivyo kadiri tunavyolielewa vizuri zaidi Neno la Mungu na kuthamini nguvu zake. Utu mpya wa Kikristo tunaositawisha utatulinda dhidi ya mbinu za ujanja za Shetani.

20 Mtume Petro anatukumbusha hivi: “Kama watoto watiifu, acheni kufanyizwa kulingana na tamaa mlizokuwa nazo hapo zamani,” badala yake “iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote.” (1 Pet. 1:14, 15) Kama tutakavyoona katika makala inayofuata, tutapata baraka nyingi tukijitahidi kabisa kuacha mitazamo na maoni tuliyokuwa nayo zamani na kukubali Neno la Mungu litugeuze.

^ fu. 18 Tazama mfano ulio katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Februari 1, 1994, ukurasa wa 10, fungu la 7.