Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Upainia Huimarisha Uhusiano Wetu na Mungu

Upainia Huimarisha Uhusiano Wetu na Mungu

“Ni vema kumpigia Mungu wetu muziki.”ZAB. 147:1.

1, 2. (a) Inakuwaje tunapomfikiria mtu tunayempenda na kuzungumza kumhusu? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.) (b) Tutachunguza maswali gani?

TUNAWEZA kuimarisha uhusiano wetu na mtu tunayempenda kwa kumfikiria na kuzungumza kumhusu. Tunaweza kuimarisha uhusiano wetu na Yehova Mungu tukifanya vivyo hivyo. Akiwa mchungaji, Daudi alikuwa na wakati wa kutazama nyota usiku na kutafakari kuhusu Muumba mkuu. Aliandika hivi: “Ninapoziona mbingu zako, kazi za vidole vyako, mwezi na nyota ambazo umetayarisha, mwanadamu anayeweza kufa ni nini hivi kwamba umweke akilini, na mwana wa mtu wa udongo hivi kwamba umtunze?” (Zab. 8:3, 4) Mtume Paulo alisema hivi baada ya kuona kusudi la Yehova kuhusiana na taifa la Israeli la kiroho likitimia kwa njia ya pekee: “Lo! Jinsi kilivyo kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi!”Rom. 11:17-26, 33.

2 Tunapohubiri, tunafikiri na kuzungumza kumhusu Yehova. Kufanya hivyo huimarisha uhusiano wetu naye. Watumishi wengi wa wakati wote wameona kwamba upendo wao kumwelekea Mungu umeongezeka kwa sababu ya kutumia wakati mwingi zaidi kuhubiri habari njema ya Ufalme. Iwe wewe ni mtumishi wa wakati wote au unajitahidi kufikia mradi huo, fikiria hili: Utumishi wa wakati wote unaweza kuimarishaje uhusiano wako na Yehova? Ikiwa wewe ni painia, jiulize hivi: ‘Ni nini kitakachonisaidia kuendelea na utumishi huu wenye kuthawabisha?’ Ikiwa kwa sasa wewe si painia, jiulize, ‘Ninahitaji kufanya marekebisho gani ili niwe painia?’ Acheni tuzungumzie jinsi utumishi wa wakati wote unavyoweza kuimarisha uhusiano wetu na Mungu.

 UTUMISHI WA WAKATI WOTE UNAIMARISHA UHUSIANO WETU NA MUNGU

3. Tunafaidikaje tunapozungumza na wengine katika huduma kuhusu baraka za Ufalme za wakati ujao?

3 Tunapozungumza na wengine kuhusu baraka za Ufalme za wakati ujao tunamkaribia zaidi Yehova. Unapenda kutumia andiko gani unapohubiri nyumba kwa nyumba? Labda unapenda kutumia Zaburi 37:10, 11; Danieli 2:44; Yohana 5:28, 29; au Ufunuo 21:3,  4. Kila mara tunapozungumza na wengine kuhusu ahadi hizo, tunakumbuka kwamba Mungu wetu aliye mkarimu ni mpaji wa “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu.” Na hilo hutufanya tumkaribie zaidi.Yak. 1:17.

4. Kwa nini tunazidi kuthamini wema wa Mungu tunapoona hali mbaya ya kiroho ya watu wengine?

4 Tunazidi kuithamini kweli tunapoona hali mbaya ya kiroho ya watu tunaowahubiria. Watu ulimwenguni hawana mwongozo unaotegemeka wa kuwasaidia kufanikiwa na kupata furaha maishani. Wengi wana wasiwasi kuhusu wakati ujao na hawana tumaini. Wanatafuta kusudi maishani. Isitoshe, wanadini wengi hawajui sana Maandiko. Hali yao ni kama ya watu wa jiji la kale la Ninawi. (Soma Yona 4:11.) Tunaposhiriki zaidi katika kazi ya kuhubiri, tunaona waziwazi kwamba hali ya kiroho ya wale tunaowahubiria ni tofauti sana na ya watumishi wa Yehova. (Isa. 65:13) Hilo hutukumbusha kwamba Yehova ni mwema kwa sababu ametuandalia mahitaji mengi sana ya kiroho naye huwakaribisha wote waje kupata burudisho la kiroho na tumaini la kweli.Ufu. 22:17.

5. Tunapowafundisha wengine kweli, tunahisije kuhusu matatizo yetu?

5 Tunapowafundisha wengine kweli tunajifunza kutohangaikia kupita kiasi matatizo yetu. Trisha, ambaye ni painia wa kawaida, aliona ukweli wa jambo hilo wazazi wake walipotalikiana. Anasema hivi: “Hali hiyo ilinivunja moyo sana.” Siku moja alikuwa amehuzunika sana naye hakutaka kuondoka nyumbani, hata hivyo, aliamua kwenda kujifunza Biblia na watoto watatu waliokabili hali ngumu nyumbani kwao. Baba yao aliwaacha, na kaka yao aliwatesa. Trisha anasema hivi: “Hali yao ilikuwa mbaya zaidi kuliko yangu. Hata hivyo, wakati wa funzo, macho yao yaling’aa, nao walicheka kwa msisimko. Niliwaona watoto hao kuwa zawadi kutoka kwa Yehova, hasa siku hiyo.”

6, 7. (a) Imani yetu huimarishwaje tunapofundisha kweli za Biblia? (b) Tunahisije kuhusu hekima ya Mungu tunapoona wanafunzi wa Biblia wakitumia kanuni za Kimaandiko kufanya mabadiliko maishani?

6 Kufundisha kweli za Biblia huimarisha imani yetu. Mtume Paulo aliandika hivi kuhusu Wayahudi fulani katika siku zake ambao hawakutenda yale waliyosema: “Je, wewe, . . . unayemfundisha mtu mwingine, hujifundishi mwenyewe?” (Rom. 2:21) Mapainia wako tofauti kabisa na Wayahudi hao. Wana fursa nyingi za kuwafundisha wengine kweli na kuongoza mafunzo ya Biblia. Ili kufundisha kwa ustadi, wanahitaji kutayarisha kwa ajili ya kila funzo na labda kufanya utafiti ili kujibu maswali. Painia anayeitwa Janeen anasema hivi: “Kila mara ninapopata fursa ya kuwafundisha wengine kweli, ni kana kwamba kweli hizo zinatia mizizi ndani ya akili na moyo wangu. Hivyo, imani yangu imezidi kukua.”

7 Tunathamini zaidi hekima ya Mungu tunapoona wanafunzi wa Biblia wakitumia kanuni za Biblia kufanya mabadiliko maishani. (Isa. 48:17, 18) Hilo linatusaidia kuazimia hata zaidi kuendelea kutumia kanuni hizo maishani mwetu. Painia mwingine anayeitwa Adrianna anasema hivi: “Maisha ya watu huharibika wanapotegemea hekima yao. Lakini wanapoanza kutegemea hekima ya  Yehova wanaanza kufaidika mara moja.” Naye Phil anasema hivi: “Unaona jinsi watu walioshindwa kubadilika mwanzoni wanavyosaidiwa na Yehova kufanya marekebisho maishani mwao.”

8. Tunajengwa jinsi gani tunapohubiri pamoja na ndugu na dada zetu?

8 Ndugu na dada zetu hutujenga kiroho tunapohubiri pamoja nao. (Met. 13:20) Mapainia wengi hutumia wakati mwingi kuhubiri na ndugu na dada zao. Hivyo, wanapata fursa nyingi za “ubadilishanaji wa kitia-moyo.” (Rom. 1:12; soma Methali 27:17.) Painia anayeitwa Lisa anasema hivi: “Mara nyingi watu hushindana na kuoneana wivu mahali ninapofanya kazi. Kila siku unawasikia watu wakipiga porojo na kusema maneno machafu. Wanafanya yote wawezayo ili kupandishwa cheo kazini. Unadhihakiwa nyakati nyingine kwa sababu ya mwenendo wako wa Kikristo. Hata hivyo, ninajengwa kwelikweli ninapohubiri pamoja na Wakristo wenzangu. Ninaporudi nyumbani jioni, mimi huhisi nimeburudishwa sana licha ya uchovu.”

9. Ndoa huimarika jinsi gani wenzi wa ndoa wanapofanya upainia pamoja?

9 Kufanya upainia na mwenzi wetu wa ndoa huimarisha ndoa yetu ambayo ni kamba yenye nyuzi tatu. (Mhu. 4:12) Madeline, anayefanya upainia pamoja na mume wake, anasema hivi: “Mimi na mume wangu huzungumza kuhusu mambo tuliyojionea katika utumishi au jambo tulilosoma katika Biblia tunaloweza kutumia katika huduma yetu. Uhusiano wetu unaimarika zaidi kila mwaka kwa sababu ya kufanya upainia pamoja.” Naye Trisha anasema: “Sisi hujitahidi kuepuka madeni, na hilo limetusaidia kutogombana kuhusu pesa. Kwa kuwa  tunafuata ratiba ileile ya utumishi, tunapata wakati wa kuwa pamoja katika ziara za kurudia na mafunzo ya Biblia, hilo hutusaidia kuwa imara kiroho na huimarisha uhusiano wetu.”

Utakuwa na maisha yenye kuridhisha ukiwa mtumishi wa wakati wote mwenye bidii (Tazama fungu la 9)

10. Tunapotanguliza masilahi ya Ufalme na kuona Yehova akitusaidia, tunachochewaje kumtegemea?

10 Tunamtegemea Yehova hata zaidi tunapoona akitusaidia na kujibu sala zetu tunapotanguliza masilahi ya Ufalme. Ni kweli kwamba Wakristo wote washikamanifu humtegemea Yehova. Hata hivyo, watumishi wa wakati wote wanajua kwamba hawawezi kuendelea kuwa mapainia wasipomtegemea Yehova. (Soma Mathayo 6:30-34.) Curt, ambaye ni painia na mwangalizi badala wa mzunguko, alikubali kutembelea kutaniko ambalo lilikuwa mwendo wa saa mbili na nusu kutoka nyumbani kwake. Wenzi hao mapainia walikuwa na kiasi kidogo cha mafuta katika gari lao ambacho kingeweza kuwafikisha tu kwenye kutaniko hilo, na walitarajia kupata pesa baada ya juma moja. Curt anasema hivi: “Nilianza kufikiri kwamba nilifanya uamuzi usiofaa.” Baada ya kusali, walifikia mkataa kwamba wangetimiza mgawo huo wakiwa na uhakika kwamba Mungu angetosheleza mahitaji yao. Walipokaribia mwisho wa ziara, dada mmoja aliwapigia simu na kuwaambia kwamba anataka kuwapa zawadi. Aliwapa kiasi cha pesa walichohitaji ili kurudi nyumbani. Curt anasema hivi: “Unapojionea mambo kama hayo tena na tena, unaona wazi kwamba Yehova anakutegemeza.”

11. Ni baraka gani wanazopata mapainia?

11 Mara nyingi mapainia wametambua kwamba wanapojitoa kikamili katika utumishi wa Yehova na kusitawisha uhusiano wa karibu naye, ‘wanafikiwa’ na baraka nyingi sana. (Kum. 28:2) Hata hivyo, upainia una changamoto zake. Watumishi wote wa Mungu wanapambana na matatizo yanayosababishwa na uasi wa Adamu. Ingawa baadhi ya mapainia wamelazimika kuacha upainia kwa muda kwa sababu ya hali fulani, kwa kawaida hali hizo zinaweza kuepukwa au kusuluhishwa. Ni nini kinachoweza kuwasaidia mapainia kuendelea kufurahia pendeleo lao la utumishi?

KUENDELEA NA UTUMISHI WA WAKATI WOTE

12, 13. (a) Painia anapaswa kufanya nini ikiwa anashindwa kutimiza takwa la saa? (b) Kwa nini ni muhimu sana kutenga wakati wa kusoma Biblia kila siku, kufanya funzo la kibinafsi, na kutafakari?

12 Mapainia wengi wana ratiba yenye shughuli nyingi. Inaweza kuwa vigumu kutimiza kila jambo, hivyo ni muhimu kupanga mambo vizuri. (1 Kor. 14:33, 40) Painia anaposhindwa kutimiza takwa la saa, huenda akahitaji kuchunguza jinsi anavyotumia wakati wake. (Efe. 5:15, 16) Anaweza kujiuliza hivi: ‘Ninatumia muda mwingi kadiri gani katika tafrija au burudani? Je, ninahitaji kujidhibiti zaidi? Ninaweza kurekebisha ratiba yangu ya kazi ya kimwili?’ Kila Mkristo atakubali kwamba ni rahisi kufuatilia mambo mengi tusiyopangia; kwa hiyo, huenda watumishi wa wakati wote wakahitaji kuchunguza ratiba yao kwa ukawaida na kufanya marekebisho yanayohitajiwa.

13 Ratiba ya painia inapaswa kutia ndani kusoma Biblia kila siku, kufanya funzo la kibinafsi, na kutafakari. Painia anahitaji kujidhibiti ili shughuli zisizo muhimu sana zisichukue wakati aliotenga kwa ajili ya mambo hayo ya maana. (Flp. 1:10) Kwa mfano, mfikirie painia anayerudi nyumbani baada ya kuhubiri siku nzima. Amepanga kutayarisha mikutano jioni. Hata hivyo, kwanza anaamua kusoma barua-pepe. Kwa hiyo, anawasha kompyuta ili asome na kujibu barua-pepe. Kisha, anaamua kufungua kituo fulani cha Intaneti ili aone ikiwa bei ya kitu fulani alichotaka kununua imeshuka. Bila kujua, saa mbili hivi zimepita na hajaanza kutayarisha mikutano.  Kwa nini hilo ni tatizo? Ni lazima wanariadha wenye uzoefu watunze miili yao ili waendelee na riadha kwa miaka mingi. Vivyo hivyo, ili mapainia waendelee na utumishi wakati wote wanahitaji kujijenga kiroho kwa kufuata ratiba nzuri ya funzo la kibinafsi.1 Tim. 4:16.

14, 15. (a) Kwa nini mapainia wanapaswa kuishi maisha rahisi? (b) Painia anapaswa kufanya nini anapokabili matatizo?

14 Mapainia wanaofanikiwa katika utumishi hujitahidi sana kurahisisha maisha yao. Yesu aliwahimiza wanafunzi wake wawe na jicho rahisi. (Mt. 6:22) Alirahisisha maisha yake ili atimize huduma yake bila kukengeushwa. Alisema hivi: “Mbweha wana mapango na ndege wa mbinguni wana viota, lakini Mwana wa binadamu hana mahali popote pa kulaza kichwa chake.” (Mt. 8:20) Mapainia wanaoiga mfano wa Yesu wanakumbuka kwamba wakiwa na vitu vingi vya kimwili watalazimika kuvitunza, kuvirekebisha, au kununua vingine vipya.

15 Mapainia wanatambua kwamba pendeleo lao la utumishi halimaanishi kwamba wao ni bora kuliko wengine. Badala yake, tuna zawadi au pendeleo lolote la utumishi kwa sababu ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu. Kwa hiyo, ili kuendelea na utumishi huo, ni lazima kila painia amtegemee Yehova. (Flp. 4:13) Mapainia watakabili matatizo na hali ngumu. (Zab. 34:19) Chini ya hali hizo, mapainia wanapaswa kutafuta mwongozo wa Yehova ili awasaidie, badala ya kuamua haraka kuacha pendeleo lao la utumishi. (Soma Zaburi 37:5.) Wanapoona jinsi Mungu anavyowasaidia kwa upendo, watachochewa kumkaribia zaidi Baba yao wa mbinguni anayejali.Isa. 41:10.

JE, UNAWEZA KUWA PAINIA?

16. Unapaswa kufanya nini ikiwa ungependa kufanya upainia?

16 Ikiwa ungependa kupata baraka ambazo watumishi wa wakati wote wanafurahia, mwambie Yehova tamaa yako. (1 Yoh. 5:14, 15) Zungumza na mapainia. Jiwekee miradi itakayokusaidia hatua kwa hatua kuwa painia. Keith na Erika walifanya hivyo. Walikuwa wakifanya kazi ya kuajiriwa ya wakati wote, na kama wenzi wengi wa ndoa wa rika lao, walinunua nyumba na gari jipya mara tu baada ya kufunga ndoa. Wanasema hivi: “Tulifikiri kwamba tungeridhika na vitu hivyo, lakini mambo hayakuwa hivyo.” Keith alipofutwa kazi, alitumikia akiwa painia msaidizi. Anakumbuka hivi: “Upainia ulinikumbusha shangwe nyingi inayotokana na kuhubiri.” Walianzisha urafiki na wenzi wa ndoa mapainia ambao waliwasaidia kuona kwamba wangepata shangwe kwa kuishi maisha rahisi na kufanya upainia. Keith na Erika walifanya nini? Wanasema hivi: “Tuliandika orodha ya miradi yetu ya kiroho na kuibandika kwenye friji, kisha tulitia alama kila mradi tuliotimiza.” Baada ya muda, tuliweza kufanya upainia.

17. Kwa nini ni jambo la hekima kurekebisha ratiba au kurahisisha maisha yako ili uwe painia?

17 Je, unaweza kuwa painia? Ikiwa huwezi kwa sasa, fikiria jinsi unavyoweza kufikia mradi huo, fanya yote uwezayo kuimarisha uhusiano wako na Yehova kwa kushiriki kikamili katika huduma. Baada ya kusali na kujichunguza, huenda ukatambua kwamba unaweza kuwa painia ukirekebisha ratiba au kurahisisha maisha yako. Mambo uliyojinyima hayawezi kamwe kulinganishwa na shangwe nyingi utakayopata ukiwa upainia. Utaridhika zaidi ukitanguliza masilahi ya Ufalme badala ya mapendezi yako. (Mt. 6:33) Utapata furaha zaidi inayotokana na kutoa. Zaidi ya hayo, utakuwa na fursa zaidi za kufikiri na kuzungumza kumhusu Yehova. Utampenda zaidi na hivyo kuufurahisha moyo wake.