Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Maulizo ya Wasomaji Wetu

Maulizo ya Wasomaji Wetu

Kulingana na Yohana 11:35, sababu gani Yesu alitokwa na machozi mbele ya kumufufua Lazaro?

Hata ikiwa alimupenda Lazaro, Yesu hakulia kwa sababu Lazaro alikuwa amekufa. Masimulizi ya Yohana yanaonyesha kwamba alilia kwa sababu ya kusikilia familia ya Lazaro na marafiki wake huruma.​—Yoh. 11:36.

Yesu aliposikia kwamba Lazaro alikuwa mugonjwa, hakuenda mara moja kumuona ili amuponyeshe. Simulizi hilo linasema hivi: “[Yesu] aliposikia kwamba [Lazaro] alikuwa mugonjwa, ndipo kwa kweli akakaa siku mbili mahali alipokuwa.” (Yoh. 11:6) Kwa nini hakuenda haraka? Alikuwa na kusudi fulani. Alisema hivi: “Lengo la ugonjwa huu si kifo, bali ni kwa ajili ya utukufu wa Mungu, ili Mwana wa Mungu atukuzwe kupitia huo.” (Yoh. 11:4) “Lengo” ao kusudi la ugonjwa wa Lazaro halikuwa kifo. Yesu alikusudia kutumia kifo cha Lazaro “kwa ajili ya utukufu wa Mungu.” Namna gani? Yesu alikuwa karibu kufanya muujiza fulani wa ajabu kwa kumuamusha rafiki yake kutoka katika kaburi.

Alipokuwa akizungumuza na wanafunzi wake wakati huo, Yesu alilinganisha kifo na usingizi. Hiyo ndiyo sababu aliwaambia kwamba ‘anafunga safari kuenda huko ili kumwamusha [Lazaro] kutoka usingizini.’ (Yoh. 11:11) Kwa maoni ya Yesu, kumufufua Lazaro ni kama vile muzazi anavyoweza kumuamusha mutoto wake katika usingizi. Kwa hiyo hakuwa na sababu yoyote ya kuhuzunikia kifo cha Lazaro.

Kwa hiyo basi, sababu gani Yesu alitokwa na machozi? Simulizi hilo linatoa jibu. Yesu alipokutana na Maria, dada ya Lazaro, na wengine wakilia, ‘aliugua rohoni na kutaabika.’ Alipoona uchungu wao, Yesu aliumia sana na hata ‘aliugua rohoni na kutaabika.’ Hiyo ndiyo sababu ‘Yesu alitokwa na machozi.’ Yesu alihuzunika sana kwa sababu ya kuwaona marafiki wake aliowapenda wakiteseka sana.​—Yoh. 11:33, 35.

Habari hii inaonyesha kwamba Yesu ana uwezo wa kufufua na kuponya wapendwa wetu katika ulimwengu mupya unaokuja. Inatusaidia pia tuelewe kwamba Yesu anawasikilia huruma wale ambao wamefiwa na wapendwa wao. Jambo lingine tunaloweza kujifunza katika habari hii ni kwamba tunapaswa kusikilia huruma wale wanaohuzunika kwa sababu ya kufiwa na wapendwa wao.

Yesu alijua kwamba atamufufua Lazaro. Hata hivyo, alilia kwa sababu aliwapenda sana marafiki wake na aliwasikilia huruma. Vilevile, kujitia pa nafasi ya wale waliofiwa, kunaweza kutuchochea ‘tulie pamoja na wale wanaolia.’ (Rom. 12:15) Kufanya hivyo hakuonyeshe kwamba mutu hana imani katika tumaini la ufufuo. Kwa hiyo basi, Yesu alipolia, ijapokuwa alikuwa karibu kumufufua Lazaro, alituachia mufano muzuri wa kuwasikilia huruma wale wanaofiwa.