Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kazi ya Upainia Inatia Nguvu Uhusiano Wetu pamoja na Mungu

Kazi ya Upainia Inatia Nguvu Uhusiano Wetu pamoja na Mungu

‘Ni vema kumupigia Mungu wetu muziki.’​—ZAB. 147:1.

1, 2. (a) Kufikiri na kuzungumuza kuhusu mutu fulani ambaye tunapenda kunaweza kuwa na matokeo gani? (Ona picha mwanzoni mwa habari hii.) (b) Tutazungumuzia maulizo gani?

 KUFIKIRI na kuzungumuza kuhusu mutu fulani tunayependa kunaweza kutia nguvu uhusiano wetu pamoja naye. Ni hivyo pia kuhusu uhusiano wetu pamoja na Yehova Mungu. Alipokuwa muchungaji, Daudi alitumia wakati mwingi usiku ili kutazama mbingu zenye nyota na kutafakari juu ya Muumbaji wa ajabu wa vitu hivyo. Daudi aliandika hivi: ‘Ninapoziona mbingu zako, kazi za vidole vyako, mwezi na nyota ambazo umetayarisha, mwanadamu anayeweza kufa ni nini hivi kwamba umuweke akilini, na mwana wa mutu wa udongo hivi kwamba umutunze?’ (Zab. 8:3, 4) Kisha kuchunguza namna makusudi ya Yehova yalivyokuwa yakitimia kwa njia ya ajabu kuhusu Israeli la kiroho, mutume Paulo alisema hivi: “Lo! Jinsi kilivyo kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi!”​—Rom. 11:17-26, 33.

2 Tunapohubiri, tunafikiri na kuzungumuza kumuhusu Yehova. Jambo hilo lina matokeo mazuri juu yetu. Wengi ambao wamefanya utumishi wa wakati wote wametambua kwamba kuongeza utendaji wao katika kazi ya kuhubiri kumewasaidia wamupende Mungu sana. Ikiwa unafanya kwa sasa utumishi wa wakati wote ao unafikiria kuanza utumishi huo, fikiria ulizo hili: Namna gani utumishi wa wakati wote unaweza kutia nguvu uhusiano wako pamoja na Yehova? Ikiwa wewe ni painia, jiulize hivi: ‘Ni nini inaweza kunisaidia nibaki katika utumishi huu unaoleta baraka?’ Ikiwa haujaanza bado kazi ya upainia, jiulize hivi: ‘Ninaweza kufanya mabadiliko gani ili nianze kazi ya upainia?’ Acheni tuchunguze namna gani utumishi wa wakati wote unaweza kutia nguvu uhusiano wetu pamoja na Mungu.

UTUMISHI WA WAKATI WOTE NA UHUSIANO WETU PAMOJA NA MUNGU

3. Tunapata faida gani tunapozungumuza na wengine kuhusu baraka ambazo Ufalme utaleta wakati ujao?

3 Kuzungumuza pamoja na wengine kuhusu baraka ambazo Ufalme utaleta wakati ujao kunatufanya tumukaribie Yehova zaidi. Ni andiko gani unapenda kutumia unapohubiri nyumba kwa nyumba? Je, unapenda kutumia Zaburi 37:10, 11; Danieli 2:44; Yohana 5:28, 29; ao Ufunuo 21:3, 4? Kila mara tunapozungumuzia ahadi hizo, hilo linatukumbusha kwamba Mungu wetu mukarimu, ni mutoaji kabisa wa “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu.” Jambo hilo linatufanya tumukaribie zaidi.​—Yak. 1:17.

4. Sababu gani tunapendezwa zaidi na wema wa Mungu tunapoona hali mbaya ya kiroho ya wengine?

4 Kuona hali mbaya ya kiroho ya watu tunaohubiria kunatuchochea tuipende sana kweli. Katika ulimwengu, watu hawana muongozo unaotegemeka unaoweza kuwasaidia wafanikiwe na kupata furaha. Wengi wana wasiwasi kuhusu wakati ujao na hawana tumaini lolote. Wanatafuta kuwa na maisha yenye maana. Hata wengi wanaopenda sana mambo ya dini wana ujuzi mudogo wa Maandiko. Hali yao inafanana sana na ile ya wakaaji wa jiji la zamani la Ninawi. (Soma Yona 4:11.) Kupitisha wakati mwingi katika kazi ya kuhubiri, kunatusaidia kuona waziwazi zaidi tofauti iliyo kati ya hali ya kiroho ya wale tunaohubiria na hali ya kiroho ya watumishi wa Yehova. (Isa. 65:13) Tunapopitisha wakati mwingi katika kazi ya kuhubiri, tunajionea kwamba, zaidi ya kutosheleza mahitaji ya kiroho ya watumishi wake, Yehova anaonyesha wema wake kwa kuwaalika wote wapate kitia-moyo na tumaini la kweli.​—Ufu. 22:17.

5. Kuwasaidia wengine kiroho kunatufanya tuwe na maoni gani kuhusu magumu yetu?

5 Kuwasaidia wengine kiroho kunafanya iwe rahisi zaidi kwetu kuepuka kuwa wenye kulemewa na magumu yetu. Trisha, ambaye ni painia wa kawaida, alijionea ukweli huo wazazi wake walipoachana. Dada huyo anasema hivi: “Hilo lilikuwa moja kati ya mambo yaliyosumbua sana akili yangu maishani.” Siku moja alikuwa na huzuni sana na alijisikia kwamba ni vizuri tu akae nyumbani. Hata hivyo, alienda kujifunza Biblia pamoja na watoto watatu waliokuwa na magumu mengi katika familia yao. Baba yao alikuwa amewaacha, na ndugu yao mukubwa alikuwa amewatesa sana. Trisha anasema hivi: “Watoto hao waliteseka sana kuliko mimi. Tulipoendelea kujifunza, furaha ilionekana katika macho yao na walicheka kwa sababu ya furaha na shangwe. Watoto hao walikuwa baraka kutoka kwa Yehova, zaidi sana siku hiyo.”

6, 7. (a) Namna gani imani yetu inatiwa nguvu tunapofundisha wengine kweli za Biblia? (b) Tunapoona namna wanafunzi wa Biblia wanavyofanya mabadiliko kwa kutumia kanuni za Maandiko katika maisha yao, hilo linatufanya tuone hekima ya Mungu namna gani?

6 Kufundisha kweli za Biblia kunatia nguvu imani yetu. Mutume Paulo aliandikia hivi Wayahudi fulani wa siku zake ambao hawakutenda kulingana na yale waliyokuwa wakihubiri: ‘Je, wewe unayemufundisha mutu mwingine, haujifundishe mwenyewe?’ (Rom. 2:21) Mapainia hawafanye hivyo leo! Kwa kawaida, mapainia wana nafasi nyingi za kuwafundisha wengine kweli na kuongoza mafunzo ya Biblia. Ili wafundishe vizuri, mapainia wanaombwa kutayarisha kila funzo na hata kufanya utafiti ili kujibu maulizo fulani. Janeen, dada painia, anaeleza hivi: “Kila wakati ninapopata nafasi ya kufundisha wengine kweli, ninajisikia kwamba kweli hizo zinakaziwa katika akili na moyo wangu. Kwa hiyo, imani yangu inaendelea kukomaa.”

7 Kuona namna wanafunzi wa Biblia wanavyofanya mabadiliko katika maisha yao kwa kutumia kanuni za Biblia kunatufanya tupendezwe zaidi na hekima ya Mungu. (Isa. 48:17, 18) Jambo hilo linatusaidia tuazimie zaidi kuendelea kutumia kanuni hizo katika maisha yetu. Painia mwingine anayeitwa Adrianna, anaeleza hivi: “Maisha ya watu yanaweza kuwa na matatizo wanapotegemea hekima yao wenyewe. Lakini, wanapoanza kutegemea hekima ya Yehova, maisha yao yanabadilika mara moja.” Vivyo hivyo, ndugu Phil naye anasema hivi: “Unaona namna Yehova anavyoweza kubadili maisha ya watu ambao walishindwa walipojaribu kufanya hivyo wao wenyewe.”

8. Kuhubiri pamoja na ndugu na dada zetu kunatusaidia namna gani?

8 Kuhubiri pamoja na ndugu na dada zetu kunatujenga kiroho. (Met. 13:20) Mapainia wengi wanatumia wakati mwingi katika utumishi pamoja na wahubiri wenzao. Hilo linawatolea nafasi nyingi kwa ajili ya “ubadilishanaji wa kitia-moyo.” (Rom. 1:12; soma Methali 27:17.) Painia anayeitwa Lisa anasema hivi: “Kila mara kuna roho ya kushindana na ya wivu mahali ninapofanya kazi. Kila siku unasikia watu wakipiga porojo na kusema maneno machafu. Hakuna jitihada inayofanywa ili kuzuia hali hiyo. Nyakati fulani, unazarauliwa ao kuchekwa kwa sababu ya mwenendo wako wa Kikristo. Lakini, kuhubiri pamoja na Wakristo wenzangu kunanitia moyo kabisa. Kisha mahubiri, ninarudi nyumbani nikiwa mwenye kuburudishwa, hata ikiwa nimechoka.”

9. Kufanya kazi ya upainia pamoja na bibi ao bwana yetu kunaweza kuwa na matokeo gani juu ya kamba ya ndoa yenye nyuzi tatu?

9 Kufanya kazi ya upainia pamoja na bibi ao bwana yetu kunatia nguvu kamba ya ndoa yenye nyuzi tatu. (Mhu. 4:12) Madeline, anayefanya kazi ya upainia pamoja na bwana yake, anaeleza hivi: “Mimi na bwana yangu tuna wakati mwingi wa kuzungumuzia mambo tuliyofanya katika mahubiri ao jambo fulani tulilovumbua katika usomaji wetu wa Biblia na ambalo tunaweza kutumia katika mahubiri. Kufanya kazi ya upainia pamoja kila mwaka kunatusaidia tuwe na uhusiano wa karibu zaidi.” Vivyo hivyo, dada Trisha anasema hivi: “Sisi wawili tunafikiria sana namna ya kuepuka madeni, kwa hiyo, hatubishane kuhusu mambo ya feza. Tuna programe moja ya kuhubiri, kwa hiyo tunafanya pamoja ziara zetu za kurudia na kuongoza mafunzo yetu ya Biblia, jambo hilo linatusaidia tukaribiane na tumukaribie Yehova zaidi.”

Kufanya utumishi wa wakati wote kunatuletea furaha maishani (Ona fungu la 9)

10. Tunapotia faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza na kujionea namna Mungu anavyotutegemeza, hilo linakuwa na matokeo gani juu yetu?

10 Kuendelea kutia faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza, kuona namna Yehova anavyotutegemeza, na namna anavyojibu sala zetu kunatufanya tumutumaini zaidi. Wakristo wote waaminifu wamejionea jambo hilo. Lakini wale walio katika utumishi wa wakati wote wametambua kwamba kumutegemea Yehova kunaweza kuwasaidia wabaki katika kazi ya upainia. (Soma Mathayo 6:30-34.) Ndugu Curt, ambaye ni painia na mwangalizi wa badala, alikubali kutembelea kutaniko lililokuwa umbali wa mwendo wa saa mbili na nusu kutoka nyumbani kwake. Yeye na bibi yake, ambaye pia ni painia, hawakuwa na esanse ya kutosha katika gari lao ambayo ingewapeleka na kuwarudisha, na angelipwa mushahara wake kisha juma moja. Curt anaeleza hivi: “Nilianza kujiuliza ikiwa nilichukua uamuzi muzuri kwa kukubali mugawo huo.” Kisha kusali, waliamua kwamba wataenda katika mugawo huo, wakiwa na tumaini kwamba Mungu angewatimizia mahitaji yao. Walipokaribia kuondoka, dada mumoja aliwaita na kusema kwamba alikuwa na zawadi ya kuwatolea. Aliwatolea kiasi cha feza ambacho walihitaji kabisa ili kulipia garama yote ya safari yao. Curt anasema hivi: “Mara nyingi unapojionea mambo kama haya, ni rahisi kuona kwamba Yehova anakutegemeza.”

11. Ni baraka gani ambazo mapainia wanapata?

11 Bila shaka, mapainia wamejionea mara nyingi kwamba kadiri wanavyojitoa katika kazi ya Yehova na kuendelea kuwa na urafiki wa karibu pamoja naye, baraka nyingi kama maji ya muto ‘zinawafikia.’ (Kum. 28:2) Hata hivyo, mapainia wanapatwa na matatizo fulani. Watumishi wote wa Mungu wanapatwa na matatizo yaliyoletwa na uasi wa Adamu. Mapainia fulani wamefikiri kwamba wanapaswa kuacha kazi hiyo kwa muda fulani kwa sababu ya matatizo fulani, lakini kuna njia za kutatua ao hata kuepuka matatizo hayo. Ni nini inayoweza kuwasaidia mapainia waendelee kufurahia pendeleo lao la utumishi?

BAKI KATIKA UTUMISHI WA WAKATI WOTE

12, 13. (a) Painia anapaswa kufanya nini ikiwa ana tatizo la kueneza saa ambazo anaombwa? (b) Sababu gani ni jambo la lazima sana painia awe na programe ya kusoma Biblia kila siku, kufanya funzo la pekee na kutafakari?

12 Mapainia wengi wana programe yenye kujaa mambo mengi. Wanaweza kukosa wakati wa kufanya mambo fulani, kwa hiyo, ni jambo la maana kuwa na programe yenye kupangwa vizuri. (1 Kor. 14:33, 40) Ikiwa painia ana tatizo la kueneza saa anazoombwa, anapaswa kuchunguza tena namna anavyotumia wakati wake. (Efe. 5:15, 16) Anapaswa kujiuliza hivi: ‘Ninatumia kiasi gani cha wakati katika mambo ya kujifurahisha ao katika michezo? Je, ninahitaji kujizuia zaidi katika mambo hayo? Je, ninapaswa kubadili programe yangu ya kazi ya kimwili?’ Kila Mukristo atakubali kwamba ni rahisi kuongeza mambo mengi kwenye programe yake; kwa hiyo, wale walio katika utumishi wa wakati wote wanahitaji kuchunguza programe zao kila mara na kufanya mabadiliko yanayohitajiwa.

13 Painia anapaswa kuwa na programe ya kusoma Biblia kila siku, kufanya funzo la pekee, na kutafakari. Kwa hiyo, painia anahitaji kujizuia ili mambo yasiyo ya lazima yasichukue wakati ambao alipanga kwa ajili ya mambo hayo ya lazima sana. (Flp. 1:10) Kwa mufano, fikiria painia anayerudi nyumbani kisha kupitisha siku muzima katika mahubiri. Anataka kutumia wakati wa mangaribi ili kutayarisha mikutano. Lakini, anaanza kusoma barua alizopokea. Kisha anafungua ordinatere na kuanza kusoma na kujibu ujumbe mbalimbali kwenye Internete. Anapoendelea kutumia Internete, anafungua adresi fulani ili apate habari kuhusu bei ya kitu fulani anachopenda kununua. Bila kujua, anapitisha saa mbili kwenye Internete na bado hajaanza kujifunza mambo aliyopanga kujifunza mangaribi hiyo. Sababu gani ni jambo la maana painia aheshimu programe yake ya kujifunza? Wakimbiaji wazuri wanapaswa kuhangaikia sana afya yao ikiwa wanapenda kufanya kazi hiyo kwa muda murefu. Vivyo hivyo, mapainia wanapaswa kuwa na programe nzuri ya funzo la pekee ili waendelee kuwa na nguvu kiroho ikiwa wanapenda kubaki katika utumishi wa wakati wote.​—1 Tim. 4:16.

14, 15. (a) Sababu gani mapainia wanapaswa kuendelea kuwa na maisha rahisi? (b) Painia anapaswa kufanya nini ikiwa anapata matatizo fulani?

14 Mapainia wenye mafanikio wanajikaza kuendelea kuwa na maisha rahisi. Yesu aliwatia moyo wanafunzi wake wawe na jicho rahisi. (Mt. 6:22) Alifanya maisha yake yawe rahisi ili atimize huduma yake bila kukengeushwa. Ndiyo sababu alisema hivi: “Mbweha wana mapango na ndege wa mbinguni wana viota, lakini Mwana wa binadamu hana mahali popote pa kulaza kichwa chake.” (Mt. 8:20) Ni vizuri painia anayetamani kufuata mufano wa Yesu akumbuke kwamba, kuwa na vitu vingi vya kimwili kutamuomba wakati mwingi zaidi wa kuvitunza, kuvitengeneza ao kuvibadili.

15 Mapainia wanajua kwamba hawapewe pendeleo hilo la utumishi kwa sababu wao ni bora kuliko wengine. Tofauti na hilo, tuna uwezo ao pendeleo fulani kwa sababu ya fazili zisizostahiliwa za Mungu. Kwa hiyo, kila painia anapaswa kumutegemea Yehova ili aendelee kufanya kazi hiyo. (Flp. 4:13) Lakini matatizo hayatakosa kutokea. (Zab. 34:19) Kuliko kuacha haraka pendeleo lao la utumishi kwa sababu ya matatizo fulani, mapainia wanapaswa kutafuta muongozo wa Yehova na kuacha mambo katika mikono yake. (Soma Zaburi 37:5.) Kadiri watakavyojionea namna Mungu anavyowasaidia kwa upendo, mapainia watamukaribia zaidi Baba yao wa mbinguni anayewahangaikia.​—Isa. 41:10.

JE, UNAWEZA KUWA PAINIA?

16. Ikiwa unataka kuwa painia, unapaswa kufanya nini?

16 Ikiwa ungependa kupata baraka ambazo wale walio katika utumishi wa wakati wote wanafurahia, umuambie Yehova tamaa yako katika sala. (1 Yoh. 5:14, 15) Zungumuza na mapainia. Jiwekee miradi itakayokusaidia uwe painia. Keith na Erika walifanya hivyo. Walipitisha saa nyingi katika kazi yao ya kimwili na, kama vile bibi na bwana wengi walio na miaka kama yao, walikuwa wamenunua nyumba na gari mupya kisha tu kufunga ndoa. Wanasema hivi: “Tulifikiri kwamba vitu hivyo vingetuletea furaha, lakini haikuwa hivyo hata kidogo.” Alipopoteza kazi yake, Keith alianza kufanya upainia musaidizi. Keith anakumbuka: “Kufanya kazi ya upainia kulinikumbusha furaha nyingi ambayo mutu anapata anapokuwa katika utumishi.” Keith na Erika wakawa marafiki wa bibi na bwana ambao ni mapainia waliowasaidia kuona furaha inayotokana na upainia na kuishi maisha rahisi. Keith na Erika walifanya nini? Wanasema hivi: “Tuliandika miradi yetu ya kiroho kwenye karatasi, tukabandika karatasi hiyo kwenye frigo, na tulitia alama kisha kutimiza muradi fulani.” Kisha muda fulani, walianza kazi ya upainia.

17. Sababu gani ingekuwa vizuri ubadili mambo fulani katika programe yako na maisha yako ili uwe painia?

17 Je, unaweza kuwa painia? Ikiwa unaona kwamba haujakuwa tayari sasa, fanya yote unayoweza ili kumukaribia Yehova zaidi kwa kufanya mengi katika kazi ya kuhubiri. Kisha kusali na kufikiri kwa uangalifu, unaweza kuona kwamba kubadili mambo fulani katika programe ao maisha yako kutakusaidia uwe painia. Ikiwa unakuwa painia, utapata furaha nyingi sana kuliko jitihada utakazofanya. Utakuwa mwenye kutosheka sana kwa sababu ya kutia faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza katika maisha yako. (Mt. 6:33) Utajionea furaha nyingi inayotokana na kutoa. Zaidi ya hilo, utakuwa na nafasi nyingi za kufikiri na kuzungumuza kuhusu Yehova, jambo hilo litakufanya umupende Yehova zaidi na kumufurahisha.