Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa nini Yesu alitokwa na machozi kabla ya kumfufua Lazaro kama andiko la Yohana 11:35 linavyosema?

Mpendwa wetu anapokufa, kwa kawaida tunatokwa na machozi kwa sababu tutamkosa. Ingawa Yesu alimpenda Lazaro, hakutokwa na machozi kwa sababu ya Lazaro kufa. Alitokwa na machozi kwa sababu aliwahurumia waliofiwa, kama simulizi la Yohana linavyoonyesha.Yoh. 11:36.

Mwanzoni Yesu aliposikia kwamba Lazaro ni mgonjwa, hakuenda mara moja kumponya. Simulizi hilo linasema hivi: “[Yesu] aliposikia kwamba [Lazaro] alikuwa mgonjwa, ndipo kwa kweli akakaa siku mbili mahali alipokuwa.” (Yoh. 11:6) Kwa nini Yesu alikawia? Alikawia kwa kusudi fulani. Alisema hivi: “Lengo la ugonjwa huu si kifo, bali ni kwa ajili ya utukufu wa Mungu, ili Mwana wa Mungu atukuzwe kupitia huo.” (Yoh. 11:4) “Lengo” la ugonjwa wa Lazaro halikuwa kifo au haungesababisha kifo. Yesu alikusudia kutumia kifo cha Lazaro ‘kumtukuza Mungu.’ Jinsi gani? Yesu angefanya muujiza wa pekee kwa kumfufua rafiki yake mpendwa.

Yesu alipozungumza na wanafunzi wake pindi hiyo, alilinganisha kifo na usingizi. Ndiyo sababu aliwaambia kwamba ‘anafunga safari kwenda huko ili kumwamsha Lazaro kutoka usingizini.’ (Yoh. 11:11) Yesu angemfufua Lazaro kama mzazi anavyomwamsha mtoto anayelala. Hivyo, hakuwa na sababu ya kuhuzunika kwa sababu ya kifo cha Lazaro.

Basi kwa nini Yesu alitokwa na machozi? Muktadha unajibu swali hilo pia. Yesu alipokutana na Maria, dada ya Lazaro na kumwona akilia na wengine pia wakilia, “akaugua rohoni na kutaabika.” Yesu alipoona uchungu waliokuwa nao akaumia sana hivi kwamba “akaugua rohoni.” Ndiyo sababu ‘Yesu alitokwa na machozi.’ Yesu alihuzunika sana kuona rafiki zake wapendwa wakiomboleza.Yoh. 11:33, 35.

Simulizi hilo linaonyesha kwamba Yesu ana nguvu na uwezo wa kuwafufua wapendwa wetu na kuwapa afya nzuri katika ulimwengu mpya. Linatuonyesha pia kwamba Yesu ana hisia-mwenzi kuelekea watu waliowapoteza wapendwa wao kwa sababu ya kifo cha Adamu. Jambo lingine tunalojifunza kutokana na simulizi hilo ni kwamba tunapaswa kuwahurumia watu wanaoomboleza kifo cha mpendwa wao.

Yesu alijua kwamba angemfufua Lazaro. Hata hivyo, alitokwa na machozi kwa sababu aliwapenda sana na kuwahurumia rafiki zake. Vivyo hivyo, huenda tukachochewa na hisia-mwenzi ‘kulia pamoja na watu wanaolia.’ (Rom. 12:15) Kulia kwa sababu ya huzuni hakuonyeshi kwamba mtu haamini tumaini la ufufuo. Kwa hiyo, Yesu alituwekea mfano mzuri sana alipowahurumia waliofiwa na kulia kikweli hata ingawa alijua kwamba angemfufua Lazaro.